Ulimwengu Mpya U Karibu!
WANASIASA wengi wamesema mengi juu ya utengemano mpya wa ulimwengu wenye kufanyizwa na wao wenyewe. Wao husema juu ya kuuondolea ulimwengu hofu na vizuizi vya ushirikiano kati ya watu na mataifa. Lakini je, ni daraka la wanadamu kuleta ulimwengu mpya?
Ainabinadamu imekuwa na karne nyingi za kuimarisha ulimwengu wenye amani na usalama. Bila shaka, wengi wamekuwa wenye moyo mweupe sana katika juhudi hizo. Hata hivyo, bila kujali muundo wa serikali zinazowaziwa na wanadamu ili kutimiza miradi hiyo, maneno ya Biblia yamethibitika kuwa ya kweli: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
Ulimwengu Mpya Waahidiwa
Hata hivyo, Neno hilo hilo la Mungu lenye kupuliziwa roho laandaa uhakikisho kwamba kutakuwako ulimwengu mpya. Baada ya kutabiri mwisho wa mfumo wa mambo wa kale, mtume Mkristo Petro alitangaza rasmi hivi: “Twangojea mbingu mpya na dunia mpya ambayo imejaa uadilifu.”—2 Petro 3:10-13, HNWW.
Hiyo ni ahadi ya nani? Inatolewa si na mwingine yeyote ila na Yehova “aliye juu, juu ya nchi yote.” (Zaburi 83:18) Atatimiza yale ambayo wanadamu hawawezi. Ndiyo, Yehova Mungu atatokeza ulimwengu mpya. Lakini wakati gani?
Ulimwengu Mpya U Karibu Sana!
Kabla ya ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu haujawa jambo la halisi kabisa, lazima “ulimwengu,” au “mfumo wa mambo,” uliopo ufikie mwisho wao. Kuhusu hilo, wanafunzi wa Yesu Kristo waliuliza hivi: “Tuambie, mambo haya yatakuwa lini? na ni nini itakayokuwa ile ishara ya kuja kwako, na ya mwisho wa ulimwengu?” (Mathayo 24:3, King James Version) Kama vile Biblia ya New World Translation iliyo sahihi zaidi isemavyo, wafuasi wa Yesu waliuliza hivi: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”
Kwa kujibu, Yesu alitabiri sehemu nyingi za ile ishara ya kuwapo kwake kusikoonekana akiwa mtu wa kiroho katika mamlaka ya Ufalme wa kimbingu. (1 Petro 3:18) Kwa mfano, alisema hivi: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na matetemeko ya nchi mahali mahali.” Tangu “mwanzo wa utungu” katika 1914, “kizazi hiki” kilichoelekezewa na Yesu kimeona mwendelezo wa vita, upungufu wa chakula, na matetemeko ya dunia, yakiwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake kusikoonekana.—Mathayo 24:7, 8, 34.
Vita vimepata kizazi hiki kwa njia isiyo na kifani tangu mwaka wa 1914. Vita ya Ulimwengu 1 yakadiriwa kuwa iliua watu milioni 14. Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, askari na raia milioni 55 waliuawa. Tangu 1914 zaidi ya watu milioni 100 wameuawa vitani! Kwa uhakika, hiyo inatia alama sehemu ya ishara ya kuwapo kwa Yesu.
Upungufu wa chakula, uliotabiriwa pia na Kristo, ulikumba nchi nyingi baada ya kila ya hivyo vita vya ulimwengu. Yajapokuwa maendeleo ya kisayansi, karibu robo moja ya ulimwengu ina njaa leo. Kila mwaka, mamilioni ya watoto na wengine hufa kwa sababu ya utapiamlo (ugonjwa wa kukosa chakula kinachofaa mwilini). The World Book Encyclopedia yasema hivi: “Nchi zilizo nyingi za Afrika, Esia, na Amerika ya Kilatini, zinazositawi, hazina chakula cha kuwatosha watu wazo. Mamilioni katika nchi hizo huwa wenye njaa. Uzalishaji wa chakula au ununuzi kutoka nchi za nje unapopungua kwa sababu yoyote, njaa huenda ikatokea na maelfu au mamilioni ya watu huenda wakafa.”
Matetemeko ya dunia yameua idadi kubwa ya watu pindi ya kizazi hiki yakitia alama “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Makadirio ya wanaojeruhiwa katika matetemeko yanatofautiana. Lakini tangu 1914 uharibifu wenye kusababishwa na matetemeko umeongezeka sana kotekote duniani, nayo yameua mamia ya maelfu ya watu. Yorkshire Post likieleza juu ya mawili yayo tu, lilitaarifu hivi: “Katika 1920 tetemeko katika mkoa wa Jiangsu wa China liliua 180,000, na siku ya Julai 28, 1976, China ilipatwa na tetemeko lililokuwa baya zaidi ya yote katika historia yayo ya kisasa. Angalau watu 240,000 walikufa wakati jiji la Tangshan lililo kaskazini-mashariki lilipokuwa karibu libomolewe kabisa kwa tetemeko lenye kipimo cha 7.8 kwenye kipimio cha nguvu ya tetemeko cha Richter kisicho na kipimo thabiti.” Gazeti-habari hilo liliorodhesha matetemeko ya dunia makubwa mengineyo zaidi ya 30 katika karne ya 20.
