Msaada Bora Zaidi Unapatikana!
KWA Mkristo, uchaguzi na kadiri ya utunzi wa wagonjwa mahututi waweza kuzusha maswali ya maana. Kwa mfano:
Je! lingekuwa jambo lisilo la kimaandiko kukosa kufanya kila jambo liwezekanalo ili kuhifadhi uhai? Na ikiwa inakubalika kimaadili kuruhusu mtu kufa kiasili, bila miingilio ya kishujaa ili kurefusha uhai, namna gani euthanasia—kitendo cha makusudi, cha kukomesha kuteseka kwa mgonjwa kwa kufupiza au kukatisha uhai wake?
Katika siku na kizazi hiki chetu, maswali hayo ni ya maana. Hata hivyo, si kwamba hatuna msaada katika kuyajibu.
Mwandikaji aliyepuliziwa roho alisema: “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1) Jambo hilo ni kweli kwetu sisi pia tunapofikiria habari hii. Yehova Mungu ndiye chanzo cha msaada wa hekima zaidi, wenye ustadi zaidi. Yeye ametazama maisha za maelfu ya mamilioni ya watu. Yeye ajua—vizuri zaidi ya daktari, mwanamaadili, au wakili yeyote—kile kilicho bora zaidi. Kwa hiyo acheni tuone ni msaada gani anaofanya upatikane kwetu.—Zaburi 25:4, 5; Waebrania 4:16.
Maoni Yafaayo ya Uhai
Ni vema kung’amua kwamba wazo la kuhifadhi uhai kwa vyovyote si la wanatekinolojia wa tiba peke yao. Ni zao la kiasili la mawazo ya kilimwengu ya ki-siku-hizi. Kwa nini iko hivyo? Ikiwa uhai wa sasa ndio uu huu tu, basi inaweza kuonekana kwamba uhai wetu wa kibinafsi wapasa uhifadhiwe katika hali zote na kwa vyovyote. Lakini wazo hilo la kilimwengu limetokeza maono ya kuhofisha kitiba katika visa fulani—watu waliozirai wakiendelezwa kuwa “hai” kwa mashine kwa muda wa miaka mingi.
Kwa upande mwingine, kuna wale wanaoamini kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu. Kulingana na mawazo yao, uhai huu ni kama kituo tu kilichoko barabarani kuelekea kitu bora zaidi. Plato, mmoja wa waanzilishi wa wazo hilo, alisema:
“Aidha kifo ni hali ya utupu na kutokuwa na fahamu kabisa, au, kama vile watu husema, kunakuwa na badiliko na kuhama kwa nafsi kutoka ulimwengu huu hadi mwingine. . . . Sasa ikiwa kifo kinatokeza hali hiyo, mimi ninasema kuwa kufa ni faida.”
Mtu aliye na itikadi kama hiyo huenda akaona kifo kuwa rafiki, cha kutamanika na labda hata cha kuharakishwa. Walakini Biblia hufunza kwamba uhai ni mtakatifu kwa Yehova. Mtunga zaburi aliyepuliziwa roho aliandika, “Maana kwako Wewe iko chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Basi je! inafaa Mkristo kushiriki katika uuaji wa huruma?
Wengine huonelea kuwa kuna rejezo la Kimaandiko kwa habari hiyo wakati Mfalme Sauli, aliyejeruhiwa vibaya sana, alipomwomba mbeba silaha zake amwue. Wao wameona hilo kuwa aina ya uuaji wa huruma, tendo la makusudi la kuharakisha kifo kwa mtu ambaye tayari alikuwa anakufa. Mwamaleki mmoja baadaye alidai kuwa alikubali ombi la Sauli kwamba auawe. Lakini je! Mwamaleki huyo alidhaniwa kuwa alikuwa amefanya vema kukomesha kuteseka kwa Sauli? Sivyo. Daudi, mpakwa-mafuta wa Yehova, aliamuru kwamba Mwamaleki huyo auawe kwa hatia yake ya damu. (1 Samweli 31:3, 4; 2 Samweli 1:2-16) Basi, tukio hilo la Kibiblia halimpi Mkristo haki ya kushiriki kwa vyovyote katika uuaji wa huruma.a
Hata hivyo je! hilo linamaanisha kwamba lazima Mkristo afanye yote yawezekanayo kitekinolojia ili kurefusha uhai unaokwisha? Je! ni lazima mtu aurefushe mwendo wa kufa kwa kadiri iwezekanavyo? Maandiko yanafundisha kwamba kifo si rafiki ya mwanadamu, bali ni adui. (1 Wakorintho 15:26) Isitoshe, wafu hawateseki wala hawaoni shangwe, bali wamo katika hali kama ya usingizi. (Ayubu 3:11, 13; Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14; Matendo 7:60) Matarajio ya wakati ujao ya uhai kwa wafu yanategemea kabisa uwezo wa Mungu wa kuwafufua kupitia Yesu Kristo. (Yohana 6:39, 40) Kwa hiyo tunaona kwamba Mungu ametuandalia maarifa haya yenye msaada: Kifo si jambo la kutamanika, lakini pia hakuna lazima ya kufanya jitihada zozote za kurefusha mwendo wa kufa.
Miongozo ya Kikristo
Ni miongozo gani ambayo Mkristo aweza kutumia katika hali ambapo mpendwa yumo katika hali mahututi?
Kwanza, ni lazima tukubali kwamba kila hali inayohusu ugonjwa mahututi ni tofauti, ni msiba tofauti, na hakuna sheria za kotekote. Isitoshe, Mkristo apaswa awe mwangalifu kufikiria sheria za nchi katika visa kama hivyo. (Mathayo 22:21) Kumbuka pia kwamba, hakuna Mkristo yeyote mwenye upendo ambaye angetetea kupuuzwa kwa tiba.
Ni wakati tu ambapo kwa hakika kuna ugonjwa wa kufisha (hali ambayo imeonekana wazi kuwa haina tumaini) ndipo ifikiriwe kuomba vitegemeza-uhai vya kitekinolojia viondolewe. Katika hali kama hizo hakuna sababu za Kimaandiko za kusisitizia tekinolojia ya kitiba ambayo ingerefusha tu mwendo wa kufa ambao umeendelea sana.
Mara nyingi hali hizo huwa ngumu sana na zinaweza kuhusisha maamuzi yenye kutaabisha. Kwa mfano, mtu aweza kujuaje wakati ambao hali haina tumaini? Ingawa hakuna awezaye kuwa na uhakika kabisa, kufikiri kuzuri kwaweza kufanywa pamoja na shauri lenye uangalifu. Gazeti moja la tiba likiwashauri madaktari lasema:
“Ikiwa kuna kutoafikiana kuhusu utambuzi au kisio la maendeleo ya ugonjwa au yote mawili, shughuli za kutegemeza uhai zapasa kuendelezwa mpaka kuwe na maafikiano yanayofaa. Hata hivyo, katika visa ambavyo kwa wazi havina matumaini, kusisitiza kupata uhakikisho wa kupita kiasi kwaweza kumzuia tabibu anayeshughulikia vibadala vya tiba. Ripoti isiyo ya kawaida ya mgonjwa aliyekuwa na hali hiyohiyo na kuokoka siyo sababu kuu ya yote ya kuendelea na matibabu ya kila aina. Uwezekano huo duni wa kitarakimu haushindi matarajio yanayofaa ya matokeo yatakayoongoza maamuzi ya tiba.”
Katika hali ngumu kama hiyo, Mkristo, awe ni mgonjwa au mtu wa ukoo, kwa haki angetazamia kupata msaada kutoka kwa tabibu wake. Gazeti hilo la kitiba lamalizia: “Kwa vyovyote vile, si jambo la haki kuandaa tu habari na vibadala vingi vya kitiba na kuacha mgonjwa ametatanishwa bila mwongozo zaidi wa njia za badala za kutenda na kutotenda.”
Wazee wa kundi la kwenu, wakiwa wahudumu wakomavu, waweza pia kuwa msaada mkubwa. Bila shaka, ni lazima mgonjwa pamoja na familia yake ya karibu wafanye uamuzi wao wenyewe wenye usawaziko katika hali hiyo ya kihisia-moyo.
Mwishowe, fikiria mambo haya. Wakristo wanataka sana waendelee kuwa hai ili wafurahie kumtumikia Mungu. Hata hivyo, wao wanang’amua kwamba katika mfumo uliopo, sisi sote tunakufa; katika maana hiyo sisi sote ni wagonjwa mahututi. Ni kupitia tu damu ya Yesu Kristo yenye kufidia kwamba tuna tumaini lolote la kubadili hali hiyo.—Waefeso 1:7.
Ikiwa kifo kinampata mpendwa wetu, hilo likiwa jambo la kusikitisha sana, hatuachwi na maumivu makuu na kuhuzunika “kama na wengine wasio na matumaini.” (1 Wathesalonike 4:13) Badala yake, tunaweza kupata faraja kwamba tulifanya yote tuliyoweza kwa ajili ya mpendwa wetu aliyekuwa mgonjwa na kwamba msaada wowote wa kitiba tuliotumia ulikuwa wa kufaa kwa muda. Hata hivyo, tuna ahadi ya furaha ya Yule atakayetuweka huru na matatizo hayo yote wakati ‘adui wa mwisho, kifo, atakapobatilishwa.’—1 Wakorintho 15:26, NW.
Naam, mwishowe msaada ulio bora kabisa kwa wanaokufa utakuja kutoka kwa Mungu aliyewapa wanadamu wa kwanza uhai na ambaye huahidi ufufuo kwa wale wanaojizoeza imani kwake na Mwana wake, Yesu Kristo.—Yohana 3:16; 5:28, 29.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi kuhusu kile kiitwacho eti uuaji wa huruma, ona Amkeni! ya Machi 8, 1978, kurasa 4-7, na la Mei 8, 1974, kurasa 27-8, Kiingereza.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Je! kifo cha Sauli kinaunga mkono uuaji wa huruma?