Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 7/8 kur. 22-25
  • Ziara ya Papa kwa UM—Ilitimiza Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ziara ya Papa kwa UM—Ilitimiza Nini?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ziara ya Papa kwa UM—Ilitimiza Nini?
  • Kwa Nini Alizuru?
  • Amani ya Kweli—Kutoka Chanzo Gani?
  • Hiyo Ziara—Ilikuwa na Uvutano Gani?
  • Je, Kanisa Liko Katika “Hatua Muhimu ya Kukata Shauri”?
  • Umoja wa Mataifa—Njia Bora Zaidi?
    Amkeni!—1992
  • Fumbo Lenye Kutia Hofu Lafumbuliwa
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Hakuna Amani kwa Wajumbe Wasio wa Kweli!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Amani Kutoka kwa Mungu Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 7/8 kur. 22-25

Ziara ya Papa kwa UM—Ilitimiza Nini?

KWENYE safari yake ya ndege kuvuka Atlantiki ili kuhutubia UM katika New York City, Papa John Paul 2 alipita ile alama ya kilometa 1,000,000 katika safari zake kuzunguka ulimwengu. Ilikuwa Oktoba 4, 1995, na hii ilikuwa safari yake ya 68 kwenda ng’ambo akiwa papa. Bila shaka, yeye ndiye papa aliyesafiri sana katika historia ya Kanisa Katoliki ya Kiroma.

Alifika Newark International Airport, New Jersey, katika Jumatano yenye mvua, akilindwa na maofisa wa usalama wengi mno kuliko waliopata kuwekewa mkuu yeyote. Ilikadiriwa kwamba maofisa wa serikali na wa usalama wa jiji wapatao 8,000 walipewa mgawo wa kumlinda papa. Ripoti moja iliuita “usalama ulio kama gamba lenye kulinda,” kukiwa na helikopta na waruka-mtumbwi.

Kwa Nini Alizuru?

Katika hotuba yake alipowasili kwenye uwanja wa ndege, papa alikumbuka kwamba mtangulizi wake, Papa Paul 6, alikuwa amehutubia Mkutano Mkuu wa UM kwa ombi kwa ajili ya amani: “Hakuna vita tena, hakuna vita tena kamwe!” John Paul 2 alisema alikuwa akirudi kwa UM “kueleza usadikisho [wake] wa kina kwamba miradi na nia ambazo ziliongoza kwenye kuanzishwa kwa UM nusu karne iliyopita ni za muhimu zaidi kuliko wakati mwingineo wote katika ulimwengu unaotafuta kusudi.”

Kwenye sala za jioni katika Sacred Heart Cathedral, Newark, papa alionyesha tena utegemezo wake kwa UM, akisema: “Shirika hilo lipo ili kutumikia hali-bora ya familia ya kibinadamu, na kwa hivyo inafaa kwamba papa azungumze hapo akishuhudia ujumbe wa Gospeli wenye tumaini.” Yeye aliongeza: “Kwa hivyo sala yetu ya amani pia ni sala kwa ajili ya Shirika la Umoja wa Mataifa. Mtakatifu Francis wa Assisi . . . anasifika kuwa mpenda-amani na mfanyakazi stadi wa amani. Acheni tuombe msaada wa Mtakatifu Francis juu ya jitihada za Umoja wa Mataifa za kutafuta haki na amani kotekote ulimwenguni.”

Katika hotuba yake kwa UM, yeye alisifu mabadiliko ya kisiasa yasiyo na jeuri ya 1989 katika Ulaya Mashariki, ambapo nchi kadhaa zilirudishiwa uhuru. Alitia moyo “uzalendo wa kweli” badala ya “utukuzo wa taifa wenye upendeleo na wenye kutenga.” Alizungumzia ukosefu wa haki wa mfumo wa sasa, akisema: “Wakati mamilioni ya watu wanateseka kutokana na umaskini ambao unamaanisha njaa, utapia-mlo, ugonjwa, kutojua kusoma na kuandika, na kutwezwa, ni lazima . . . tujikumbushe kwamba hakuna aliye na haki ya kumnyonya mwingine kwa faida yake mwenyewe.”

Kisha akataarifu: “Tukabilipo magumu haya makubwa, twaweza kukosaje kutambua fungu la Shirika la Umoja wa Mataifa?” Alisema kwamba UM lahitaji “kuwa kitovu cha adili ambapo mataifa yote ya ulimwengu yajihisi huru.” Yeye alikazia uhitaji wa kuchochea “muungano wa familia nzima ya kibinadamu.”

Amani ya Kweli—Kutoka Chanzo Gani?

Bila shaka, yeye alitoa maoni mengi yenye kuheshimika. Hata hivyo, je, katika hotuba yake ndefu, kuna wakati wowote alipoelekeza viongozi wa ulimwengu kwenye suluhisho la Mungu kwa matatizo ya wanadamu—utawala wake wa Ufalme kupitia Kristo Yesu? (Mathayo 6:10) La. Kwa hakika, kamwe hakunukuu Biblia katika hotuba yake kwa UM. Kinyume na hilo, yeye alisema kwamba “kwa msaada wa huruma za Mungu, twaweza kufanyiza katika karne ijayo na mileani ifuatayo ustaarabu umfaao binadamu, tamaduni ya kweli ya uhuru.” Kwa wanafunzi wa Biblia, maoni hayo huenda yakaelekea kurudia maoni kama hayo yaliyotamkwa na wale waliokuwa Babiloni ya kale zaidi ya miaka 4,000 iliyopita, ambao walifikiri wangeweza kusaidia wanadamu waunganike kwa njia ya kibinadamu: “Haya, na tujijengee mji, na mnara, na kilele chake kifike mbinguni, tujifanyie jina.” (Mwanzo 11:4) Kwa hiyo, kutokana na maoni haya, ni viongozi wa kisiasa wa kibinadamu, wakiwakilishwa na UM, ambao watafanyiza ustaarabu mpya unaotegemea uhuru.

Lakini Biblia yatoa unabii upi kuhusu wakati ujao wa serikali za kisiasa za mwanadamu na UM lenyewe? Vitabu vya Danieli na Ufunuo hutoa ono lililo wazi la wakati ujao unaongojea serikali na UM. Danieli alitoa unabii kwamba katika siku za mwisho, Mungu ataanzisha utawala wake wa Ufalme, kama jiwe kubwa mno ‘lisilokatwa kwa mikono ya binadamu.’ Litachukua hatua gani? “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele . . . .; Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Mahali pa serikali za mwanadamu patachukuliwa na utawala mmoja wenye uadilifu kwa wanadamu wote.—Danieli 2:44, 45.

Ni nini kitakachopata UM? Ufunuo sura ya 17 huonyesha UM (na shirika lililolitangulia ambalo lilidumu kwa muda mfupi, Ushirika wa Mataifa) kuwa hayawani mwitu mwenye rangi nyekundu-nyangavu kwamba ‘atakwenda kwenye uharibifu.’ (Ufunuo 17:8)a Chanzo cha Yehova cha amani ya kweli si njia isiyokamilika ya kibinadamu, haidhuru waamini wayo ni wenye moyo mweupe kadiri gani. Amani ya kweli itakuja kupitia Ufalme wa Mungu ulioahidiwa, mikononi mwa Kristo Yesu aliyefufuliwa mbinguni. Huo ndio msingi wa utimizo wa ahadi ya Mungu kwenye Ufunuo 21:3, 4: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”

Hiyo Ziara—Ilikuwa na Uvutano Gani?

Papa aliporejezea Biblia kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika hotuba zake, je, waumini Wakatoliki walitiwa moyo kutoa Biblia zao na kuchunguza marejezo hayo? Uhakika wa mambo ni kwamba, walio wengi hata hawakubeba Biblia. Ni mara chache sana papa alifanya marejezo hususa ili kufanya iwe rahisi kwa wasikilizaji kusoma Biblia.

Kielelezo kimoja kilikuwa wakati alipozungumza na watu 83,000 kwenye Giants Stadium, New Jersey, na kusema: “Twangojea kurudi kwa Bwana kuwa hakimu wa wanaoishi na waliokufa. Twangojea kurudi kwake katika utukufu, kuja kwa ufalme wa Mungu kwa ukamili. Huo ni mwaliko wa daima wa Zaburi: ‘Umngoje Bwana, uwe hodari, upige moyo konde, naam, umngoje Bwana.’” Lakini ni andiko gani alikokuwa akilinukuu kutoka Zaburi? Na ni Bwana gani aliyekuwa akimrejezea—Yesu au Mungu? (Linganisha Zaburi 110:1.) Kulingana na gazeti la Vatikani L’Osservatore Romano, alikuwa akinukuu Zaburi 27:14, ambalo husomeka waziwazi zaidi hivi: “Weka tumaini lako katika Yahweh, uwe na nguvu, acha moyo wako uwe jasiri, weka tumaini lako katika Yahweh.” (The Jerusalem Bible) Ndiyo, twapaswa kuweka tumaini letu katika Yahweh, au Yehova, Mungu wa Bwana Yesu.—Yohana 20:17.

Je, katika historia yote, makasisi na viongozi Wakatoliki wamechochea amani miongoni mwa mataifa? Je, mafundisho ya Katoliki yametumika kutatua tofauti za vikundi vya kikabila na kijamii? Machinjo ya 1994 katika Rwanda, Afrika mashariki-kati, na vita vya kuangamizana vya miaka michache iliyopita katika ile iliyokuwa Yugoslavia hutoa kielezi kwamba itikadi za kidini kwa kawaida hukosa kuondoa chuki na ubaguzi wenye kina uliojificha katika moyo wa binadamu. Wala kuungama dhambi kijuu-juu wala kuhudhuria Misa kila juma hakutabadili njia ya watu ya kufikiri na kutenda. Lazima kuwe na uvutano wenye kina zaidi, unaokuja wakati Neno la Mungu liruhusiwapo kuupenya moyo na akili ya mwamini.

Mwenendo uliobadilika wa Mkristo wa kweli hautegemei itikio la kihisia-moyo linalochochewa na sherehe ya ibada ya kidini, bali unategemea uelewevu ufaao wa mapenzi ya Mungu kwa kila mtu. Mtume Paulo alitaarifu: “Msijifanyize wenyewe kulingana na mwenendo wa ulimwengu unaowazunguka, lakini acheni mwenendo wenu ubadilike, ukifanyizwa na akili yenu mpya. Hii ndiyo njia pekee ya kugundua mapenzi ya Mungu na kujua lililo jema, lile ambalo Mungu ataka, lile ambalo ni jambo kamilifu kufanya.” (Warumi 12:1, 2, JB) Mwenendo huu mpya unapatikana kwa kujifunza Neno la Mungu ambalo huongoza kwenye ujuzi sahihi wa mapenzi yake. Huo hufanyiza kani ya kiroho ambayo hutendesha akili na matokeo ni mwenendo wa Kikristo.—Waefeso 4:23; Wakolosai 1:9, 10.

Je, Kanisa Liko Katika “Hatua Muhimu ya Kukata Shauri”?

Gazeti la Hispania El País lilimfafanua Papa John Paul 2 kuwa na “uvutano upitao wa kawaida” kwa mtu wa umri wa miaka 75, na gazeti moja la Marekani lilimwita “mahiri wa vyombo vya habari.” Yeye ni stadi katika kushughulika na waandishi wa habari na katika kufanyiza mahusiano na umati wa watu na watoto wao. Katika safari zake yeye huwakilisha kwa kufaulu Makao Matakatifu ya Papa yaliyoko Vatican City. Hata ingawa Vatikani yatambuliwa rasmi kwenye UM, baraka ya papa juu ya shirika hilo haitalihakikishia baraka ya Yehova Mungu.

Maitikio kwa ziara ya papa yalitofautiana. Wengi wa Wakatoliki waliopata tikiti za Misa iliyofanywa nje walihisi wakiwa wamechangamshwa na ono hilo kihisia-moyo. Hata hivyo, viongozi fulani Wakatoliki walikuwa na maoni hasi kwa ziara hiyo na athari ambazo zingeweza kutokea. Gazeti The New York Times lilimnukuu Timothy B. Ragan, rais wa Catholic National Center for Pastoral Leadership, akisema kwamba “ziara ya Papa ilikuwa fursa iliyopotezwa. Ingawa safari hiyo ‘ilikuwa yenye kuchangamsha na jambo kuu kisakramenti kwa watu wengi,’” kwa viongozi wengi Wakatoliki ziara hiyo haikutoa “pindi kwa yeye kusikiliza na hakukuwa na andalizi kwa ajili ya mazungumzo ya pande mbili.” Wakatoliki wengi huhisi kwamba kwa masuala kama vile useja, kudhibiti uzazi, na talaka, wanalazimishwa kusikiliza upande mmoja tu bila kutoa maoni.

Wakuu fulani Wakatoliki wanakubali, kwamba “kanisa liko katika hatua muhimu ya kukata shauri,” na wanahofu kwamba Wakatoliki wengi, “hasa wachanga, wanapoteza umaana wa kile kinachomaanishwa na kuwa Mkatoliki.” James Hitchcock, mwanamapokeo Mkatoliki, “aona tatizo kuwa vita baridi yenye uharibifu kati ya wakuu wasiotaka mabadiliko na viongozi wa katikati wenye kutaka mabadiliko.”

Kuhusu jinsi ambavyo ziara ya papa itaathiri tatizo katika vyeo vya kanisa, Hitchcock alitaarifu: “Papa aja hapa, anasifiwa mno, naye arudi nyumbani—na hakuna kinachotendeka. Kulingana na maoni yangu matokeo yanakatisha tamaa.” Papa kwa hakika alipoteza fursa ya kuwaeleza viongozi wa kisiasa katika UM mahali ambapo pana chanzo cha amani ya kweli.

Ingawa Katiba ya UM na propaganda za kibinadamu hukazia mradi wa “Amani na usalama,” usidanganywe. Biblia huonya: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 Wathesalonike 5:3) Amani na usalama wa kweli utakuja kwa mapenzi ya Mungu tu na kwa njia yake—kupitia utawala wake wa Ufalme, si kupitia UM.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi ya kina juu ya unabii huu katika Ufunuo, ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! kurasa 240-251, kilichotangazwa katika 1988 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

Picha za UN

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki