Vijana Huuliza . . .
Kunusa Gundi—Je! Kweli Kwaweza Kuniumiza?
“NI JAMBO zuri sana—ni kama tu kutazama katuni.” Ndivyo asemavyo Sveta, msichana wa miaka 13 kutoka Moscow, Urusi.a Lakini Sveta hapayuki juu ya filamu au video ya karibuni zaidi. Anaeleza alilojionea kutokana na namna fulani ya utumizi mbaya wa dawa upendwao na maelfu ya vijana kotekote ulimwenguni—kunusa gundi (gamu).
Ingawa hivyo, gundi ni kimojapo tu vitu vingi ambavyo vijana fulani wananusa. Kwa kielelezo, katika Uingereza vipulizo vya manukato, umafuta wa kuwashia moto, na “vitu vingine 20 hadi 30 vya matumizi ya kawaida nyumbani . . . vinatumiwa vibaya,” kulingana na gazeti Young People Now. Hii yatia ndani “vipulizo vya kutuliza maumivu, ving’arisha-fanicha, na vifaa vya kuziba mipira iliyotoboka ya magurudumu.” Naam, vijana fulani hata hunusa mivuke ya dawa za kuzima moto! Kwa hiyo ni sahihi zaidi kuita zoea hili lenye madhara lakini lipendwalo na wengi “utumizi mbaya wa viyeyusho” au “utumizi mbaya wa mivuke,” kama waviitavyo wastadi fulani.
Iwe ni gundi au ni ving’arisha-fanicha wanayotumia vibaya, wanusaji hutafuta matokeo yaleyale mamoja. Kulingana na chanzo kimoja, wao hutaka “kuwa na hali kama ya kulewa.” Viyeyusho ni vya bei rahisi na hupatikana kwa urahisi kuliko dawa kali zaidi za kulevya kama kokeni. Hivyo gazeti New Scientist la Uingereza liliripoti hivi: “Viyeyusho vimekuwa tena dawa ya kulevya ya walio maskini, vijana na wasio na makao: watoto wa barabarani wa Guatemala na wakaaji wa vitongoji katika Amerika Kaskazini, na pia vijana katika mahosteli na vibanda vya kujilaza usiku katika Uingereza.” Wenye mamlaka fulani huamini kwamba katika Uingereza, 1 kati ya wasichana na wavulana 10 matineja amenusa viyeyusho. Navyo havikosi madhara.
Kijitabu Drug Misuse chaeleza kwamba “mivuke ya kuyeyuka ivutwayo huvutwa kupitia mapafu na kufikia ubongo upesi sana.” Viyeyusho huathiri mfumo mkuu wa mishipa ya fahamu na vyaweza, kama kileo, kutokeza raha nyingi ya muda. Katika watumiaji fulani, hivyo hata hutokeza maono mbalimbali ya ajabu-ajabu kwa muda mfupi—na si yote yaliyo ya kupendeza kama yale yaliyoelezwa na Sveta pale mwanzoni. “Mimi niliona panya wengi sana,” asema kijana mmoja aitwaye David aliyenusa gundi akiwa na umri wa miaka 14. “Walikuwa maelfu—wale wadogo wakitoka katika wale wakubwa zaidi. Nilifikiri walikuwa wakimla rafiki yangu.” Kijana mmoja Mjapani jina lake Kazuhiko, ambaye alianza kunusa gundi akiwa na umri wa miaka 17, akumbuka hivi: “Niliiona ardhi ikiachana kwa kupasuka, na hayawani wakinishambulia.”
Basi, kwa nini kunusa gundi huvutia sana vijana fulani? Lee, aliyeanza kunusa gundi alipokuwa na miaka 13, asema hivi: “Hasa, sababu ya watu kufanya hivyo ni kujaribu kuyakimbia magumu ya maisha.” Ndiyo, vijana fulani huona kwamba kuwa na hali kama ya kulewa kutokana na viyeyusho ni njia ya kusahau matatizo. Wengine hutamani ule msisimko; wao hufikiri kwamba maono ya kuogopesha sana ni kama filamu ya maogofyo yenye kutumbuiza. “Sababu nyinginezo,” yasema Idara ya Afya ya Ireland, “zatia ndani kutaka kujua, kuitikia mkazo wa marika, majaribio ya kupata heshima ya juu, kujazia ukosefu wa kujiheshimu na hisia za kukosa utoshelevu.”
Kifo cha Ghafula
Hata kunusa viyeyusho kuwe kwavutia kadiri gani, hilo ni zoea lenye kuua! Lilisababisha vifo 149 katika Uingereza katika 1990, na nyakati fulani huua kwa muda wa dakika chache tu. Hicho huitwa “kifo cha ghafula cha unusaji.” Kwa kielelezo, Rachel alikuwa akimwaga umajimaji wa kufuta makosa ya chapa za taipureta juu ya mkono wa vazi lake na kuunusa akiwa shuleni. Siku moja aliunusa akisafiri ndani ya basi. Alitoka kwenye basi hiyo akaanguka chini. Alisimama kwa muda na kubwagika chini tena—maiti! Rachel alikuwa na miaka 15.
Jambo la kuogopesha hasa ni uhakika wa kwamba viyeyusho vyaweza kukuua mara ileile ya kwanza uvitumiapo vibaya! Re-Solv, ambalo ni shirika la ufadhili la Uingereza lililoanzishwa ili kupambana na utumizi mbaya wa viyeyusho, laripoti kwamba “asilimia 18 ya waliouawa na utumizi mbaya wa viyeyusho kati ya 1971 na 1989 walikuwa ‘wanusaji’ wa mara ya kwanza.” Aliye mchanga zaidi kufa alikuwa na umri wa miaka tisa tu. Kama vile ilivyo kuhusu utumizi mbaya wa kileo, utumizi mbaya wa viyeyusho waweza kusemwa kuwa huuma ‘kama nyoka na kuchoma kama fira.’—Mithali 23:32.
Wanusaji waweza kufa pia kutokana na aksidenti zitukiazo wakiwa wamelewa viyeyusho. Baadhi yao wameanguka kutoka kwenye majengo au wakafa maji. Wengine wamepoteza fahamu na kusongwa pumzi na matapiko yao wenyewe. Baadhi hata wamekufa kutokana na kunusa wakiwa wamefunika vichwa vyao kwa mfuko wa plastiki; walilewa kiasi cha kwamba walishindwa kuuondoa mfuko huo, basi wakaishiwa pumzi. Hata hivyo wengine wamechomeka hadi kufa wakati vile viyeyusho viliposhika moto.
Uchafuzi wa Mwili na Hatari Nyinginezo
Ingawa matokeo yenye msiba hivyo hayawapati watu wote, mstadi mmoja aandika hivi: “Mtumizi mbaya wa kawaida ajua kwamba ‘anachafua’ mfumo wake naye hupatwa na maumivu ya kifua, kukosa usawaziko, maumivu ya kichwa, upotevu wa kumbukumbu na wingi wa dalili nyinginezo ambazo ni mara chache sana yeye hukubali kwamba anazo.” Lee (aliyenukuliwa mapema kidogo) akumbuka hivi: “Nilipata maumivu ya kichwa ambayo ndiyo yamepata kuwa mabaya zaidi maishani mwangu.” Shirika Re-Solv lasema kwamba viyeyusho vyaweza pia kuharibu figo na ini, vyaweza kuleta uharibifu wa akili, na vyaweza kusababisha mshuko wa moyo.
Halafu kuna zile hatari za kiadili. Wanusaji fulani wamekuwa wezi ili kutegemeza zoea lao. Au fikiria lile lililoripotiwa katika Daily Yomiuri la Japani: “Mmoja wa wale vijana watatu walioshtakiwa kwa mauaji ya msichana mmoja tineja [alisema] kwamba hakuhisi hatia yoyote alipokuwa akiua msichana huyo kwa sababu alikuwa amelewa [viyeyusho] wakati huo.”
Mwishowe, utumizi mbaya wa viyeyusho waweza kutokeza kutegemea viyeyusho kihisiamoyo—uraibu. “Yapata asilimia 10 ya wale waliotumia vibaya viyeyusho walipata kuwa wanusaji wa daima,” lasema Glasgow Herald la Scotland. Jambo hili laweza kuzuia tu ukuzi wa mtu wa kihisiamoyo na wa kiroho. Fikiria maneno ya Biblia kwenye 1 Wakorintho 14:20: “Msiwe watoto katika akili zenu; lakini . . . katika akili zenu mkawe watu wazima.” Mtu huwaje mtu mzima katika jambo hili? Biblia hueleza hivi kwenye Waebrania 5:14: “Chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” Mraibu hushindwa kusitawisha nguvu zake za ufahamu. Badala ya kukabiliana na matatizo, yeye hujaribu kuyaepuka kwa mpumbao wenye kuchochewa na dawa za kulevya. Gazeti Young People Now lilisema kwamba wanusaji wa daima ‘hunaswa mtegoni wakiwa matineja—wasiweze kuingia utu mzima.’
Usijaribu Kamwe!
Huenda ikawa wajua marika wako fulani ambao wamejaribu kunusa viyeyusho, na ni kawaida sana kutaka kujua. Lakini Biblia yasema hivi: “Na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kwa nini ujaribu kitu ambacho huchafua mwili wako au kisababishacho upoteze udhibiti wa akili yako, hata kwa muda tu? Shauri la Neno la Mungu kwetu ni “tukeshe.” (1 Wathesalonike 5:6) Kifungu hiki humaanisha kwa halisi “na tuwe timamu.” Badala ya kuchafua uwezo wake wa kufikiri wenye thamani, kwa hekima Mkristo huulinda.—Mithali 2:11; 5:2.
Kazuhiko asema hivi: “Najuta kwamba hata nilianza zoea hilo.” Lee akubali, akisema: “Ni upumbavu. Kufanya hivyo ni hatari sana sana.” Jiepushe na maumivu na huzuni nyingi, na usijaribu kunusa viyeyusho palepale mwanzoni. Tenda kama vile Biblia isemavyo: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”—Mithali 22:3.
Ingawa hivyo, huenda isiwe rahisi kutumia shauri hili. “Mkazo wa marika” husemwa kuwa moja ya sababu za kawaida zaidi zifanyazo vijana wanaswe katika utumizi mbaya wa viyeyusho. “Ndugu yangu ndiye aliyenifanya nipendezwe na kunusa gundi,” asema kijana David. “Rafiki zangu ndio walionijulisha juu yayo,” aongezea Kazuhiko. Ndiyo, kama vile 1 Wakorintho 15:33, New World Translation, isemavyo, “mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” Kwa nini uache marika waharibu maisha yako? Yehova Mungu, Baba yetu wa kimbingu, ahimiza hivi: “Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, wewe usikubali.”—Mithali 1:10.
Kwa hekima, na uwajulishe wazazi wako ikiwa wengine wanakubana utumie dawa za kulevya. Wao waweza kusaidia kuimarisha azimio lako la kukataa. Kwa upande mwingine, labda wewe washawishwa kujaribu kunusa viyeyusho kwa sababu wahisi ukibanwa au ukilemewa na matatizo. Kitulizo kizuri zaidi cha mbano ni kuongea juu ya matatizo yako pamoja na wazazi wako au mtu mzima mwingine aliyekomaa, mwenye huruma. Wahitaji mwongozo, si kukimbia matatizo kwa kuchochewa na dawa za kulevya. Waweza pia kujifaidi na uandalizi wa sala ili ikusaidie kukabili hali. “Mtumainini [Mungu] sikuzote,” asema mtunga-zaburi. “Ifunueni [“mwageni,” NW] mioyo yenu mbele zake.”—Zaburi 62:8.
Kunusa viyeyusho huenda kukaonekana kuwa kunasisimua, lakini hakutatatua matatizo yako. Kwa kweli, kwaweza kuharibu maisha yako. Uwe na akili. Usijaribu kamwe.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Usiruhusu mkazo wa marika ukuvute katika zoea lenye kufisha