Ubatizo wa Vitoto Vichanganga—Sababu Inayofanya Mapadri Wengine Wakatae!
ALAN na Sonia walitaka mtoto wao abatizwe tu, basi. Kwa hiyo walishtuka wakati padri wao wa Kianglikani alipokataa kuifanya desturi hiyo ya kidini, na isitoshe, akaongezea shauri hili: “Mbatizeni ninyi wenyewe.” Sababu ilikuwa nini? Alan wala Sonia hawakuwa wakienda kanisani kwa ukawaida.—The Christian Century, Juni 3-10, 1981.
Hesabu kubwa ya waume na wake waliooana wamekataliwa kwa njia hiyo—kiishara cha wazi kwamba makanisa fulani yanabadili maoni yao Juu ya ubatizo wa vitoto vichanga. Lifikirie Kanisa Katoliki la Roma. Baada ya mkutano wa baraza la Vatikani ya Pili, kanisa lilifanya mabadiliko katika desturi zake za kubatiza vitoto vichanga. Ndiyo, kanisa lingali likibatiza vitoto, lakini sasa ni lazima kwanza wazazi waonyeshe mahakikisho ya kwamba watamlea mtoto huyo akiwa Mkatoliki. Vatikani ilitangaza hivi: “Mahakikisho hayo yasipofanywa kwa uzito kweli kweli, kunaweza kuwa na sababu za kuiahirisha sakramenti; na ikiwa kwa uhakika mahakikisho hayo hayapatikani, wanapaswa hata kukatazwa sakramenti.”—L’Osservatore Romano, “Agizo juu ya Ubatizo wa Vitoto Vichanga,” Desemba 1, 1980.
Hilo ni badiliko kubwa sana likilinganishwa na siku ambazo, kulingana na maneno ya padri Mkatoliki Joseph M. Champlin, “wamisionari wenye bidii [walikuwa] wakibatiza vitoto vya wapagani vilivyotorokwa na kuachwa barabarani,” nao mapadri “wakawasihi wazazi kwamba kitoto kichanga kisikawizwe zaidi ya mwezi mmoja kabla hakijapata Ubatizo ili kisije kikaendelea kuwa na ile dhambi ya kifo.”
Ni jambo gani linalochochea mielekeo hiyo ya kubadili maoni leo? Kwanza, sasa viongozi wa makanisa wanatambua kwamba si ubatizo unaofanya mtu awe Mkristo. Mambo ambayo yametokeza hangaiko kubwa ni upungufu wa hudhurio la watu kanisani na ukosefu wa jumla katika hali ya kujitoa miongoni mwa Wakatoliki waliobatizwa. “Kwa sababu gani kanisa liongezee tatizo lenyewe kwa kubatiza watoto ambao inaonekana wazi kwamba wataelekea kuwa watu wazima wasiotenda?” Hiyo ndiyo hoja inayotolewa na makala moja katika kichapo U.S. Catholic.
Ingawa hivyo, maoni hayo ya kuweka masharti magumu juu ya ubatizo yanaonyesha wazi mtengano mkubwa kati ya wanatheolojia. Kama vile anavyosema mwandikaji Mkatoliki Joseph Martos, viongozi wa kidini wengi hawaamini kwamba ubatizo wa vitoto vichanga ni “desturi ya kidini inayogeuza nafsi kimuujiza kwa njia isiyoonekana.” Wao wanaona kwamba maoni hayo ni ya zamani zile zisizokuwa na maarifa, na hayafai tena kufuatwa.
Basi, si ajabu kwamba Wakatoliki wengi wenye mioyo myeupe wamevurugika maoni. Je, kwani sikuzote kanisa halikufundisha kwamba vitoto vichanga visivyobatizwa vingeweza kujikuta ndani ya moto wa mateso au vikaekae katika purgatori kwa muda fulani? Ikiwa hiyo ni kweli, wengine wao wanataka kujua, kwa sababu gani vikatazwe ubatizo chini ya hali zo zote’? Hayo ni maulizo ya maana. Kama vile padri Mkatoliki Vincent Wilkin alivyosema, jumla ya wale waliokufa bila kubatizwa ni “hesabu kubwa sana isiyohesabika, hivi kwamba ni rahisi kuwazia kwamba walio katika hali hiyo ndio wengi zaidi katika jamii ya kibinadamu.”
Basi, acheni tuutazame kwa ufupi ubatizo wa vitoto vichanga—kihistoria na Kibiblia.