Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 7/8 kur. 8-11
  • Maisha ya Ndoa—Kuyafanya Yawe Yenye Furaha Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maisha ya Ndoa—Kuyafanya Yawe Yenye Furaha Zaidi
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ufunguo wa Ndoa Yenye Furaha
  • Kuonyesha Upendo kwa Jirani Yako wa Karibu Zaidi
  • Acheni “Malazi Yawe Safi”
  • Waume, Pendeni na Kuthamini Wake Zenu
  • “Yakikolea Munyu”
  • Je! Ndoa Yako Yaweza Kufanikiwa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Jinsi ya Kufanikiwa Katika Ndoa ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Funguo Mbili za Kuwa na Ndoa Yenye Kudumu
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Maisha ya Jamaa—Namna Unavyoweza Kufanikiwa
    Furaha​—Namna ya Kuipata
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 7/8 kur. 8-11

Maisha ya Ndoa—Kuyafanya Yawe Yenye Furaha Zaidi

Ni nini kinachoweza kufanya ndoa ifanikiwe?

Ni uongozi wa nani unaoweza kuleta furaha ya ndoa?

Matatizo ya mawasiliano yanaweza kusuluhishwaje?

WAKISHAWISHIWA na vitabu wanavyosoma juu ya uhuru wa wanawake, Yasuhiro na msichana rafiki yake, Kayoko, walianza kuishi pamoja wakifikiria kwamba wangeweza kuvunja uhusiano wao wakati wowote. Walihalalisha ndoa yao baada tu ya Kayoko kushika mimba. Hata hivyo, Yasuhiro aliendelea kutilia shaka mpango wa familia. Matatizo ya kifedha yalipoingia pamoja na hisi za kutokupatana, walitalikiana bila tatizo lolote.

Muda fulani baada ya talaka, na bila wote wawili kujua, Yasuhiro na Kayoko walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda kila mmoja wao alitambua juu ya masomo hayo na wangeweza kuona mabadiliko yaliyokuwa yakifanywa na yule mwingine kwa kutumia kanuni za Biblia. Waliamua kuoana tena. Sasa, wakiwa na maoni ya Mungu juu ya ndoa, bado wako tayari kujidhabihu ili wasuluhishe matatizo yao.

Ni nini iliyofanya ndoa yao ya pili ifanikiwe? Ilikuwa ni staha yao kwa Mwanzilishi wa ndoa. (Mwanzo 2:18-24) Mwelekezo unaotolewa na mshauri wa ndoa mwenye ujuzi zaidi, Yehova Mungu, ndio ufunguo unaofungua mlango wa furaha ya ndoa.

Ufunguo wa Ndoa Yenye Furaha

Matatizo ya ndoa yanaweza kusuluhishwa na ndoa ziokolewe kama wote wawili mume na mke wanatumia maishani yale maneno ambayo Yesu Kristo alitaja: “Mpende BWANA [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:37-39) Hapa pana ufunguo wa ndoa yenye furaha. Wote wawili mume na mke ni lazima wampende Yehova kabla ya kujipenda au kupendana wenyewe. Uhusiano huo waweza kulinganishwa na kamba ya nyuzi tatu. “Ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga; wala kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.”—Mhubiri 4:12.

Kwa sababu kumpenda Mungu kwamaanisha kutii amri zake, ni lazima mume na mke waweke kwanza maishani mwao sheria na kanuni zake zinazoongea juu ya tabia ya kibinadamu. Kwa kufanya hivyo wanafanyiza kamba ya nyuzi tatu ambayo ndani yayo uzi wenye nguvu zaidi ni upendo wao kwa Yehova. Na “amri zake si nzito,” 1 Yohana 5:3 husema.

Jambo hilo linatufanya tuone ndoa kuwa mpango wa kudumu. (Malaki 2:16) Wakiwa na msingi kama huo katika ndoa yao, mume na mke watasukumwa kutatua matatizo ya ndoa badala ya kuyaacha matatizo hayo kwa kupata talaka.

