Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 3/15 kur. 4-7
  • Je! Watoto Wachanga Wabatizwe?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Watoto Wachanga Wabatizwe?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Pokeo la Mungu au la Wanadamu?
  • ‘Katika Ukingo wa Moto wa Mateso’
  • Mjadala Unawaka Moto Tena
  • Ubatizo wa Vitoto Vichanga na Mtoto Wako
  • Ubatizo wa Vitoto Vichanganga—Sababu Inayofanya Mapadri Wengine Wakatae!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Ubatizo
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Je, Watoto Wachanga Wanapaswa Kubatizwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Ubatizo Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 3/15 kur. 4-7

Je! Watoto Wachanga Wabatizwe?

Kitoto kichanga hakionekani kuwa kitenda dhambi. Hata hivyo kusudi la desturi hii ya kidini ya tangu kale ni kusafisha dhambi. Mtu yule mwenye kukisimamia kitoto katika jambo hili anamkana Shetani na matendo yake mara tatu. Halafu padri anachukua chombo kidogo na kumimina maji polepole juu ya kipaji cha mtoto mara tatu, akisema, “Mimi nakubatiza kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu.”

KWA muda wa karibu mileani mbili vitoto vichanga vimebatizwa katika sherehe kama hiyo. Huenda wazazi wakalieleza kuwa tukio lenye kukugusa sana moyo. Lakini, je, chanzo cha zoea hilo ni Neno la Mungu? Wanatheolojia Wakatoliki wanakiri kwamba ndivyo ilivyo.​—Ona New Catholic Encyclopedia, buku la 2, ukurasa 69.

Jisomee mwenyewe kitabu cha Biblia cha Matendo, nawe utaona upesi kwamba kati ya Wakristo wa kwanza, ubatizo ulikuwa wa wale wenye kuweza ‘kusikia na kupokea maneno kwa ufahamu na kuweza ‘kufanya kitubio.’ (Matendo 2:14, 22, 38, 41, Douay Version) Ni vigumu kitoto kichanga kufanya mambo hayo! Ni kweli kwamba Biblia inataja kwamba nyumba nzima-nzima,a kama ile ya Kornelio, zilibatizwa. Lakini hata iwapo hivyo, ubatizo ulikuwa kwa ajili ya wale “waliolisikia lile neno”​—si kwa ajili ya vitoto vichanga.​—Matendo 10:44-47.

Pokeo la Mungu au la Wanadamu?

Kwa kuwa hawawezi kuonyesha kanuni fulani ya Kibiblia inayohusiana na jambo hilo, makao ya Vatikani yanasema, “Zoea la kubatiza vitoto vichanga linahesabiwa kuwa kawaida ya pokeo la tangu zamani zisizokumbukika.” Lakini je, pokeo hilo lilianzishwa na Yesu Kristo? Hapana, kwa maana ubatizo wa vitoto vichanga halikuwaka moto mpaka muda fulani baada ya kifo cha mitume. Mwishoni mwa karne ya pili, Tertullian baba wa kanisa alibisha akisema, “Acheni [watoto] wawe Wakristo wakiisha kuweza kumjua Kristo.”

Lakini, mtume Paulo alionya kwamba mwishowe ungekuja wakati ambao “watu hawatavumiliana na fundisho lililo la utimamu.” (2 Timotheo 4:3, The New American Bible) Baada ya mitume kufa wakawa hawawezi tena ‘kuwa kama kizuizi,’ mazoea yasiyo ya Kimaandiko yalianza kupenya ndani ya ibada ya Kikristo. (2 Wathesalonike 2:6, NW) Kati ya hayo ulikuwapo ubatizo wa vitoto vichanga. Lakini ubatizo wa vitoto vichanga haukufanywa uwe kawaida mpaka karne ya tano. Wakati huo mjadala mkali sana ulitokea ukaibadili milele Jumuiya ya Wakristo.

Ulianza wakati mtawa-mume Mwingereza, jina lake Pelagius, alipofunga safari kwenda Roma. Kwa kushangazwa sana na ufisadi aliouona huko kati ya wenye kuitwa Wakristo, kiongozi huyo wa kidini alianza kuchochea watu wafanye “jitihada zaidi ya kufuata adili.” Mwanadamu hangeweza kuilaumu ile ‘dhambi ya asili’ kwa sababu ya udhaifu wake wa namna mbalimbali, akasema Pelagius. “Kila lililo jema na kila lililo ovu . . . linafanywa na sisi, wala halizaliwi pamoja na sisi.” Fundisho hilo la Pelagius likawa ndiyo maongezi makuu katika Jumuiya ya Wakristo.

Lakini haikuendelea hivyo kwa muda mrefu. Viongozi wa kanisa waliiona hatua hiyo ya kuliachilia mbali wazo la ‘dhambi ya asili’ kuwa uzushi. Naye Pelagius hakujua kwamba kwa kuipendelea ile desturi iliyofuatwa sana ya kubatiza vitoto vichanga, alikuwa akiwapa viongozi hao nafasi nzuri sana ili wapinge wazo lake. Askofu mwenye kuitwa Augustino aliyaona mawazo hayo mawili kuwa yasiyopatana kabisa. ‘Ikiwa ni lazima vitoto vichanga vibatizwe,’ Augustino akatoa hoja yake, ‘namna gani vile visivyobatizwa?’ Wazo hilo lilipoelekea kuwa limethibitishwa, ndipo Augustino alipoiangusha dharuba yake: Kwa kuwa vitoto vichanga visivyobatizwa vililaaniwa vikaingie katika mateso, ni kitu gani kingine kingefanya mambo yawe hivyo kama si ile ‘dhambi ya asili’?

Ndivyo lilivyoangamia fundisho la Pelagius. Ndipo baraza la kanisa katika Carthage lilipoyatangaza mafundisho ya Pelagius kuwa uzushi. Fundisho la ‘dhambi ya asili’ likafuatwa sana likiwa sehemu ya Ukatoliki sawa na vile walivyoifuata desturi ya kuungama dhambi. Na sasa kanisa likawa na kichocheo cha kugeuza watu kwa wingi wafuate dini yao​—mara nyingi hiyo ikiwa ni kwa kuwalazimisha​—ili kuwaokoa wasije wakaingia katika ‘mioto ya mahali pa mateso.’ Ubatizo wa vitoto vichanga uliacha kuwa desturi ya kikawaida tu yenye kufuatwa na watu wengi, ukawa chombo rasmi ya kupatia wokovu, chombo ambacho Uprotestanti ungerithi baadaye.

‘Katika Ukingo wa Moto wa Mateso’

Fundisho la Augustino lilitokeza maulizo yenye kutatanisha sana: Mungu wa upendo angeweza kutaabishaje motoni watoto wachanga wasio na hatia? Je! watoto wachanga wasiobatizwa wangepokea adhabu moja na watenda dhambi wa kuzoea? Imekuwa vigumu wanatheolojia kupata majibu. Padri Mkatoliki Vincent Wilkin anasema: “Wengine wamesema kwamba vitoto vichanga visivyobatizwa vinaingia ndani kabisa ya miali ya moto wa mateso, wengine wakawa wanaamini kwamba havikuchomwa sana na miali hiyo ya mateso bali vilipashwa moto mpaka vikasumbuka-sumbuka kweli kweli; wengine walikuwa wakisema kwamba masumbuko hayo yalikuwa ya kiasi kidogo kabisa katika moto wa mateso . . . Wengine walikuwa wakisema kwamba vitoto hivyo viliingia katika paradiso ya duniani.”b

Ingawa hivyo, nadharia yenye kufuatwa na wengi zaidi ni ile inayosema kwamba nafsi za vitoto visivyobatizwa zinawekwa katika limbo. Kwa uhalisi neno hilo linamaanisha “ukingo” (kama vile ukingo au upindo wa vazi) na linaeleza jimbo linalosemwa kuwa liko kwenye kingo za moto wa mateso. Wanatheolojia wanaliona wazo la limbo kuwa lenye kufaa sana. Wana maoni ya kwamba angalau hiyo inapunguzia vitoto vichanga yale mateso makali sana.

Lakini kama vile ilivyo nadharia yo yote ya kibinadamu, limbo ina matatizo. Mbona haitajwi katika Maandiko? Je! watoto wachanga wanaweza kutoka katika limbo? Na kwa sababu gani watoto wachanga wasio na hatia walazimike kuingia humo mara ya kwanza? Kulingana na hayo, inaweza kuonekana ni kwa nini kanisa linasema kwamba limbo “si fundisho rasmi la Kikatoliki.”c—New Catholic Encyclopedia.

Mjadala Unawaka Moto Tena

Kwa karne nyingi Wakatoliki wameshikilia kwa kadiri kubwa maoni ya Augustino kisha wakabatizisha watoto wao ili wasiweze kuingia limbo. Lakini, tangu miaka ya 1950 ule mjadala unaohusu kubatiza vitoto vichanga umefufuliwa kwa njia ya kutazamisha. Wanachuo Wakatoliki wameanza kuonyesha mashaka mazito kama zoea hilo ni la Kibiblia. Huenda wengine wakakiri kwamba hawawezi kukubali wala mawazo ya Agustino kuhusu moto wa mateso wala wazo la limbo.

