Maoni ya Biblia
Kipaimara—Je! Ni Takwa la Kikristo
“Kipaimara ni sakramenti ambayo hupa Mkristo aliyebatizwa maisha kamili ya Kikristo, yakimfanya kuwa mtu mzima kiroho, askari, na shahidi wa Kristo.”—The Catholic Enyclopedia for School and Home.
WAPROTESTANTI wengi hukataa wazo la kwamba kipaimara ni sakramenti. Hata hivyo, mwanatheolojia Mkatoliki wa karne ya 13 Thomas Aquinas aliandika kwamba “kipaimara ni kikamilisho cha sakramenti ya ubatizo.” Kwa vyovyote vile, maswali hutokea: Je! Wakristo wa mapema walikuwa na kipaimara? Je! sherehe hiyo ni takwa la Kikristo leo?
“Hakuna lolote katika Gospeli linaloonyesha kwamba Yesu mwenyewe alianzisha Sakramenti ya Kipaimara,” yakubali New Catholic Encyclopedia. Kwa hiyo kwa nini walimu wa kanisa walitoa wazo la kwamba inayofuata ubatizo, kanuni ya pili, ambayo inatia ndani kupakwa mafuta na kuwekelewa mikono, kulihitajiwa ili kumfanya mtu awe mshiriki kamili wa kanisa?
Kipaimara Kilianzaje?
Ubatizo wa vitoto vichanga ulikuwa mojapo wa mambo makuu ambayo yaliongoza kwenye uhitaji wa sakramenti nyingine. “Yakijua matatizo yanayotokana na kubatiza watoto,” kikasema kitabu Christianity, “makanisa . . . yanawakumbusha wale ambao wamebatizwa lile linalomaanishwa na ‘kipaimara’ wao baadaye maishani.” Je! kipaimara kweli huwakumbusha kile ubatizo humaanisha, au husetiri ukweli kuhusu ubatizo?
Ni wazi kwamba ubatizo wa vitoto vichanga hauungwi mkono katika Maandiko. Kunyunyizia mtoto maji, kwa mfano, hakumwondolei mtoto dhambi ya asili; ni imani tu katika dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu inayoweza kufanya hivyo. (Yohana 3:16, 36; 1 Yohana 1:7) Ubatizo wa maji ni wonyesho wa nje ambao mtu anayebatizwa amejiweka wakfu kupitia Yesu ili afanye mapenzi ya Yehova Mungu. Ubatizo wa maji ni wa wanafunzi—‘waitikadi’—si vitoto vichanga.—Mathayo 28:19, 20; Matendo 8:12.
“Ubatizo ulikomea wapi na kipaimara kilianzia wapi?” yauliza New Catholic Encyclopedia. Inajibu: “Labda tusijaribu kutofautisha kwa makini sana, kwa kuwa twashughulika na kanuni moja katika kanisa la mapema.” Naam, katika karne ya kwanza, “kanuni moja” ambayo ilileta ushirika kamili katika kundi la Kikristo ni ubatizo.—Matendo 2:41, 42.
Je! sherehe ya kipaimara, pamoja na kuwekelea mikono, kunahitajiwa kabla ya mtu kuweza kupokea roho takatifu? Hasha. Katika kundi la Kikristo la kwanza, kuwekelewa kwa mikono kukifuatia ubatizo kulikuwa ni kwa kufanya mipango ya kipekee au kuleta vipawa vya miujiza vya roho. Vipawa hivi viliisha wakati mitume walipokufa. (1 Wakorintho 13:1, 8-10) Na kuwekelea mikono kunafungamanishwa, si na ubatizo wa maji, lakini na kazi fulani hasa kuhusu utendaji wa umishonari. (Matendo 6:1-6; 13:1-3) Hivyo, wazo hilo la kwamba kipaimara huendeleza kuwekelewa mikono kwa kimitume na ni, kama kitabu Basics of Faith: A Catholic Catechism chasema, “sakramenti inayobadilisha mtu katika njia ya maana sana hivi kwamba inaweza kupokewa mara moja tu,” haliwezi kuthibitishwa likichunguzwa.