Utendaji wa kuhubiri Ufalme ulitabiriwa pia kuwa mojawapo wa sehemu za ishara ya kuwapo kwa Yesu kusikoonekana. Aliambia wanafunzi wake wenye kuuliza: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kama vile Yesu alivyotoa unabii, kazi hiyo ya kuhubiri inafanywa sasa duniani pote katika nchi 212 na Mashahidi wa Yehova zaidi ya 4,000,000.
Utimizo wa unabii huu na mwingine mbalimbali wa siku zilizopo unathibitisha kwamba sisi kwa kweli tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Mbele yetu tu kuna “dhiki kubwa” iliyotabiriwa pia na Yesu Kristo. Ikiwa na upeo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni, italeta mwisho wa huu mfumo mwovu wa mambo uliopo. (Mathayo 24:21; Ufunuo 16:14-16) Kisha ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa utakuwa jambo halisi.a
Mibaraka Ambayo Wanadamu Hawawezi Kuleta
Wanasiasa hujigamba juu ya utengemano mpya wa ulimwengu wenye kufanyizwa na wao wenyewe. Lakini Yehova, Mungu wa mbingu na dunia, hakuwaomba kamwe wanadamu kuweka ulimwengu mpya mahali pa mfumo uliopo. Yeye mwenyewe atafanya hivyo kwenye siku na saa zinazojulikana na yeye peke yake. (Mathayo 24:34, 36) Mtume Yohana aliyezeeka alikuwa na mwono-mbele huu wa yale ambayo Mungu, si binadamu, atafanya:
“Kisha nikaona mbingu mpya na dunia mpya. Mbingu ile ya kwanza na dunia ile ya kwanza vilikuwa vimetoweka, nayo bahari pia haikuwako tena. Nikaona mji mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka kwa Mungu mbinguni. Ulikuwa umetayarishwa vizuri kama bibi arusi aliyepambwa tayari kukutana na mumewe. Kisha nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha enzi ikisema, ‘Tazama! Mungu amefanya makao yake kati ya watu. Atakaa kati yao, nao watakuwa watu wake, naye atakuwa Mungu wao. Yeye atayafuta machozi yao yote; maana hakutakuwako tena na kifo, wala uchungu, wala kilio, wala maumivu; maana ile hali ya kale imepita!’ Kisha yule aliyeketi juu ya kiti cha enzi akasema, ‘Tazama, nafanya yote mapya.’ Tena akaniambia, ‘Andika hili, maana maneno haya ni ya kuaminika na ya kweli!’”—Ufunuo 21:1-5, HNWW.
“Mbingu mpya” ni Ufalme wa kimbingu wa Yesu Kristo. “Dunia mpya” si tufe jingine la kidunia, bali ni jamii mpya ya watu juu ya sayari hii—wote wakiwa raia watiifu wa Ufalme wa Kristo, bila migawanyiko ya rangi, taifa, au lugha. (Linganisha Zaburi 96:1.) Mbingu na dunia za sasa zilizo za ufananisho—mfumo wa mambo wa Ibilisi pamoja na muundo wao wa kiserikali wenye kuongozwa na Shetani na roho waovu wake—utakuwa umeharibiwa. (1 Yohana 5:19) Ingawa bahari za kihalisi zitabaki, bahari ya ufananisho ya ainabinadamu isiyotulia yenye uovu haitakuwako. Watawala wa kimbingu wenzi wa Yesu ndio huwa Yerusalemu Mpya na kwa ushirikiano naye huwa tengenezo kuu ambalo litaongoza jamii ya kibinadamu yenye uadilifu. Mungu ‘atafanya makao yake’ pamoja na ainabinadamu watiifu kwa kuwakilishwa wakati wanapopatanishwa naye kikamili kupitia Kristo pindi ya Siku ya Hukumu ya miaka elfu.—Ufunuo 14:1-4; 20:6.
Chini ya utawala wa Ufalme kutakuwa sababu nyingi za furaha. Uchungu, kilio, na maumivu yanayotokana na ugonjwa, kihoro, na mambo kama hayo yatakuwa maono ya zamani. Hata kifo kilichoenea kwa ainabinadamu kutoka kwa mzazi wetu wa kwanza, Adamu mwenye dhambi, hakitakuwapo tena. (Warumi 5:12) Ni shangwe iliyoje itakayoenea wakati hiki kisababishi cha machozi ulimwenguni pote kitakapoondolewa milele!
Si wanadamu wanaokufa bali ni Mungu mwenyewe atoaye uhakikisho kuhusu mibaraka hiyo. Yeye ndiye asemaye hivi: “Tazama, nafanya yote mapya.” Naam, na Yehova Mungu alimwambia mtume Yohana hivi: “Andika hili, maana maneno haya ni ya kuaminika na ya kweli.”
Mahitaji ya Msingi Yatoshelezwa Kikamili
Katika ulimwengu mpya wenye kufanywa na Mungu, dunia itakuwa paradiso hatimaye. Hiyo ni hakika, kwa kuwa Yesu aliahidi mtenda mabaya mwenye kutubu aliyetundikwa kando yake: “Kweli kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Kati ya hali za kiparadiso, mahitaji ya kibinadamu kama vile chakula na nyumba yataandaliwa kikamili.
Upungufu wa chakula unagharimu mamilioni ya watu leo. Hata jitihada za kulisha walio na njaa ziwe bora jinsi gani, pupa na mambo mengine huzuia wanadamu wasisuluhishe matatizo kama hayo. Kwa mfano, Saturday Star, gazeti-habari la Johannesburg, Afrika Kusini, linaripoti hivi: “Magombano ya kisiasa, ongezeko la bei za fueli na uchovu wa ujumla kwa ajili ya mapigano ya Afrika ambayo huonekana hayaishi kamwe huunganika kuchelewesha msaada . . . Katika Sudan, mojawapo kati ya nchi zilizoathiriwa vibaya zaidi kwa njaa, kati ya watu milioni 5 na milioni 6 wanakabili njaa katika 1991.” Lakini njaa itasahauliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. Chini ya utawala wa Ufalme “kutakuwako na nafaka tele juu ya dunia; na juu ya milima kutakuwako mfuriko.”—Zaburi 72:16, NW.
Nyumba ni uhitaji mwingine wa binadamu ambao hautimizwi vya kutosha kwa wengi katika siku zetu. Mamilioni huishi katika vibanda vibovu-vibovu au hawana nyumba yoyote kabisa. Kulingana na The New York Times, katika nchi moja ya Mashariki, “kwenye shirika la elektroniki . . . , waajiriwa wenye umri wa miaka 20 hukabili orodha ya kungojea ya miaka 73 ili kupata nyumba,” na ripoti ya serikali inaonyesha kwamba ni lazima watu fulani waishi katika “bohari, maofisi au hata vyoo.” Lakini itakuwa tofauti jinsi gani katika ulimwengu mpya! Katika Paradiso ya wakati ujao, “watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:21, 22.
Matatizo ya kiikolojia (kimazingira) yatatoweka katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa. Uchafuzi wa hewa unaotisha uhai na kuharibu mavuno hautakuwapo tena. Uchafuzi na uharibifu wa makazi unaohatarisha jamii nyingi za mimea na wanyama wakati huo hautakuwa tisho. Na mambo kama upungufu wa tabaka la gesi ozoni hayatahatarisha uhai duniani. Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu atasuluhisha matatizo hayo yote, kwa kuwa Neno lake latuhakikishia kwamba hivi karibuni ‘ataangamiza wale wanaoangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18, NW.
Katika ulimwengu mpya, vita vitakuwa pia jambo la zamani lakini si kwa sababu wanasiasa wamefaulu katika kuondolea mataifa silaha. Bali, Mungu atatimiza yale ambayo watawala wa kisiasa wameshindwa kutimiza. Ataletea ainabinadamu watiifu amani kulingana na maneno haya ya mtunga zaburi: “Njooni myatazame matendo ya BWANA [Yehova, NW], jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” (Zaburi 46:8, 9) Katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa ambao u karibu sana, watu hawatapigana vita tena bali wataonea shangwe amani na usalama wa kweli.—Mika 4:2-4.
Je! Utakuwako?
Waweza kuwa na uhakika katika ulimwengu mpya unaoahidiwa na Yehova Mungu. Hasemi uwongo. (Waebrania 6:17, 18) Neno lake, Biblia, ni kweli, na yale inayoahidi hutukia sikuzote.—Yohana 17:17.
Habari njema ya mibaraka ya ajabu kwa ainabinadamu watiifu ni jambo ambalo Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushiriki pamoja na watu wote wenye mioyo yenye kufuatia haki. Unapaswa kufanya jitihada sasa ili ujipatie maarifa ya kusudi la kimungu, na kuziamini ahadi nzuri ajabu zinazopatikana katika Maandiko Matakatifu. Mwendo huo waweza kuongoza kwenye uhai usio na mwisho, kwa maana Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Kisha utapendelewa kuonea shangwe nyakati za furaha zilizo mbele tu, kwa maana ulimwengu mpya wa Mungu u karibu!
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura 17 na 18 za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.