Ingawa hivyo, mara ya kwanza viongozi wa makanisa wasiotaka mabadiliko walikataa kuchukua hatua. Mwaka 1951 Papa Pius wa 12 alitolea hotuba kikundi cha wakunga wa kike. Akirudia kuthibitisha imani ya kwamba “wakati wa kufa mtu anahitajiwa kabisa awe ana hali ya neema ndipo aweze kupata wokovu,” aliwatia moyo wakunga hao wajiongozee desturi hiyo ya kidini ikielekea kuwa mtoto mwenye kuzaliwa sasa hivi angekufa. “Basi, msikose kuufanya utumishi huu wa fadhili,” akawahimiza. Vivyo hivyo, mwaka 1958 makao ya Vatikani yalitoa onyo kali kwamba “vitoto vichanga vinapasa kubatizwa upesi iwezekanavyo.”

Hata hivyo, ubishi ulitokea tena baada ya ule mkutano unaojulikana sana wa baraza la Pili la Vatikani. Kanisa lilishangaza kwa kujaribu kuyatenganisha maoni ya wasiotaka mabadiliko na ya wale wenye kutaka mabadiliko. ‘Ubatizo unahitajiwa kabisa ndipo mtu aweze kupata wokovu,’ likasema baraza hilo. Ingawa hivyo, ajabu ni kwamba wokovu ungeweza kupatwa pia na wale ambao “si kosa lao kwamba hawaijui gospeli ya Kristo.”d

Kufuatisha hatua hiyo, ndipo kanisa liliporekebisha ile desturi ya kubatiza vitoto vichanga, Kati ya mambo mengine, sasa mapadri walikuwa na chaguo la kuweza kukataa kubatiza ikiwa wazazi wa mtoto hawakuahidi kumlea akiwa Mkatoliki. Je, sasa kanisa lilikuwa limeliacha kabisa fundisho la Augustino? Wengine walifikiri hivyo wakaanza kutia shaka juu ya uhitaji wa vitoto vichanga kubatizwa.

Ndipo makao ya Vatikani yaliposambaza lile “Agizo juu ya Ubatizo wa Vitoto Vichanga,” lililosema hivi: “Kanisa . . . halijui njia nyingine isipokuwa ubatizo ya kuhakikishia kwamba watoto wanaingia katika furaha ya milele.” Maaskofu waliagizwa ‘wawarudishe kwenye zoea lile la kawaida wale ambao . . . wameliacha.” Lakini namna gani watoto wachanga wanaokufa bila kubatizwa? “Jambo la pekee liwezalo kufanywa na Kanisa ni kuwakabidhi kwenye rehema ya Mungu.”

Ubatizo wa Vitoto Vichanga na Mtoto Wako

Bila shaka, Wakatoliki wengi wenye moyo mweupe wanahangaishwa kikweli na mambo yote hayo. Hata hivyo, huenda wengine bado wakaona kwamba, hata kama hilo ni fundisho la Kikatoliki, angalau ubatizo unampa mtoto mwanzo mzuri kidini. Lakini je, ni hivyo? Mama mmoja Mkatoliki alisema: “Mimi nina watoto wawili wadogo sana, na wote walibatizwa walipokuwa vitoto vichanga, nami sioni hata chembe moja ya neema ndani yao, mambo ni kinyume kabisa.”

Kubatiza mtoto mdogo hakumsaidii akue katika imani. Kwa kweli, kunaivunja amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi .. . kuwabatiza.” (Mathayo 28:19, NW) Ubatizo hauna maana ikiwa mtu hana umri wa kutosha aweze kuwa mwanafunzi. Ni kweli kwamba ubatizo wa vitoto vichanga umekuwa ni “pokeo la tangu zamani za kale sana.” Lakini je, Yesu hakuwalaumu wale ‘waliolitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yao’?​—Mathayo 15:6.

Kwa hiyo, Biblia inawatia moyo wazazi wazoeze watoto wao mambo ya kiroho “tangu utoto mchanga.” (2 Timotheo 3:14-17, NW) Hivyo Mashahidi wa Yehova wanachukua kwa uzito onyo la upole wanalopewa na Biblia kwamba walee watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Mara nyingi jambo hilo linafanywa kwa kuendesha programu ya ukawaida ya funzo la kijamaa’ la Biblia. Wazazi wa namna hiyo wanafundisha watoto wao kuhudhuria na kushiriki mikutano ya Kikristo. (Waebrania 10:24, 25) Wanawatia moyo watoto wao wafanye “tangazo la waziwazi” la imani yao. (Warumi 10:10, NW) Baada ya muda, huenda watoto wao wakasukumwa na moyo wao wafanye wakfu wao wenyewe kwa Yehova Mungu na kuuonyesha kwa kubatizwa katika maji. Hilo ni jambo la Kimaandiko nalo ni la maana na la kuridhisha kuliko kutazama desturi rasmi ya kidini ikifanywa juu ya kitoto kichanga kisicho na utambuzi.

