Kufuatia Hatua za Wazazi Wangu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA HILDA PADGETT
“Maisha yangu yamewekwa wakfu kwa utumishi wa Aliye Juu Zaidi,” gazeti likaripoti, “nami siwezi kutumikia mabwana wawili.” Maneno hayo kutoka katika taarifa yangu kwa wakuu wa Wizara ya Wafanyakazi na Utumishi wa Kitaifa ya Uingereza katika 1941 yalitoa sababu yangu ya kukataa mwelekezo wao wa kufanya kazi hospitalini wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Muda mfupi baada ya hapo nilionwa kuwa na hatia na kuhukumiwa kifungo cha miezi mitatu kwa ajili ya kukataa.
NI NINI kilichofanya nifungwe? Haikuwa sababu ya hali fulani ya ujana au tabia ya uasi, la. Badala ya hivyo, sababu ni za tangu nilipokuwa mtoto.
Bidii ya Baba kwa Ajili ya Ufalme
Nilizaliwa katika Juni 5, 1914, katika Horsforth karibu na Leeds, kaskazini mwa Uingereza. Wazazi wangu, Atkinson na Pattie Padgett, walikuwa walimu wa shule ya Jumapili na washiriki wa kwaya katika kanisa la Primitive Methodist ambapo baba alicheza kinanda. Nilipokuwa mtoto, nyumbani petu palikuwa penye furaha ila kwa jambo moja. Hali ya ulimwengu ilimhangaisha baba. Alichukia vita na jeuri na aliamini amri hii ya Biblia: “Usiue.”—Kutoka 20:13.
Katika 1915 serikali ilisisitiza wanaume vijana wote wajiunge na jeshi kwa hiari na hivyo kuzuia kuandikishwa kwa lazima. Akiwa na mashaka baba alisimama siku nzima huku akinyeshewa akingoja nafasi yake ya kujiandikisha kuwa mwanajeshi. Siku iliyofuata tu, maisha yake yote yakabadilika!
Huku akifanya kazi ya kuweka mifereji katika nyumba fulani kubwa, alizungumza na wafanyakazi wengine kuhusu matukio ya ulimwengu. Mtunza-bustani huyo akampa baba trakti ndogo, Gathering the Lord’s Jewels. Baba akaja nayo nyumbani, akaisoma, na kuisoma tena. “Ikiwa hiyo ni kweli,” yeye akasema, “basi mengine yote ni uwongo.” Siku iliyofuata, aliomba habari zaidi, na kwa majuma matatu usiku wote hadi saa za alfajiri, alijifunza Biblia. Alijua alikuwa ameipata kweli! Jumapili, Januari 2, 1916, kitabu chake cha kuandikia mambo ya kila siku chasema: “Nilienda kanisani asubuhi, nikaenda I.B.S.A. [International Bible Students Association, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo katika Uingereza] usiku—nikasoma Waebrania 6:9-20—ziara yangu ya kwanza kwa akina ndugu.”
Upesi upinzani ukaanza. Watu wetu wa ukoo na washiriki wenzetu wa kanisa walifikiri baba amerukwa akili. Lakini alikuwa amefanya uamuzi. Mikutano na funzo yalikuwa ndiyo mambo ya maana katika maisha yake, na kufikia Machi alikuwa ameweka maisha yake wakfu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Baada ya baba kwenda peke yake mikutanoni kwa majuma machache, mama alikuwa amechoka kukataa kwenda mikutanoni. Akaniweka katika kigari cha kubebea mtoto na kutembea kilometa 8 hadi Leeds, akafika mkutano ulipokuwa ukimalizika tu. Wazia shangwe ya baba alipomwona mama. Tangu wakati huo na kuendelea, familia yetu ikaungana katika utumishi wa Yehova.
Hali ya baba ilikuwa ngumu sana—mjitoleaji katika jeshi kisha baada ya majuma machache, mkataaji kidhamira. Alipoitwa alikataa kubeba bunduki, na kufikia Julai 1916 alikabili hukumu ya kwanza kati ya tano zilizotolewa na mahakama ya kijeshi, akihukumiwa kifungo cha siku 90 gerezani. Baada ya kutumikia kifungo cha kwanza, baba alikuwa na likizo ya majuma mawilli, yakifuatiwa na hukumu nyingine ya mahakama ya kijeshi ya siku 90 gerezani. Kufuatia kifungo chake cha pili, alihamishwa kwenye kikosi cha Royal Army Medical Corps, na katika Februari 12, 1917, alisafiri kwa meli ya kijeshi hadi Rouen, Ufaransa. Kitabu chake cha kurekodi mambo chasema kwamba huko akachukizwa hata zaidi kila siku na hali yake. Alitambua kwamba alikuwa tu akiwatunza wanajeshi waliojeruhiwa ili warudi kwenye vita.
Tena akakataa kukubali. Wakati huu mahakama ya kijeshi ikamhukumu miaka mitano katika gereza la kijeshi la Uingereza katika Rouen. Baba alipoendelea kuomba ahamishwe kwenye gereza la raia akiwa mkataaji kidhamira, alipewa nidhamu ya miezi mitatu ya kula mkate na maji, ikifuatiwa na chakula cha kawaida cha gerezani hadi uzito wake ulipoongezeka; kisha akarudia tena mkate na maji. Mikono yake iliwekwa pingu kwa nyuma mchana na kuwekwa upande wa mbele usiku na nyakati za chakula. Maisha yake yote, alikuwa na alama nyingi kwenye viwiko ambapo pingu zilizokuwa ndogo sana zilibanwa ndani ya nyama yake, zikitokeza vidonda vyenye usaha. Pia alikuwa na pingu miguuni zikiunganishiwa kwenye kiuno chake.
Wenye mamlaka wa kijeshi walifanya kila walichoweza kuvunja msimamo wake lakini hawakufaulu. Alinyang’anywa Biblia yake na vitabu vyake. Hakuwa akipata barua kutoka nyumbani, wala hangetuma zozote. Baada ya miaka miwili aliamua kuonyesha unyoofu wake kwa kukataa chakula. Kwa siku saba alishikamana na azimio lake, asile wala kunywa, ikitokeza kuhamishwa kwake hadi hospitali ya gereza, akiwa mgonjwa sana. Alithibitisha kwamba alikuwa mnyoofu, ingawa karibu apoteze uhai wake. Katika miaka yake ya baadaye alikubali kwamba alifanya makosa kuhatarisha uhai wake kwa njia hiyo, naye hangechukua mwendo kama huo tena.
Vita vikakoma Novemba 1918 baba akiwa angali gerezani katika Rouen, lakini mapema mwaka uliofuata, alihamishwa kwenye gereza la raia katika Uingereza. Wazia furaha yake alipopokea barua zote kutoka kwa mama na vifurushi vilivyokuwa vimerundamana, pamoja na Biblia na vitabu vyake vya thamani! Alipelekwa Gereza la Winchester, alikokutana na ndugu kijana ambaye mambo aliyoona wakati wa vita yalifanana na yake. Aliitwa Frank Platt, ambaye baadaye alitumika katika Betheli ya London kwa miaka mingi. Wakafanya mipango kukutana siku iliyofuata, lakini kufikia wakati huo Frank alikuwa amehamishiwa mahali pengine.
Katika Aprili 12, 1919, mama alipokea barua kwa simu: “Haleluya! Naja nyumbani—napiga simu nikiwa Betheli ya London.” Ulikuwa wakati wenye shangwe kama nini baada ya miaka mitatu ya mtihani, jaribu, na kutenganishwa! Wazo la kwanza la baba lilikuwa kupiga simu na kukutana na ndugu wa Betheli ya London. Alikaribishwa kwa upendo katika makao ya Betheli yaliyokuwa kwenye 34 Craven Terrace. Baada ya kuoga na kunyoa ndevu na kuvalia suti na kofia alizoazima, baba akarudi nyumbani. Je, waweza kuwazia muungano wetu? Wakati huo nilikuwa karibu mwenye umri wa miaka mitano, nami sikumkumbuka baba.
Mkutano wake wa kwanza aliohudhuria baada ya kuachiliwa huru ulikuwa Ukumbusho. Akipanda ngazi kuelekea jumba, kumbe ndugu wa kwanza aliyekutana naye alikuwa Frank Platt, aliyekuwa amepelekwa hospitali ya kijeshi katika Leeds. Walikuwa na shangwe kama nini kushiriki mambo waliyoona! Tangu wakati huo hadi kuachiliwa kwake kutoka hospitali, Frank alitutembelea mara kwa mara kwa sababu alijihisi huru akiwa pamoja nasi.
Utumishi Mwaminifu wa Mama
Wakati wote ambao baba hakuwepo, mama alifulia watu nguo kuongezea mapato kidogo aliyopewa na serikali. Ndugu walikuwa wenye fadhili sana kwetu. Kila baada ya majuma machache mmoja wa wazee wa kutaniko alimpa mama bahasha ndogo yenye zawadi isiyo na jina. Sikuzote mama alisema ni upendo wa ndugu uliomleta karibu na Yehova na kumsaidia kuvumilia nyakati hizo zenye kujaribu. Kwa uaminifu alihudhuria mikutano ya kutaniko kipindi chote baba alipokuwa hayupo. Mtihani wake mgumu sana ulikuwa wakati, zaidi ya mwaka mmoja, hakujua kama baba alikuwa hai au amekufa. Kuongezea mzigo huo, katika 1918 mama pamoja nami tukashikwa na Homa ya Kihispania. Watu walikuwa wakifa kila mahali kutuzunguka. Majirani waliokwenda kusaidia majirani wenzao walishikwa na ugonjwa huo na kufa. Bila shaka upungufu wa chakula wakati huo uliongezea upungufu wa uwezo wa watu wa kukinga magonjwa.
Maneno ya mtume Petro yalithibitika kuwa kweli sana kwa familia yetu: ‘Mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, Mungu, atawathibitisha, na kuwatia nguvu’! (1 Petro 5:10, NW) Kuteseka kwa wazazi wangu kulijenga ndani yao imani thabiti kabisa katika Yehova, uhakikisho wa kweli kabisa kwamba yeye hutujali na kwamba hakuna kitu kiwezacho kututenganisha na upendo wa Mungu. Mimi hasa nilibarikiwa kuwa na malezi kama hayo katika imani.—Warumi 8:38, 39; 1 Petro 5:7.
Utumishi wa Ujanani
Kufuatia kuachiliwa kwa baba, utumishi wa Ufalme ukawa kitu cha maana maishani mwetu. Siwezi kukumbuka kamwe nikikosa mkutano, ila nilipokuwa mgonjwa. Muda mfupi baada ya baba kurudi nyumbani, aliuza kamera yake na ushanga wa mama wa dhahabu ili apate pesa za kuhudhuria mkusanyiko. Ingawa hatungeweza kugharimia likizo, hatukukosa kamwe mikusanyiko, kutia ndani ile iliyokuwa London.
Miaka ya kwanza miwili au mitatu baada ya vita ilikuwa nyakati za burudiko. Baba na mama walichukua nafasi na fursa zote kushiriki na wengine. Naweza kukumbuka jinsi tungetembelea ndugu na dada wengine, nami nikiwa msichana mdogo, ningeketi nikichora kwa rangi na kwa kalamu huku watu wazima wakizungumza kwa muda wa saa nyingi juu ya uelewevu mpya mbalimbali wa kweli. Kuzungumza pamoja, kuimba, kufurahia ushirika mzuri, kuliwafanya wawe na furaha sana na kuburudika.
Wazazi wangu hawakunilea kwa mchezo. Nikiwa shuleni nilikuwa tofauti, hata nikiwa na umri wa miaka mitano, nilibeba “Agano Jipya” langu nikasome darasa linapojifunza katekisimu. Baadaye nilisimamishwa mbele ya shule nzima kuwa “mkataaji kidhamira” kwa sababu singeshiriki katika sherehe ya Siku ya Mashujaa.a Mimi sijutii malezi yangu. Kwa kweli, yalikuwa ulinzi na kufanya iwe rahisi kudumu katika ‘barabara nyembamba.’ Popote wazazi wangu walipoenda iwe ni mikutanoni au shambani, nilikuwepo.—Mathayo 7:13, 14.
Hasa nakumbuka ile Jumapili asubuhi nilipoanza kuhubiri kwa mara ya kwanza nikiwa peke yangu. Nilikuwa na umri wa miaka 12 tu. Nikiwa katika ujana wangu, naweza kukumbuka Jumapili moja asubuhi nikisema kwamba nitabaki nyumbani. Hakuna aliyenikemea au kunilazimisha kwenda, hivyo nikakaa bustanini nikisoma Biblia yangu nikihisi vibaya sana. Baada ya juma moja au mawili ya kufanya hivyo, nilimwambia baba: “Nafikiri nitaenda na wewe asubuhi hii!” Tangu wakati huo na kuendelea sijarudi nyuma.
Mwaka wa 1931 ulikuwa wa ajabu kama nini! Tulipokea jina letu jipya, Mashahidi wa Yehova, na nikazamishwa tukiwa katika mkusanyiko wa kitaifa katika jumba la Alexandra Palace, London. Sitasahau kamwe siku hiyo. Tulivaa majoho meusi marefu, na langu likawa limelowa tayari kwa kuwa lilikuwa limetumiwa na mwingine aliyebatizwa!
Tamaa yangu sikuzote nikiwa mtoto ilikuwa niwe kolpota, kama wahubiri wa wakati wote walivyoitwa wakati huo. Nilipoendelea kukua, nilihisi napaswa kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Hivyo katika Machi 1933, nikiwa na umri wa miaka 18, nilijiunga na watumishi wa wakati wote.
Shangwe ya pekee kwetu ilikuwa yale “Majuma ya Kupainia” ambapo watumishi wa wakati wote kama 12 hivi wangekutana, katika miji fulani mikubwa, kukaa na ndugu wa mahali hapo, na kufanya kazi kama kikundi. Tulipelekea viongozi wa kidini na watu wengine mashuhuri vijitabu. Ilihitaji ujasiri kuwaendea. Mara nyingi tulikaribishwa kwa dharau, na wengi walifungiwa mlango kwa fujo usoni pao. Hilo halikutuhangaisha, kwa kuwa tulikuwa na shauku nyingi sana hata tukafurahi kudharauliwa kwa ajili ya jina la Kristo.—Mathayo 5:11, 12.
Katika Leeds tulibadili kigari, baiskeli ya miguu mitatu, na pikipiki na kigari chayo, na baadaye gari la baba lilibeba kinanda na vikuza sauti. Ndugu wawili wangeenda barabarani na kinanda, na kuweka rekodi ya muziki ili kujulisha watu na kuwachochea waje milangoni pao, kisha kufuatisha hilo na hotuba ya dakika tano iliyorekodiwa na Ndugu Rutherford. Halafu wangeenda barabara nyingine huku sisi, wahubiri, tukitoa fasihi ya Biblia.
Kwa miaka mingi, kila Jumapili jioni baada ya mikutano, tungeenda kwenye ua wa Town Hall penye jukwaa la kuhutubia na kutoa utegemezo kwa kusikiliza moja ya hotuba zilizorekodiwa za Ndugu Rutherford zenye muda wa saa nzima, kisha kugawanya trakti na kurudia wowote walioonyesha kupendezwa. Tukaja kujulikana sana hapo. Hata polisi walituheshimu. Jioni moja tulikusanyika kama ilivyokuwa kawaida wakati ambapo, kwa umbali, tulisikia sauti ya ngoma na nyimbo. Kisha Wafashisti karibu mia moja wakaja. Walizunguka nyuma yetu kisha wakasimama huku bendera zao zikipepea juu. Wakanyamaza, na kukawa na utulivu mara tu sauti ya Ndugu Rutherford ilipoanza kusikika: “Waacheni waheshimu bendera zao na kusifu wanadamu wakipenda. Sisi tutamwabudu na kumsifu Yehova Mungu wetu pekee!” Hatukujua ni jambo gani litatokea! Hakuna lililotokea, ila tu walipata ushahidi mzuri, na polisi wakawanyamazisha ili tuweze kusikia hotuba yote iliyofuata.
Kufikia sasa kinanda kilikuwa kikianza kutumika ili kutusaidia kutoa ushahidi mzuri. Mlangoni, tulisikiliza rekodi kwa makini sana ili kutia watu moyo kusikiliza kwa dakika zote tano mahubiri ya Biblia yaliyorekodiwa. Mara nyingi wenye-nyumba walitukaribisha ndani nao walipenda turudi tena ili wasikilize habari zaidi iliyorekodiwa.
Mwaka wa 1939 ulikuwa wenye shughuli nyingi sana na mgumu, kukiwa na upinzani na jeuri. Kabla ya mojapo mikusanyiko yetu, ndugu walifanyiwa ghasia na umati wenye ghasia barabarani na kupigiwa kelele. Hivyo wakati wa kusanyiko, walifanya mipango ili ndugu kadhaa waende kwa magari kuhubiri kwenye maeneo yaliyokuwa na ghasia huku akina dada na ndugu wengineo wakienda kulikokuwa salama. Tulipokuwa tukifanya kazi tukiwa kikundi barabarani, nilipitia kijia fulani kutembelea nyumba zilizokuwa nyuma. Nilipokuwa katika mlango fulani, nilisikia kelele fulani ikianza—kulikuwa na kelele na kilio barabarani. Niliendelea tu kuzungumza na mtu huyo mlangoni, nikirefusha mazungumzo hadi niliposikia kwamba hali imetulia. Kisha nikapitia kijia kile nikarudi barabarani nikakuta kwamba ndugu na dada wale wengine walipatwa na wasiwasi waliponikosa! Hata hivyo baadaye, wenye kufanya fujo walijaribu kuvuruga mkutano wetu, lakini walitolewa nje na akina ndugu.
Vita ya Ulimwengu ya 2 Yatokea
Kufikia sasa watu walikuwa wakiandikishwa jeshini kwa lazima, ndugu wengi vijana walifungwa kwa miezi 3 hadi miezi 12. Basi baba akapokea pendeleo jingine, la kutembelea ndugu waliofungwa. Kila Jumapili aliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi katika gereza la mahali petu. Jumatano jioni aliwatembelea ndugu ndani ya seli zao. Akiwa amepata kuwa gerezani kwa muda mrefu wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, alipendezwa hasa kutumikia wale waliokuwa wakipitia majaribu kama hayo. Alifanya hivyo kwa miaka 20, hadi kifo chake katika 1959.
Kufikia 1941 tulikuwa tumeanza kuzoea uchungu na uhasama ambao watu wengi walionyesha juu ya hali yetu ya kutokuwamo. Haikuwa rahisi kusimama barabarani na magazeti na kukabili hayo. Wakati uleule, tulishangilia kusaidia wakimbizi waliokuwa wakiishi katika eneo letu. Walatvia, Wapoland, Waestonia, Wajerumani—ilikuwa shangwe kama nini kuona wakifurahi walipoona Mnara wa Mlinzi au Consolation (sasa Amkeni!) kwa lugha zao wenyewe!
Kisha jaribu langu likaja kwa ajili ya msimamo wa kutokuwamo niliochukua wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Nikiwa nimefungiwa ndani ya seli kwa muda wa saa zipatazo 19 kwa kila saa 24, niliona maisha ya kifungo yakiwa magumu. Siku tatu za kwanza zilikuwa ngumu zaidi, kwa kuwa nilikuwa peke yangu. Siku ya nne, niliitwa kwenye ofisi ya gavana ambapo nilikuta wasichana wengine wawili wakiwa wamesimama. Mmoja wa wasichana hao akaninong’onezea: “Kwa nini umefungwa?” Nikasema: “Utashangaa ukijua.” Akauliza kwa mnong’ono wenye mkazo: “Je wewe ni Shahidi wa Yehova?” Msichana yule mwingine akamsikia naye akatuuliza sote wawili: “Je, ninyi ni Mashahidi wa Yehova?” na sote watatu tukakumbatiana. Hatukuwa peke yetu tena!
Utumishi wa Wakati Wote Wenye Kupendeza
Nikiwa nimefunguliwa kutoka gerezani, niliendelea na utumishi wangu wa wakati wote, na msichana mdogo wa miaka 16 aliyetoka tu kumaliza shule akajiunga nami. Tulihamia Ilkley, mji wenye kupendeza ulioko kwenye ncha ya Yorkshire Dales. Kwa miezi yote sita, tulijaribu kwa bidii kutafuta mahali panapofaa pa kufanyia mikutano yetu. Mwishowe tulikodi gereji ndogo, ambayo tulibadili ikawa Jumba la Ufalme. Baba alitusaidia, kwa kutuletea taa na kipasha joto. Pia aliturembeshea jengo hilo. Kwa miaka mingi kutaniko lililokuwa karibu lilitutegemeza, likiwapa akina ndugu mgawo wa kutoa hotuba ya watu wote kila juma. Kwa baraka ya Yehova tulisitawi na kuongezeka, na mwishowe kutaniko likaanzishwa.
Katika Januari 1959, kwa ghafula baba akawa mgonjwa. Nikaitwa nyumbani naye akafa Aprili. Miaka iliyofuata ilikuwa migumu. Afya ya mama pamoja na uwezo wake wa kukumbuka ziliharibika, ikifanya iwe vigumu kwangu. Lakini roho ya Yehova ilinisaidia kuendelea, nami niliweza kumtunza hadi kifo chake katika 1963.
Nimepata baraka nyingi sana kutoka kwa Yehova miaka yote. Ni nyingi sana zisihesabike. Nimeona kutaniko la nyumbani kwetu likiongezeka na kugawanywa mara nne, likitoa wahubiri na mapainia, wengine wakiwa wamishonari kwenye nchi za mbali kama vile Bolivia, Laos, na Uganda. Sikuolewa wala kuwa na familia. Jambo hilo halijanihuzunisha; nimekuwa na shughuli nyingi mno. Ingawa sina watu wa ukoo wa kimwili, nina watoto na wajukuu wengi katika Bwana, hata mara mia.—Marko 10:29, 30.
Mara nyingi mimi hukaribisha mapainia wachanga na vijana wengineo nyumbani kwangu ili kufurahia ushirika wa Kikristo. Sisi hutayarisha pamoja Funzo la Mnara wa Mlinzi. Pia sisi huelezana mambo yaliyoonwa na kuimba nyimbo za Ufalme, kama vile wazazi wangu walivyokuwa wakifanya. Nikiwa nimezingirwa na vijana wengi wenye furaha, mimi hudumisha hali ya uchanga na yenye furaha. Hakuna maisha bora kwangu kama utumishi wa painia. Namshukuru Yehova kwamba nimepata pendeleo la kufuata hatua za wazazi wangu. Sala yangu ni kwamba niendelee kumtumikia Yehova kwa umilele wote.
[Maelezo ya Chini]
a Ukumbusho wa mwisho wa uhasama katika 1918 na baadaye, 1945.
[Picha katika ukurasa wa23]
Hilda Padgett pamoja na wazazi wake, Atkinson na Pattie
[Picha katika ukurasa wa23]
Trakti iliyomvutia baba katika kweli