Kufanya Kazi kwa Bidii—Wakati Kunapofaa
KOTEKOTE katika Esia ya Kusini-Mashariki, wajakazi wengi wachanga huacha kazi zao za jikoni na kuketi wakitazama televisheni zao wakati programu ya TV ya Oshin iliyofanyizwa Japani inapoanza. Ni hadithi ya kutoka kwa umaskini hadi utajiri ya mwanamke mmoja anayefaulu baada ya kuvumilia miaka mingi ya kazi ngumu na taabu. Wakiwa na machozi machoni mwao, wasichana hao hufananisha hali yao na Oshin, huyo shujaa. Hadithi hizo zaonekana kuwa mambo wanayohitaji hasa ya kuwasaidia kukabili siku nyingine tena ya kazi ngumu.
Kwa kweli, watu wanapofanya kazi sana siku baada ya siku kufikia kiwango cha kuhatarisha afya na maisha yao, ni lazima wawe na sababu za kufanya hivyo. Ni kwa nini wanafanya hivyo? Kama ilivyo na wajakazi wa Esia, kutaka kuinua kiwango cha maisha kwa kweli ni sababu ya kawaida na pia yenye nguvu inayochochea kufanya kazi kwa bidii. Ingawa hivyo, kwa wazi, si ufanisi wa kimwili pekee unaohusika.
“Ufanisi wa kifedha, ni kichocheo kinachotamaniwa, lakini kinachotukia chenyewe,” aandika Stephen D. Cohen kuhusu tabia ya kazi ya Wajapani. Basi, ni nini huchochea Wajapani wafanye kazi kwa bidii hivyo? “Mafanikio ya mauzo ya kampuni yakilinganishwa na yale ya washindani wayo ni chanzo cha majivuno mengi na uradhi. Kazi yenye bidii inayotokeza mafanikio hayo ni thawabu,” aeleza Cohen. Ujitoaji kwa makampuni yao unakuwa sababu inayofanya wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii, na kazi inakuwa njia ya pekee ya wao kuonyesha ustahili wao. Jambo ambalo halipasi pia kupuuzwa ni tamaa ya kupandishwa cheo katika kampuni. Uwezekano wa kufikia cheo cha juu zaidi siku moja unabaki kuwa kichocheo kikubwa cha kazi yenye bidii.
Je! Mtu Ahatarishe Afya Yake kwa Sababu Hizo?
Je! hizo ni sababu zinazofaa za kufanya mtu ahatarishe afya yake na uhai wake? Kwa yule anayefanya kazi ili apate utajiri wa kimwili, Biblia yasema hivi, “macho yake hayashibi utajiri.” Hatimaye mtu huyo huenda akajiuliza: “Ni kwa ajili ya nani nafanya kazi, na kujinyima nafsi yangu mema?” (Mhubiri 4:8) Wale wanaofanya kazi kwa bidii ili wawe matajiri hawaonekani kama wanajua wataacha lini au wapi. Wanajikuta wamenaswa katika mviringo mbaya wa kazi, kazi na kazi zaidi. Biblia inaonya kwa usahili hivi: “Usijitaabishe ili kupata utajiri.”—Mithali 23:4.
Namna gani juu ya ushikamanifu kwa kampuni? Ingawa unaweza kufaa, uwezekano wa athari ya kufanya kazi nyingi kupita kiasi ni lazima ufikiriwe. “Ikiwa mtu anaugua uchovu,” akasema ofisa mmoja mkuu wa kampuni moja ya Amerika, “hata sitaki kumwajiri.” Mke mmoja wa “shujaa wa kampuni” aliandikia gazeti moja hivi baada ya mume wake kufa kabla ya kufika umri wa miaka 40 kwa sababu ya kufanya kazi nyingi kupita kiasi: “Tunapata faraja gani kwa usemi wa kampuni, ‘Tunasikitika kwa kumpoteza mtu mwenye thamani hivyo’? Watu hao wanaofia makampuni, mara wanapokufa, wanatendewa kama ‘bidhaa za kutupwa.’”
Hata ikiwa mtu haugui uchovu wa kazi au hafi kwa kufanya kazi nyingi kupita kiasi, ni nini hutokea wanapofika umri wa kustaafu? “Wajapofanyia makampuni kazi kwa bidii sana,” asema Motoyo Yamane, mtangazaji wa Japani, “wanajulishwa kwamba kampuni haiwahitaji tena na kwamba wao ni bure.” Kwa makampuni yasiyojali, wafanyakazi wenye kufanya kazi kwa bidii ni sehemu isiyo na maana katika kampuni yao kubwa, sehemu inayobadilishwa inapochakaa. Si ajabu kwamba Wajapani wengi wanapoteza imani kwa makampuni yao! Wanaanza kung’amua kwamba ujitoaji wao kwa kampuni ni upendo usiothaminiwa.
Ni jambo gani laweza kusemwa juu ya kupanda cheo katika kampuni? Wale ambao wamefikia vyeo vya madaraka ya katikati wanang’amua upesi kwamba si kila mmoja ataweza kufikia cheo cha juu kabisa. Basi, ni nini hutokea? Wakiwa hawana matumaini ya kupandishwa cheo, wanaanza kufanyia kampuni moja kazi na kuacha na kwenda. Ushikamanifu na bidii kwa kampuni havithawabishi!
Maoni Yenye kusawazika ya Kufanya Kazi kwa Bidii
Ingawa kazi yenye bidii inayochochewa na upendo wa fedha, ushikamanifu kwa kampuni, au roho ya mashindano hatimaye hufadhaisha na kuvunja moyo, Biblia haipuuzi thamani ya kazi ngumu. “Ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.” (Mhubiri 3:13) Biblia hupendekeza kufurahia matunda ya kazi ngumu aliyofanya mtu. Jambo hilo latoa dokezo juu ya maoni yenye kusawazika kwa habari ya kazi ya bidii.
Wizara ya Afya na Hali Njema ya Japani hivi karibuni iliwashauri wafanyakazi “wasahau mambo ya kazi baada ya kazi (na) wale mlo wa jioni pamoja na familia zao.” Wakubwa fulani wa kibiashara wanaonekana wanathamini hekima ya shauri hilo. Kwa mfano, msimamizi wa kampuni moja inayokua ya tekinolojia ya biolojia alitangaza hivi: “Nataka wafanyakazi wetu wote watunze ifaavyo familia zao mbele ya mambo mengine yoyote. Kazi yao katika kampuni yetu ni njia tu ya kuandalia familia riziki.”
Kwa kweli, uhusiano mzuri wa familia ni mradi unaofaa wa kufanyia kazi. Hali yenye uchangamfu ya familia ikihatarishwa au afya yako ikidhoofika kwa sababu ya kazi yako, basi wewe hujiburudishi kwa mema katika kazi yako yote.
Hata hivyo, katika jamii ya Kijapani, ambamo mfumo wa ukubwa hufuatwa, wengine wamesitawisha mwelekeo wa: “Usikose kuja kazini, wala usiwe mzembe, wala usifanye kazi.” Wanajifanya kuwa wenye bidii kazini kwa kuendelea kufanya kazi baada ya saa kwisha lakini wanangojea tu msimamizi wa kazi aende nyumbani. Kenji, muuzaji wa kampuni ya mapambo ya nyumba katika Hiroshima, alikuwa na mawazo kama hayo. Alikuwa mzembe kazini, akitumia wakati katika mkahawa au katika jumba la mchezo wa piniboli.
Je! mwelekeo kama huo hutokeza furaha? “Mvivu atalipishwa kodi [atalazimishwa kufanya kazi, NW],” yasema mithali moja ya Biblia. Leo, huenda mtu asilazimishwe kihalisi kufanya kazi kwa sababu ya uvivu wake. Hata hivyo, kazi yaweza kuwa yenye kuchosha, ya kulazimishwa tukisema kiakili. Kwa upande mwingine, mithali iyo hiyo inataja manufaa ya bidii ya kazi: “Mkono wa mwenye bidii utatawala.” (Mithali 12:24) Hata ikiwa hutatawala nchi au kampuni, angalau utaheshimiwa na familia yako nawe utajiongoza vizuri. Kwa kuongezea, huenda ukatumainiwa na mwajiri wako, na vilevile kupata dhamiri safi.
Kenji aliona ukweli wa jambo hilo. Aliamua kujifunza Biblia, na maisha yake yakabadilika kwa njia yenye kutazamisha. “Kwa kutumia kanuni ya unyoofu kazini,” yeye asema, “Nilianza kufanya kazi kwa kudhamiria iwe mkubwa wa kazi alikuwapo au la. Jambo hilo lilimfanya anitumaini.”
Wakati Kufanya Kazi kwa Bidii Kunapofaa
Ukweli ni kwamba, ili kazi iwe yenye maana, ni lazima inufaishe wengine. ‘Kazi inayoridhisha,’ akafafanua mwandikaji wa habari za biashara, ‘ni kazi inayoleta mafaa, starehe au furaha kwa maisha ya watu wengi.’ Kazi kama hiyo huleta uradhi wa ndani kwa huyo mfanyakazi. Ni kama vile Yesu Kristo alivyosema: “Ni heri [kuna furaha zaidi, NW] kutoa kuliko katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Ingawa kufanya kazi kwa ajili ya manufaa ya wengine kunastahili pongezi, bado kuna jambo jingine muhimu la kupata uradhi katika kazi na maisha. Mfalme Sulemani, baada ya kupata anasa zote na utajiri wote ambao maisha yaweza kutoa, alifikia mkataa huu mtukufu: “Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13.
Kwa wazi, ni lazima tufikirie mapenzi ya Mungu katika kazi yoyote tunayofanya. Je! tunafanya kazi kupatana na mapenzi yake ama dhidi ya mapenzi yake? Je! tunajitahidi kumfurahisha au tunajifurahisha wenyewe tu? Tukipuuza kufanya mapenzi ya Mungu, tutakuja tu kuwa watu wanaopenda vitu vya kimwili au anasa na hatimaye tutaugua maumivu ya upweke, utupu, na kukata tamaa.
Basi kumbuka kwamba kumtumikia Yehova Mungu—kufanya kazi inayompendeza Muumba wetu—hakutatuacha katika hali ya kukosa uradhi. Yehova mwenyewe ni mfanyakazi mwenye bidii, naye anatualika tuungane naye tuwe ‘wafanyakazi pamoja naye.’ (1 Wakorintho 3:9; Yohana 5:17) Lakini, je, kazi ya bidii kama hiyo hakika inaleta furaha ya kweli?
Wakati mmoja, mkurugenzi msimamizi mmoja wa kampuni ya kuchapa alizuru kiwanda cha kuchapa cha Watch Tower katika Japani ili achunguze jinsi kilivyofanya kazi. Uangalifu wake ulivutwa kwa mambo mengine mbali na mashine. Aliona vijana wanaofurahia kazi yao, na alishangaa kusikia kwamba wote ni wafanyakazi wa kujitolea na kwamba wengine wengi walikuwa wametoa maombi kwa hamu ili wajiunge nao. Ni kwa nini alishangaa? “Katika kampuni yetu,” alieleza, “tunapoajiri watu kumi, ni lazima tulione kuwa jambo zuri ikiwa wanne kati yao bado wanafanya kazi na sisi baada ya mwaka mmoja. Nyinyi watu wa Watchtower mna hazina katika wafanyakazi hao vijana!”
Ni nini kinachofanya vijana hao wawe wenye furaha na kuwa wenye bidii ya kazi jinsi hiyo? Wakiwa wafanyakazi wa kujitolea, kwa wazi hawafanyi kazi kwa ajili ya fedha. Basi, nini kinawachochea? Wakfu wao na uthamini wao kwa Yehova, Muumba wao, na upendo wao kwa jirani zao. Mwelekeo wao waonyesha kwamba hawafanyi kazi ‘kama wajipendekezao kwa wanadamu; bali kama watumwa wa Kristo, wakitenda yampendezayo Mungu kwa moyo.’—Waefeso 6:6.
Hayo yote ni matangulizi ya mambo yatakayokuja. Wale wanaofanya kazi kwa bidii kumtumikia Yehova wanaweza kutazamia wakati ambapo karibuni atarudisha Paradiso na dunia yote itajawa na kazi zenye kufaa. Isaya, nabii wa kale wa Mungu, alitabiri hivi kuhusu maisha ya wakati huo: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; . . . wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:21, 22.
Kazi itakuwa baraka kama nini wakati huo! Kwa kujifunza mapenzi ya Mungu ni nini kwako na kufanya kazi kupatana nayo, na uwe miongoni mwa wabarikiwa wa Yehova na nyakati zote ‘uone mema katika kazi yako yote.’—Mhubiri 3:13.
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Maoni Yenye Kusawazika ya Kazi Yaokoa Ndoa
Kwa habari ya Yasuo, anayeishi katika Hokkaido, Japani, kazi ilikuwa kipisha wakati cha pekee mpaka miaka michache iliyopita. Alikuwa na cheo cha madaraka ya katikati, na alikuwa na tamaa sana ya kuongeza mauzo. Kila siku alifanya kazi mpaka karibu saa 5:00 ya usiku bila kuchukua likizo. Kisha, yeye akumbuka: “Nikang’amua kwamba hata nijitahidi jinsi gani, hakuna furaha niliyokuwa nikipata kwa kazi yangu.” Hali ya afya ya Yasuo ikaanza kudhoofika. Alipozungumza na mke wake, aling’amua kwamba kulikuwa na kitu kingine cha maana zaidi kuliko kazi yake—familia yake. Alibadili mtindo wa maisha yake na kujiunga na mke wake katika kujifunza Biblia. Sasa yeye ni kichwa cha familia yenye furaha anayependwa na kustahiwa.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kazi yako isihatarishe uhusiano wa familia
[Picha katika ukurasa wa 10]
Hivi karibuni wote watafurahia kufanya kazi ya kutengeneza dunia kuwa paradiso