Mtoto wa Mkristo akifa kabla ya ubatizo, wazazi wake hawana haja ya kuogopa kwamba anachomwa ndani ya moto wa mateso au anakaa-kaa katika limbo. Biblia inafundisha kwamba wafu hawajui neno. (Mhubiri 9:5, 10) Hivyo wazazi wanaweza kupata faraja katika ahadi ya Yesu kwamba “saa inakuja ambayo katika hiyo wale wote walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake watoke” wakiwa na taraja la kupata uzima katika Paradiso itakayokuwa imerudishwa. (Yohana 5:28, 29; Luka 23:43) Tumaini hilo lenye msingi wa Kibiblia linafariji kuliko mapokeo ya kibinadamu yanayoweza kubadilika, tena yenye kuvuruga.

[Maelezo ya Chini]

a Nyakati nyingine neno “nyumba” katika Biblia kwa wazi halitii ndani vitoto vichanga. Kwa mfano, andiko la Tito 1:11 linawataja waasi-imani kuwa ‘wakipindua watu wa nyumba nzima.’​—Ona pia 1 Samweli 1:21, 22.

b Augustino alipendekeza kwamba vitoto vichanga visivyobatizwa “vitahusika katika laana iliyo pole kuliko zote.”

c Wakati mkutano wa maafisa wa kanisa ulipofanywa karne ya 18 ukajaribu kutangaza limbo kuwa “hadithi ya Kipelagia,” Papa Pius wa 6 alisambaza agizo rasmi la makao ya papa akiulaani mkutano huo kuwa wa kutokeza uzishi. Ingawa halikukubaliana na limbo kwa ukamili, agizo rasmi la papa liliachilia nadharia hiyo iendelee kuwapo.

d Tad Guzie mwanatheolojia Mkatoliki aliuita msimamo mpya wa kanisa kuwa ni “mawazo yasiyo ya utimamu yanayohusu sakramenti ambayo kubatizwa katika maji ndiyo hatua ya kwanza ya wokovu iliyo muhimu kwa vitoto vichanga, lakini ikiwa pia ndiyo hatua ya mwisho ya mwendo mrefu zaidi kwa mtu mwingineye yote.”

[Chati katika ukurasa wa 7]

Mambo Makuu ya Historia ya Kubatiza Vitoto Vichanga

Tarehe (W.K.) Tukio

kama 193 Tertullian anatoa hoja zake akitaka watu wazima

ndio wabatizwe

253 Barazala Carthage lina tangaza kwamba ‘watoto

wachanga wanapaswa kubatizwa bila kukawia’

412-417 Mjadala kati ya Pelagius na Augustino kuhusu

ile ‘dhambi ya asili’

417 Baraza la Carthage linalaumu maoni ya Pelagia

kuwa uzushi.

Ubatizo wa vitoto vichanga unakuwa jambo la

kudumu katika Ukatoliki.

1201, 1208 Papa Innocent wa 3 anaandika kwa kupendelea

ubatizo wa vitoto vichanga

1545-1563 Baraza la Trent linatangaza “laana ya kanisa”

juu ya mtu ye yote anayekataza ubatizo wa vitoto

vichanga

1794 Agizo rasmi la makao ya papa linaloitwa Auctorem

Fideil linaulaumu mkutano Jansenist wa maafisa wa

kanisa, ulisema limbo ni uzushi

1951 Papa Pius wa 12 anakazia uhitaji wa kubatiza

vitoto vichanga kwa kuwatia moyo wakunga wa kike

waifanye desturi hiyo ya kidini katika matukio ya

dharura

1958 Vatikani inaagiza kwamba ‘vitoto vichanga vitapaswa

kubatizwa upesi iwezekanavyo’

1963-1965 Baraza la Pili la Vatikani linaagiza kwamba wokovu

unaweza kupatikana bila ubatizo Linaagiza kwamba

desturi ya kidini ya kubatizwa vitoto vichanga

irekebishwe

1980 Makao ya Vatikani yanaimarisha desturi ya kubatiza

vitoto vichanga, yakisema kwamba ‘hayajui njia

nyingine yo yote ya watoto kuingia katika furaha ya

milele’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki