Umoja wa Mataifa—Njia Bora Zaidi?
Utangulizi wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa waonyesha malengo haya mema: “Sisi watu wa Umoja wa Mataifa tukiwa tumepiga moyo konde kuokoa vizazi vijavyo kutokana na janga la vita, ambalo kwa mara mbili maishani mwetu limeleta huzuni isiyoelezeka kwa ainabinadamu, . . . na [tukitamani] kuunganisha nguvu zetu ili kudumisha amani na usalama wa kimataifa, . . . tumeazimia kuunganisha jitihada zetu ili tutimize malengo hayo.”
Je! Umoja wa Mataifa ‘ulitimiza malengo hayo’? Je! uliweza kuyafanya mataifa yaunganishe nguvu zao na kudumisha amani na usalama? La, siyo kufikia sasa, ingawa UM umejaribu kweli kuwa njia bora zaidi kuliko Ushirika wa Mataifa ulivyokuwa. Hata hivyo, kizazi kilichoona kuanzishwa kwao katika 1945 kimekumbwa na vita, maasi, uvamizi, mapinduzi, na uchokozi katika sehemu nyingi za dunia tangu wakati huo. Na jeuri hiyo ilihusisha mengi ya mataifa ambayo yalikuwa yameazimia “kudumisha amani na usalama wa kimataifa.”
Bado Siyo Njia Bora Zaidi
Hata hivyo, wachambuzi ambao hulaumu Umoja wa Mataifa kwa kukosa kukomesha ole hizi huenda wakawa wanasahau jambo la maana—nguvu za shirika lolote hutegemea juu ya uwezo linaopewa na mkataba walo na juu ya washirika walo kutimiza ahadi ya kutekeleza wajibu wao mbalimbali chini ya mkataba huo. Kwanza kabisa, Mkataba wa Umoja wa Mataifa hauweki UM uwe serikali ya ulimwengu yenye uwezo mkuu juu ya mataifa yote yaliyo washiriki.
Fungu la 2(7) huagiza hivi: “Hakuna chochote kilicho katika Mkataba wa sasa kitakachoupa Umoja wa Mataifa mamlaka ya kuingilia mambo ya ndani ya taifa lolote.” UNCIO (Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Kuzungumzia Ushirikiano Mzuri), uliokutana katika San Francisco kuanzia Aprili 25 hadi Juni 26, 1945, ili kukamilisha mkataba, ulionelea kwamba ni jambo la maana “kuhakikisha kwamba Umoja wa Mataifa ukitegemea hali za ulimwengu za wakati uliopo haupaswi kuvuka mipaka inayokubalika au kukiuka sheria zinazopasa.”
Je! umeona fungu hilo la maneno lenye kuweka mipaka, “ukitegemea hali za ulimwengu zenye kuenea pote”? Ikiwa hali hizo zingebadilika, UNCIO ilidai kwamba pitisho hilo lingeweza kukuzwa “kwa kadiri hali ya ulimwengu, maoni ya umma ulimwenguni, na utegemeano hakika wa ulimwengu wafanya lihitajike na kufaa.”
Kusudi lililokatibiwa la Umoja wa Mataifa la kudumisha “amani na usalama wa kimataifa” hutaja lengo lenye kutamanika kwa ainabinadamu. Kwa kweli ulimwengu ungekuwa salama zaidi ikiwa mataifa yangetii Fungu la 2(4) la Mkataba wa UM: “Washiriki wote wataepuka . . . kutisha au kutumia nguvu dhidi ya nchi fulani au uhuru wa kisiasa wa taifa lolote.” Lakini ubinafsi wa mataifa washiriki umelemaza mara nyingi jitihada za UM kuelekea kutimiza kusudi lao. Badala ya kutekeleza ahadi zao kwa UM za “kusuluhisha magomvi yao ya kimataifa kwa njia ya amani,” mataifa au miungano mizima ya mataifa imegeukia vita mara nyingi, ikidai kwamba ‘jambo lenyewe lilihusu mambo yao ya ndani tu.’—Fungu la 2(3,7).
Si kwamba tu mataifa yamepuuza taratibu za amani za UM bali yamedharau na yakakaidi waziwazi maagizo ya shirika hilo ya kusuluhisha mahitilafiano. Na wakuu wa serikali hizo mara nyingi wamesimama kwenye mimbari ya UM na kutoa hotuba ndefu wakijaribu kutetea matendo yao ya uchokozi. Mara nyingi uepaji huu wa maagizo yaliyowekwa kuwa sheria ya kudumisha amani umelemeza UM katika nyakati za hatari na kuharibu sana sifa yao. Maafisa wa UM wanaoshiriki mikutano hiyo huwa mara nyingi wanahangaika kiakili. Mwishowe, mazungumzo kama hayo mara nyingi huthibitika kuwa maneno ya hali ya juu tu ambayo hujaribu kupuuza au kutetea jeuri na umwagaji wa damu unaotokea. Haishangazi basi kuwa Katibu-Mkuu wa UM Javier Pérez de Cuéllar alisema kwamba UM “huonwa kama mnara wa Babeli na vikundi mbalimbali vya watu na kama tu mahali pa mijadala ambayo mara nyingi haifanikiwi.”
Kuna sababu nyingine kwa nini UM umepata ugumu wa kujithibitisha kwamba huo ndiyo njia bora hiyo. Ulipoanza kutenda katika Oktoba 24, 1945, “hakuna njia yoyote ya ustadi ya kutafuta amani iliyotolewa,” akasema Pérez de Cuéllar. Bila hilo, Umoja wa Mataifa ungewezaje kuwa uwezo thabiti wa kuleta amani ya ulimwengu kama ulivyokusudiwa uwe?
Ni Amani ya Aina Gani Ungeweza Kupata?
Pérez de Cuéllar ajibu: “Amani haitaleta mwisho wa mahitilafiano yote. Itafanya tu mahitilafiano yaweze kudhibitiwa kwa njia nyingine mbali na utumizi wa nguvu au matisho. . . . Umoja wa Mataifa unataka tuwe na malengo hayo akilini.” Hivyo amani pekee ambayo UM waweza kupata ni kudhibiti jeuri.
Je! kweli hiyo ni amani yenye usalama? Ni kweli, “kuwa mshiriki katika Umoja wa Mataifa ni wazi kwa . . . mataifa yote yenye kupenda amani.” (Fungu la 4(1)) Lakini je! taifa lenye kupenda amani linapoungana na UM litadumu likiwa hivyo? Serikali huwa zabadilika, na watawala wapya huleta sera mpya. Namna gani ikiwa mshiriki ageuka kuwa mwasi, akiwa na malengo ya kutukuza taifa na tamaa zenye pupa ya kunyakua maeneo ya wengine? Na namna gani ikiwa anaanza kujipatia silaha za nyukilia na za kikemia? Umoja wa Mataifa ungekuwa sasa na kombora linalohesabu wakati kwa kusonga mbele hadi likalipuke. Na bado, kama vile matukio ya hivi karibuni katika Mashariki ya Kati yameonyesha, badiliko kama hilo la matukio labda ndilo jambo linalohitajiwa hasa kuyafanya mataifa yaimarishe UM ili uondoe tisho hilo kwa usalama wao.
Je! Mataifa Yaweza Kuifanya Iwe Njia Bora Zaidi?
Sasa mataifa yanatambua sana zaidi ya wakati uliopita, kile UNCIO ulichokiita “utegemeano hakika wa ulimwengu.” Hakuna taifa linaloweza kuishi kwa kujitegemea lenyewe tu. Mataifa yote ni washirika wa jumuiya moja ya kimataifa. Yote yanapambana na mfululizo wa matatizo ya kawaida: uchafuzi mbaya wa mazingira, umaskini, maradhi yenye kudhoofisha, biashara haramu ya dawa za kulevya katika kila bara kuu, uvamizi haramu, silaha za hali ya juu za kinyukilia katika mabohari ya mataifa yanayoongezeka. Mambo hayo yanalazimisha mataifa ama yatafute amani na usalama chini ya mwelekezo wa Umoja wa Mataifa au sivyo yote yajiue.
Aliyekuwa waziri wa Urusi wa mambo ya nchi za kigeni Shevardnadze alisema: “Umoja wa Mataifa waweza kutenda kwa uwezo kama ungepewa mamlaka na washiriki walo, kama mataifa yanakubali kwa hiari na kwa muda kuutolea sehemu ya haki zao za kitaifa na kuukabidhi jukumu la kushughulikia mambo fulani kwa manufaa ya walio wengi.” Aliongezea hivi: “Ni kwa njia hiyo pekee ndiyo tunaweza kufanya muhula wa amani uwe wa kudumu na usiobadilika.”
Kama hilo lingeweza kufanywa, basi cheo cha UM cha mamlaka kingeuwezesha kushutumu taifa lolote linalotisha amani ya ulimwengu. Ukiwa wenye nguvu nyingi mikononi mwayo, ungeweza kukomesha wenye uchokozi kwa uthabiti na haraka. Lakini Je! mataifa washiriki wa UM watakuja kuupa mamlaka hiyo, ‘kuupa majeshi yao, msaada na vifaa’ ili kupata amani? (Fungu 43(1)) Huenda wangefanya hivyo—kama jambo fulani la hatari lingetisha kuharibu msingi ule wenyewe enzi zao za kitaifa zinautegemea. Ikiwa mataifa yataona kwamba ‘kuunganisha nguvu zao ili kudumisha amani na usalama’ chini ya mwelekezo wa UM kwaweza kuondoa matisho kama hayo, huenda yakauheshimu zaidi.
Labda unajiuliza, ‘Je, sehemu ambayo UM ulishiriki katika mzozo wa Ghuba ya Uajemi ilikuwa mwanzo wa jambo hilo?’ Ingeweza kuwa hivyo. Mataifa mengi yalikumbwa na uwezekano wa anguko lenye msiba la uchumi wao. Na kama uchumi wao uliofumanika ungeanguka, ndivyo na wa ulimwengu mzima. Hivyo mataifa yalikuja pamoja chini ya Umoja wa Mataifa. Baraza la Usalama liliidhinisha mfululizo wa maazimio ya UM ili kukomesha mzozo huo kwa amani, na wakati hilo liliposhindwa, likaunga mkono azimio la UM la kutumia nguvu katika Ghuba.
Waziri wa Mambo ya Serikali wa U.S. James Baker, akiomba kuwe na azimio hilo, alisema: “Historia sasa imetupatia nafasi nyingine. Vita baridi ikiwa tayari imekwisha, sasa tuna nafasi kujenga ulimwengu uliotarajiwa kuonwa na waanzilishi wa . . . Umoja wa Mataifa. Tuna nafasi ya kufanya hili Baraza la Usalama na Umoja wa Mataifa huu kuwa vifaa vya kweli kwa amani na haki toka upande huu wa tufe hadi ule mwingine. . . . Ni lazima tutimize lengo letu sote la ulimwengu wenye amani na haki kufuatia ile vita baridi.” Kuhusu mjadala juu ya utumizi wa nguvu katika Ghuba alisema hivi: “Mimi ninafikiri [huo utahesabiwa] kuwa moja la [matukio] yenye maana zaidi katika historia ya Umoja wa Mataifa. Kwa kweli itachukua sehemu kubwa katika kuamua wakati ujao wa shirika hili.”
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwa dhati kwamba Umoja wa Mataifa utakuwa na daraka kubwa katika matukio ya ulimwengu ya hivi karibuni sana. Hakuna shaka kwamba matukio hayo yatakuwa ya kutazamisha sana. Na matokeo yatakuwa na uvutano mkubwa sana kwa maisha yako. Tunakusihi uwaombe Mashahidi wa Yehova katika ujirani wako kwa habari zaidi kuhusu jambo hilo. Biblia huonyesha wazi kwamba Umoja wa Mataifa utapewa uwezo na mamlaka hivi karibuni. Halafu UM utafanya mambo ya kustaajabisha sana ambayo yaweza kukustaajabisha. Na utasisimuka kujua kwamba bado kuna njia nyingine bora zaidi iliyo karibu sana ambayo kwa hakika italeta amani na usalama wa milele!
[Picha katika ukurasa wa 9]
Guido de Marco, msimamizi wa Baraza Kuu la UM (kulia), na Katibu-Mkuu Pérez de Cuéllar katika mkutano wa 45 wa Baraza hilo
[Hisani]
UN photo 176104/Milton Grant