Je! Neno la Mungu Hufundisha Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine?
MTU yeyote anayechunguza Biblia akiwa na matumaini ya kuungwa mkono kwa fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine kwa hakika atatamauka. Hakuna popote katika Biblia utakapopata kwamba wanadamu wameishi maisha ya awali. Zaidi ya hilo, hutapata katika Biblia misemo kama vile “kuzaliwa upya katika mwili mwingine” au “kuhamishwa kwa nafsi” au “nafsi isiyoweza kufa.”
Hata hivyo, wale wanaoamini katika kuzaliwa upya katika mwili mwingine hujaribu kuelezea huku kutokuungwa mkono na Biblia kwa kusema kwamba wazo la kuzaliwa upya katika mwili mwingine lilijulikana sana nyakati za kale hivi kwamba maelezo yoyote hayangekuwa ya lazima. Ni kweli, fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine ni la awali sana, lakini bila kujali ni la awali kadiri gani au lilijulikana kadiri gani au sivyo, bado swali ni, Je! Biblia hulifundisha?
Kwenye 2 Timotheo 3:16, 17, mtume Paulo aliandika hivi: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” Naam, Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa, uwasiliano wake na familia ya kibinadamu. Na kama vile Paulo alivyoandika, inamwezesha mtafiti mwenye moyo mweupe awe “kamili, amekamilishwa” kujibu maswali yote muhimu kuhusu maisha, kutia na maswali juu ya wakati uliopita, wakati wa sasa, na wakati ujao.
Paulo pia aliandika: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli.” (1 Wathesalonike 2:13) Kwa kuwa Biblia ina mawazo ya Mungu, si yale ya mwanadamu asiye mkamilifu, haipaswi kutushangaza kwamba mara kwa mara Biblia hutofautiana na mawazo ya mwanadamu hata kama hayo yamejulikana kwa miaka mingi. Lakini huenda ukasema, ‘Je! Biblia haidokezi mahali pengine, angalau kudokeza kuzaliwa upya katika mwili mwingine?’
Maandiko Yanayoeleweka Vibaya
Wale wanaoamini kuzaliwa upya katika mwili mwingine husema kwamba Biblia hurejezea jambo hilo kifupi kwenye Mathayo 17:11-13, ambamo Yesu ahusianisha Yohana Mbatizaji na nabii wa kale Eliya. Andiko hili lasomeka hivi: “Kweli Eliya yuaja kwanza, naye atatengeneza yote; ila nawaambia, ya kwamba Eliya amekwisha kuja . . . Ndipo wale wanafunzi walipofahamu ya kuwa amesema nao habari za Yohana Mbatizaji.”
Kwa kusema hivyo, je, Yesu alimaanisha kwamba Yohana Mbatizaji alizaliwa upya katika mwili wa nabii Eliya? Yohana mwenyewe alijua kuwa hakuwa. Katika pindi moja alipoulizwa, “U Eliya wewe?” Yohana alijibu waziwazi: “Mimi siye.” (Yohana 1:21) Hata hivyo, ilikuwa imetabiriwa kwamba Yohana angemtangulia Mesiya “katika roho ya Eliya, na nguvu zake.” (Luka 1:17; Malaki 4:5, 6) Yaani, Yohana Mbatizaji alikuwa “Eliya” katika maana ya kwamba alifanya kazi iliyolingana na ile ya Eliya.
Kwenye Yohana 9:1, 2, twasoma: “Hata [Yesu] alipokuwa akipita alimwona mtu, kipofu tangu kuzaliwa. Wanafunzi wake wakamwuliza wakisema, Rabi, ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu?” Watu fulani wanaoamini kuzaliwa upya katika mwili mwingine wanadokeza kwamba kwa kuwa mtu huyo alizaliwa akiwa kipofu, dhambi yake ni lazima iwe ilitukia katika maisha yake ya awali.
Lakini chochote kilichowafanya wanafunzi waulize swali hilo, jibu alilopeana Yesu ni lazima liwe ndilo jambo la kuamulia. Yeye alisema hivi: “Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake.” (Yohana 9:3) Hilo lapinga kuzaliwa upya katika mwili mwingine, ambako kwaonyesha kwamba kasoro za mwili zategemea dhambi za maisha ya awali. Jambo la kwamba hakuna mtu yeyote awezaye kufanya dhambi kabla hajazaliwa lilisemwa pia na Paulo alipoandika kuhusu Esau na Yakobo kwamba ‘walikuwa bado hawajazaliwa wala kuzoea kufanya jambo jema au ovu.’—Warumi 9:11, New World Translation.
Ufufuo, Si Kuzaliwa Upya Katika Mwili Mwingine
Ijapokuwa Biblia haiungi mkono fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine, hakuna mtu yeyote anayepaswa kutamauka. Ujumbe wa Biblia hutoa jambo fulani lenye kufariji zaidi kuliko wazo la kuzaliwa tena katika ulimwengu uliojaa magonjwa, huzuni, maumivu, na kifo. Na si kwamba kile Biblia inatoa ni chenye kufariji pekee bali ni kweli, Neno la Mungu mwenyewe.
Paulo alielezea fundisho lenye kutia moyo katika njia hii: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” Neno “ufufuo,” au namna yake, hupatikana zaidi ya mara 50 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na Paulo aongea juu yao likiwa fundisho la msingi la imani ya Kikristo.—Matendo 24:15; Waebrania 6:1, 2.
Ufufuo kutoka wafu wamaanisha, kwa wazi, kwamba kifo kipo. Hakuna popote katika Biblia utakapopata dokezo lolote kwamba mtu ana nafsi isiyoweza kufa. Ikiwa mtu alikuwa na nafsi isiyoweza kufa ambayo ilitenganishwa na mwili wakati wa kifo na ikaenda kwenye makao ya milele katika mbingu au katika helo au ikazaliwa upya katika mwili mwingine, basi hakungekuwa na uhitaji wa ufufuo. Kwa upande mwingine, maandiko ya Biblia yapatayo mia moja hivi yaonyesha kwamba nafsi ya kibinadamu, si isiyoweza kufa, bali iwezayo kufa na kuharibiwa. Biblia huongea kwa upatani juu ya kifo kuwa kinyume cha uhai, yaani, kutokuwapo kukitofautishwa na kuwapo.
Kifo, au kutokuwapo, kulikuwa adhabu kwa dhambi ya Adamu na Hawa dhidi ya Mungu. Kilikuwa adhabu, si kuingia kwenye uhai usioweza kufa mahali pengine. Mungu alisema waziwazi kwamba walikuwa warudi kule walikotoka—mavumbi ya mchangani: “Katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Hawakuwa na nafsi isiyoweza kufa kabla hawajaumbwa na Mungu na kuwekwa duniani, katika bustani ya Edeni, na hawakuwa na yoyote baada ya kufa.
Ufufuo kutoka wafu unafananishwa na kuamuka kutoka usingizini, au pumzikoni. Kwa kielelezo, Yesu alisema juu ya Lazaro ambaye alikuwa anaenda kumfufua: “Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha.” (Yohana 11:11) Kuhusu nabii Danieli, twasoma: “Utastarehe, nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.”—Danieli 12:13.
Uhai wa Milele Duniani
Ni nini litakalokuwa tokeo kwa wale watakaofufuliwa kutoka kifo? Biblia husema juu ya ufufuo wa aina mbili—wa kimbingu na ule wa kidunia. Ufufuo wa kidunia utakuwa tokeo la wengi wale walioishi na wakafa. Ni wachache tu ndio walio na ufufuo wa kimbingu, watawale na Kristo katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu. (Ufunuo 14:1-3; 20:4) Ufufuo wa kidunia utaanza lini? Utaanza baada ya mfumo mbovu wa sasa kuharibiwa na Mungu na “dunia mpya,” jamii mpya yenye uadilifu ya kibinadamu imekuwa hakika.—2 Petro 3:13; Mithali 2:21, 22; Danieli 2:44.
Katika “dunia mpya,” hakutakuwapo magonjwa wala kuteseka. Hata kifo hakitakuwapo tena bali mahali pake patachukuliwa na matazamio ya uhai wa milele. “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” (Ufunuo 21:4) Pia, mtunga-zaburi alitabiri hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Vivyo hivyo, Yesu alisema: “Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.”—Mathayo 5:5.
Linganisha ahadi hizo tukufu za Mungu na fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine. Kulingana na wazo hilo, inafikiriwa kwamba unarudi kuishi mara kwa mara katika mfumo huu huu wa mambo wa kale uliofisidika. Hilo lamaanisha kwamba utaendelea kuzungukwa na maovu, kuteseka, ugonjwa, na kufa kwa mizunguko isiyo na mwisho. Huo ni wakati ujao usio na tumaini jinsi gani!
Hivyo, Biblia yajibu maswali, Je! umepata kuishi awali? na, Je! utaishi tena? katika njia hii: La, hujapata kuishi maisha yoyote isipokuwa ya sasa. Lakini inawezekana kwako kufanya maisha yako yadumu, naam, ya milele. Leo, katika hizi “siku za mwisho” za mfumo wa sasa, unaweza kuwa na tumaini la kuokoka mwisho wa ulimwengu huu na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu bila kufa. (2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 7:9-15) Au ukifa kabla ya ulimwengu mpya wa Mungu kufika, unaweza kuwa na tumaini la kufufuliwa kwenye uhai wa milele katika paradiso duniani.—Luka 23:43.
Ukitia imani katika Yesu, bila kujali litakalotokea, maneno ya Yesu kwa Martha wakati ndugu yake Lazaro alipokufa pia yatumika kwako: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—Yohana 11:25, 26.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Adamu hakuwa na nafsi isiyoweza kufa bali alirudi mavumbini alipokufa
[Picha katika ukurasa wa 9]
Neno la Mungu hufundisha ufufuo, si kuzaliwa upya katika mwili mwingine