Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 5/1 kur. 13-18
  • Hakuna Amani kwa Wajumbe Wasio wa Kweli!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hakuna Amani kwa Wajumbe Wasio wa Kweli!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Waitwao Eti Wajumbe wa Amani
  • UM Likiwa Mfanya-Amani?
  • Sababu za ‘Kutoa Machozi kwa Uchungu’
  • Amani Kutoka kwa Mungu Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Umoja wa Mataifa—Njia Bora Zaidi?
    Amkeni!—1992
  • Fumbo Lenye Kutia Hofu Lafumbuliwa
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
  • Ziara ya Papa kwa UM—Ilitimiza Nini?
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 5/1 kur. 13-18

Hakuna Amani kwa Wajumbe Wasio wa Kweli!

“Watenda mabaya wataharibiwa . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—ZABURI 37:9, 11.

1. Kwa nini tutarajie kukuta wajumbe wa kweli na wasio wa kweli, katika “wakati wa mwisho”?

WAJUMBE—wasio wa kweli au wa kweli? Kulikuwa na aina zote hizo katika nyakati za Biblia. Lakini namna gani siku yetu? Kwenye Danieli 12:9, 10, twasoma kwamba mjumbe wa kimbingu alimwambia nabii wa Mungu hivi: “Maneno haya yamefungwa, na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho. Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya [“waovu,” NW] watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima [“wale walio na ufahamu wenye kina,” NW] ndio watakaoelewa.” Sasa tunaishi katika “wakati [huo] wa mwisho.” Je, twaona tofauti iliyo wazi kati ya “waovu” na “wale walio na ufahamu wenye kina”? Kwa hakika twaiona!

2. Isaya 57:20, 21 linatimizwaje leo?

2 Kwenye sura ya 57, mistari 20 na 21, twasoma maneno ya mjumbe wa Mungu Isaya: “Wabaya [“waovu,” NW] wanafanana na bahari iliyochafuka; maana haiwezi kutulia, na maji yake hutoa tope na takataka. Hapana amani kwa wabaya [“waovu,” NW]; asema Mungu wangu.” Maneno haya yanafafanua ulimwengu huu kwa kufaa kama nini unapokaribia karne ya 21! Watu fulani hata huuliza, ‘Je, tutapata kuifikia karne hiyo?’ Wajumbe walio na ufahamu wenye kina wana nini la kutuambia?

3. (a) Ni tofauti gani inayotokezwa kwenye 1 Yohana 5:19? (b) Walio na “ufahamu wenye kina” wanafafanuliwaje katika Ufunuo sura ya 7?

3 Mtume Yohana alikuwa na ufahamu wenye kina uliopuliziwa kimungu. Kwenye 1 Yohana 5:19, inataarifiwa hivi: “Sisi twajua twatokana na Mungu, lakini ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” Walio tofauti na ulimwengu huu ni Waisraeli wa kiroho 144,000, ambao baki lao linalozeeka lingali nasi. Wanaojiunga nao leo ni “umati mkubwa . . . kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” ambao sasa wanajumlika kuwa zaidi ya milioni tano, walio pia na ufahamu wenye kina. “Hawa ndio wale watokao katika dhiki kubwa.” Na ni kwa nini wanathawabishwa? Ni kwa sababu wao pia “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” kwa kudhihirisha imani katika fidia ya Yesu. Wakiwa wajumbe wa nuru, wao pia “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku.”—Ufunuo 7:4, 9, 14, 15.

Waitwao Eti Wajumbe wa Amani

4. (a) Kwa nini waitwao eti wajumbe wa amani katika ulimwengu wa Shetani hawatafanikiwa? (b) Waefeso 4:18, 19 latumikaje leo?

4 Ingawa hivyo, vipi juu ya wale waitwao eti wajumbe wa amani katika mfumo wa kilimwengu wa Shetani? Kwenye Isaya sura ya 33, mstari wa 7 (NW), twasoma hivi: “Tazama! Mashujaa wao wenyewe wamelia barabarani; wajumbe wa amani wenyewe watatoa machozi kwa uchungu.” Hili ni kweli kama nini kuhusu wale wenye kukimbia-kimbia huku na huku bila utulivu wakienda kutoka jiji moja la ulimwengu hadi jiji lingine, wakijaribu kuleta amani! Ni ubatili kama nini! Kwa nini hivyo? Ni kwa sababu wanapambana na dalili za matatizo ya ulimwengu badala ya kushughulikia visababishi vya msingi. Kwanza kabisa, wao ni vipofu kwa habari ya kuwapo kwa Shetani, ambaye mtume Paulo amfafanua kuwa “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4) Shetani amepanda mbegu za uovu miongoni mwa jamii ya kibinadamu, matokeo yakiwa kwamba walio wengi, kutia ndani wengi wa watawala, sasa wanafaana na ufafanuzi wa Waefeso 4:18, 19: “Huku wao wakiwa katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutokuwa na ujuzi ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ukosefu wa hisi wa mioyo yao. Wakiisha kuishiwa na hisia zote za adili, walijikabidhi wenyewe kwenye mwenendo mlegevu ili wafanye ukosefu wa usafi wa kila namna pamoja na pupa.”

5. (a) Kwa nini mashirika ya wanadamu hushindwa kufanikiwa kuwa wafanya-amani? (b) Zaburi 37 yatoa ujumbe gani wenye kufariji?

5 Hakuna shirika la wanadamu wasiokamilika liwezalo kung’oa kutoka mioyo ya kibinadamu pupa, ubinafsi, na chuki ambazo zimeenea sana leo. Ni Muumba wetu tu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, awezaye kufanya hivyo! Na zaidi, ni wapole tu, walio wachache miongoni mwa wanadamu, ambao wako tayari kujitiisha kwa mwongozo wake. Matokeo ya hawa na ya waovu wa ulimwengu yanatofautishwa kwenye Zaburi 37:9-11: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi. Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”

6, 7. Ni rekodi ipi ya dini za ulimwengu huonyesha kwamba zimeshindwa kutumika zikiwa wajumbe wa amani?

6 Basi je, wajumbe wa amani waweza kupatikana miongoni mwa dini za ulimwengu huu unaougua? Basi, ni ipi iliyo rekodi ya dini kufikia wakati huu? Historia yaonyesha kwamba dini imeshiriki, ndiyo, hata imekuwa kichochezi cha umwagaji-damu mwingi katika karne zote. Kwa kielelezo, Christian Century la juma la Agosti 30, 1995, likiripoti juu ya msukosuko katika ile iliyokuwa Yugoslavia, lilitaarifu hivi: “Katika Bosnia yenye kuongozwa na Waserbia, makasisi hukaa kwenye safu ya mbele ya linalojiita bunge, na wamo pia kwenye mistari ya mbele ya kivita, ambapo vikosi na hata silaha hubarikiwa kabla ya mapigano.”

7 Karne ya kazi ya umishonari ya Jumuiya ya Wakristo katika Afrika haikuleta matokeo mazuri zaidi, kama vile ilivyotolewa kielezi vizuri katika Rwanda, bara lijulikanalo kuwa na Wakatoliki asilimia 80. Gazeti The New York Times la Julai 7, 1995, liliripoti hivi: “Golias, gazeti huru la Kikatoliki lenye kuandikwa na watu wasio makasisi linalochapishwa katika Lyons [Ufaransa], lapanga kutambua makasisi 27 zaidi wa Rwanda na watawa wa kike wanne ambao lasema waliua au kuchochea mauaji katika Rwanda mwaka jana.” Shirika la haki za kibinadamu katika London, liitwalo African Rights, lilikuwa na elezo hili: “Licha ya kulaumika kwa sababu ya kunyamaza, makanisa yanalaumika kwa sababu ya ujihusishaji kamili wa baadhi ya makasisi, mapadre na watawa wa kike katika mauaji ya kikabila.” Hiyo yafanana na hali katika Israeli wakati mjumbe wa kweli wa Yehova Yeremia, alipofafanua “aibu” ya Israeli, pamoja na watawala walo, makuhani walo, na manabii walo, akiongeza hivi: “Katika pindo za mavazi yako zimeonekana alama za damu ya nafsi zao maskini wasio na hatia.”—Yeremia 2:26, 34, NW.

8. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yeremia alikuwa mjumbe wa amani?

8 Mara nyingi Yeremia ameitwa nabii atabiriye msiba, lakini angeweza kuitwa pia mjumbe wa amani wa Mungu. Yeye alirejezea amani mara nyingi kama alivyofanya Isaya kabla yake. Yehova alimtumia Yeremia kutangaza hukumu juu ya Yerusalemu, akisema: “Kwa kuwa mji huu umekuwa sababu ya kunitia hasira, na sababu ya ghadhabu yangu, tangu siku ile walipoujenga hata siku hii ya leo; ili niuondoe usiwe mbele za uso wangu; kwa sababu ya mabaya yote ya wana wa Israeli, na ya wana wa Yuda, waliyoyatenda ili kunitia hasira, wao, na wafalme wao, na wakuu wao, na makuhani wao, na manabii wao, na watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu.” (Yeremia 32:31, 32) Hili lilikuwa kivuli cha hukumu ya Yehova juu ya watawala na makasisi katika Jumuiya ya Wakristo leo. Ili amani ya kweli ienee, ni lazima wachochezi hawa wa ubaya na jeuri waondolewe! Kwa hakika wao si wajumbe wa amani.

UM Likiwa Mfanya-Amani?

9. UM limedaije kuwa mjumbe wa amani?

9 Je, Umoja wa Mataifa haliwezi kuwa mjumbe wa kweli wa amani? Kwa vyovyote, taarifa ya utangulizi ya mkataba walo, iliyotolewa Juni 1945, siku 41 tu kabla ya bomu la atomi kuharibu Hiroshima, ilitaarifu kusudi lalo: “kuokoa vizazi vinavyofuata kutokana na pigo la vita.” Mataifa 50 yaliyotazamiwa kuwa washiriki wa Umoja wa Mataifa yalipaswa “kuunganisha nguvu [zayo] ili kudumisha amani na usalama wa kimataifa.” Leo UM lina washiriki 185, eti yaliyojitoa kwa ajili ya sababu hiyohiyo.

10, 11. (a) Viongozi wa kidini wamejulishaje kutegemeza kwao UM? (b) Ni katika njia ipi mapapa wamewakilisha isivyofaa “Habari Njema ya Ufalme wa Mungu”?

10 Kwa miaka yote, UM limesifiwa sana, hasa na viongozi wa kidini. Aprili 11, 1963, Papa John wa 23 alitia sahihi barua yake iliyokuwa na kichwa “Pacem in Terris” (Amani Duniani) ambayo katika hiyo alitaarifu hivi: “Ni tamanio letu lenye bidii kwamba—katika muundo walo na katika nyenzo zalo—shirika la Umoja wa Mataifa lipate kuwa na uwezo wa kutosha wa kushughulikia kazi zalo kubwa na zilizo bora.” Baadaye, katika Juni 1965, viongozi wa kidini, waliosemekana kuwa waliwakilisha nusu ya idadi ya watu ulimwenguni, walisherehekea mwaka wa 20 wa kuanzishwa kwa UM katika San Fransisco. Pia katika 1965, Papa Paul wa 6, alipokuwa akizuru UM, alilifafanua kuwa “tumaini la mwisho la upatano na amani.” Katika 1986, Papa John Paul wa 2 alishirikiana katika kudhamini Mwaka wa Amani wa Kimataifa wa UM.

11 Tena, wakati wa ziara yake katika Oktoba 1995, papa alitangaza hivi: “Leo tunasherehekea Habari Njema ya Ufalme wa Mungu.” Lakini je, kweli yeye ni mjumbe wa Mungu wa habari njema ya Ufalme? Akinena juu ya matatizo ya ulimwengu, aliendelea kusema hivi: “Tukabilipo magumu haya makubwa mno, twaweza kukosaje kulitambua fungu la Shirika la Umoja wa Mataifa?” Chaguo la papa ni UM, badala ya Ufalme wa Mungu.

Sababu za ‘Kutoa Machozi kwa Uchungu’

12, 13. (a) UM limetendaje katika njia inayofafanuliwa kwenye Yeremia 6:14? (b) Kwa nini uongozi wa UM unahusishwa katika ufafanuzi kwenye Isaya 33:7?

12 Sherehe ya ukumbusho wa mwaka wa 50 wa UM imekosa kufunua taraja lolote la kweli la “amani duniani.” Sababu moja ilionyeshwa na mwandikaji mmoja katika The Toronto Star la Kanada, aliyeandika hivi: “U.M. ni simba asiye na meno, ambaye hunguruma anapokabiliwa na ukatili wa kibinadamu, lakini analazimika kungojea washiriki wake wamwekee meno yake ya bandia kabla ya kuweza kuuma.” Mara nyingi mno umo hilo limekuwa dogo sana na lililochelewa mno. Wajumbe wa amani katika mfumo wa ulimwengu uliopo, na hasa wale walio katika Jumuiya ya Wakristo, wamekuwa wakisema sawasawa na maneno ya Yeremia 6:14: “Wameiponya jeraha ya watu wangu kwa juu juu tu, wakisema, Amani, Amani, wala hapana amani.”

13 Makatibu-wakuu wa UM mmoja baada ya mwingine wamefanya kazi kwa bidii, na bila shaka kwa moyo mweupe, ili kufanya UM lifaulu. Lakini mizozano ya daima miongoni mwa wale washiriki 185 wenye miradi mingi tofauti kuhusu jinsi ya kuwekea mipaka vita, kupanga sera, na kushughulikia fedha imezuia mataraja ya mafanikio. Katika ripoti yake ya mwaka kwa ajili ya 1995, katibu-mkuu wa wakati huo aliandika juu ya kupungua kwa “tisho la msiba wa kinyuklia tufeni pote” kuwa kwenye kufungulia njia “mataifa kufanya kazi pamoja kuelekea maendeleo ya kiuchumi na ya kijamii kwa ajili ya jamii yote ya kibinadamu.” Lakini aliongeza hivi: “Kwa kuhuzunisha, rekodi ya mambo ya ulimwengu kwa miaka michache iliyopita imetofautiana sana na matarajio hayo ya mambo mazuri.” Kwa kweli, wale ambao wangekuwa wajumbe wa amani ‘wanatoa machozi kwa uchungu.’

14. (a) Kwa nini yaweza kusemwa kwamba UM limefilisika kifedha na kimaadili? (b) Yeremia 8:15 linatimizwaje leo?

14 Kichwa kikuu katika The Orange County Register la California kilisomeka hivi: “U.M. Limefilisika Kifedha, Kiadili.” Makala hiyo ilitaarifu kwamba kati ya 1945 na 1990, kulikuwa na vita zaidi ya 80, vikiua watu zaidi ya milioni 30. Lilimnukuu mwandikaji mmoja wa toleo la Reader’s Digest la Oktoba 1995 ambaye “afafanua shughuli za kijeshi za UM kwamba huainishwa kwa ‘makamanda wasio na sifa za ustahili, wanajeshi wasio na nidhamu, miungano pamoja na wachokozi, kushindwa kuzuia matendo ya kinyama na nyakati fulani hata kuchangia hofu kubwa.’ Isitoshe, ‘kiwango cha ufujaji, ulaghai, na matumizi mabaya kimepita kiasi.’” Katika kisehemu chenye kichwa “UM ufikiapo miaka 50,” gazeti The New York Times lilikuwa na kichwa kikuu “Usimamizi Mbaya na Uharibifu Wamomonyoa Madhumuni Bora Zaidi ya UM.” Gazeti The Times la London, Uingereza, lilipatia makala moja kichwa chenye maneno, “Likiwa Dhaifu Linapofikia Miaka Hamsini—UM lahitaji programu ya mazoezi ili lijipatie nguvu upya.” Kwa kweli, ni kama tusomavyo kwenye Yeremia sura ya 8, mstari wa 15: “Tulitazamia amani, lakini hayakuja mema yo yote; tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!” Na tisho la maangamizi makubwa ya nyuklia lingali latisha wanadamu. Kwa wazi, UM si mjumbe wa amani ambaye wanadamu wahitaji.

15. Babiloni la kale na wazao walo wa kidini wamethibitikaje kuwa waharibifu na wenye kupumbaza akili?

15 Matokeo ya haya yote yatakuwa nini? Neno la kiunabii la Yehova haliachi shaka lolote. Kwanza, ni nini kinachongojea dini zisizo za kweli za ulimwengu ambazo mara nyingi sana zimekuwa na urafiki kupita kiasi pamoja na UM? Hizo ndizo wazao kutoka chanzo kimoja cha uzinzi, Babiloni la kale. Kwa kufaa, zinafafanuliwa kwenye Ufunuo 17:5 kuwa “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa mambo yenye kuchukiza sana ya dunia.” Yeremia alifafanua hukumu ya tengenezo hili lenye unafiki. Kama kahaba, limewatongoza wanasiasa wa dunia, likirairai UM na kufanyiza mahusiano haramu pamoja na mamlaka za kisiasa zilizo washiriki walo. Limekuwa mshiriki mkuu katika vita vya historia. Mtoa-maelezo mmoja alitaarifu hivi akirejezea vita vya kidini katika India: “Karl Marx alirejezea dini kuwa kasumba ya umma. Lakini taarifa hiyo haiwezi kuwa sahihi sana kwa sababu kasumba ni kitulizaji, hiyo hutuliza watu kuwapumbaza akili. Badala ya hivyo, dini ni kama kokeni kali. Hiyo huchochea jeuri nyingi mno na ni kani haribifu sana.” Lakini mwandikaji huyo hayuko sahihi sana. Dini isiyo ya kweli ni yenye kupumbaza akili na haribifu vilevile.

16. Kwa nini watu wenye mioyo ya kufuatia haki wapaswa sasa kukimbia kutoka Babiloni Mkubwa? (Ona pia Ufunuo 18:4, 5.)

16 Basi, je, watu wenye mioyo ya kufuata haki wapaswa wafanye nini? Mjumbe wa Mungu Yeremia anatupa jibu: “Kimbieni kutoka kati ya Babeli [“Babiloni,” NW], kila mtu na ajiokoe nafsi yake. . . . Maana ni wakati wa kisasi cha BWANA [“Yehova,” NW].” Tunafurahi kwamba mamilioni yamekimbia kutoka Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Je, wewe ni mmoja wa haya? Basi waweza kuelewa vema jinsi ambavyo Babiloni Mkubwa ameathiri mataifa ya dunia: “Mataifa wamekunywa mvinyo wake; kwa sababu hiyo mataifa wameingiwa na wazimu [“kichaa,” NW].”—Yeremia 51:6, 7.

17. Ni hukumu gani ikaribiayo kutekelezwa juu ya Babiloni Mkubwa, na ni nini hufuata tendo hilo?

17 Muda si muda, washiriki wa UM ‘walioingiwa na kichaa’ watatumiwa na Yehova kushambulia dini isiyo ya kweli, kama ilivyofafanuliwa kwenye Ufunuo 17:16: “Hawa watamchukia kahaba na watamfanya ukiwa na kuwa uchi, na watakula kabisa sehemu zake zenye nyama na watamchoma kabisa kwa moto.” Hili litatia alama mwanzo wa dhiki kubwa ambayo yarejezewa kwenye Mathayo 24:21 nayo itafikia upeo kwenye Har–Magedoni, vita ya siku kuu ya Mungu Mweza Yote. Sawa na Babiloni la kale, Babiloni Mkubwa atapata hukumu iliyotangazwa kwenye Yeremia 51:13, 25: “Ewe [mwanamke] ukaaye juu ya maji mengi, uliye na hazina nyingi, mwisho wako umewadia, kadiri ya tamaa zako. Tazama, mimi ni juu yako, Ee mlima uharibuo, asema BWANA; wewe uharibuye dunia nzima; nami nitaunyosha mkono wangu juu yako, na kukufingirisha chini toka majabalini; nami nitakufanya kuwa mlima ulioteketezwa.” Mataifa yenye ufisadi, yenye kuchochea vita yatafuata dini isiyo ya kweli katika uharibifu siku ya Yehova ya kisasi iyaangukiapo hayo pia.

18. Ni lini na jinsi gani Isaya 48:22 litakavyotimizwa bado?

18 Kwenye 1 Wathesalonike 5:3, yasemwa hivi kuhusu waovu: “Wakati wowote ule ambao wanasema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa hapohapo juu yao kama vile maumivu makali ya ghafula ya taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataponyoka kwa vyovyote.” Hawa ndio ambao Isaya alisema hivi juu yao: “Tazama! . . . wajumbe wa amani watatoa machozi kwa uchungu.” (Isaya 33:7, NW) Kwa kweli, kama vile tusomavyo kwenye Isaya 48:22 (NW) “‘hapana amani’ Yehova amesema ‘kwa waovu.’” Lakini ni wakati ujao wa aina gani uwangojeao wajumbe wa kweli wa amani ya kimungu? Makala yetu inayofuata itatuambia.

Maswali ya Kupitia

◻ Manabii wa Mungu wamefichua wajumbe wasio wa kweli kwa maneno gani yenye nguvu?

◻ Kwa nini mashirika ya wanadamu yameshindwa kufanikiwa katika kujaribu kutokeza amani yenye kudumu?

◻ Wajumbe wa kweli wa amani wanatofautianaje na watetezi wa UM?

◻ Ni lazima wapole wafanye nini ili wafurahie amani iliyoahidiwa ya Yehova?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Isaya, Yeremia, na Danieli wote walitabiri kushindwa kufanikiwa kwa jitihada za wanadamu duni za kupata amani

[Picha katika ukurasa wa 16]

“Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.”—Mtume Yohana

[Picha katika ukurasa wa 17]

‘Wako katika giza kiakili.’ —Mtume Paulo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki