Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 12/8 kur. 24-27
  • Kuwastahi Wanawake Katika Maisha ya Kila Siku

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwastahi Wanawake Katika Maisha ya Kila Siku
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Wanawake Wanavyoonwa
  • Kuonyesha Staha Nyumbani
  • Kuonyesha Staha Kazini
  • Kuonyesha Upendo na Staha Ukiwa Mume
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuonyesha Upendo na Staha Ukiwa Mke
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Wanawake Wana Wakati Ujao Gani?
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 12/8 kur. 24-27

Kuwastahi Wanawake Katika Maisha ya Kila Siku

IKIWA wanawake watastahiwa zaidi ya sasa, badiliko lapaswa lianze lini na wapi? Upendeleo na chuki zisizo na sababu kwa kawaida hutokea lini na wapi? Nyumbani, na shuleni, katika miaka ya ukuzi. Sisi husitawisha mitazamo yetu kwa kadiri kubwa chini ya uvutano wa wazazi. Kwa hiyo, ni nani kwa kufaa anayeweza kuwa na athari yenye nguvu juu ya mitazamo ya wakati ujao ya vijana wanaume kuelekea wanawake? Bila shaka, ni baba na mama. Kwa hiyo mmojawapo funguo za tatizo hili ni elimu ifaayo ambayo yaweza kupenya nyumbani na kuwavuta wazazi.

Jinsi Wanawake Wanavyoonwa

Jambo la kwamba chuki isiyo na sababu hukaziwa kikiki nyumbani linatolewa kielelezo na Jenny, sekretari aliyeolewa, na aliye mkubwa zaidi kati ya wasichana wanne, aliyesema: “Tukiwa wanawake wachanga, tulitambua sikuzote ukweli wa kwamba katika United States, kuna wanawake wengi kuliko wanaume. Kwa hiyo ukitaka kuolewa ni lazima kujitoa upatikane.

“Halafu pia, wanawake wanafanywa wafikiri kuwa wao ni viumbe wa chini. Nyakati nyingine hata wazazi wako wanakufanya ufikiri kuwa wavulana wanastahili zaidi ya wewe. Mwanamume fulani aingiapo maishani mwako, yeye akupa wazo lilelile, kwamba wewe ni wa chini kuliko wanaume.

“Na kwa nini msingi wa kujistahi kwetu utegemee hasa ukubwa na uzuri wa mwili au ukosefu wa huo? Je! wanaume hukadiriwa hivyo?”

Betty, aliyeolewa kwa miaka 32, na pia aliyekuwa meneja wa duka, alisema jambo jingine: “Kwa nini wanawake hukadiriwa kwa jinsia yao badala ya ujuzi, uwezo na weledi wao? Jambo ninaloomba tu ni kwamba wanaume wasikilize maoni yangu. Usinidharau kwa msingi wa jinsia yangu!

“Mara nyingi sana wanaume huwaona wanawake kana kwamba sisi sote ni wapumbavu au wajinga—wapumbavu sana hivi kwamba hatuwezi kufanya uamuzi. Unajua nisemacho? Acheni watutendee kama vile wangependa kutendewa. Hilo litabadili maoni yao upesi!” Analoomba tu ni kwamba wanaume watumie ile Kanuni ya Kidhahabu. “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.

Wanawake hao wanatoa madokezo ya maana. Thamani ya kweli ya mwanamke haipasi kutegemea sura na upendezi wake wa juujuu tu wala utamaduni fulani unaopendelewa kuliko ule mwingine. Mithali ya Kihispania hueleza hivi: “Mwanamke mrembo hupendeza macho; mwanamke mwema hupendeza moyo. Ikiwa wa kwanza ni kito cha thamani, wa pili ni hazina.”

Biblia hutoa wazo kama hilo katika njia tofauti: “Urembo wako usitegemee mitindo ya nywele zenye madoido au kuvalia vito au mavazi mazuri, bali utu wa ndani—uzuri usiofifia wa roho yenye utulivu na uanana, jambo lenye thamani kubwa machoni pa Mungu.” Na kama vile tusivyopaswa kukadiria kitabu kwa jalada lacho, hivyo hatupaswi kukadiria watu kwa jinsia yao.—1 Petro 3:3, 4, Phillips.

Kuonyesha Staha Nyumbani

Lalamiko la haki la wanawake wengi, hasa wake wafanyao kazi na kina mama pia, ni kwamba waume zao hawatambui kuwa kazi za nyumbani ni kazi za ziada, na kwa kawaida waume hawafanyi sehemu yao. Susan Faludi, aliyenukuliwa mwanzoni, asema: “Wala wanawake hawafurahii usawa katika nyumba zao wenyewe, ambamo wangali wanafanya asilimia 70 ya kazi za nyumbani.” Suluhisho la ukosefu huo wa haki ni nini?

Ingawa labda haipendezi waume wengi katika tamaduni fulani, mpango wa kazi za nyumbani wenye haki wapaswa kufanywa, hasa ikiwa mwanamke anapaswa kwenda kazini pia. Bila shaka kushirikiana kokote katika kazi huenda kukahusisha utendaji mbalimbali ambao kwa kawaida ni daraka la mwanamume—kutunza gari, kutunza ua na bustani, kazi ya kutunza mifereji ya maji, kazi ya stima, na kadhalika—ambazo hata hivyo, hulingana mara chache sana na wakati ambao mke hutumia katika kazi za nyumbani. Katika nchi nyingine waume hata humtazamia mke ahakikishe gari limeoshwa na kuwa safi kana kwamba ni sehemu ya nyumba!

Kwa njia fulani, pendekezo hilo la kushiriki katika kazi za nyumbani lapatana na shauri la mtume Petro kwa waume la kukaa na wake zao “kwa akili.” (1 Petro 3:7) Pamoja na mambo mengine, hili lamaanisha kwamba mume hapaswi kuwa tu asiye na hisia wala huruma kwa mwenzake, mshiriki-chumba asiye na huruma au mwenzi wa nyumba. Anapaswa kustahi weledi na ustadi wa mke wake. Anapaswa pia kuelewa mahitaji ya mke wake akiwa mwanamke, mke, na mama. Hilo lahusisha ndani zaidi ya uhitaji wa kuwa mpata riziki wa kuleta machumo nyumbani; wanawake wengi wafanyao kazi hufanya hivyo pia. Mume anapaswa kuelewa mahitaji ya mke wake ya kimwili, kihisia-moyo, kiakili, kingono, na zaidi ya yote, yale ya kiroho.

Kwa mume anayedai kufuata kanuni za Kikristo, kuna daraka kubwa zaidi linalohusika—lile la kuiga mfano wa Kristo. Alitoa mwaliko wenye kupendeza kwa wale wote ‘waliokuwa wakisumbuka na kulemewa na mizigo,’ akisema: “Nitawapumzisha. . . . Mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.” (Mathayo 11:28, 29) Hilo ni takwa kama nini kwa upande wa waume na baba Wakristo! Kila mmoja apaswa ajiulize: ‘Je! mimi humburudisha mke wangu au humkandamiza? Je! mimi ni mwenye fadhili na mwenye kufikiwa kwa urahisi, au naelekea kuwa mdhalimu, mwonezi, au mwamrishaji? Je! mimi huonyesha “shauku ya kidugu” kwenye mikutano ya Kikristo halafu kuwa asiyevumilika nyumbani?’ Hakupaswi kuwa na waume wenye nyutu mbili katika kundi la Kikristo.—1 Petro 3:8, 9.

Kwa hiyo, haiwezi kufaa mume awe kama huyu anayesimuliwa hivi na mke mmoja Mkristo aliyetendwa vibaya: “Mkristo aliye kichwa anayeijiona kiume ambaye ni mzuri sana katika Jumba la Ufalme na hununulia wengine zawadi lakini lakini humtenda mke wake kama kinyangarika tu.” Staha inayomfaa mke haina nafasi ya kumkandamiza na kumshusha cheo. Bila shaka, hii ni kama senti yenye pande mbili; mke apaswa pia aonyeshe heshima inayofaa kwa mume wake.—Waefeso 5:33; 1 Petro 3:1, 2.

Kwa kuthibitisha yaliyo juu, Dakt. Susan Forward aandika: “Msingi wa uhusiano mzuri ni kuonyeshana staha.” Hilo huwapa wenzi wote wawili daraka la kufanya mambo yafanikiwe. Yeye aendelea: “Inatia ndani kujali na kuona hisia na mahitaji ya mmoja na mwenzake, pamoja na uthamini wa mambo yanayomfanya kila mwenzi awe wa pekee. . . . Wenzi wanaopendana hutafuta njia zenye matokeo za kushughulikia tofauti zao; hawaoni kila pambano kuwa vita ya kushinda au kushindwa.”—Men Who Hate Women & the Women Who Love Them.

Biblia hutoa pia shauri zuri kwa waume kwenye Waefeso 5:28: “Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe.” Kwa nini habari hiyo ni kweli? Kwa sababu ndoa ni kama akiba ya benki ya watu wawili ambamo wote wameweka asilimia 50. Mume akitumia vibaya kiasi chochote cha pesa hizo, anadhuru hali ya kifedha ya wote wawili. Vilevile, mume akimdhuru mke wake katika njia yoyote, basi iwe kwa muda mfupi au mrefu yeye anajidhuru mwenyewe pia. Kwa nini? Kwa sababu ndoa yake ni akiba ya ushirika. Ukidhuru akiba hiyo, unadhuru washirika wayo wote wawili.

Kuna jambo moja la maana la kukumbukwa kuhusu staha—haipasi kudaiwa. Ijapokuwa kila mwenzi apaswa kumstahi mwenzake, ni lazima pia istahiliwe. Kristo hakupata kamwe staha kwa kujaribu kulazimisha uwezo au cheo chake cha juu zaidi.a Vilevile, katika ndoa, mume na mke hupata staha kwa mwendo wao wa kufikiriana, si kwa kutumia Maandiko ya Biblia kuwa nyundo ili kuidai.

Kuonyesha Staha Kazini

Je! wanaume wapaswa kuona wanawake kuwa tisho la hali yao ya kuwa wanaume? Katika kitabu chake Feminism Without Illusions, Elizabeth Fox-Genovese aliandika: “Kwa kweli, wanawake wengi leo hutaka yale ambayo wanaume hutaka: kuwa na mapato yanayofaa, kuwa na maisha yenye kufurahisha, na kufaulu ulimwenguni bila magumu mengi.” Je! hamu au tamaa hiyo ya makuu ionwe kuwa tisho kwa wanaume? Yeye alisema pia: “Kwa nini tusitambue kwamba, ijapokuwa mabadiliko yote ambayo ulimwengu wetu umeona au huenda ukaona, tofauti zaendelea kuwapo na zaweza kufurahiwa?”

Wanaume Wakristo wanaotumika wakiwa wakubwa au wasimamizi kazini wanahitaji hasa kustahi cheo cha wafanyakazi wenzio wa kike na kukumbuka kwamba mwanamke aliyeolewa ana mwanamume mmoja tu akiwa “kichwa” chake katika maana ya Kibiblia, yaani mumeye. Wengine huenda wakawa na vyeo vya kusimamia na wanastahiwa kwa ajili yavyo; lakini tena katika maana sahihi ya Kibiblia, hakuna mwanamume mwingine ila mumeye ndiye “kichwa” cha mwanamke huyo.—Waefeso 5:22-24.

Mazungumzo kazini yapaswa kuwa ya adili nzuri sikuzote. Wanaume wanapoanza mazungumzo yanayotia ndani maana mbili au vidokezo vibaya vya kingono, hawaonyeshi staha kwa wanawake, wala hawajiletei sifa nzuri. Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru.”—Waefeso 5:3, 4.

Kubadilisha mgawo wa kazi bila kujali hisia za mwanamke ni njia nyingine ya kukosa kuonyesha staha. Mwuguzi wa kike, Jean alisema: “Ingekuwa vizuri sana ikiwa tungeombwa maoni yetu kabla mabadiliko hayajafanywa katika migawo yetu ya kazi. Kwa kweli ingekuwa mawazo mazuri. Wanawake wanahitaji huruma na wanahitaji kuhisi kwamba ni wenye thamani na wanastahiwa.”

Sehemu nyingine ya staha kazini ni kile kizuizi kinachoitwa na wanawake wengine “dari ya kioo.” Hilo lamaanisha ule “upendeleo mbalimbali wa kimashirika unaowazuia wanawake wasipate vyeo vya juu katika viwanda vya watu binafsi.” (The New York Times, Januari 3, 1992) Likiwa tokeo, uchunguzi wa karibuni katika United States ulionyesha kwamba asilimia ndogo ya kazi za vyeo vya juu hufanywa na wanawake, kutoka asilimia 14 katika Hawaii na asilimia 18 katika Utah hadi asilimia 39 katika Louisiana. Ikiwa staha inaonyeshwa, kupandishwa cheo katika kazi ya kimwili hakutategemea jinsia bali uwezo na ujuzi. Mkurugenzi wa utafiti Sharon Harlan alisema: “Inakuwa afadhali, lakini . . . bado kuna vizuizi vingi vya kazini vinavyokabili wanawake.”

[Maelezo ya Chini]

a Ona Mnara wa Mlinzi Mei 15, 1989, kurasa 10-20, “Kuonyesha Upendo na Staha Ukiwa Mume” na “. . . Ukiwa Mke.”

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

STAHA Wanawake Wanaweza Kufanya Nini?

● JISTAHI na udumishe kujistahi

● Elewesha wazi unaloruhusu lisemwe na kufanywa ukiwepo

● Weka mipaka inayofaa ya mwendo na usemi unaokubalika

● Usijaribu kushindana na wanaume katika mizaha yenye matusi na isiyo na adabu; haikufanyi uwe mwanamke mwenye kuheshimika wala hakuwafanyi wawe wanaume waungwana

● Usivalie katika njia ya kuamsha tamaa, haidhuru ni mtindo gani wa kisasa uliopo; jinsi unavyovalia huonyesha kiasi chako mwenyewe cha kujistahi

● Pata staha kwa mwendo wako; watendee wanaume kwa staha unayotazamia kutoka kwao

● Usiwe mwenye kucheza kimahaba

STAHA Wanaume Wanaweza Kufanya Nini?

● Watendee wanawake wote kwa staha na adabu; usihisi kutishwa na mwanamke mwenye kudai mamlaka

● Usimzoelee sana mtu asiye mke wako, ukitumia maneno yasiyofaa ya mapenzi

● Epuka mizaha isiyo na adabu na kukodolea macho kunakoamsha mahaba

● Usisifu kupita kiasi, na epuka kugusa-gusa kusikofaa

● Usishushe au kudharau kazi yake au utu wake

● Omba maoni, sikiliza, na wasiliana katika njia inayofaa

● Onyesha uthamini kwa kazi ya mwanamke

● Saidia na kazi za nyumbani. Ikiwa unahisi kwamba hilo lashusha cheo chako, je! vipi chake?

● Ikiwa unaishi na wazazi wako, uwe mwepesi kutambua misongo ambayo mke wako hustahimili. Yeye sasa ndiye daraka lako la kwanza na anahitaji utegemezo wako (Mathayo 19:5)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki