Wataka Ulimwengu wa Aina Gani?
KAMA ungekuwa na uwezo, je, ungeumba ulimwengu mpya, ulimwengu usio na matatizo yanayosumbua wanadamu leo? Kama ungefanya hivyo, basi, je, haipatani na akili kutazamia kwamba Muumba wetu mwenye upendo, Yehova Mungu, ambaye ana uwezo huo, ataumba ulimwengu mpya wenye uadilifu?
Biblia yasema hivi: “BWANA [Yehova, New World Translation] ni mwema kwa watu wote, na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zaburi 145:9, 16) Baadhi ya tamaa zako ni zipi? Unatamani ulimwengu wa aina gani?
Katika kitabu chao A Sane and Happy Life: A Family Guide, Abraham na Rose Franzblau waliandika hivi: “Kama tungechukua maoni ya watu wa ulimwengu na kuuliza wanadamu aina ya ulimwengu ambao sisi sote tungependa kuishi ndani, yaelekea sana kwamba sisi sote tungekubaliana juu ya matakwa fulani machache.”
Ebu tuchunguze matakwa yaliyoorodheshwa na madaktari hao na tuone kama hayo si mambo yaleyale unayotaka. Tufanyavyo hivyo, tutaona pia kama Muumba wetu mwenye upendo ameahidi kuyaandaa mambo ayo hayo.
Takwa la Kwanza
Madaktari hao waliorodhesha kwanza “ulimwengu usio na vita.” Baada ya kupatwa na vita kadhaa vyenye kutisha sana, watu wengi hutamani ulimwengu ambamo watu hawatapigana na kuuana tena kamwe. Tumaini lao laonyeshwa katika maandishi yaliyoko kwenye ukuta katika Uwanja wa Umoja wa Mataifa katika Jiji la New York, yasemayo hivi: WATAFUA PANGA ZAO ZIWE MAJEMBE. NA MIKUKI YAO IWE MIUNDU: TAIFA HALITAINUA UPANGA JUU YA TAIFA LINGINE. WALA HAWATAJIFUNZA VITA TENA KAMWE.
Je! ulijua kwamba maneno hayo ni sehemu ya ahadi iliyotolewa na Yehova Mungu? Maneno hayo yamerekodiwa (kwa Kiingereza) katika Biblia Takatifu kwenye Isaya sura ya 2, mstari wa 4, katika tafsiri ya King James Version. Kwa kusoma pia Zaburi 46:8, 9, utapata kwamba ni kusudi la Mungu kuharibu silaha zote na ‘kukomesha vita hata mwisho wa dunia.’ Katika ulimwengu wenye amani, usio na vita unaofanyizwa na Mungu, unabii huu wa Biblia wenye kufurahisha utatimizwa: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.
Je! hungeorodhesha “ulimwengu bila vita” kuwa takwa la msingi la aina ya ulimwengu unayotaka? Na ebu fikiria, Muumba wetu Mkuu ameuahidi!
Ulimwengu Wenye Utele
Takwa lako la pili lingekuwa gani? Je! lingefanana na hili linalofuata kutolewa, “ulimwengu bila njaa, ambamo njaa kubwa na uhitaji ungeondolewa milele”? Je! halingekuwa jambo la ajabu kama hakungekuwa tena na mtoto anayekufa njaa? Bila shaka ungependa kuishi katika ulimwengu wenye utele. Lakini ni nani awezaye kuhakikisha jambo hilo?
Fikiria ahadi hii ya Mungu: “Nchi [itatoa, NW] mazao yake.” “[Kutakuwa na, NW] wingi wa nafaka katika ardhi.” (Zaburi 67:6; 72:16) Naam, katika ulimwengu mpya wa Mungu, chakula bora kitajaa tele. Biblia yatuhakikishia kwamba Yehova “atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta.”—Isaya 25:6.
Ingawa binadamu hana uwezo wa kuandaa ulimwengu usio na njaa, Mungu ana uwezo wa kuuleta. Mwana Wake, Yesu Kristo, alionyesha kwamba kuandaa chakula kwa wote hakutakuwa tatizo chini ya Ufalme wa Mungu. Alipokuwa duniani, Yesu alilisha maelfu ya watu kwa kuongeza kimwujiza mikate michache na samaki wachache.—Mathayo 14:14-21; 15:32-38.