Mtume Paulo alionya juu ya kwenda kinyume cha kweli ya msingi ya Biblia: “Hakika kuna wakati unaokuja ambapo, badala ya kuridhika na mafundisho timamu, watu watakuwa na tamaa ya mambo ya kigeni . . . na halafu, badala ya kuusikiliza ukweli, watageukia hekaya.” (2 Timotheo 4:3, 4, The Jerusalem Bible) Tena, wale wanaoamini katika kanuni ya kipaimara wananukuu mifano miwili ya Kimaandiko kama udhibitisho.
Msingi wa Kimaandiko?
Habari inayopatikana katika Matendo 8:14-17 hutumiwa kila mara kama msingi wa kipaimara. Hata hivyo, kuwekelewa mikono ili kupokea roho takatifu kulikuwa pindi ya pekee. Jinsi gani hivyo? Wasamaria hawakuwa Wayahudi waongofu. Hivyo, wakawa watu wa kwanza wasio wayahudi kuingizwa katika kundi la Kikristo. Wakati mwanafunzi Filipo alipohubiri katika Samaria, Wasamaria wengi “waliendelea kubatizwa, wanaume na wanawake,” lakini hawakupokea roho takatifu mara hiyo. (Matendo 8:12) Kwa nini?
Kumbuka, ilikuwa ni Petro ndiye Yesu alimkabidhi “zile funguo za ufalme”—pendeleo la kutoa kwanza nafasi kwa kuingia katika “ufalme wa mbinguni” kwa vikundi tofauti vya waongofu. (Mathayo 16:19) Haikutokea hadi wakati Petro na Yohana walipoenda Samaria na kuwekelea mikono juu ya hawa wanafunzi wa kwanza wasio Wayahudi kwamba roho takatifu ilimwagwa juu yao kama ishara ya ushirika wao wa baadaye katika “ufalme wa mbinguni.”
Wengine huona kwenye Matendo 19:1-6 ushuhuda wa kwamba Wakristo wa mapema walikuwa na kanuni tofauti inayofuata ubatizo. Hata hivyo, katika kisa hiki, ni wazi kwamba sababu ya kuzuiwa kwa roho takatifu kwa wanafunzi wengine katika mji wa Efeso ilikuwa ni kwamba waamini hawa wapya walikuwa wamebatizwa kwa “ubatizo wa Yohana,” ambao haukuwa na nguvu tena. (Ona pia Matendo 18:24-26.) Wakati walipoelezwa hilo, mara moja “walibatizwa kwa jina lake Bwana Yesu.” Na wakati huu, mtume Paulo “aliwekelea mikono yake juu yao” ili kwamba wapokee baadhi ya vipawa vya miujiza vya roho takatifu ya Mungu zaidi ya kuwa warithi wa kuwa wana wa Mungu wa kiroho.—Warumi 8:15, 16.
Kuhusu habari hizi, kitabu New Dictionary of Theology chasema: “Hakuna utumizi wa kuendelea unaoweza kuonekana katika visa hivi, na, hata ikiwa vinatoa kiolezo cha zamani, ni jambo lenye kutiliwa shaka kuwa vinapasa kuwa desturi ya Kikristo katika njia ya kwamba ubatizo wa maji ulivyo. . . . Matendo ya Mitume kina mifano mingi ya utumizi wa ubatizo wa maji bila kufuatiwa kwa kuwekelewa mikono. (ili kwamba mambo haya kwa kweli yaonekane kuwa tofauti).” Ndiyo, haya yalikuwa matendo ya kipekee ili kuwezana na hali za kipekee.
“Kanuni inayoitwa ‘kipaimara,’” inamalizia New Dictionary of Theology, “imekuwa ‘kanuni katika kutafuta theolojia.’” Kwa kweli, ni kanuni isiyo ya Kimaandiko, mojapo ya mafundisho yenye kasoro, na kwa hakika si takwa la Kikristo.