Jitihada Inayoendelea ya Kutafuta Utengemano Mpya wa Ulimwengu
“HAKUNA ramani zozote za kutuongoza mahali tuendapo, kwenye huo ulimwengu mpya uliobuniwa na sisi wenyewe. Ulimwengu unapofikiria yaliyotukia wakati wa miaka tisini (90) ya vita, ya ugomvi, ya shuku, acheni nasi pia tufikirie yaliyo mbele—kwenye karne mpya, na mileani mpya, ya amani, uhuru na usitawi.”
George Bush, rais wa U.S. alitoa maelezo hayo siku ya Januari 1, 1990. Ndipo katika ujumbe kama huo, rais wa Urusi Mikhail Gorbachev akashauri kuwe na ushirikiano katika miaka ya 1990 ili kuondolea “ulimwengu hofu mbalimbali na shuku, silaha zisizohitajiwa, mawazo ya kisiasa na mafundisho ya kijeshi ya kizamani, na vizuizi visivyo vya asili kati ya watu na nchi mbalimbali.” Ndivyo lilivyoripoti Mainichi Daily News la Japan la Januari 3, 1990.
Kwa wazi, matazamio yalikuwa makubwa. Mwaka mmoja baadaye yalikuwa hivyo bado. Katika ujumbe wa Taifa la Muungano siku ya Januari 29, 1991, Rais Bush alitaja vita katika Ghuba ya Uajemi akasema hivi: “Kilicho hatarini ni zaidi ya nchi ndogo moja [Kuwait], ni wazo kubwa—utengemano mpya wa ulimwengu ambapo nchi tofauti-tofauti zinaunganishwa kwenye mradi mmoja ili kutimiza tamaa za ainabinadamu: amani na usalama, uhuru na hali ambapo sheria inatawala.”
Si Utafutaji Usio na Matatizo
Matatizo mengi yanazuia mwanadamu katika utafutaji wake wa utengemano mpya wa ulimwengu. Kwa hakika vita vya silaha huzuia. Gazeti Time la Januari 28, 1991, likirejezea uhasama uliokuwa ukiendelea wakati huo katika Iraq na Kuwait, lilisema hivi: “Mabomu yalipokuwa yakianguka na makombora kurushwa, matumaini ya utengemano mpya wa ulimwengu yalipotea, ukabaki ukosefu wa utengemano ule ule.” Jarida hilo likaongeza hivi: “Mtu yeyote asiote kwamba utengemano mpya wa ulimwengu unaoonewa fahari sana unawezekana au hata kwamba u karibu.”
Ushirikiano wa kimataifa haujatimizwa kamwe, na hilo huzuia jitihada za wanadamu za kusimamisha utengemano mpya wa ulimwengu. Katika ripoti iliyotokea katika kichapo The World & I (Januari 1991), wanachuo walichunguza “sera za kigeni zilizokuwa zikizuka za mataifa yenye nguvu na matokeo ambayo yamkini kuupata utengemano mpya wa ulimwengu.” Mhariri alimalizia hivi: “Historia yadokeza kwamba mstari ulio kati ya vita na amani ni mwembamba wakati hali ziko njema kabisa. Ushirikiano wa kimataifa, hasa kati ya mataifa makubwa, ni wa maana sana ili kuweko kufanikiwa katika kumaliza Vita Baridi na kuleta utengemano mpya wa ulimwengu.”
Matatizo ya kimazingira pia huzuia utengemano mpya wa ulimwengu ambao wengi huwazia. Katika State of the World 1991 (ripoti ya Worldwatch Institute), Lester R. Brown alisema hivi: “Hakuna yeyote awezaye kusema kwa uhakika jinsi utengemano mpya utakavyokuwa. Lakini ikiwa tutafanyiza wakati ujao wenye kutumainiwa kwa ajili ya kizazi kinachofuata, basi jitihada kubwa inayohitajiwa ili kupindua hali mbaya ya kimazingira ya sayari itachukua sehemu kubwa ya mambo ya ulimwengu kwa makumi mengi ya miaka inayokuja.” Ripoti hiyo ilionyesha kwamba uchafuzi wa hewa ulikuwa “umefikia usawa wa kutisha afya katika mamia ya majiji na usawa wa kuharibu mavuno katika nchi nyingi mbalimbali.” Iliongezea hivi: “Idadi ya wanadamu wanaokalia sayari iongezekapo, idadi ya jamii za mimea na wanyama hupunguka. Uharibifu wa mazingira na uchafuzi unapunguza utofauti-tofauti wa kibayolojia wa dunia. Kupanda kwa kadiri ya hali-joto na upungufu wa tabaka la gesi ozoni kungeweza kuongezea hasara.”
Kwa wazi, basi, jitahada ya mwanadamu ya kutafuta utengemano mpya wa ulimwengu imejaa matatizo. Je! utafutaji huo utathibitika kuwa wenye kufanikiwa? Je! kwaweza kusemwa kwamba ulimwengu mpya u karibu? Ikiwa ndivyo, utaletwaje?