Ulimwengu Mpya—Je! Utapata Kuja?
MNAMO Aprili 13, 1991, George Bush, ambaye wakati huo alikuwa rais wa United States, alitoa hotuba katika Montgomery, Alabama, yenye kichwa: “Uwezekano wa Taratibu ya Ulimwengu Mpya.” Katika kumalizia, alisema hivi: “Ulimwengu mpya unaotukabili . . . , ni ulimwengu mzuri ajabu wa uvumbuzi.”
Miezi miwili baadaye The Bulletin of the Atomic Scientists lilisema kwamba kwa kuanguka kwa tawala za Kikomunisti katika Ulaya Mashariki, “taratibu ya ulimwengu mpya unaotegemea amani, haki, na demokrasi yaonekana imewadia.”
Mazungumzo kama hayo ya ulimwengu mpya yameendelea mpaka 1993. Gazeti The New York Times liliripoti katika Januari juu ya mkataba ulioazimia kupunguza silaha za kinyukilia. Gazeti hilo lilisema hivi: “Jambo hilo laweka Amerika na Urusi kwenye ‘ukingo wa ulimwengu mpya wenye tumaini,’ katika maneno yaliyoteuliwa vizuri ya Rais Bush.”
Majuma mawili baadaye rais mpya wa U.S., Bill Clinton, alitangaza hivi katika hotuba yake ya kutawazwa: “Leo, taratibu ya kale ipitapo, ulimwengu mpya una uhuru zaidi lakini si thabiti sana.” Hata alidai hivi: “Ulimwengu huu mpya hata tayari umenufaisha maisha ya mamilioni ya Waamerika.”
Kwa hiyo kumekuwa na mazungumzo mengi kuhusu ulimwengu mpya—ulio tofauti na ulio bora zaidi. Kulingana na hesabu moja, katika kipindi cha muda mfupi tu kwa kulinganisha, George Bush alitaja “Taratibu ya Ulimwengu Mpya” mara 42 katika taarifa zake za hadhara.
Lakini, je, mazungumzo hayo ni ya kipekee? Je! yamepata kusikiwa hapo awali?
Kwa Kweli Hakuna Jambo Jipya
Katika Mei 1919, baada tu ya Vita ya Ulimwengu 1, Baraza la Churches of Christ katika Amerika lilikuwa na mkutano katika Cleveland, Ohio, ambapo ‘uwezekano wa ulimwengu mpya ulio bora zaidi’ ulitangazwa. Msemaji mmoja alisisitiza hivi: “Utakuwa ni ulimwengu mpya ambamo kanuni ya mashindano itabadilishwa na kanuni ya ushirika na upatano. Utakuwa ni ulimwengu mpya ambamo kanuni ya umoja itachukua mahali pa kanuni ya mgawanyiko . . . Utakuwa ni ulimwengu mpya ambamo udugu na urafiki utakuwa umeondoa uadui wote ila tu ile vita dhidi ya uovu.”
Makanisa yaliamini ulimwengu huu mpya ungekujaje? Kwa kupitia serikali ya Ufalme wa Mungu iliyoahidiwa katika Biblia? La. Walitazamia shirika moja la kisiasa lilete ulimwengu mpya kama huo. “Lile tunaloliita Ushirika wa Mataifa leo,” kiongozi mmoja wa kanisa alisema, “ni sehemu isiyotenganika wala isiyoweza kuepukika ya imani yetu yote ya Kikristo na jitihada zetu katika ulimwengu.” Viongozi wa kanisa wa wakati huo hata waliinua Ushirika wa Mataifa kuwa “onyesho la kisiasa la Ufalme wa Mungu duniani.”
Kwa upande mwingine, kiongozi mmoja mwenye nguvu katika Ujerumani, Adolf Hitler, alipinga Ushirika wa Mataifa na katika miaka ya 1930 akaanzisha Utawala wa Nazi. Alidai kwamba Utawala huo ungedumu kwa miaka elfu moja na ungetimiza mambo ambayo Biblia yasema ni Ufalme wa Mungu tu waweza kutimiza. “Ninaanza na vijana,” Hitler alisema. “Nikiwa nao naweza kutengeneza Ulimwengu mpya.”
Hitler aliagiza stediamu kubwa sana ijengwe Nuremberg kwa ajili ya kuonyesha uwezo wa Nazi. Jambo la maana ni kwamba nguzo kubwa-kubwa 144 zilijengwa kwenye jukwaa lenye upana wa karibu meta 300. Kwa nini ziwe nguzo 144? Biblia yataja watu 144,000 ambao wangetawala na “mwana-kondoo” Yesu Kristo, na kwamba utawala wao ungekuwa wa miaka elfu moja. (Ufunuo 14:1; 20:4, 6) Ni wazi kwamba kujengwa kwa nguzo 144 katika stediamu ya Nuremberg hakukuwa aksidenti tu ya hesabu, kwa sababu vichapo vingi vimeonyesha jinsi maofisa wa Nazi walivyotumia lugha na ishara za Biblia.
Matokeo ya jitihada za wanadamu kutimiza jambo ambalo Biblia yasema litatimizwa na Ufalme wa Mungu pekee yalikuwa nini?
Kushindwa kwa Jitihada za Mwanadamu
Historia yathibitisha wazi kwamba Ushirika wa Mataifa lilishindwa kuleta ulimwengu mpya wenye amani. Shirika hilo lilianguka wakati mataifa yalipojiingiza katika Vita ya Ulimwengu ya 2. Na zaidi, baada tu ya miaka 12, ule Utawala wa Nazi ulikuwa umeanguka ukawa magofu. Shirika hilo lilishindwa kabisa, likawa aibu kubwa kwa familia ya kibinadamu.
Katika historia yote, jitihada za kibinadamu za kufanyiza ulimwengu mpya wenye amani zimeshindwa kufaulu. “Kila ustaarabu ambao umepata kuwapo ulianguka hatimaye,” akaonelea aliyekuwa Katibu wa Mambo ya Nchi wa U.S. Henry Kissinger. “Historia ni simulizi la jitihada ambazo hazikufua dafu, matamanio ambayo hayakutimizwa.”
Basi, vipi juu ya taratibu ya ulimwengu mpya ambayo viongozi wa ulimwengu wamekuwa wakitangaza karibuni? Kufyatuka kwa jeuri za kikabila kumefanya wazo lile la ulimwengu mpya kuwe dhihaka. Kwa kielelezo, katika Machi 6 iliyopita, mwandikaji wa gazeti William Pfaff alisema hivi kwa kudhihaki: “Taratibu ya ulimwengu mpya imefika. Inafanya kazi vizuri na kwa kweli ni mpya, ikitakasa ushambulizi, uchokozi na uonevu wa kikabila kuwa mwenendo wa kimataifa unaokubaliwa.”
Ule ugomvi na ukatili ambao umetokea tangu kuanguka kwa Ukomunisti unaogofya mno. Hata George Bush alikiri hivi muda mfupi kabla ya kuacha urais kirasmi katika Januari: “Baada ya muda, ulimwengu mpya waweza kuwa wenye kutisha kama ule wa kale.”
Je! Kuna Sababu ya Kutumaini?
Je! hiyo yamaanisha kwamba haiwezekani kuwa na hali nzuri? Je! ulimwengu mpya ni ndoto tu? Kwa wazi, wanadamu wameshindwa kufanyiza ulimwengu mpya. Lakini namna gani kuhusu ahadi ya Muumba ya kufanyiza ulimwengu mpya? Biblia yasema kwamba “kama ilivyo ahadi yake [Mungu], tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya.”—2 Petro 3:13.
Hiyo mbingu mpya inayoahidiwa na Mungu ni utawala mpya juu ya dunia. Utawala huo mpya ni Ufalme wa Mungu, serikali yake ya kimbingu ambayo Yesu alifundisha watu wasali kuihusu. (Mathayo 6:9, 10) Wakati huo serikali hiyo ya kimbingu itafanyizwa na Yesu Kristo na watawala-wenzi 144,000, na hiyo dunia mpya itakuwa ni jamii mpya ya watu. Naam, wataishi katika ulimwengu mpya wenye utukufu unaotegemeza utawala wa Mungu kwa uaminifu.
Serikali ya Ufalme wa Mungu itatawala juu ya ulimwengu mpya ulioahidiwa. Kwa hiyo ulimwengu mpya huu hautakuwa umeletwa na binadamu. “Ufalme wa Mungu haumaanishi kamwe hatua inayochukuliwa na wanadamu au mfumo wanaoanzisha,” yaeleza ensaiklopedia moja ya Biblia. “Ufalme huo ni tendo la kimungu, si utimizo wa kibinadamu wala si utimizo wa Wakristo waliojiweka wakfu.”—The Zondervan Pictorial Encyclopedia of the Bible.
Ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu utakuja kwa hakika. Waweza kutegemea ahadi ya kuja kwao kwa sababu ahadi hiyo inatolewa na “Mungu asiyeweza kusema uongo.” (Tito 1:2) Tafadhali, chunguza jinsi ulimwengu mpya wa Mungu utakavyokuwa.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Picha ya NASA