Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 3/1 kur. 3-5
  • Mipango ya Mwanadamu kwa Ajili ya Usalama wa Kimataifa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mipango ya Mwanadamu kwa Ajili ya Usalama wa Kimataifa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mpango Mkuu wa Mwanadamu
  • Vita Baridi
  • “Enzi ya Baada ya Vita Baridi”
  • Ni Nini Kinachotendeka Kwenye Umoja wa Mataifa?
    Amkeni!—1992
  • Kuna Wakati Ujao Gani kwa Vita?
    Amkeni!—1999
  • Je! Amani ya Ulimwengu Yatazamiwa Kuwa Karibu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Umoja wa Mataifa—Njia Bora Zaidi?
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 3/1 kur. 3-5

Mipango ya Mwanadamu kwa Ajili ya Usalama wa Kimataifa

“Mambo hayo yote yanapoisha, tunataka tuwe waponyaji. Tunataka kufanya lile tuwezalo ili kuuleta ule ambao kwa hakika ninaweza kuita utaratibu wa ulimwengu mpya.”—Rais wa U.S. George Bush, Januari 1991, muda mfupi baada ya vita pamoja na Iraq kuanza.

“Wazo la Rais Bush kuhusu Utaratibu wa Ulimwengu Mpya hukazia umaana wa kanuni ya sheria na ile imani kwamba mataifa yana daraka la pamoja kwa ajili ya uhuru na haki. Vita Baridi ikiwa inaisha, enzi mpya inatokea.”—Balozi wa U.S. katika Australia, Agosti 1991.

“Usiku huu, nionapo matukio ya demokrasia yakisitawi kotekote duniani, labda—labda tuko karibu zaidi na ule ulimwengu mpya kuliko wakati mwingine wowote.”—Rais wa U.S. George Bush, Septemba 1991.

WATAWALA wengi wa ulimwengu wanasema, kama Rais Bush, wakiwa na matazamio mazuri kuhusu wakati ujao. Je! wana sababu nzuri ya kuwa na matazamio mazuri? Je! matukio ya tangu Vita ya Ulimwengu 2 hutegemeza matazamio hayo mazuri? Je! wewe wafikiria wanasiasa waweza kuleta usalama wa kimataifa?

Mpango Mkuu wa Mwanadamu

“Katika miaka miwili ya mwisho ya vita ya ulimwengu ya pili,” ikaeleza programu ya televisheni Goodbye War, “watu zaidi ya milioni moja walikuwa wanauawa kila mwezi.” Wakati huo, mataifa waliona uhitaji wa hima kuwa na mpango ambao ungezuia vita kama hiyo isitukie tena. Vita hiyo ilipokuwa ingali inaendelea, wawakilishi wa mataifa 50 walitokeza mpango mkuu zaidi kwa ajili ya usalama wa kimataifa uliopata kubuniwa na mwanadamu: Hati ya Katiba ya Umoja wa Mataifa. Dibaji ya Hati ya Katiba hiyo ilionyesha azimio la “kuokoa vizazi vijavyo kutokana na pigo la vita.” Wale ambao wangekuwa washiriki wa Umoja wa Mataifa walipaswa “waunganishe nguvu [zao] ili kudumisha amani na usalama wa kimataifa.”

Siku 41 baadaye, ndege moja iliangusha bomu la atomu Hiroshima, Japani. Hilo lililipuka juu ya kitovu cha jiji hilo, likiua watu zaidi ya 70,000. Mlipuko huo, na ule uliofuata siku tatu baadaye juu ya Nagasaki, ulikomesha kwa mafanikio vita pamoja na Japani. Kwa kuwa Ujerumani iliyokuwa imejiunga na Japani ilikuwa imejisalimisha katika Mei 7, 1945, Vita ya Ulimwengu 2 hivyo ikaisha. Hata hivyo, je, huo ulikuwa mwisho wa vita vyote?

La. Tangu Vita ya Ulimwengu 2, ainabinadamu imeona vita vidogo vidogo zaidi ya 150 ambavyo vimeua watu zaidi ya milioni 19. Kwa wazi, mpango mkuu wa UM haujaleta bado usalama wa kimataifa. Ni nini kilichoharibu mambo?

Vita Baridi

Wale waliopanga UM hawakutazamia ushindani uliositawi upesi kati ya nchi zilizoungana katika Vita ya Ulimwengu 2. Nchi nyingi ziliunga mkono pande tofauti-tofauti katika mapambano hayo ya utawala, yaliyokuja kuitwa Vita Baridi na yaliyokuwa, kwa sehemu, mapambano kati ya Ukomunisti na ubepari. Badala ya kuunganisha nguvu zao ili kukomesha vita, vikundi hivyo viwili vya mataifa viliunga mkono pande zenye kushindana katika mapigano ya maeneo na katika njia hiyo walipigana katika Esia, Afrika, na Visiwa vya Amerika.

Katika mwisho-mwisho wa miaka ya 1960, Vita Baridi ilianza kupoa. Kupoa huko kulikuwa na upeo katika 1975 wakati Nchi 35 zilipotia sahihi ule uitwao Mwafaka wa Helsinki. Miongoni mwa nchi zilizoshiriki mlikuwa Urusi na United States, pamoja na nchi za Ulaya zilizojiunga nazo. Nchi zote ziliahidi kufanyia kazi “amani na usalama” na “kuepuka . . . kutisha au kutumia nguvu dhidi ya haki ya kieneo au uhuru wa kisiasa wa Nchi yoyote, au kutenda kwa njia nyingine yoyote isiyopatana na makusudi ya Umoja wa Mataifa.”

Lakini mawazo hayo hayakuwa na matokeo. Kufikia miaka ya mapema ya 1980, ushindani huo kati ya mataifa yenye uwezo mkubwa ukawa moto moto tena. Hali ikawa mbaya sana hivi kwamba katika 1982 katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa aliyetoka kuchaguliwa, Dkt. Havie Peres di Kweya, alikiri kushindwa kwa shirika lake na akaonya juu ya “mchafuko mpya wa kimataifa.”

Hata hivyo, leo, katibu mkuu wa UM na viongozi wengine huonyesha matazamio mazuri. Ripoti za habari hurejezea “enzi ya baada ya Vita Baridi.” Badiliko hilo lilitokeaje?

“Enzi ya Baada ya Vita Baridi”

Jambo moja la maana lilikuwa mkutano mmoja wa Baraza la Usalama na Ushirikiano katika Ulaya la mataifa 35. Katika Septemba 1986 walitia sahihi ile iitwayo Hati ya Stockholm, wakithibitisha tena ushikamano wao kwa ule Mwafaka wa Helsinki wa 1975.a Hiyo Hati ya Stockholm hutia ndani kanuni nyingi za kuongoza usimamizi wa utendaji mbalimbali wa kijeshi. “Matokeo ya miaka mitatu iliyopita yanatia moyo na yale ambayo yametimizwa yanaanza kupita masharti yaliyoandikwa ya Hati ya Stockholm,” ikaripoti SIPRI (Taasisi ya Uchunguzi wa Amani ya Kimataifa Stockholm) katika Yearbook 1990 yayo.

Halafu, katika 1987, yale mataifa yenye uwezo mkubwa yakafikia mwafaka wa kutokeza uliohitaji waharibu makombora yao yote ya kurushwa kutoka chini yaliyo na uwezo wa kwenda umbali wa kati ya kilometa 500 na 5,500. “Kuharibu kihalisi makombora ya kurushwa na vyombo vya kuyarusha ni kama vile kumeratibiwa na masharti ya maafikiano yanafuatwa ipasavyo na kila upande,” yasema SIPRI.

Hatua nyinginezo zimechukuliwa ili kupunguza hatari ya vita ya nyukilia. Kwa mfano, katika 1988 mataifa yenye uwezo mkubwa yalitia sahihi mwafaka mmoja kuhusu “makombora yenye uwezo wa kusafiri kati ya mabara na makombora yanayorushwa kutoka manowari za majini.” Kabla ya kurusha silaha hizo, ni lazima kila upande ujulishe ule mwingine “kabla ya saa zisizopungua 24, kuhusu tarehe iliyopangwa, mahali pa kurushia, na eneo linalolipuliwa.” Kulingana na SIPRI, maafikiano kama hayo “karibu hufuta uwezekano wa matukio ya mahali fulani kuzidi hadi kuwa vita ya nyukilia ya ulimwenguni pote.”

Wakati ule ule, mipango ya kufanyia maendeleo usalama wa kimataifa ilizidi kufanikiwa. Katika Mei 1990, wakati wa mkutano wa yale mataifa yenye uwezo mkubwa katika Washington, D.C., rais wa Urusi Mikhail Gorbachev alipendekeza kwamba vikundi viwili vya mataifa ya Ulaya vitie sahihi mkataba wa amani. Katika Julai, yale mataifa 16 ya Magharibi ya NATO (Shirika la Mkataba Atlantiki Kaskazini) yalikutana katika London. Itikio lao kwa pendekezo la Mikhail Gorbachev lilikuwa kwamba kila upande utie sahihi “tangazo rasmi la pamoja ambalo katika hilo tunataarifu kwa heshima kwamba sisi si maadui tena na tunathibitisha nia yetu ya kuepukana na tisho au matumizi ya nguvu.” Kichwa cha ukurasa wa juu wa gazeti moja la habari la Afrika kilieleza hilo kuwa “Hatua Kubwa Sana Kuelekea Amani ya Ulimwengu.”

Kisha, muda mfupi kabla ya mkutano wa yale mataifa yenye uwezo mkubwa katika Helsinki, Finlandi, mnenaji mmoja wa serikali wa U.S. alisema kwamba “uwezekano wa vita [katika Mashariki ya Kati] unatokeza mpango mpya wa kikundi kwa ajili ya amani ya ulimwengu.” Amani ilipata kikwazo wakati Iraq iliposhambulia Kuwait na vita hiyo ilitisha kuenea katika nchi zote za Mashariki ya Kati. Lakini chini ya mamlaka ya Umoja wa Mataifa, jeshi la kimataifa lenye kuongozwa na United States lilifukuza majeshi yenye kushambulia kurudi nchi yayo yenyewe. Umoja wa kusudi wa kimataifa ulioonyeshwa katika vita hiyo ulitia moyo wengine watumaini kwamba enzi mpya ya ushirikiano ilikuwa imefika.

Tangu wakati huo, matukio ya ulimwengu yamesitawika hata zaidi. Hasa, hali ya mahali palipokuwa Urusi wakati mmoja imebadilika sana. Majimbo ya Baltiki yaliruhusiwa yatangaze uhuru wayo, na jamhuri nyinginezo katika Urusi zikafuata mfano huo. Ushindani wenye jeuri wa kikabila ulitokea katika nchi zilizoonekana kuwa na umoja chini ya utawala wa Kikomunisti wenye kuongozwa kutoka mahali pamoja. Wakati ule ule, nchi za Ulaya Mashariki ziliendea adui yazo ya zamani zikitafuta msaada ili kukinga matatizo makubwa ya kiuchumi.

Mabadiliko hayo makubwa katika hali ya kisiasa ya ulimwengu yametolea shirika la Umoja wa Mataifa nafasi ya kutenda. Kuhusu jambo hilo, gazeti The New York Times lilisema: “Kupungua kwa uvutano mbalimbali ulimwenguni pote na ile roho mpya ya ushirikiano kati ya United States na Urusi kwaweza kumaanisha, daraka jipya lenye nguvu zaidi katika mambo ya kimataifa kwa lile shirika la ulimwengu.”

Je! wakati umewadia wa shirika hilo lenye umri wa miaka 47 kujisimamia? Je! kwa kweli tunaingia katika hali ambayo United States iliita “karne mpya, na mileani mpya, ya amani, uhuru na ufanisi”?

[Maelezo ya Chini]

a Mwafaka huo ni wa kwanza na wa maana zaidi wa ule mfululizo wa maafikiano yaliyotiwa sahihi katika Helsinki na Kanada, United States, Urusi, na nchi nyingine 32. Jina rasmi la mwafaka huo mkuu ni Sheria ya Mwisho ya Baraza la Usalama na Ushirikiano katika Ulaya. Mradi walo wa msingi ulikuwa ni kupunguza uvutano wa kimataifa kati ya Mashariki na Magharibi.—World Book Encyclopedia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki