Tulipewa Mradi Maishani
Imesimuliwa na Russell Cantwell
NIMEONA kwamba ni vijana wachache leo wanaojua jinsi ya kutumia maisha yao. Wengi hawakujiwekea lengo maishani. Mimi nawashukuru wazazi wangu kwa sababu niliwekewa lengo maishani.
Wazazi wangu wangali hai, ingawa Baba ana miaka 90 naye Mama ana miaka 80 na kitu. Wote kwa ujumla wametumia zaidi ya miaka 90 ‘wakipainia,’ kama vile Mashahidi wa Yehova wanavyoiita kazi ya kuhubiri habari za Biblia nyakati zote.
Baba na Mama walianza kujifunza Biblia kwa bidii karibu na mwaka wa 1908. Mojawapo mambo ya zamani ninayokumbuka ni kwamba, niliiona Photo Drama of Creation, yaani masimulizi ya hadithi ya Biblia yenye vipande vya picha (slides) na sinema. Niliiona katika shule ndogo ya mashambani ambako Baba alikuwa mwalimu, katika Arkansas. Bila shaka nilikuwa na umri wapata miaka mitatu.
Mwaka 1924, nilipokuwa wa miaka minne, Baba alihamisha jamaa tukaenda mashariki ya Tennessee. Alianza upesi kuongea na jirani wa huko juu ya alivyomwamini Mungu. Jamaa ya akina Kamer ilipendezwa, tena mikutano ya Biblia ilifanywa kila juma.
Jambo jingine la zamani ninalokumbuka ni ziara za “wahaji,” kama vile wajumbe wenye kusafiri wa Mashahidi wa Yehova walivyokuwa wakiitwa. Sisi wavulana watatu tuliwaachia dada zetu vitanda vyetu tukalala sakafuni ili mgeni huyo alale chumbani mwa dada zetu. Sisi watoto tumefaidika kutokana na fadhili na maneno yenye kututia moyo ya wanaume hao.
UBORA WA MAMBO YA KIROHO
Baba na Mama walitukazia ubora wa kujifunza Biblia na kushirikiana na Wakristo wenzetu kwa kutufundisha na kutuwekea mfano, nasi tumeyakumbuka mambo hayo daima. Nakumbuka kisa kimoja kilicho mfano mzuri sana; nilikuwa na umri wapata miaka sita au saba tu wakati huo.
Ilikuwa asubuhi ya Jumapili, tukakutana na magari matatu yaliyojaa watu wa ukoo wetu tulipokuwa tukitembea kuelekea nyumbani kwa akina Kamer kujifunza Biblia kama kawaida. Ingawa Baba hakuwa ameonana nao muda mwingi, aliwaomba waende nasi kwenye funzo badala ya kurudi nao nyumbani, au sivyo waende nyumbani wakatungoje turudi. Mimi nina hakika kwamba hata kama watu hao wote wangalienda zao kwa hasira, Baba asingaliona wasiwasi kwa sababu alijisikia akiwa na wajibu mkubwa wa kutia jamaa yake nguvu za kiroho, na wa kuongoza jamaa ya Kamer wajifunze Biblia.
Baba alituzoeza kuongea na watu pia juu ya mambo tuliyokuwa tukijifunza kuhusu ufalme wa Mungu. Kadiri niwezavyo kukumbuka, alikuwa akienda na sisi watoto kutembelea watu nyumbani kwao. Mwaka 1927 Baba aliamua kwamba nilikuwa na umri wa kutosha kuweza kwenda milangoni peke yangu.
MAISHA YETU YA JAMAA
Ni kweli kwamba tulikuwa na kazi nyingi ngumu katika shamba letu, tena tulikuwa na shughuli nyingi za Kikristo. Lakini, wazazi wetu walitupangia tafrija pia. Baba alitufundisha kuogelea. Tena jamaa yetu ilikuwa na mandari (pikniki) na ilikusanyika pamoja na jamaa nyingine, basi tukawa na tafrija na ushirika mzuri.
Jambo jingine lililounganisha jamaa yetu ni kwamba Baba na Mama walipatana sana, na nyakati zote waliongea nasi. Nina hakika walikosana nyakati nyingine, lakini hawakubishana kamwe mbele yetu wala kupingana. Ndivyo tulivyojifunza kuheshimu mamlaka ya wazazi.
