Ndoa-Sababu Inayofanya Wengi Waivunje
LIKIKAZIA talaka katika Hong Kong, ambako tamaduni za Mashariki na Magharibi zakutana, Asia Magazine laonelea hivi: “Kukosa kuwasiliana, kukosa uaminifu katika ndoa, matatizo na kutokupatana kingono ndizo sababu ambazo kwa kawaida husababisha hitilafu katika ndoa za Wachina na vilevile za Magharibi.” Hali ni iyo hiyo katika sehemu nyinginezo ulimwenguni.
Wote wanaume na wanawake ambao wana akili ya kazi kwanza hudhabihu haraka familia zao kwa ajili ya kazi yao. Hivyo, wanafunga mawasiliano ya familia. Akiwa amechoka baada ya kazi ya siku, mume hujizamisha katika kusoma gazeti. Junichi na mke wake walikuwa na hoteli tatu na kufanya kazi kutokea saa mbili ya asubuhi mpaka saa nne ya usiku katika mahali tofuati-tofauti. “Hakukuwa na mawasiliano kati yetu tukiwa mume na mke,” akiri Junichi. Ukosefu huo wa mawasiliano ulitokeza matatizo makubwa ya ndoa.
Sababu nyingine inayotokeza kuvunjika kwa ndoa ni maoni ya watu juu ya ngono ya nje ya ndoa. Ngono ya nje ya ndoa imeenea sana hivi kwamba asilimia 20 ya waume na asilimia 8 ya wanawake waliokubali kuhojiwa katika Japani walikiri kwamba walikuwa wamekuwa na ngono ya nje ya ndoa yao ya mke mmoja kwa mwaka uliopita. Jambo la kawaida ni mwanamke anayefikiria kazi yake katika Japani aliyekuwa na uhusiano wa kingono na wanaume wengine ambao si mume wake. Aliruka huku na huko kutoka kwa mwanamume mmoja hadi mwingine, akifikiria, “mume wangu akigundua, nitamtaliki tu.” Jamii ya kisasa inajifanya kuwa haioni mambo hayo.
Jamii iyo hiyo ya kisasa huendeleza mwelekeo wa mimi-kwanza, ili mume na mke vilevile wawe wa kujifikiria tu, jambo ambalo linatokeza kutopatana, ambayo ni sababu nyingine ya talaka. “Sisi tungeachana wakati wowote tukiwa mume na mke,” asema Kiyoko. “Mara tu tulipooana, mume wangu aliniambia niwe kama roboti na nifanye tu ninayoambiwa. Mambo yalipokuwa mazuri kwake, hali haikuwa mbaya sana, lakini mambo yalipokuwa mabaya, hangeweza kukiri makosa yake na kuweka kila lawama kwa watu wengine. Mimi pia nilikuwa na lawama kwa sababu nilikuwa nikiasi mamlaka. Niliona ugumu sana kumtii mume wangu wakati alipokuwa hafuatii haki.”
Sababu nyinginezo za talaka ni ujeuri na ulevi, matatizo ya kifedha, matatizo ya wakwe, na kutendwa vibaya kiakili.
Ni Nini Husababisha Talaka?
Hata sababu za talaka ziwe tofauti-tofauti kadiri gani, kuna kitu kingine zaidi kinachochochea ongezeko kubwa la talaka ulimwenguni pote. Ingawa Mashariki inalaumu uvutano wa jamii ya Magharibi kwa ajili ya mabaya yayo, kukubaliwa kwa talaka katika Magharibi ni tukio la karibuni tu. Kwa kweli, talaka katika United States ziliongezeka mara tatu na katika Uingereza ziliongezeka mara nne katika miongo michache tu ya miaka. Andrew J. Cherlin wa Taasisi ya Miji (shirika la utafiti linalochunguza matatizo ya kijamii na kiuchumi katika United States), ingawa anakiri kwamba visababishi vya ongezeko havieleweki vizuri, anaorodhesha “uhuru unaoongezeka wa kiuchumi wa wanawake” na “mwelekeo wenye kubadilika wa jamii” kuwa miongoni mwa visababishi vya ongezeko hilo.
Kwa wanawake katika United States, na vilevile wale walio katika nchi zilizoendelea kiuchumi, kuolewa na kufanya kazi nje ni jambo la kawaida siku hizi. Hata hivyo, sehemu ya mume ya kazi ya nyumbani imekuwa ikiongezeka polepole sana. Haishangazi kwamba wanawake wengine hunung’unika hivi: “Kile ambacho kila mwanamke aliyeajiriwa anahitaji zaidi ni mtu wa kufanya kazi nyumbani!”
Huku wanawake wakifanya kazi kwa bidii sana wakifua, wakifanya usafi, wakitayarisha milo, na kutunza watoto, katika United States, “wanaume wengi hufurahia wakati wanaotumia ‘kuzurura-zurura,’” chasema kitabu The Changing American Family and Public Policy. Jambo hilo hutukia ulimwenguni pote, wastadi wa elimu ya binadamu wasema. Katika Japani ni jambo la kawaida kwa wanaume kwenda kufurahia pamoja baada ya kazi. Wanadai kwamba ni jambo la lazima kwa sababu ya uhusiano mzuri wa kibinadamu katika mahali pao pa kazi, huku wakipuuza uhusiano mzuri wa kibinadamu nyumbani. Kwa sababu wanaume, kulingana na fikira zao, ndio wenye kuandaa riziki, wanawake na watoto hawapaswi kunung’unika. Hata hivyo kukiwa na wanawake wengi wanaofanya kazi, fikira kama hizo ni za kutoa udhuru tu.
Jambo jingine linalochangia kuvunjika kwa ndoa ni “mwelekeo wenye kubadilika wa jamii” au, kama vile Journal of Marriage and the Family linavyolitaja, “kupunguka kwa uzuri wa ndoa yenye kudumu.” Kwa bwana na bibi arusi wa miaka ya 1990, ile nadhiri ya kidesturi ya ndoa ya “mpaka kifo kitutenganishe” haimaanishi hivyo siku hizi. Wanaendelea kutafuta mwenzi anayefaa zaidi. Ikiwa hivyo ndivyo mume na mke waliotoka tu kufunga ndoa wanavyoona ushikamano wao, basi ushikamano huo utakuwa na nguvu kadiri gani?
Mabadiliko hayo ya kijamii hayashangazi wanafunzi wa Biblia hata kidogo. Kitabu hicho chenye pumzi ya Mungu kinafunua kwamba tangu 1914 tumekuwa tukiishi katika “siku za mwisho,” ambazo ni “nyakati za hatari.” Watu ni wenye “kujipenda wenyewe, . . . wasio na shukrani, wasio safi [wasio waaminifu, New World Translation] wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu.” (2 Timotheo 3:1-3) Kwa hiyo, kwa watu wanaojipenda wenyewe kuliko waume zao au wake zao, wale wanaokosa kuwa waaminifu kwa waume zao au wake zao, na ambao hawawezi kufanya suluhu yoyote katika ndoa yao, talaka inakuwa njia ya pekee ya kusuluhisha matatizo yao ndoa.
Je! Ni Mlango wa Kupata Furaha Zaidi?
Talaka, katika visa vingi, haijathibitika kuwa mlango wa kupata furaha.a “Talaka ni danganyifu,” asema mtafiti wa afya ya akili Judith Wallerstein baada ya uchunguzi wa miaka 15 wa wa-ume na wake 60 waliotaliki. “Kisheria ni kitendo kimoja, lakini kiakili ni mambo mengi—nyakati nyingine mfululizo mrefu—wa matukio, kuhama-hama, na kukatiza-katiza uhusiano mbalimbali ambao unatukia baada ya muda.” Uchunguzi wake waonyesha kwamba robo ya wanawake na sehemu moja kati ya tano ya wanaume hawakuwa wamerudia maisha ya kawaida miaka kumi baada ya talaka.
Wanaoathiriwa zaidi hasa ni watoto wa talaka. Kutokana na utafiti uo huo, Wallerstein alipata kwamba kwa karibu watoto wote waliohusika, talaka ilikuwa na “madhara makubwa na yasiyotazamiwa kabisa.” Watoto wengi wanaoonekana kuwa hawana hisia zozote juu ya talaka ya wazazi wao huenda kwa ghafula wakapata hisia hizo zikitokea baadaye maishani mwao wanapotafuta mume au mke.
Jambo hilo halimaanishi kwamba wote wanaoathiriwa na talaka hawatapata kamwe furaha maishani mwao, kwa sababu wengine wana furaha. Kwa hao, utu wenye kufanyizwa upya hutokea, kutokana na masalio ya utu wa kale. Kwa mfano, mara mshtuko wa talaka pamoja na huzuni na shaka za kujistahi ambazo hufuata zinapoisha, mume au mke asiye na hatia anaweza kutoka kwenye jaribu hilo akiwa mtu kamili mwenye nguvu na nishati zaidi.
Mke mmoja ambaye mume wake alimwacha kwa ajili ya mke mwingine anaeleza kwamba baada ya uchungu na hasira kuanza kupungua, “unapata kwamba wewe ni tofauti ndani. Hisia zako zimebadilika. Huwezi kuwa yule mtu uliyekuwa zamani.” Yeye ashauri hivi: “Chukua wakati upate kujijua mwenyewe ukiwa mtu tena. Katika ndoa waume na wake kwa kawaida hukandamiza mapendezi na tamaa zao kwa heshima ya mwenzi mwingine, lakini baada ya talaka, unapaswa kuchukua wakati ili upate kujua ni mambo gani yanayokupendeza na ni yapi hayakupendezi sasa. Ukikandamiza hisia zako, bado ziko. Siku moja zitakuja tena, na utalazimika kuzikabili. Kwa hiyo ni bora ukabili hisia zako na kuzifanyia kazi.”
Kwa sababu ya matatizo yanayoendelea kuonekana ambayo talaka huleta, inakuja kuwa chaguo lisilopendwa sana. Gazeti Time laripoti kwamba washauri wachache wanaoendelea kuongezeka sasa wanatia moyo hivi waume na wake wenye matatizo: “Mwishi pamoja.” David Elkind wa Chuo Kikuu cha Tufts aliandika hivi: “Kupatwa na talaka ni kama kuvunja mguu wakati wa [mchezo wa] kuteleza juu ya theluji: hata watu wengi kadiri gani katika mahali pa mchezo huo wavunjike miguu, mguu wako uliovunjika utaendelea tu kuuma.”
Talaka si suluhisho rahisi kwa matatizo ya ndoa. Basi, ni njia gani iliyo bora ya kusuluhisha matatizo ya ndoa?
[Maelezo ya Chini]
a Talaka halali au kutengana kihalali kwaweza kuandaa ulinzi wa kadiri fulani kutokana na kutendwa vibaya sana au ukosefu wa kutokuandaliwa riziki kimakusudi.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mara nyingi leo waume na wake hawawezi kuwasiliana