Kuonyesha Upendo kwa Jirani Yako wa Karibu Zaidi

Ili uwe na ushikamano wa kudumu na mwenzi wako, ni lazima ukuze upendo kwake, jirani yako wa karibu zaidi. Ni lazima upendo huo usiwe wa kibinafsi. Ona jinsi Biblia inavyohimiza kanuni hii: ‘Mwe wenye mapenzi mamoja, wenye roho moja, mkinia mamoja. Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’—Wafilipi 2:2-4.

Ni kweli kwamba ni vigumu kufanya neno lolote kwa kushindana wala kwa majivuno katika ulimwengu huu wenye ubinafsi. Mwenzi wako asipotangulia kuonyesha upendo, ni vigumu hata zaidi kutokuwa na ubinafsi; lakini kwa kuonyesha unyenyekevu wa akili, ukimhesabu mwenzi wako kuwa bora kuliko wewe, utapata ikiwa rahisi zaidi kufikiria mapendezi ya mwenzi wako. Biblia inatuonya kwa upole kwamba tuwe na mwelekeo wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu. Alikuwa roho mwenye nguvu sana, lakini “akatwaa namna ya utumwa,” akawa mwanadamu. Na si hilo tu, lakini alipokuwa duniani, “alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti,” jambo lililonufaisha hata wanadamu ambao hawakumkaribisha. (Wafilipi 2:5-8) Kwa kuonyesha mwelekeo huo, Yesu alikuja kupendwa na wapinzani wengi, na kwa kumwiga Yesu, wanafunzi wake vilevile walifanya hivyo. (Matendo 6:7; 9:1, 2, 17, 18) Jambo hilo laweza kukutokea pia. Kwa kuona mwenzi wako kuwa bora kuliko wewe na kwa kufikiria mambo ya binafsi ya mwenzi wako, polepole unaweza kumfanya akupende.

Hata hivyo, kumwona mwenzi wako kuwa bora kuliko wewe hakuhitaji mke ajitii kimya-kimya ukatili wa mume, kama ambavyo imekuwa katika Mashariki. Ni lazima wote wawili mume na mke waone kila mmoja kuwa bora zaidi kwa njia ya kwamba kila mmoja yuko tayari kujidhabihu kwa ajili ya mwingine. Mume na mke wanapozungumza juu ya matatizo yao wakiwa na unyenyekevu wa akili, wanapoonyesha upendezi usio na ubinafsi kwa kila mmoja, na wanapofuata mashauri ya Mungu, basi wako katika njia ya kutatua matatizo yao. Sasa ebu tuone baadhi ya mashauri ya Mungu.

Acheni “Malazi Yawe Safi”

Yehova aliyeanzisha mpango wa ndoa, ana mpango unaofaa kwa uhusiano kati ya mtu na mke wake. Alipoulizwa kama ilikuwa halali mtu kumtaliki mke wake kwa sababu yoyote, Yesu Kristo alijibu hivi: “Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” Alionyesha kwamba kulikuwa na sababu moja tu halali ya talaka na kuoa au kuolewa tena alipoendelea kusema hivi: “Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini.”—Mathayo 19:3-9.

Ngono ya nje ya ndoa, hata kama inafanywa kwa ajili ya upendo, si wonyesho wa upendo hata kidogo kwa ama mume ama mke. Mtu mmoja katika Japani alikuwa na uhusiano wa kingono na wanawake kadhaa nje ya ndoa. Mke wake akawa anamshuku na kufadhaika. Ndoa yao ikapatwa na matatizo. Kisha siku ikaja ambapo mmoja wa wapenzi wake alimwambia kwamba ataenda kujijulisha kwa mke wa huyo mtu na kutaka kwa nguvu kwamba amwoe. “Uhusiano kama huo haufurahishi mtu yeyote,” mtu huyo akumbuka kwa moyo wa toba. Aliokoka tu matatizo hayo baada ya kuumiza kila mtu aliyehusika. Kiwango cha Biblia ni wazi sana juu ya jambo hili. “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi, kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4) Kwa kutii sheria hiyo, mtu huepuka magonjwa ya kuambukizwa kingono, matatizo ya ndoa, na mikazo ya kuwa na mapenzi na mwingine nje ya ndoa.

Waume, Pendeni na Kuthamini Wake Zenu

Ile kanuni ya ukichwa katika familia pia imetajwa na Mungu. “Enyi wake watiini waume zenu, kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa,” Waefeso 5:22, 23 husema. Kutumia shauri hilo si rahisi. “Lilikuwa gumu kama mlima mkubwa kwangu,” akiri Shoko, aliyekuwa akinyakua haki ya mume ya kufanya maamuzi ya mwisho. Akifikiria kwamba ni lazima mwanamume anunue nyumba akiwa katika miaka yake ya mwisho-mwisho ya 20, alilazimisha mume wake anunue nyumba ambayo tayari mke huyo alikuwa amepata. Lakini alipojifunza kanuni za Biblia zinazohusika, alianza kumwona mume wake kwa njia tofauti. Ile tabia iliyoonekana kuwa dhaifu na isiyo ya kiume, ilipotazamwa vizuri, kumbe ilikuwa tabia yenye utambuzi, unyenyekevu, na upole.

Kanuni hiyo inahitaji waume watambue kwamba wako chini ya mamlaka ya juu ya Kristo Yesu. (1 Wakorintho 11:3) Akiwa chini ya mamlaka ya Kristo, mume anapaswa kumpenda na kumthamini mke wake kwa njia ileile ambayo Yesu anavyowapenda wafuasi wake. (Waefeso 5:28-30) Hivyo, mume Mkristo atafikiria kwa uangalifu hisia, tamaa, na mipaka ya mke wake kabla ya kufanya maamuzi.

“Yakikolea Munyu”

Hisako alikuwa na matatizo katika kuwasiliana na mume wake. Wakati wowote alipojaribu kuzungumza naye juu ya jambo fulani, mume wake angeepuka mazungumzo hayo kwa kusema: “Fanya utakavyo.” Hisako akumbuka: “Nafikiria tatizo lilikuwa ni ukosefu wangu wa upole. Ingekuwa bora zaidi kama ningesema kwa utulivu zaidi.” Leo, yeye na mume wake wanaweza kuzungumzia mambo wakiwa na furaha. Badiliko hilo limetokea tangu Hisako alipotumia maishani shauri hili linalofuata: “Maneno yenu yawe na neema sikuzote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Kama chakula kilichokolea munyu kilivyo kitamu, maneno yaliyofikiriwa vizuri kwa njia ya neema yanasikilizwa kwa urahisi. (Mithali 15:1) Kwa kweli, kwa kuwa tu mwenye kufikiria katika namna unavyosema, mara nyingi utengano katika ndoa waweza kuepukwa.

Naam, kumpenda Yehova Mungu na kustahi kanuni zake ni suluhisho kweli. Upendo kwa Yehova wakuchochea uone ndoa yako kuwa ufungamano wa kudumu na unakusaidia kuweka bidii ya kuihifadhi. Mungu ameandaa mielekezo inayofaa itakayokusaidia kushughulika na matatizo ya ndoa na kusuluhisha matatizo yako, hata yawe makubwa kama nini. La, katika visa vingi talaka si mlango wa kupata maisha yenye furaha zaidi, lakini kutumia kanuni za Biblia maishani ndio mlango wa kupata maisha yenye furaha zaidi. Unaweza kufungua mlango huo kwa kusitawisha upendo wako kwa Yehova. Mbona usijifunze zaidi juu ya shauri lake kutoka kwa kitabu chenye mamlaka zaidi cha mielekezo juu ya ndoa, Biblia?

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Talaka Inapokuwa Chaguo la Mtu

INGAWA Biblia inakubali talaka na kuoa au kuolewa tena kwa sababu ya uasherati, uzinzi hauvunji tu mara moja uhusiano kati ya mume na mke. Yule mwenzi asiye na hatia ana chaguo la ama kupata talaka au la.—Mathayo 19:9.

Yasuko alikabiliwa na uamuzi huo. Mume wake alikuwa akiishi na mwanamke mwingine. Mama ya mume wake alimlaumu Yasuko na kusema: “Ni kwa sababu yako kwamba mwana wangu anatenda hivyo.” Yasuko alikuwa akilia kila wakati. Watu wengi walimshauri lakini hakuna hata mmoja aliyeshutumu matendo ya mume wake. Kisha mama yake mwenyewe, ambaye alikuwa ameanza kujifunza Biblia, alimwambia hivi: “Katika Biblia, inasemwa waziwazi kwamba ni vibaya kufanya uzinzi.” (1 Wakorintho 6:9) Yasuko alifarijika sana kujua kwamba bado kuna kipimo cha kujua mema na mabaya katika ulimwengu wetu leo.

Sasa Yasuko alikuwa na chaguo. Ingawa alifikiria kutaliki mume wake, angeweza kuona baada ya kujifunza na Mashahidi wa Yehova kwamba hata yeye hakuwa akitimiza fungu lake. Kwa hiyo aliamua kujaribu kanuni za Biblia katika kusuluhisha matatizo yake. Alianza kuzitumia maishani. (Waefeso 5:21-23) “Haikuwa rahisi,” akumbuka. “Nilikuwa ninarudia tena na tena mambo ya zamani. Mara nyingi nilisali kwa Yehova kwa machozi.” Alipokuwa akibadilika, mume wake naye akaanza kubadilika polepole pia. Miaka yapata mitano baadaye, mume wake alivunja uhusiano wote na yule mwanamke. Yasuko amalizia hivi: “Nina uhakika kwamba kutii Neno la Mungu kwa wazi kunanufaisha.”

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Kutopatana Kingono na Talaka

WAUME wengi na wake wengi hutaja kutopatana kingono kuwa sababu yao ya kuchukua talaka. Kikielekezea mahali matatizo yanapotokea, kitabu kinachoshughulikia mpango unaobadilika wa familia, chenye kichwa Sekkushuaritii to Kazoku (Ngono na Familia), kinasema hivi: “Mpango wa ndoa ya mke mmoja na habari za ngono zenye kukazia nyege hazipatani leo. Habari nyingi za kingono hupotoa mapenzi kati ya mume na mke na kuharibu shauku ya kawaida. Tepu za video na vitabu vya kuchekesha vyenye kuonyesha miili ya wanawake hazionyeshi tu ngono kuwa kitu cha kuuzwa, bali pia zinapotoa akili na mioyo ya kibinadamu. Kwa hiyo, wake wanapata pigo la kulazimishwa na ngono, na waume wanaokataliwa hupatwa na uhanithi wa kingono.”

Vichapo visivyo vya adili, vidio, na programu za TV hupotoa ngono. Hazifundishi kitu kinachotokeza furaha katika ndoa. Pia zinaharibu utumainifu ambao mume na mke lazima wasitawishe ili kuwa na ndoa yenye mafanikio. Psychology Today chaeleza hivi: “Utumainifu unakusaidia kuweka hisia na hofu zako za ndani zaidi mkononi mwa mwenzi wako, ukijua kwamba zitashughulikiwa kwa uangalifu. Ingawa hisia za upendo au ngono zaweza kuongezeka na kupunguka kwa muda fulani, kwa kweli, utumainifu unadumu.”

Ngono si msingi ambao maisha ya ndoa yenye mafanikio yanategemea. Mke ambaye amepitia matatizo makubwa ya ndoa asema hivi: “Mambo yale yaliyonitia moyo zaidi yalikuwa maneno katika kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha: ‘Kwa ujumla, ikiwa uhusiano mwingine wote katika ndoa ni mzuri, ikiwa kuna upendo, heshima, kuwasiliana kuzuri na kufahamiana, ngono haitakuwa jambo gumu mara nyingi.’”a

Kitu kinachotokeza uhusiano wa karibu kati ya waume na wake si ngono bali ni upendo. Ngono bila upendo ni bure, lakini upendo waweza kuendelea bila ngono. Kwa kuweka ngono mahali panapoifaa, bila kuifanya kuwa kitu kikuu maishani mwao, waume na wake wanaweza kufurahia ndoa yao na kutatua tatizo hilo la kutopatana kingono.

[Maelezo ya Chini]

a Kimechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kustahi kanuni za Biblia kutasaidia mume na mke wawasiliane kwa uhuru

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki