Sura 18
“Mwisho wa Ulimwengu” Ni Karibu!
1. Wafuasi wa kidunia wa Kristo wangejuaje ameanza kutawala mbinguni?
YESU KRISTO alipofukuza Shetani na malaika zake mbinguni na kuanza utawala wake wa Ufalme, ilimaanisha kwamba mwisho wa Shetani na taratibu (mfumo) yake mbovu ulikuwa karibu. (Ufunuo 12:7-12) Lakini wafuasi wa Kristo hapa duniani wangewezaje kujua kwamba tukio hilo lisiloonekana kwa macho yao lilikuwa limetukia huko mbinguni? Wangewezaje kujua kwamba Kristo alikuwa amekuwapo katika mamlaka ya Ufalme bila kuonekana na kwamba “mwisho wa ulimwengu” ulikuwa karibu? Wangeweza kujua kwa kuchunguza waone kama ile “ishara” ambayo Yesu alitoa ilikuwa ikitimizwa.
2. Ni ulizo gani ambalo wanafunzi wa Kristo walimwuliza?
2 Muda mfupi kabla ya kufa kwa Yesu, alipokuwa amekaa juu ya Mlima wa Mizeituni, wanne kati ya mitume wake walikuja wakamwomba awape “ishara.” Hivi ndivyo ulizo lao limesomwa na mamilioni ya watu katika tafsiri ya King James: “Tuambie, mambo haya yatakuwa lini? na ni nini itakayokuwa ile ishara ya kuja kwako, na ya mwisho wa ulimwengu?” (Mathayo 24:3) Lakini semi hizo, “kuja kwako” na “mwisho wa ulimwengu,” zina maana gani hasa?
3. (a) Semi hizi, “kuja kwako” na “mwisho wa ulimwengu,” zina maana gani hasa? (b) Basi, ulizo ambalo wanafunzi wa Kristo waliuliza linatafsiriwaje kwa usahihi?
3 Hapa neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kuja” ni parousia, na maana yake ni “kuwapo.” Hivyo, basi, ile “ishara” inapoonwa, inamaanisha tungejua Kristo yupo ijapokuwa haonekani, kwamba amekwisha kuja katika mamlaka ya Ufalme. Usemi “mwisho wa ulimwengu” vilevile unapoteza sana watu. Haumaanishi mwisho wa dunia, bali mwisho wa taratibu (mfumo) ya mambo ya Shetani. (2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo ulizo la mitume linasomwa kwa usahihi hivi: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa taratibu ya mambo?”—Mathayo 24:3, New World Translation.
4. (a) Ni nini iliyo sehemu ya “ile ishara” ambayo Yesu alitoa? (b) Ni katika njia gani “ile ishara” inaweza kulinganishwa na alama ya vidole?
4 Yesu hakutoa tukio moja tu liwe ndilo “ile ishara.” Alisimulia matukio mengi na hali nyingi. Waandikaji wengine pia wa Biblia, wala si Mathayo tu, walitaja matukio ya ziada ambayo yangekuwa alama ya zile “siku za mwisho.” Mambo yote hayo yaliyotabiriwa yangetukia katika wakati ambao waandikaji wa Biblia waliuita zile “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4) Matukio hayo yangekuwa kama ile mistari tofauti-tofauti inayofanyiza alama ya vidole vya mtu, chapa isiyoweza kuwa ya mtu mwingine ye yote. Zile “siku za mwisho” zina namna yazo zenyewe ya alama nyingi au matukio. Hizo zinafanyiza “alama ya vidole” isiyoweza kuwa ya kipindi kingine cho chote cha wakati.
5, 6. Unapochunguza mambo 11 ya ushuhuda wa “siku za mwisho” katika kurasa zinazofuata, unafahamu nini juu ya “umalizio wa taratibu ya mambo”?
5 Katika sura ya 16 ya kitabu hiki tulichunguza ushuhuda wa Biblia unaoonyesha kwamba Kristo alirudi akaanza kutawala katikati ya adui zake mwaka wa 1914. Sasa zichunguze kwa uangalifu sehemu mbalimbali za “ile ishara” ya kuwapo kwa Kristo na ushuhuda zaidi wa zile “siku za mwisho” za taratibu (mfumo) mbovu ya mambo ya Shetani. Unapochunguza mambo hayo yaliyotabiriwa yaliyo katika kurasa nne zinazofuata, angalia uone namna yamekuwa yakitimizwa tangu mwaka wa 1914.
“TAIFA LITAINUKA JUU YA TAIFA NA UFALME JUU YA UFALME.” —Mathayo 24:7, NW.
Bila shaka wewe umeona sehemu hii ya ile “ishara” ikitimizwa tangu mwaka wa 1914! Katika mwaka huo Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilianza. Katika historia hapajapata kuwapo vita mbaya sana kama hiyo. Ilikuwa vita ya jumla. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa kubwa kuliko vita vyote vikubwa vilivyopiganwa wakati wa miaka 2,400 iliyotangulia mwaka wa 1914. Hata hivyo miaka 21 tu baada ya kumalizika vita hiyo, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilianza. Nayo ilikuwa yenye kuleta hasara kubwa mara nne kuliko Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.
Vita vibaya sana vinaendelea kupiganwa. Tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili imalizike mwaka wa 1945, zaidi ya watu milioni 25 wameuawa katika vita 150 vilivyopiganwa kuzunguka dunia yote. Kila siku, kumekuwako kwa wastani vita 12 vikipiganwa mahali fulani katika ulimwengu. Na kuna tisho lenye kuendelea la kutokea kwa vita nyingine ya ulimwengu. United States peke yake ina silaha za nyukilia zinazotosha kuharibu kila mwanamume, mwanamke na mtoto aliye duniani zaidi ya mara 12!
“KUTAKUWAKO UPUNGUFU WA CHAKULA.”—Mathayo 24:7, NW. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ikatokea njaa iliyo kubwa kuliko zote katika historia. Upande wa kaskazini wa China peke yake watu 15,000 waliuawa kila siku na njaa. Lakini upungufu huo wa chakula ukawa mkubwa hata zaidi baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili. Robo moja ya ulimwengu ilikuwa ikifa njaa wakati huo! Na tangu wakati huo, chakula kimeendelea kuwa haba kwa watu wengi duniani.
“Kila nukta 8.6 mtu fulani katika nchi zinazoendelea anakufa kwa sababu ya ugonjwa wa kukosa chakula kinachofaa,” likasema gazeti New York “Times” katika mwaka wa 1967. Mamilioni yangali yakifa njaa—milioni 50 kila mwaka! Kufikia mwaka 1980, karibu robo moja ya watu waliomo duniani (watu 1,000,000,000) walikuwa wenye njaa kwa sababu hawakuweza kupata chakula cha kutosha. Hata mahali ambako chakula ni kingi, wengi ni maskini mno wasiweze kukinunua.
‘KILA MAHALI MAGONJWA YA KUAMBUKIZA.’—Luka 21:11, HNWW.
Muda mfupi baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza watu zaidi waliuawa na homa ya mafua ya Kispania kuliko waliokufa kwa maradhi yo yote ya kuambukiza katika historia ya wanadamu. Watu waliokufa walikuwa milioni 21! Hata hivyo magonjwa ya kuambukiza (ya kipuku) na maradhi yanaendelea kuwaka yakiua watu. Mamilioni wanakufa kila mwaka kwa ugonjwa wa moyo na wa kansa. Ugonjwa wa kaswende na kisonono unaendelea kwa haraka. Magonjwa mengine yaliyo mabaya sana, kama vile maleria, kichocho na upofu unaosababishwa na mto yanatokea nchi baada ya nchi, sana-sana katika Asia, Afrika na Latin Amerika.
“HAPA NA PALE PATAKUWA MTETEMEKO WA NCHI.” —Matayo 24:7, HNWW.
Tangu mwaka wa 1914 mpaka sasa, kumekuwako mitetemeko mikubwa iliyo mingi kuliko ya kipindi kingine cho chote katika historia iliyoandikwa. Kwa zaidi ya miaka 1,000, tangu mwaka 856 W.K. mpaka 1914, ilikuwako mitetemeko mikubwa ya nchi 24 tu, ikisababisha vifo vya watu 1,973,000. Lakini katika miaka 63 tangu 1915 mpaka 1978, jumla ya watu ka-ma 1,600,000 walikufa katika mitetemeko mikubwa 43 ya nchi.
“ONGEZEKO LA UHALIFU.”—Matayo 24:12, HNWW.
Ripoti kutoka mahali pote ulimwenguni zinaeleza juu ya ongezeko la uvunjaji wa sheria na uhalifu. Uhalifu wenye jeuri, kama vile uuaji wa kukusudia, kulala wanawake kinguvu na wivi wa kutumia nguvu, unaongezeka mno sasa. Katika United States peke yake, uhalifu mbaya unafanywa kwa wastani ya karibu kila nukta. Katika mahali pengi hakuna mtu anayejiona kuwa salama akiwa katika barabara za mjini, hata saa za mchana. Usiku watu wanakaa katika nyumba zao zikiwa zimefungwa kwa kufuli na makomeo, wakiogopa kutoka nje.
“WATU WATAZIRAI KWA SABABU YA WOGA.”—Luka 21:26, HNWW.
Labda woga ndilo ono moja la moyoni lililo kubwa zaidi katika maisha ya watu leo. Muda mfupi baada ya kulipuka kwa makombora ya kwanza ya nyukilia, Harold C. Urey, mwanasayansi wa nguvu za atomi, alisema hivi: “Tutakula woga, tutalalia woga, tutaishi katika woga na kufa katika woga.” Hilo ndilo linaloipata sehemu kubwa ya wanadamu. Wala si kwa sababu tu ya hatari iliyopo wakati wote ya uwezekano wa kutokea vita ya nyukilia. Vilevile watu wanaogopa uhalifu, uchafuzi wa hewa, maji na ardhi, magonjwa, infuleshoni na mambo mengine mengi yanayohatarisha usalama wao na maisha zao zenyewe.
‘KUTOKUTII WAZAZI.’—2 Timotheo 3:2.
Mara nyingi leo wazazi hawana uwezo mwingi wa kuongoza watoto wao. Vijana wanaasi mamlaka yote. Hivyo kila nchi duniani inapatwa na pigo hilo la uhalifu wa vijana. Zaidi ya nusu ya uhalifu wote mkubwa unaofanywa katika nchi fulani unafanywa na watoto wenye umri wa kati ya miaka 10 na 17. Mauaji ya kukusudia, kulala wanawake kinguvu, kushambulia, unyang’anyi, wivi wa kuvunja nyumba usiku, wivi wa motokaa—mambo yote hayo yanafanywa na watoto. Hakuna wakati katika historia ambao kutokutii wazazi kumekuwa jambo la kawaida sana kama wakati huu.
“WENYE KUPENDA FEDHA.”—2 Timotheo 3:2.
Po pote unapotazama leo unaweza kuona matendo ya pupa. Watu wengi watafanya karibu kila kitu ili wapate fedha. Wataiba au hata kuua. Ni jambo la kawaida kwa wenye pupa kutengeneza na kuuza bidhaa zinazojulikana, kwa njia moja au nyingine, kuwa zinawafanya wengine wawe wagonjwa au kuwaua. Kwa njia ya wazi ama kwa jinsi wanavyoishi, watu wanasema hivi juu ya fedha: ‘Huyu ndiye mungu wangu.’
“WAPENDAO ANASA KULIKO KUMPENDA MUNGU.”—2 Timotheo 3:4.
Watu wengi leo wanafikiria tu kufanya yanayowapendeza wao au jamaa zao tu, wala si yale yanayompendeza Mungu. Hasa wengi wanapenda yale ambayo Mungu anakataza, kutia na uasherati, uzinzi, ulevi, kuzoea dawa za kulevya na mambo mengine yaitwayo anasa ati. Hata zile ambazo katika zenyewe zinaweza kuwa anasa nzuri, zinawekwa mbele ya jitihada zo zote za kujifunza juu ya Mungu na kumtumikia.
“WENYE NAMNA YA UTAWA LAKINI HAWAONGOZWI NA NGUVU ZAKE.”—2 Timotheo 3:5, NW.
Mara nyingi viongozi wa ulimwengu na watu wasio na cheo pia wanajionyesha ki-nje kuwa watawa. Huenda wakahudhuria ibada za kanisa na kutoa michango ya fedha kusaidia mipango ya kidini. Wale walio katika serikali huenda wakaweka mkono wao juu ya Biblia wanapoapishwa katika cheo. Lakini mara nyingi matendo hayo yanakuwa ni ‘namna tu ya utawa’ na basi. Kama Biblia ilivyotabiri, ibada ya kweli ya Mungu haiwi kani ya kuongoza maisha za watu wengi leo. Hawachochewi na nguvu halisi ya kutenda mema.
‘KUIHARIBU DUNIA.’—Ufunuo 11:18.
Ile hewa tunayopumua, yale maji tunayokunywa na ile ardhi inayokuza chakula chetu vinachafuliwa. Hali hiyo ni mbaya sana hivi kwamba mwanasayansi Barry Commoner alionya hivi: “Ninaamini kwamba dunia ikiendelea kuchafuliwa, bila kizuizi, mwishowe uchafuzi huo utaharibu sayari hii iwe mahali pasipofaa kuishi wanadamu.”
6 Baada ya kuchunguza mambo yaliyotangulia, je! si wazi kwamba ile “ishara” ambayo Kristo alitoa na ule ushuhuda mwingi uliotabiriwa na wanafunzi wake inatimizwa sasa? Ijapokuwa kuna mambo mengine mengi ya kuhakikisha hivyo, yale yaliyotajwa hapa yametosha kuonyesha kwamba kweli tunaishi katika wakati ambao Biblia iliutabiri kuwa “siku za mwisho.”
7. (a) Ni nini kinachofanya unabii mbalimbali wa Bibliajuu ya kuwapo kwa Kristo na “siku za mwisho” uwe wenye kufaa kuangaliwa sana? (b) Tofauti na Biblia ilivyotabiri, viongozi wa ulimwengu walikuwa wakitabiri nini muda mfupi tu kabla ya mwaka wa 1914?
7 Hata hivyo huenda watu fulani wakasema: ‘Mambo kama vita, njaa kubwa, magonjwa ya kipuku na matetemeko ya ardhi yametukia mara nyingi katika historia. Kwa hiyo haingekuwa vigumu kutabiri kwamba yangetukia tena.’ Lakini ebu fikiri: Biblia haikutabiri tu mambo hayo, bali ilionyesha kwamba yangetukia ulimwenguni pote. Vilevile, Biblia ilisema kwamba mambo haya yote yangekipata kizazi kile kilichokuwa kikiishi katika mwaka wa 1914. Hata hivyo ni mambo gani ambayo viongozi mashuhuri wa ulimwengu walikuwa wakitabiri muda mfupi tu kabla ya mwaka wa 1914? Walisema amani ilielekea sana kuwa ulimwenguni kuliko zamani. Hata hivyo taabu kubwa zilizotabiriwa na Biblia zilianza kwa wakati barabara, mwaka wa 1914! Kwa kweli, sasa viongozi wa ulimwengu wanasema mwaka wa 1914 ulikuwa mwaka wa badiliko kubwa katika historia.
8. (a) Ni kizazi gani ambacho Yesu alionyesha kingeuona mwisho wa taratibu (mfumo) hii ya mambo? (b) Basi tunaweza kuwa na hakika ya jambo gani?
8 Akiisha kuvuta fikira kwenye mambo mengi ambayo yametukia katika kile kipindi cha kutoka mwaka wa 1914 na kuendelea, Yesu alisema: “Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote [kutia na mwisho wa mfumo huu] yatakapotimia.” (Mathayo 24:34, 14) Ni kizazi gani ambacho Yesu alimaanisha? Ni kile kizazi cha watu waliokuwa wakiishi katika mwaka wa 1914. Sasa watu wa kizazi hicho waliobaki bado ni wazee sana. Walakini, wengine kati yao watakuwa wangali hai wauone mwisho wa hii taratibu mbovu. Basi tunaweza kuwa na hakika kwamba: Karibuni kutatokea mwisho wa ghafula wa uovu wote na waovu wote penye Har-Magedoni.
[Picha katika ukurasa wa 149]
Yesu aliwaambia wanafunzi wake kile ambacho kingekuwa uhakikisho unaoonekana wa kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 154]
1914—HAR-MAGEDONI
Wengine wa kizazi kilichokuwa kikiishi mwaka 1914 watauona mwisho wa taratibu (mfumo) ya mambo na kuuokoka