Shuleni tulidhihakiwa mara nyingi na watoto wa dini nyingine. Kwa mfano, walikuwa wakituita “akina hakuna moto,” kwa sababu hatukuamini kwamba Mungu anatesa watu motoni. Lakini Baba na Mama walikuwa wakitusaidia kutayarisha majibu kutokana na Biblia, tuwe nayo turudipo shuleni. Basi tulipata nguvu, tukasadiki kwamba tuliijua kweli ya Neno la Mungu, tena tulifurahia kuwa watu tofauti, kama watumishi wa zamani wa Mungu.
Miaka mingi kabla ya hapo, mjomba mmoja asiyeifurahia dini ya Baba alimwambia hivi: “Newt ingalikuwa vema kama watoto wangu wangalikuwa kama wako.” Lakini, wakati Baba alipomkumbusha tena kwamba tulikuwa watu tofauti kwa sababu ya kufundishwa Biblia, mjomba alichukizwa. Hata alimkataza Baba asimtaje tena Mungu wala Biblia nyumbani mwake!
TWAWEKEWA MRADI
Baba alitaka kutumia wakati mwingi zaidi kuwapa watu ushuhuda, kwa hiyo mwaka 1929 tukahamia West Plains, Missouri. Huko tuliweza kuwapa vyumba watangazaji Ufalme wawili wa wakati wote. Mfano uliowekwa na Mashahidi hao ulifanya jamaa yetu ianze kufikiria kupainia.
Kwa sababu ya Taabu Kuu iliyotokea miaka hiyo, tulirudia shamba letu katika Tennessee, lakini hatukuacha kufikiria kupainia. Mwaka 1931 mhaji mmoja jina lake Louis Larson alimfahamisha Baba jinsi angeweza kupata pesa za kutunza jamaa akiwa painia.
Watoto wetu sita tulikuwa tungali nyumbani, na watatu kati yetu tulikuwa tukienda shuleni. Jamaa yetu ilifanya mkutano, na baada ya kusali tukakubaliana tuuze shamba na kumtumaini kabisa Yehova atupatie riziki. Ikaamuliwa kwamba sisi watatu tuliokuwa wachanga zaidi tuendelee na masomo, na wale wengine wakubwa wapainie.
Wazazi wangu walinisaidia sana maishani kwa sababu ya kumwamini na kumtumaini Yehova. Usiku huo nilisali nikamwambia Yehova kwamba ningefanya mapenzi yake kama watu wetu na kutembea katika nyayo za Kristo. Nilichangamka sana Baba aliponibatiza baadaye nionyeshe kwamba nimejiweka wakf kwa Yehova!
Shamba letu lilitangazwa kwamba linauzwa, lakini kwa sababu ya Taabu Kuu (iliyopunguza thamani ya pesa), liliuzwa nusu ya kiasi tulichotaka hapo kwanza. Halafu mkasa na ugonjwa mbaya ukaipata jamaa, Baba akaishiwa na hela zote nasi tukawa hatuna kitu. Lakini yeye alisema tulikuwa na jambo moja tu la kufanya, yaani, kuendelea tu na kazi ya wakati wote ya kuwapa watu ushuhuda. Nilizidi kutaka kumtumikia Yehova kwa sababu ya azimio hilo, na kwa sababu Baba na Mama walijikaza nyakati zote.
MWANZO WA KAZI YA MAISHA
Mwaka 1934 tulihamia mgawo fulani magharibi ya Tennessee. Tulipokuwa huko niliamua kuacha masomo nianze kazi ya kuwapa watu ushuhuda wakati wote. Baba alikubali nifanye hivyo, ikiwa kusudi langu lilikuwa kupainia maisha yote, si kuepa masomo. Basi nilipotimu miaka kumi na minne nilianza kazi yangu ya maisha ya kutoa ushuhuda mashambani, katika ujirani wa Waverly, Tennessee.
Ni kweli kwamba tulipatwa na majaribu wakati wa Taabu Kuu iliyotokea miaka ya 1930. Nyakati nyingine tulikula chakula kile kile siku nyingi, tukajisikia tukitaka cha namna nyingine. Lakini Baba alituonyesha kwamba tulikuwa tumeacha kutafuta pesa na bado hatukukosa chakula, na huku karibu kila siku jamaa zilikuja kwetu kuomba chakula cha kulisha watoto wao wenye kulia kilio cha njaa, na bado jamaa hizo zilikuwa zikijaribu kufanya kazi zipate pesa.
Maeneo tuliyopainia katika kusini yote ya United States hayakuwa na Mashahidi karibu. Kwa hiyo ushirika wetu mwingi wa jamaa ulitulinda tusishirikiane na wasioamini. (1 Kor. 15:33; 2 Kor. 6:14) Tena tuliweka akiba ya mapeni yetu muda wa miezi mingi ili kuendesha gari maili mia moja au zaidi (karibu kilomita 160) tukakutane na vijana wengine Mashahidi na kucheza dansi nzuri, au tuwe na ushirika wa namna nyingine, kama kupunga upepo milimani.
MIGAWO MIPYA
Mwaka 1937, katika kusanyiko la Columbus, Ohio, tulisikia Baba akiitwa jina katika kikuza-sauti, pamoja na watu wengine 200 waliochaguliwa waanze kazi mpya ya painia wa pekee. Baba alilikubali upesi pendeleo hilo jipya la utumishi, halafu jamaa yote tukakaribishwa tushiriki. Tulipewa mgawo New Haven, Connecticut.
Sheria moja ya serikali katika Connecticut ilimpa mkuu wa polisi mamlaka ya kuzuia kazi ya kidini ya kuhubiri mlango kwa mlango katika mtaa wa kwao, basi Mashahidi wa Yehova wakawa wakikamatwa mkoani mwote. Mei 1938 mimi nilikamatwa pamoja na Baba na ndugu yangu mdogo, Jesse, tulipokuwa tukitembelea watu nyumbani kwao kuwaeleza habari za Biblia. Ingawa mamia ya ndugu na dada zetu Wakristo walikuwa wamekwisha kamatwa nyakati mbalimbali, Watch Tower Society iliamua kutumia kisa chetu waijaribu sheria ya serikali waone kama inafaa. Mwishowe Mahakma Kuu ya United States ilipelekewa habari za kisa hicho, naye Yehova akatupatia ushindi.
Ndipo tulipohamishwa tukiwa mapainia wa pekee twende Staten Island, mjini New York, tukapata huko pendeleo la kufanya kazi na watumishi wa kituo cha radio WBBR, cha Watch Tower Society. Halafu Januari 1939 tuliombwa tusaidie kundi lililokuwa limeanzwa majuzi katika Mlima Vernon, New York, nao Milton Henschel, Lyman Swingle na washiriki wengine wa jamaa ya Betheli wakaagizwa waende huko pia. Ebu waza jinsi tulivyoshangaa mwezi uliofuata wakati ndugu zangu wawili walipokaribishwa wasaidie kiwanda cha Sosaiti cha uchapaji muda wa juma chache. Lakini waliendelea kutumikia huko muda wa miaka sita. Tukio moja lililotukia Septemba 8, 1943, lilituletea mgawo mwingine.
Hapo ndipo Evie Sullivan aliponijulisha kwa Gladys akiwa katika sebule la Betheli, akaniomba nimpeleke Gladys na painia mwenzake vyumbani mwao, hatua kadha kutoka hapo. Gari lao lilihitaji sana kutengenezwa, basi nikalitengeneza muda wa saa kadha usiku huo, huku wasichana hao wakiwa wameketi kando na kunisimulia maono yao katika kazi ya kuwapa watu ushuhuda. Hapo nikapata nafasi nyingi ya kuona kwamba walikuwa na roho nzuri ya kumtumikia Yehova.
Masika ya mwaka 1944 Gladys alihudhuria darasa la tatu la Gilead School nilipokuwa ningali Betheli, halafu mwaka uliofuata tukaoana kisha nikajiunga na Gladys kufanya upainia. Mwaka 1950 nilikaribishwa nitumikie katika kazi ya mzunguko nikiwa mjumbe mwenye kusafiri wa Watch Tower Society. Binti yetu Darla Lynn alizaliwa Januari 30, 1956, lakini tukaonyeshwa upendo kwa kupangiwa tuendelee na kazi ya mzunguko.
KUWAPA WENGINE MRADI MAISHANI
Tulisali tukamwomba Yehova atusaidie kulea binti yetu kama wazazi wetu walivyotulea, tukitanguliza faida za Ufalme sikuzote, lakini tulikuwa na kiasi wala hatukuachilia madaraka yetu ya jamaa. Niliongoza funzo letu la jamaa kila juma, naye Gladys akawa akitumia muda mchache kumfundisha binti yetu Neno la Mungu, halafu binti akawa akifunzwa muda mrefu zaidi kadiri umri wake ulivyoongezeka.
Tulishangaa kuona siku zimekwenda upesi sana hata Darla akafikia umri wa kwenda shuleni. Sikuzote tulizungumza naye waziwazi hata juu ya mambo yale ya ndani-ndani, kwa hiyo alipokuwa mkubwa ilikuwa vyepesi kuzungumza naye, na kwa njia hiyo hakukuwa na mtengano. Tulimshauri kwa uangalifu kuhusu watu atakaoshirikiana nao, tukamsaidia aepuke mashirika mabaya ambayo yangeweza kumwingiza katika makosa. Vilevile, tulifurahi kwa sababu alitaka kueleza wanadarasa wenzake habari za ufalme wa Mungu. Alianza funzo lake la kwanza la Biblia na mwanadarasa mwenzake wa darasa la tatu katika Chino, California. Mwanafunzi huyo alijiweka wakf kwa Yehova alipokuwa na miaka kumi na sita.
Juni 1972, katika San Francisco, California, tulipokea barua posta. Ilikuwa ajabu, maana tuliandikiwa barua hiyo na binti yetu tuliyekuwa tukiishi naye nyumba moja. Alitaka kutushukuru, lakini aliogopa kwamba asingeweza kutueleza mambo yote uso kwa uso.
Barua yake ilisema, “Nataka kuwashukuru kwa kunilea jinsi mlivyonilea. Sikuzote mmemtanguliza Yehova katika maisha yetu. Sikuzote ‘Ndiyo yenu imekuwa Ndiyo na Siyo yenu ikawa Siyo.’ . . . Nataka kuwashukuru kwa sababu ya upendo wote na fadhili mnazonionyesha. Mmekuwa mkinisikiliza ninapowaeleza jambo. Mmekuwa mkifahamu jinsi ninavyojisikia. Mmekuwa mkinivumilia nilipoonyesha hali mbalimbali za moyoni. . . . Asanteni sana kwa sababu ya mfano mwema sana mlioniwekea kiasi cha kuniwezesha kikweli ‘niwafuate ninyi kama mnavyomfuata Kristo.’”
Barua hiyo ilituchangamsha mioyo, nasi tunamshukuru Yehova kwa sababu tuliweza kumpa binti yetu mradi ule ule niliopewa na wazazi wangu, yaani, kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwake. Binti yetu na mwenzake wanatumikia kama mapainia pamoja na Kundi la Henderson, North Carolina. Wao, na sisi pia, tulifurahi sana wakati kumi na saba waliojifunza nao Biblia walipohudhuria Chakula cha Bwana cha Jioni masika yaliyopita.
Kwa muda wa miaka 43 sasa nimekuwa katika utumishi wa wakati wote. Sasa mimi ni mwalimu wa Shule ya Huduma ya Ufalme, yaani mahali pa kuzoezea wazee Wakristo. Mmoja wa ndugu zangu yumo katika kazi ya mzunguko katika United States, na yule mwingine anatumikia kama msawazishi wa tawi katika nchi ya Caribbean ya Jamhuri ya Dominican. Nao wazazi wangu wote wawili wangali katika upainia!
Maono yetu wenyewe yanatuongoza tutie sana vijana moyo wa kuufanya mradi wao uwe kazi ya kuwapa watu ushuhuda wakati wote, naam, wamtumikie Yehova Mungu maisha yao yote. Nao wazazi tunawaambia hivi: Watoto wenu hawatashtuka tu halafu siku moja wajikute wakimtumikia Yehova. Inawapasa ninyi mwape mradi huo maishani. Mkifanya hivyo, mimi nawahakikishia kwamba watafurahi milele.
[Picha katika ukurasa wa 479]
Mke wangu nami tukijifunza pamoja