Barua kwa Mama na Baba
WAZAZI wazuri ni wa maana kadiri gani? Barua ifuatayo kutoka kwa mwana mkubwa akiwaandikia mama na baba yake inaonyesha walivyo wenye thamani:
“Mama na Baba Wapendwa:
“Ni miaka 16 tangu niondoke nyumbani, kwa hiyo huenda ikawashangaza kidogo kupokea barua ya aina hii kutoka kwangu sasa. Lakini baada ya kufikiri sana, niliona kuwa lazima niiandike. Miaka mingi iliyopita, nilipoondoka nyumbani kwenu, nilichukua vitu fulani kutoka kwenu ambavyo sikuwauliza kamwe ruhusa ya kuvichukua. Labda hata hamkutambua kwamba nilivichukua. Kwa kweli, nilitumia ujanja sana kuvichukua hivi kwamba sikujua nilikuwa navyo hadi miaka kadhaa ilipopita. Nimeviorodhesha kama ifuatavyo:
“Kupenda yaliyo mema: Loo! jinsi hilo limenilinda!
“Kupenda watu: Ukubwa, umbo, na rangi si ya maana. Ni yale yaliyomo ndani tu yaliyo ya maana.
“Ufuataji haki: Kitu changu ni changu, labda cha kushiriki na wengine. Kitu cha mwingine, kiache.
“Kuazimia: Katika nyakati zangu zilizo ngumu sana, huko kumenisaidia.
“Subira: Mlikuwa wenye fadhili na upendo na subira sana kwangu. Hamkukata tamaa kamwe.
“Nidhamu: Hamkuwa kamwe wakali sana wala wenye huruma mno. Lakini wakati huo sikujua. Je! mtanisamehe?
“Uhuru: Uhuru toka uchungu ambao watoto wengi sana wamekua nao—uchungu unaotiwa na wazazi wanaoumiza kimwili, kiakili na kihisia-moyo. Wakati wote mlinipa yaliyo bora, na mkanilinda na mabaya. Sitasahau kamwe yale mliyonifanyia.
“Kupenda vitu sahili: Milima, mito, anga buluu, kukwea, kupiga kambi. Mlifanya maisha yakafurahisha sana. Hakuna wazazi wengineo wangaliweza kufanya zaidi. Na hamkuchoshwa kamwe.
“Tahadhari: “Usiwe mwenye haraka mno kuamini kila jambo usikialo. Lakini unapoliamini, shikamana nalo, hata iweje.
“Kweli ya Neno la Mungu: Ndiyo ya maana zaidi ya yote. Ndio urithi wangu. Hakuna pesa, mashua, nyumba, au mali zinazoweza kulinganishwa nayo. Itanipa kilicho cha maana zaidi—uhai wa milele.
“Ni vigumu kuweka thamani ya mambo hayo juu. Hayawezi kuwekewa bei. Nimeyatumia sana. Ikiwa sitayarudisha kwenu, ninataka kuendelea kuyatumia. Ikiwa hamkatai, nilikuwa ninatumaini kuendelea kuwapatia wanangu wachanga mambo hayo. Ninajua yatawanufaisha wanangu kama vile yameninufaisha mimi. Na wakati wote nitawajulisha wanangu nilikoyapata—kwa nyanya na babu.
“Mwana wenu,
(Jina limebanwa kwa kuombwa.)”