Urithi wa Kikristo Usio wa Kawaida
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA BLOSSOM BRANDT
Ulikuwa wakati wa theluji katika San Antonio, Texas, mnamo Januari 17, 1923, siku niliyozaliwa. Ilikuwa baridi nje, lakini nilikaribishwa katika mikono michangamfu ya wazazi Wakristo wenye upendo, Judge na Helen Norris. Kutoka katika kumbukumbu zangu za mapema zaidi, lolote wazazi wangu walilofanya lilitegemea ibada yao ya Yehova Mungu.
KATIKA 1910 Mama alipokuwa na miaka minane, wazazi wake walihama kutoka mahali karibu na Pittsburgh, Pennsylvania, hadi kwenye shamba nje ya Alvin, Texas. Wakiwa huko walishangilia kujifunza kweli za Biblia kutoka kwa jirani mmoja. Mama alitumia baki la maisha yake akijaribu kuwapendeza watu na tumaini la Ufalme. Alibatizwa katika 1912 baada ya familia kuhamia Houston, Texas.
Mama na wazazi wake walikutana kwa mara ya kwanza na Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society, alipozuru kutaniko lao katika Houston. Mara nyingi familia ilikuwa inakaribisha nyumbani kwayo wawakilishi wasafirio wa Sosaiti, walioitwa mapilgrimu wakati huo. Miaka michache baadaye, Mama alihamia Chicago, Illinois, pamoja na wazazi wake, na Ndugu Russell alikuwa pia akizuru kutaniko la huko.
Katika 1918, Nyanya alipatwa na mafua ya Kihispania na kwa sababu yaliathiri afya yake, madaktari walipendekeza kwamba aishi katika halijoto yenye joto zaidi. Kwa kuwa Babu alikuwa akifanya kazi kwenye kampuni ya magari-moshi ya abiria iitwayo Pullman, katika 1919 alirudishwa Texas. Huko, katika San Antonio, Mama alikutana na mshiriki mmoja wa kutaniko hilo mchanga na mwenye bidii, aliyeitwa Judge Norris. Walivutiana mara moja, na hatimaye wakaoana, na Judge akawa baba yangu.
Baba Ajifunza Kweli ya Biblia
Judge (Hakimu) alipewa jina lake la ajabu alipozaliwa. Baba yake alipomwona kwa mara ya kwanza, alisema: “Mtoto huyo ni mzito kama hakimu,” kisha hilo likawa jina lake. Katika 1917, Baba alipokuwa na miaka 16, alipewa zile trakti Where Are the Dead? na What Is the Soul? zilizochapwa na Watch Tower Bible and Tract Society. Babake Baba alikuwa amekufa miaka miwili kabla ya hapo, na trakti hizo zilimwandalia Baba majibu aliyokuwa akitafuta kuhusu hali ya wafu. Muda mfupi baadaye alianza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.
Baba alitaka mara moja kuanza kushiriki katika utendaji mbalimbali wa kutaniko. Alijipatia eneo ambalo angeweza kuhubiri, na baada ya shule alikuwa akienda huko kwa baiskeli yake ili kugawanya trakti. Alijihusisha kikamili katika kushiriki tumaini la Ufalme, na katika Machi 24, 1918, alifananisha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.
Mwaka uliofuata Mama alipohamia San Antonio, Baba alivutiwa mara moja na ile aliyosema ilikuwa “tabasamu yenye kupendeza sana na macho ya buluu sana” aliyopata kuona. Upesi walijulisha kwamba walitaka kuoana, lakini ilikuwa vigumu kwao kuwasadikisha wazazi wa Mama. Lakini, harusi ilitukia katika Aprili 15, 1921. Mradi wa wote wawili ulikuwa huduma ya wakati wote.
Mwanzo wa Mapema Katika Huduma
Mama na Baba walipokuwa na shughuli nyingi wakipanga kuhudhuria mkusanyiko wa Cedar Point, Ohio, katika 1922, waligundua kwamba Mama alikuwa mjamzito. Muda mfupi baada ya mimi kuzaliwa, Baba alipokuwa na miaka 22 pekee, aliwekwa kuwa mkurugenzi wa utumishi wa kutaniko. Hilo lilimaanisha kwamba alifanya mipango yote ya utumishi wa shambani. Baada ya majuma machache tu, Mama alikuwa amenipeleka katika huduma ya mlango kwa mlango. Kwa kweli, babu na nyanya yangu walipenda pia kunipeleka katika huduma pamoja nao.
Nilipokuwa na miaka miwili tu, wazazi wangu walihamia Dallas, Texas, na baada ya miaka mitatu wakaanza huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Wakati wa usiku walikuwa wakilalia kitanda kidogo kando ya barabara na kuniweka kwenye kiti cha nyuma cha gari. Bila shaka, niliona jambo hilo kuwa lenye kufurahisha, lakini upesi ilikuwa wazi kwamba hawakuwa tayari bado kwa ajili ya maisha ya painia. Kwa hiyo Baba alianza biashara. Hatimaye, alinunua trela ndogo (nyumba iliyoshikanishwa kwa gari) akitayarisha kuanza kupainia tena.
Kabla ya mimi kuanza shule, Mama alinifundisha kusoma na kuandika, na nilijua namna ya kuzidisha nambari kutoka moja hadi nne. Sikuzote alikazia kunisaidia kujifunza. Alikuwa akinisimamisha kwenye kiti karibu naye ili niweze kukausha sahani alipokuwa akiziosha, na alikuwa akinifundisha kuyatia maandiko katika kumbukumbu na kuimba nyimbo za Ufalme, au hymns (nyimbo za dini) kama tulivyoziita wakati huo.
Kumtumikia Mungu Pamoja na Wazazi Wangu
Katika 1931 sisi sote tulihudhuria ule mkusanyiko wenye kusisimua katika Kolumbasi, Ohio, tulikopokea jina Mashahidi wa Yehova. Ingawa nilikuwa na miaka minane tu, niliona hilo kuwa jina zuri zaidi nililopata kusikia. Muda mfupi tu baada ya kurudi nyumbani, biashara ya Baba iliharibiwa na moto, na Baba na Mama wakaona hilo kuwa “mapenzi ya Bwana” kwamba waanze kupainia tena. Hivyo, kuanzia kiangazi cha 1932, tulifurahia miaka mingi katika huduma ya wakati wote.
Wazazi wangu walipainia katikati ya Texas ili kukaa karibu na wazazi wa Mama, waliokuwa katika San Antonio bado. Kuhama mgawo mmoja hadi mwingine kulimaanisha kwamba nilibadili shule mara nyingi sana. Nyakati nyingine Mashahidi fulani wasiofikiri walikuwa wakisema, “Kwa nini msikae mahali pamoja na kumfanyia mtoto huyo makao,” kana kwamba sikuwa nikitunzwa vizuri. Lakini niliyaona maisha yetu kuwa yenye kusisimua na kwamba nilikuwa nikiwasaidia Baba na Mama katika huduma yao. Kwa kweli, nilikuwa nikizoezwa na kutayarishwa kwa ajili ya mtindo-maisha ambao baadaye ungekuwa wangu mwenyewe.
Kwa miezi kadhaa nilisisitiza kuwaambia Baba na Mama kwamba nilitaka kubatizwa, na mara nyingi waliongea na mimi juu ya jambo hilo. Walitaka kuhakikisha kwamba nilijua jinsi uamuzi wangu ulivyokuwa mzito. Mnamo Desemba 31, 1934, siku ilikuja kwa tukio hilo la maana sana maishani mwangu. Hata hivyo, usiku uliotangulia, Baba alihakikisha kwamba nilikuwa nimemwendea Yehova kwa sala. Kisha akafanya jambo zuri sana. Alituambia sisi sote tupige magoti, akatoa sala. Alimwambia Yehova kwamba alikuwa amefurahia sana uamuzi wa msichana wake mdogo wa kuweka wakfu maisha yake Kwake. Kwa hakika, sitasahau kamwe usiku huo, katika enzi zote zijazo!
Mazoezi Kutoka kwa Babu na Nyanya Yangu
Kati ya 1928 na 1938, nilitumia wakati mwingi nikitembelea babu na nyanya yangu katika San Antonio. Utaratibu waliofuata ulifanana sana na ule wa wazazi wangu. Nyanya alikuwa amekuwa kolpota, kama walivyokuwa wakiwaita mapainia wakati huo, kisha akawa painia wa muda-muda. Babu aliwekwa kuwa painia katika Desemba 1929, kwa hiyo utumishi wa shambani ulikuwa utendaji wa kawaida wa kila siku.
Babu alikuwa akinishika mikononi mwake wakati wa usiku na kunifundisha majina ya nyota. Alikuwa akinikariria mashairi. Mara nyingi nilisafiri naye kwa yale magari-moshi ya abiria ya Pullmans alipokuwa akifanyia kazi kampuni hiyo ya reli. Sikuzote alikuwa mtu niliyeweza kumgeukia nilipokuwa na taabu; alinifariji na kuyafuta machozi yangu. Lakini, nilipotiwa nidhamu kwa sababu ya kukosa adabu kisha nimwendee kupata kitulizo, alikuwa akisema tu (maneno ambayo sikuyaelewa wakati huo, lakini yaliyokuwa wazi sana kwa sauti aliyotumia): “Kipenzi, njia ya mkosaji ni ngumu sana.”
Miaka ya Mnyanyaso
Katika 1939, Vita ya Ulimwengu 2 ilianza, na watu wa Yehova walipatwa na mnyanyaso na jeuri ya ghasia za watu. Kufikia mwisho wa 1939, Mama alikuwa mgonjwa sana akahitaji upasuaji hatimaye, kwa hiyo tulihamia San Antonio tena.
Ghasia za watu zilikuwa zikikusanyika tulipokuwa tukifanya kazi ya magazeti kwenye barabara za San Antonio. Lakini kila juma, tulikuwa huko, tukiwa familia, kila mmoja katika kona tulikogawiwa. Mara nyingi nilitazama wakati Baba yangu alipokuwa akipelekwa kwa nguvu hadi kwenye kituo cha polisi.
Baba alijaribu kuendelea kupainia hata ingawa Mama alilazimika kuacha. Hata hivyo, hakuweza kuchuma fedha za kutosha akifanya kazi ya muda-muda, kwa hiyo yeye pia alilazimika kuacha. Nilimaliza shule katika 1939, nami pia nikapata kazi ya kuajiriwa.
Jina la Baba, Judge (Hakimu), lilisaidia sana katika miaka hiyo. Kwa kielelezo, kikundi kimoja cha Mashahidi kilienda kutoa ushahidi katika mji fulani kaskazini tu mwa San Antonio, na mkuu wa mji huo akawatia wote gerezani. Alikuwa amekamata watu wapatao 35, kutia na babu na nyanya yangu. Walimpelekea Baba ujumbe, yeye akaenda huko kwa gari. Aliingia ofisi ya mkuu huyo wa mji akasema: “Mimi ni Judge Norris kutoka San Antonio.”
“Naam Mheshimiwa, Hakimu (kwa kudhani “Judge” ni cheo wala si jina), naweza kukusaidiaje?” mkuu huyo wa mji akauliza.
“Nimekuja kushughulikia jambo la kuwaondoa watu hawa gerezani,” Baba akajibu. Papo hapo mkuu huyo akawaachilia bila dhamana—na bila maswali mengine!
Baba alipenda sana kutoa ushahidi katika majengo ya ofisi mjini, na alipenda hasa kuwazuru mahakimu na mawakili. Alikuwa akimwambia mpokezi: “Mimi ni Judge (Hakimu) Norris, na nimekuja kumwona Hakimu fulani.”
Halafu, alipokutana na hakimu huyo, sikuzote alisema hivi kwanza: “Sasa, kabla sijaongea juu ya kusudi la ziara yangu, nataka kueleza kwamba nimekuwa Judge (Hakimu) muda mrefu kuliko wewe. Nimekuwa mmoja muda wote wa maisha yangu.” Kisha alikuwa akieleza jinsi alivyopata jina lake. Huo ulikuwa utangulizi wa kirafiki, na alianzisha mahusiano mengi mazuri pamoja na mahakimu katika siku hizo.
Kushukuru kwa Ajili ya Mwelekezo wa Wazazi
Nilikuwa katika ile miaka ya utineja yenye misukosuko, na najua Baba na Mama walikuwa na nyakati nyingi zenye wasiwasi walipotazama na kujiuliza yale ambayo huenda ningefanya. Kama vile watoto wote hufanya, niliwajaribu Baba na Mama mara nyingi, nikiomba kufanya jambo fulani au kwenda mahali fulani nikijua kimbele kwamba jibu lao lingekuwa la. Nyakati nyingine machozi yalikuwako. Kwa kweli, ningaliudhika sana kama wangesema wakati wowote: “Endelea tu, fanya lolote utakalo. Hatujali.”
Nikijua kwamba nisingeweza kuwavuta wabadili viwango vyao kulinipa hisia ya usalama. Kwa kweli, hilo lilifanya iwe rahisi zaidi kwangu wakati vijana wengine walipodokeza kitumbuizo kisichofaa, kwani ningeweza kusema: “Baba yangu hataniruhusu kwenda.” Nilipokuwa na miaka 16, Baba alihakikisha kwamba nilikuwa nimejifunza kuendesha gari na kupata leseni yangu ya kuendesha gari. Pia, karibu na wakati huo alinipa ufunguo wa nyumba. Nilivutiwa sana kwamba alinitumaini. Nilihisi nimekomaa sana, na hilo lilinipa hisi ya kuwa na daraka na tamaa ya kutovunja kutumaini kwao.
Katika siku hizo, hakukuwa mashauri mengi ya kimaandiko juu ya ndoa, lakini Baba aliijua Biblia na yale iliyosema juu ya kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Alifanya iwe wazi kwangu kwamba ikiwa wakati wowote ningeleta mvulana wa kilimwengu nyumbani kukutana nao, au hata kufikiria kufanya matembezi na mmoja, angechukizwa sana. Nilijua kwamba alisema kweli, kwani nilikuwa nimeona ile furaha na kule kuunganika katika ndoa yao kwa sababu walikuwa wameoana “katika Bwana tu.”
Katika 1941, nilipokuwa na miaka 18, nilifikiria kwamba nilimpenda mwanamume kijana mmoja katika kutaniko. Yeye alikuwa painia na alikuwa akijifunza kuwa wakili. Nilisisimuka. Tulipowaambia wazazi wangu kwamba tulitaka kuoana, badala ya kukataa au kutuvunja moyo, walisema tu: “Tungependa kukuomba jambo moja, Blossom. Tunahisi kwamba wewe ni mchanga mno, na tungependa kukuomba ungojee mwaka mmoja. Ikiwa kwa kweli wampenda, mwaka mmoja hautafanya tofauti.”
Nashukuru sana kwamba nilisikiliza shauri hilo lenye hekima. Katika mwaka mmoja, nilikomaa nikaanza kuona kwamba mwanamume huyo kijana hakuwa na sifa ambazo zingefanyiza mwenzi mzuri wa ndoa. Yeye aliacha tengenezo hatimaye, nami nikaepuka hali ambayo ingekuwa yenye msiba maishani mwangu. Ni jambo zuri ajabu kama nini kuwa na wazazi wenye hekima ambao uamuzi wao waweza kutegemeka!
Ndoa na Kazi ya Kusafiri
Katika kipupwe cha 1946, baada ya kutumia miaka sita nikipainia na kufanya kazi ya muda-muda, mwanamume kijana aliye mzuri zaidi niliyepata kukutana naye aliingia Jumba la Ufalme letu. Gene Brandt alikuwa amewekwa aandamane na mtumishi wetu kwa akina ndugu asafiriye, kama vile mwangalizi wa mzunguko alivyoitwa wakati huo. Tulivutiana, na tukaoana mnamo Agosti 5, 1947.
Muda mfupi baadaye, Baba na Gene walianza biashara ya hesabu. Lakini Baba alimwambia Gene: “Siku ambayo biashara hii yatuzuia tusifanye mgawo fulani wa mkutano au wa kitheokrasi, nitaifunga.” Yehova alibariki mtazamo huo wa kiroho, na biashara hiyo iliandaa vya kutosha mahitaji yetu ya kimwili na kuruhusu wakati wa kupainia. Baba na Gene walikuwa wafanyabiashara wazuri, na tungeweza kuwa matajiri kwa urahisi, lakini huo haukuwa mradi wao kamwe.
Katika 1954, Gene alialikwa kufanya kazi ya mzunguko, lililomaanisha badiliko kubwa katika maisha zetu. Wazazi wangu wangeitikiaje? Mara nyingine tena, hawakujihangaikia bali walihangaikia masilahi ya Ufalme wa Mungu na hali njema ya kiroho ya watoto wao. Hawakutuambia kamwe: “Kwa nini msituzalie wajukuu?” Badala ya hivyo, sikuzote ilikuwa: “Twaweza kuwafanyia nini kuwasaidia katika utumishi wa wakati wote?”
Kwa hiyo siku ilipofika ya sisi kuondoka, kulikuwa maneno ya kitia-moyo tu na kushangilia pendeleo letu tukufu. Hawakutufanya kamwe tuhisi kwamba tulikuwa tukiwaacha lakini walituunga mkono kabisa sikuzote. Tulipoondoka, walijishughulisha katika kazi ya painia kwa miaka mingine kumi. Baba aliwekwa kuwa mwangalizi wa jiji la San Antonio, cheo alichokuwa nacho kwa miaka 30. Alifurahia kuona ukuzi kutoka kutaniko moja katika jiji hilo katika miaka ya 1920 hadi makutaniko 71 kabla ya yeye kufa katika 1991.
Kwa Gene na mimi, maisha yalijaa msisimuko. Tulikuwa na shangwe nyingi ya kuwatumikia ndugu na dada wapendwa katika zaidi ya majimbo 31 na, labda jambo lililokuwa kuu zaidi, ni lile pendeleo la kuhudhuria darasa la 29 la Watchtower Bible School of Gilead katika 1957. Baadaye tulirudia kazi ya kusafiri. Katika 1984, baada ya miaka 30 katika kazi ya mzunguko na ya wilaya, Sosaiti ilimpa Gene kwa fadhili mgawo wa mzunguko katika San Antonio, kwa kuwa wazazi walikuwa katika miaka yao ya 80 na wenye afya mbaya.
Kuwatunza Wazazi
Baada ya mwaka mmoja na nusu tu ya sisi kurudi San Antonio mama alipoteza fahamu akafa. Hilo lilitukia upesi sana hivi kwamba sikupata kusema mambo fulani niliyotaka kumwambia. Hilo lilinifunza kuongea sana na Baba. Baada ya miaka 65 ya ndoa, alimkosa Mama sana, lakini tulikuwa huko ili tutoe upendo na utegemezo.
Kielelezo cha Baba cha maisha yote cha kuhudhuria mikutano ya Kikristo, cha kujifunza, na cha utumishi kiliendelea hadi kifo chake. Alipenda kusoma. Kwa kuwa alilazimika kuwa peke yake tulipokuwa katika utumishi, nilikuwa nikirudi nyumbani na kuuliza, “Je! ulihisi upweke?” Alikuwa amekuwa na shughuli nyingi sana akisoma na kujifunza, hata asiwe na wazo hilo.
Kulikuwa na zoea jingine la maisha yote tulilodumisha. Sikuzote Baba alikuwa amesisitiza kwamba familia ile pamoja, hasa wakati wa kiamshakinywa, Andiko la kila siku lilipozungumziwa. Sikuruhusiwa kamwe kuondoka nyumbani bila kufanya hivyo. Nyakati nyingine nilikuwa nikisema: “Lakini Baba, nitachelewa kwenda shuleni (au kazini).”
“Si andiko linalokuchelewesha; ulichelewa kuamka,” yeye alikuwa akisema. Kisha nililazimika kukaa na kulisikiliza. Alihakikisha kwamba kielelezo hicho chema kilikuwako hadi siku zake za mwisho za maisha. Huo ni urithi mwingine alioniachia.
Baba aliendelea kuwa chonjo akilini hadi mwisho kabisa. Jambo lililofanya iwe rahisi kumtunza ni kwamba hakusumbua-sumbua kamwe wala kulalamika. Ooh, nyakati nyingine alikuwa akitaja ugonjwa wake wa uyabisi na kuchochota kwa viungo, lakini nilikuwa nikimkumbusha kwamba ugonjwa aliokuwa nao kikweli ulikuwa “Uadamu [uzee kutokana na dhambi ya Adamu],” naye alikuwa akicheka. Baba alilala usingizi wa kifo kwa amani asubuhi ya Novemba 30, 1991, wakati Gene na mimi tulipokuwa tumeketi kando yake.
Sasa nina umri wa zaidi ya miaka 70 na ningali nikinufaika kutokana na kile kielelezo chema cha wazazi wangu Wakristo wenye upendo. Na sala yangu ya bidii ni kwamba nitathibitisha uthamini wangu kamili kwa ajili ya urithi huu kwa kuutumia ifaavyo katika enzi zote zijazo.—Zaburi 71:17, 18.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mama na mimi
[Picha katika ukurasa wa 7]
1. Mkusanyiko wangu wa kwanza: San Marcos, Texas, Septemba 1923
2. Mkusanyiko wa mwisho wa Baba: Fort Worth, Texas, Juni 1991 (Baba akiwa ameketi)
[Picha katika ukurasa wa 9]
Gene na Blossom Brandt