Maoni ya Biblia
Msaada kwa Kihoro Chako
“HUZUNI HUFANYA SISI SOTE TUWE WATOTO TENA—HUHARIBU TOFAUTI ZOTE ZA VIWANGO VYA AKILI. WALIO NA HEKIMA ZAIDI HUWA HAWAJUI KITU.”
—RALPH WALDO EMERSON, MSHAIRI NA MTUNGA-INSHA MWAMERIKA WA KARNE YA 19.[1]
ULE uchungu wa kifo si kwamba tu huwatia maumivu bali pia huwatia ganzi waliofiwa—mume, mke, baba, mama, mwana, binti, au rafiki. Huenda walio na hekima wakauliza maswali lakini wasisikie majibu yoyote ya kufariji, na wenye nguvu huenda wakalia machozi kwa kulemewa na kihoro lakini wasipate kitulizo. Wasomaji wa Biblia huenda wakakumbushwa na jambo hilo juu ya kilio kilichopaazwa na Daudi wakati Absalomu mhaini alipouawa: “Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 18:33) Hicho hakikuwa kilio cha mfalme juu ya msaliti; kilikuwa kilio cha baba juu ya mwana wake mfu. Huenda ikawa wewe pia umekuwa na hisia kama hiyo ulipofiwa.
Wakati wa kihoro kingi sana, maswali ya kusumbua huenda yakaja akilini. ‘Kwa nini nipatwe na hilo? Mungu alijua ingekuwa hivyo? Kama alijua, mbona hakuzuia?’ Hata ingawa huenda mtu akawa aijua vema Biblia na kujua kwamba wafu watafufuliwa, maswali yenye kukera sana huenda yakataka kutafakari kwingi ili kupata uliwazo na faraja.
Majibu yenye makosa hayaleti uradhi wa kweli, ila faraja bandia. Kuambiwa kwamba ‘Mungu alimhitaji mpendwa wako’ husababisha mara nyingi kumwepuka Mungu kwa roho ya uchungu. Ile kweli, kama ilivyo katika Biblia, hujibu maswali juu ya kihoro na kuvuta mtu karibu zaidi na Yehova Mungu, badala ya kumsukuma mbali naye. Twahakikishiwa kwenye 2 Wakorintho 1:3, 4 kwamba yeye ndiye Baba wa rehema nyororo na ndiye Mungu wa faraja yote.
Ujuzi wa Mungu na Nguvu Vimesawazika
Yehova, Mweza Yote, ajua yote yatendekayo katika uumbaji wake ulio mkubwa sana. Zaburi 11:4 hutuhakikishia hivi: “BWANA [Yehova, NW] ambaye kiti chake kiko mbinguni, macho yake yanaangalia; kope zake zinawajaribu wanadamu.” Kwenye Waebrania 4:13 mtume Paulo aliandika hivi: “Hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake.” Si kwamba Mungu ajua tu bali pia hujali! Kasema Yesu: “Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; . . . bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”—Mathayo 10:29, 31.
Je! Mungu angaliweza kukizuia kifo cha mapema mno cha mpendwa na kihoro kilichofuata? Ndiyo, angaliweza. “Yote yawezekana kwa Mungu,” kataarifu Yesu. (Marko 10:27) Zamani za kale, Yehova alitega sikio kwa sala ya Hezekia mwenye kufa akamponya na kumwongezea miaka ya kuishi. (Isaya 38:2-5) Hakuna shaka kwamba Yehova ana uwezo wa kufanya yote apendayo, lakini ni lazima sisi tuelewe mengi zaidi juu ya penzi lake. Sisi sote tumesoma masimulizi ya watu waliokuwa wameumizwa vibaya sana au waliokuwa wagonjwa sana, na bado wakawa hai. Je! Yehova aliingilia mambo kwa ajili yao?
Watu fulani wana nguvu zisizo za kawaida za kupata nafuu na wana nia yenye nguvu ya kuishi. Hilo huenda likaeleza kwa nini wao huonekana kupona kimwujiza. Au huenda ikawa matibabu fulani mapya yalileta mafanikio. Hivyo, ni lazima tusikate shauri moja kwa moja tu kwamba ni Yehova aliyeingilia mambo.—Wafilipi 4:13.
Neno la Mungu Laeleza kwa Nini Watu Hufa
Kwenye Warumi 5:12, mtume Paulo aeleza kwa urahisi sana kwamba Adamu baba yetu wa zamani aliasi dhidi ya Muumba wake na kwa haki akahukumiwa kufa. Kwa kuwa sisi ni wazao wake, sisi ni watenda dhambi na tuko chini ya wajibu wa kufa wakati wowote. Hatuna uthibitishio kamili wa kuendelea kuwa hai. Mfalme Sulemani mwenye hekima aelewesha wazi kwamba wakati na tukio lisilotazamiwa laweza kumpata yeyote wakati wowote, iwe ni aksidenti ya kifo au ugonjwa wa ghafula ambao huleta kifo hatimaye. Au mtu aweza kuzaliwa akiwa na kasoro ya kurithi yenye kufupisha maisha yake. Sulemani aeleza pia kwamba kwa Mungu kuna wakati na majira ya kila jambo. Mungu ameweka wakati wa kuponya, si mtu mmoja tu au wachache, bali ainabinadamu yote yenye kuamini wakati wa utawala wa Kristo Yesu.—Mhubiri 3:1; 9:11; 1 Wakorintho 15:25, 26.
Kumbuka wazo hili lenye kutia makini: Wakristo hawaepushwi wasipatwe na misiba inayopata jamii ya kibinadamu na hivyo wao waweza kupatwa na mambo yaliyo kawaida ya ainabinadamu. “Majaribu ambayo mmelazimika kuyahimili hayazidi yale ambayo watu huwa nayo kwa kawaida.”—1 Wakorintho 10:13, The Jerusalem Bible.
Njia ya Kupona
Kifo ni wakati wa kutoa machozi yaliyochanganyikana na sihi ya moyo mweupe sana kwa Yehova, yule Msikiaji wa sala. Sasa zaidi ya wakati mwingine wowote, mkaribie Mungu. Sasa zaidi ya wakati mwingineo wote, mimina moyo wako katika dua ya kuomba ufahamu wenye kina, kuomba nguvu za kujipatanisha na hali. Biblia hututia moyo tufanye hivyo hasa. Petro asema hivi: “Huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.” (1 Petro 5:7) Ni yenye kufariji kama nini maneno ya Mungu kwenye Isaya 57:15: “Yeye aliye juu, aliyetukuka, akaaye milele; ambaye jina lake ni Mtakatifu; asema hivi; Nakaa mimi mahali palipoinuka, palipo patakatifu; tena pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu na kunyenyekea, ili kuzifufua roho za wanyenyekevu, na kuifufua mioyo yao waliotubu [waliopondeka hisia, NW].” Aliyepondeka hisia hujiambatisha sana kwa Baba; huwa kuna uhusiano wa kindani zaidi ya wakati mwingineo wote. “Kadiri mwendavyo karibu zaidi na Mungu, ndivyo yeye atakavyokuja karibu zaidi nanyi,” aandika Yakobo. (Yakobo 4:8, JB) Yakobo atuhakikishia kwamba Mungu ana nia ya kutupa sisi hekima ambayo yahitajika kabisa na nguvu za kupata nafuu.
Kwa kuongezea, utapata kwamba utakuwa mtu mwenye huruma zaidi kuhusu majaribu na misiba ya wengine, mwenye kuwasikitikia zaidi. Utajua mengi zaidi juu ya jinsi watu wengine huhisi na jinsi ya kutoa maneno ya faraja na tumaini. Huenda ukaweza kusaidia mtu mwenye kihoro ashinde huzuni yake. Ndiyo, utakuwa mwenye hisiamoyo nyingi zaidi kwa wengine katika msononeko wao.—Wafilipi 2:1.
Kupoteza mpendwa kwaweza kutia kihoro na maumivu kwa muda fulani, labda kwa muda mrefu. Hata hivyo, mwishowe, huenda kukatokeza maoni ya kuelewa wazi zaidi lile tumaini lililoko mbele, lile tumaini la kumtumikia Mungu bila maumizo. Twaweza hata kuwa wenye nguvu zaidi katika utu wetu wa Kikristo.—1 Petro 1:6, 7.
Kwa hiyo kujapokuwa na umivu la kihoro, usikate tamaa kamwe! Azimia kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu na kwa ushikamanifu, kwa utukufu na heshima yake na kwa wokovu wako wa milele.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]
The Day Before Parting cha Jozef Israels: Zawadi ya Alice N. Lincoln, Hisani ya Museum of Fine Arts, Bostony