Ulimwengu Usio na Ugonjwa
Huwezi kupata mtu mgonjwa mahali popote katika aina ya ulimwengu ambao sisi sote twataka. Kwa hiyo takwa la tatu halishangazi. “Ungekuwa ulimwengu usio na maradhi,” madaktari hao waliandika, “ulimwengu ambao wote wangepata nafasi ya kukua katika afya nzuri na kuishi maisha yao yote bila kupatwa na magonjwa yawezayo kuzuiwa na kutibiwa.”
Ebu fikiria utulizo tunaoweza kupata ikiwa hakuna mtu yeyote anayeugua mafua ama ugonjwa mwingine wowote! Wanadamu hawawezi kuondoa ugonjwa, lakini Yehova Mungu aweza. Naye aahidi kwamba katika ulimwengu wake mpya “hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.” Badala ya hivyo, “ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” (Isaya 33:24; 35:5, 6) Naam, Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.
Yesu Kristo alipokuwa duniani, alionyesha mambo tuwezayo kutazamia kwa kiwango kikubwa zaidi katika ulimwengu mpya wa Mungu. Alifumbua macho ya vipofu, alizibua masikio ya viziwi, alifungua ulimi wa mabubu, aliwezesha vilema kutembea, na hata alirudisha wafu kwenye uhai.—Mathayo 15:30, 31; Luka 7:21, 22.
Kazi Yenye Kuridhisha na Haki kwa Wote
Hapana shaka kwamba kazi na haki zenye kuridhisha kwa wote zingekuwapo katika ulimwengu ambao wewe na karibu kila mtu mwingine angetaka. Kwa hiyo madaktari hao waliandika hivi: “[Takwa] la nne, ungekuwa ulimwengu ulio na kazi kwa wale ambao wataka kupata riziki kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya familia zao.” Nao waliongeza hivi: “La Tano, ungekuwa ni ulimwengu ambamo kila mtu angefurahia uhuru ulio chini ya sheria, kukiwa na haki kwa wote.”
Utawala wa kibinadamu haujaweza kamwe kutimiza matakwa hayo kwa ajili ya maisha yenye furaha. Lakini ulimwengu mpya wa Mungu utafanya hivyo. Biblia yaahidi hivi kuhusu kazi yenye kunufaisha ambayo watu watafanya wakati huo: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. . . . na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:21-23.
Namna gani kuhusu uhuru na haki kwa wote? Hata watawala wa kibinadamu wawe wamejitahidi kwa unyoofu kadiri gani, wameshindwa kuziandaa kwa kila mtu. Ukosefu wa haki na uonevu waendelea kutawala ulimwenguni pote. Kwa hiyo wanadamu hawawezi kamwe kuridhisha uhitaji huo. Lakini Mungu Mweza Yote aweza. Mtawala wake aliyewekwa ni Yesu Kristo aliyefufuliwa, na Yehova asema hivi juu yake: “Mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; . . . naye atawatolea mataifa hukumu.”—Isaya 42:1; Mathayo 12:18.
Naam, Biblia yaahidi kwamba chini ya Ufalme wa Mungu “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Warumi 8:21) Utakuwa ulimwengu mpya wenye kufurahisha kama nini kutakapokuwapo uhuru na haki kwa wote!
Fursa Nyingi na Mambo Yenye Kufurahisha
Kwa kweli, katika ulimwengu unaotaka, raia wote wangefurahia fursa sawa hata wawe wa rangi gani au taifa gani. Kwa hiyo, haishangazi kwamba takwa muhimu la chini zaidi la sita lililoorodheshwa na madaktari hao ni: “Ungekuwa ni ulimwengu ambamo kila binadamu angekuwa na fursa ya kusitawisha uwezo wake na vipawa vyake kikamili, na kuthawabishwa kwa ajili ya jitihada zake, bila upendeleo.”
Wanadamu hawajaweza kamwe kusimamisha ulimwengu ambamo watu wote wafurahia kutendewa vizuri. Uonevu na hata mnyanyaso wa vikundi vya watu wachache wasiopendwa waendelea bila kukoma. Lakini, Mfalme wa ulimwengu mpya wa Mungu, Yesu Kristo, ataiga kielelezo cha Yehova, Baba yake, “asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali rushwa.” (Kumbukumbu la Torati 10:17; Warumi 2:11) Jambo litakalofanya ulimwengu mpya unaokuja uwe wa ajabu sana ni kwamba watu hawatafundishwa tu kuiga Yehova Mungu katika kutokupendelea bali watakufanya kwa matendo.—Isaya 54:13.
Mara nyingi watu wametoa uhai wao kwa kazi ngumu isiyoisha kwa kupata kitulizo kidogo tu au hata bila kupata kitulizo. Kwa hiyo kwa hakika utakubaliana na takwa la chini zaidi linalofuata, yaani: “La saba, ungekuwa ni ulimwengu ambamo watu wote wangekuwa na wasaa wa kutosha kufurahia vile vitu wanavyoona kuwa vizuri maishani.”
Akijua uhitaji wa mtu wa vipindi vya mapumziko na starehe, Yehova Mungu katika Sheria yake ya kale aliandaa siku ya kupumzika kila juma. (Kutoka 20:8-11) Kwa hiyo, twaweza kuwa na hakika kwamba katika ulimwengu wake mpya, Mungu atahakikisha kwamba uhitaji wetu wa kustarehe na namna nyingi za tafrija zenye kufaa zitakuwapo.
Aina ya Wakazi
Jambo la mwisho lililotajwa na madaktari hao laonyesha sifa za wale ambao wangeishi katika “aina ya ulimwengu ambao sisi sote tungependa kuishi ndani yayo.” Ona kama hukubali kwamba sifa hizi wanazoorodhesha ni muhimu. “La nane, ungekuwa ulimwengu ambamo thamani kubwa sana ingewekewa sifa zile zinazotofautisha mwanadamu kutokana na wanyama, kama vile werevu na uwezo wa kubuni mambo, heshima na uaminifu-maadili, upendo na uaminifu-mshikamanifu, kujistahi na kutoonyesha choyo, na hangaiko kwa ajili ya wanadamu wenzake.”
Je! hungefurahia kuishi katika ulimwengu ambamo kila mtu anazo sifa za kimaadili za uaminifu-maadili, upendo, uaminifu-mshikamanifu, ukosefu wa choyo, na hangaiko kwa wanadamu wenzake? Kwa hakika hiyo ndiyo aina ya ulimwengu unayotaka! Hakuna viongozi wa kibinadamu wawezao kuandaa mambo hayo. Ni Yehova Mungu pekee awezaye. Naye atafanya hivyo kwa sababu ulimwengu wake mpya si ndoto tu inayootwa.—Zaburi 85:10, 11.
Utakuja Lini?
Kama ilivyotajwa katika makala inayotangulia, mwandamani wa karibu wa Yesu Kristo aliandika hivi: “Kama ilivyo ahadi yake [Mungu], tunatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (2 Petro 3:13) Wakati wa kutimizwa kwa ahadi hiyo itakuwa, kama Yesu alivyosema, “katika ulimwengu mpya [uumbaji-mpya, NW], atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake.”—Mathayo 19:28.
Hapo awali Mungu aliwaagiza Adamu na Hawa, wanadamu wawili wa kwanza, wapanue bustani la Paradiso ambamo Yeye aliwaweka. Aliwataka wazae watoto na wakiwa nao wafanye dunia yote iwe bustani maridadi ya Edeni. (Mwanzo 1:26-28; 2:7-9, 15) Ingawa Adamu na Hawa walishindwa kutekeleza kusudi hilo, Paradiso ya kidunia itarudishwa katika uumbaji-mpya, Kristo akitawala katika Ufalme. Hatimaye hali za Kiedeni zitaenezwa duniani pote. Hivyo Muumba wetu mpendwa atatimiza kusudi lake la awali la kuwa na ulimwengu wenye amani na uadilifu. Lakini utakuja lini?
Je! wewe hufikiri kama wengi wasemao, ‘Aa, utakuja wakati fulani lakini si katika nyakati zetu.’ Lakini, wajuaje? Je! yawezekana kwamba wakati wetu wenye taabu isiyo na kikomo waweza kuwa ishara ya kwamba ulimwengu mpya wa Mungu umewadia? Twaweza kujuaje?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na amani, afya kamilifu, na ufanisi
[Hisani]
Watoto wa simba: Kwa hisani ya Hifadhi ya Nyoka na Wanyama ya Hartebeespoortdam
[Picha katika ukurasa wa 8]
Katika ulimwengu mpya, watu watafurahia kufanya kazi yenye matokeo
[Picha katika ukurasa wa 9]
Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na wasaa wa utendaji wenye kufurahisha