Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 10/8 kur. 10-13
  • Kuzuia Nyumbani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzuia Nyumbani
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sheria za adili
  • Kichwa cha Familia Mwenye Upendo
  • Mahali Salama Kihisiamoyo
  • Komesha Visa vya Kutendwa Vibaya
  • Mwisho wa Kutendwa Vibaya
  • Upendo na Haki Katika Ulimwengu Mwovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Mawazo Yasiyo ya Kweli Ambayo Ni ya Kawaida
    Amkeni!—1993
  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007
  • Mashaka Yako Ulimwenguni Kote
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 10/8 kur. 10-13

Kuzuia Nyumbani

Monique alikuwa na miaka tisa alipoanza kutendwa vibaya na mwanamume. Huyo mwanamume alianza kwa kumchungulia msichana alipokuwa akivua nguo; kisha akaanza kuja chumbani mwake usiku na kugusa sehemu zake za faragha. Alipomkinza mwanamume, akakasirika. Wakati mmoja yeye hata alimshambulia msichana kwa nyundo akamtupa chini kwenye ngazi. “Hakuna mtu ambaye angeweza kuniamini,” akumbuka Monique—hata mama yake. Yule aliyemtenda vibaya alikuwa baba wa kambo wa Monique.

YULE mtu aliye tisho kubwa zaidi kwa watoto, si yule asiyejulikana, mpweke anayeotea vichakani. Ni mshiriki fulani wa familia. Visa vingi vya kutendwa vibaya kingono hutukia nyumbani. Kwa hiyo ni jinsi gani nyumbani kwaweza kufanywa kuwe salama zaidi dhidi ya visa vya kutendwa vibaya?

Katika kitabu chake Slaughter of the Innocents, mwanahistoria Dakt. Sander J. Breiner achunguza ithibati ya kutenda watoto vibaya kingono katika jumuiya tano za kale—Misri, China, Ugiriki, Roma, na Israeli. Yeye akata maneno kwamba ingawa kulikuwa visa vya kutendwa vibaya katika Israeli, hiyo ilikuwa nadra kwa kulinganishwa na yale mataifa mengine manne. Kwa nini? Tofauti na majirani wao, watu katika Israeli walifunzwa kuwaheshimu wanawake na watoto—maoni yaliyonurishwa waliyopata kutoka kwa Maandiko Matakatifu. Waisraeli walipotumia sheria ya kimungu kwa maisha ya familia, wao walizuia kutenda watoto vibaya. Sasa kuliko wakati mwingine wowote, familia zinahitaji viwango hivyo safi, vinavyofanya kazi.

Sheria za adili

Je! sheria ya Biblia ina matokeo kwa familia yako? Mathalani, Mambo ya Walawi 18:6 husomeka hivi: “Mtu ye yote aliye wa kwenu asimkaribie mwenziwe aliye wa jamaa yake ya karibu ili kumfunua utupu; mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].” Vivyo hivyo, kutaniko la Kikristo leo hutekeleza sheria thabiti dhidi ya aina zote za kutendwa vibaya kingono. Mtu yeyote anayemtenda vibaya mtoto kingono hujihatirisha atengwe na ushirika, atupwe nje ya kutaniko.a—1 Wakorintho 6:9, 10.

Familia zote zapaswa zijue na kujikumbusha sheria hizo pamoja. Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 lahimiza hivi: “Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.” Kukaza sheria hizo kwamaanisha mengi zaidi ya kuwahutubia watoto wako mara kwa mara. Kunatia ndani badilishano la maoni. Mara kwa mara, mama na pia baba wapaswa wakazie sheria za Mungu dhidi ya ngono za kiukoo na sababu zenye upendo kwa ajili ya sheria hizo.

Pia huenda ukatumia hadithi kama ile ya Tamari na Amnoni, watoto wa Daudi, ili kuwaonyesha watoto kwamba katika mambo ya ngono kuna mipaka ambayo hakuna mtu yeyote—kutia na watu wa ukoo wa karibu—anayepaswa kuivuka.—Mwanzo 9:20-29; 2 Samweli 13:10-16.

Heshima kwa kanuni hizo yaweza kuonyeshwa hata katika mipango halisi ya kuishi. Katika nchi moja ya Mashariki, utafiti umeonyesha kwamba ngono nyingi za kiukoo hutukia katika familia ambako watoto hulala na wazazi hata wakati ambapo hakuna uhitaji wa kiuchumi wa kufanya hivyo. Vivyo hivyo, kwa kawaida, si jambo la hekima kwa ndugu na dada kulala kitanda kimoja au chumba kimoja wanapokuwa wakubwa zaidi, ikiwa hilo laweza kuepukwa kwa vyovyote. Hata wakati hali za kuishi za msongamano zinapokuwa jambo lisiloepukika, wazazi wapaswa watumie uamuzi mzuri katika kuamua ni wapi kila mshiriki wa familia apaswa kulala.

Sheria ya Biblia hukataza ulevi, ikidokeza kwamba waweza kuongoza kwenye upotovu. (Mithali 23:29-33) Kulingana na uchunguzi mmoja, wenye kutendwa ngono za kiukoo wapatao asilimia 60 hadi 70 waliripoti kwamba mzazi wao mwenye kuwatenda vibaya alikuwa akinywa kileo wakati kutendwa vibaya kulipoanza.

Kichwa cha Familia Mwenye Upendo

Watafiti hupata kwamba visa vya kutendwa vibaya ni vya kawaida zaidi miongoni mwa familia zenye waume wenye kupiga ubwana. Maoni yanayoshikiliwa sana kwamba wanawake wako ili kutosheleza mahitaji ya wanaume si ya kweli Kimaandiko. Wanaume fulani hutumia maoni hayo yasiyo ya kikristo ili kutetea hatua ya kugeukia binti zao kwa chochote wasichopata kutoka kwa mke. Aina hiyo ya ukandamizi yaweza kuwafanya wanawake katika hali hizo wapoteze usawaziko wao wa kihisiamoyo. Wengi hata hupoteza hisi ya asili ya kuwalinda watoto wao wenyewe. (Linganisha Mhubiri 7:7.) Kwa upande ule mwingine, uchunguzi mmoja ulipata kwamba wakati baba wapenda-kazi kupita kiasi walipokosekana nyumbani wakati mwingi, nyakati nyingine visa vya mama kumtenda vibaya mwanae kingono vimesitawi.

Namna gani juu ya familia yako? Je! wewe ukiwa mume huchukua daraka lako la ukichwa kwa uzito, au unaliacha kwa mke wako? (1 Wakorintho 11:3) Je! wewe humtendea mke wako kwa upendo, heshima, na staha? (Waefeso 5:25; 1 Petro 3:7) Je! wewe hufikiria maoni yake? (Mwanzo 21:12; Mithali 31:26, 28) Namna gani juu ya watoto wako? Je! wewe huwaona kuwa wenye thamani kubwa? (Zaburi 127:3) Au unawaona kuwa mizigo tu, wawezao kutumiwa vibaya kwa urahisi? (Linganisha 2 Wakorintho 12:14.) Ondolea mbali maoni yasiyonyooka, yasiyo ya kimaandiko juu ya madaraka ya familia katika nyumba yako, na utaifanya ikinze zaidi visa vya kutendwa vibaya.

Mahali Salama Kihisiamoyo

Mwanamke mmoja mchanga tutakayemwita Sandi asema: “Hali za familia yangu yote zilichochea kutendwa vibaya. Ilikuwa imetawanyika, na kila mshiriki alikuwa mbali na mwingine.” Kujitenga, ubaridi, na usiri mwingi mno—mitazamo hiyo isiyofaa, isiyo ya kimaandiko ni ishara za nyumba yenye kutenda vibaya. (Linganisha 2 Samweli 12:12; Mithali 18:1; Wafilipi 4:5.) Fanyiza hali ya nyumbani ambayo ni salama kwa watoto kihisiamoyo. Nyumbani panapaswa pawe mahali wanapojihisi wamejengwa, mahali wanapojihisi huru kufungua mioyo yao na kusema kwa uhuru.

Pia, watoto wana uhitaji mkubwa wa wonyesho wa upendo wa kimwili—kukumbatia, kupapasa-papasa, kushika mkono, kucheza. Usitende kwa kupita kiasi kwa sababu ya hatari za kutendwa vibaya kingono kwa kuzuia maonyesho haya ya upendo. Wafunze watoto kwa hisia changamfu, iliyo wazi na kwa kusifu kwamba wao wanathaminiwa. Sandi akumbuka hivi: “Maoni ya mama yangu yalikuwa kwamba haikufaa kumpa mtu yeyote pongezi kwa sababu ya jambo lolote. Hilo lingekufanya uwe na kiburi.” Sandi aliumia kwa angalau miaka kumi ya kutendwa vibaya kingono akiwa kimya. Watoto wanaokosa usalama kwa kukosa kujua kwamba wanapendwa, kwamba ni watu wanaothaminiwa, wanaelekea zaidi kuitikia sifa ya yule awatendao vibaya, “shauku nyororo” yake, au vitisho vyake vya kuiondoa.

Mtu mmoja aliyevutiwa na watoto kingono aliyewatenda vibaya kingono mamia ya wavulana kwa kipindi cha zaidi ya miaka 40 alikiri kwamba wale wavulana waliokuwa na uhitaji wa kihisiamoyo wa kupata rafiki kama yeye ndio walioelekea “zaidi” kutendwa vibaya. Usifanye kuwe na uhitaji huo kwa mtoto wako.

Komesha Visa vya Kutendwa Vibaya

Chini ya majaribu makali Ayubu alisema: “Nafsi yangu inachoka na maisha yangu; sitajizuia na kuugua kwangu. Nitanena kwa uchungu wa roho yangu.” (Ayubu 10:1) Vivyo hivyo, wazazi wengi wamepata kwamba wao wanaweza kuwasaida watoto wao kwa kujisaidia wenyewe. Hivi majuzi, gazeti The Harvard Mental Health Letter lilisema hivi: “Vizuizi vikali vya kijamii dhidi ya wanaume kusema kwamba wanaona uchungu yaonekana huchochea visa vya kutendwa vibaya.” Inaonekana kwamba wanaume ambao kamwe hawasemi juu ya maumivu yao kwamba wamepata kutendwa vibaya kingono wanaelekea sana kuwa watenda vibaya wao wenyewe. Kitabu The Safe Child Book charipoti kwamba wengi watendao watoto vibaya walitendwa vibaya kingono wao wenyewe walipokuwa watoto lakini hawakupata msaada na kupona. Wao huonyesha maumivu yao na hasira yao kwa kuwatenda vibaya watoto wengine.b—Ona pia Ayubu 7:11; 32: 20.

Hatari kwa watoto yaweza pia kuwa kubwa zaidi wakati mama wanaposhindwa kushughulikia visa vya kutendwa vibaya walivyopata zamani. Kwa kielelezo, watafiti wanaripoti kwamba mara nyingi wanawake waliotendwa vibaya kingono wakiwa wasichana huolewa na wanaume ambao hutenda watoto vibaya kingono. Isitoshe, ikiwa mwanamke fulani hajaweza kukabiliana na kutendwa vibaya wakati uliopita, yaeleweka kwamba huenda akaona vigumu kuzungumza juu ya kutendwa vibaya na watoto wake. Ikiwa kisa cha kutendwa vibaya kinatokea, huenda asiweze sana kukitambua na kuchukua hatua zinazofaa. Ndipo watoto wanapolipa gharama kubwa kwa ajili ya mama yao kukosa kuchukua hatua.

Hivyo, kutendwa vibaya kwaweza kupitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Bila shaka, watu wengi wanaochagua kutozungumzia masaibu waliyopatwa nayo huonekana wakiweza kuendelea vema na maisha, na hiyo inastahili pongezi. Lakini kwa wengi, maumivu hayo yanakuwa ya ndani zai-di, na wanahitaji kufanya jitihada za pekee—kutia, ikihitajika, kutafuta msaada wa wataalamu—ili kuponya majeraha hayo ya utotoni. Lengo lao si kusedeka katika kujihurumia. Wao wataka kukomesha visa hivyo vyenye kuumiza vya kutenda watoto vibaya vinavyoathiri familia yao.—Ona Amkeni! la Oktoba 8, 1991, kurasa 3 hadi 11, (Kiingereza).

Mwisho wa Kutendwa Vibaya

Ikitumiwa vizuri, habari iliyozungumzwa yaweza kufanya mengi katika kupunguza uwezekano wa watoto kutendwa vibaya nyumbani mwako. Hata hivyo, kumbuka kwamba watenda vibaya hutenda kwa usiri, wao hutumia hali ya kutumainiwa kwa faida yao, na hutumia hila ya watu wazima dhidi ya watoto wasio na hatia. Basi, bila kuepukika, wengine wao hukosa kuadhibiwa kwa uhalifu wao wenye kuchukiza.

Hata hivyo, uwe na uhakikishio kwamba Mungu huona yale wanayofanya. (Ayubu 34:22) Isipokuwa watubu na kubadilika, yeye hatasahau matendo yao maovu. Yeye atawafunua kwa wakati wake. (Linganisha Mathayo 10:26.) Naye atatekeleza hukumu. Yehova Mungu atoa ahadi juu ya wakati ambapo watu wote wenye hila kama hao ‘watang’olewa mbali na dunia,’ na ni wapole na wale waanana tu wanaompenda Mungu na wenzao watakaoruhusiwa kuendelea kuwapo. (Mithali 2:22; Zaburi 37:10, 11, 29; 2 Petro 2:9-12) Tuna tumaini hilo zuri ajabu la ulimwengu mpya kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (1 Timotheo 2:6) Ni wakati huo tu, na si mwingine, ambapo kutendwa vibaya kutakwisha milele.

Kwa wakati huu ni lazima tufanye yote tuwezayo ili kuwalinda watoto wetu. Wao ni wenye thamani kubwa! Wazazi wengi watajihatirisha wenyewe ili kuwalinda watoto wao wadogo. (Linganisha Yohana 15:13.) Tusipowalinda watoto wetu, matokeo yaweza kuwa mabaya sana. Tukiwalinda, tunawapatia zawadi nzuri ajabu—hali ya utotoni ya kujihisi bila hatia na bila msiba. Wanaweza kuhisi kama vile mtunga-zaburi alivyohisi, aliyeandika hivi: “Nitasema, BWANA [Yehova, NW] ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini.”—Zaburi 91:2.

[Maelezo ya Chini]

a Kutenda watoto vibaya kingono hutukia wakati mtu anapomtumia mtoto ili kutosheleza tamaa zake za kingono. Mara nyingi kunatia ndani kile ambacho Biblia huita uasherati, au por·neiʹa, ambayo yaweza kutia ndani kupapasa-papasa viungo vya uzazi, kufanya ngono, na ngono ya kutumia mdomo au ya mkundu. Matendo fulani mabaya, kama vile kupapasa-papasa matiti, matongozi mabaya yasiyo ya adili, kumwonyesha mtoto pornografia, kumtazama akiwa uchi, na kumfunua mavazi isivyofaa, yaweza kujumlika kuwa yale Biblia inayoshutumu kuwa “mwenendo mlegevu.”—Wagalatia 5:19-21, NW; ona Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1984, kielezi chini ukurasa 6.

b Ingawa wengi watendao watoto vibaya walitendwa vibaya wakiwa watoto, hilo halimaanishi kwamba kutendwa vibaya hufanya watoto wawe watenda vibaya. Watoto waliotendwa vibaya wanaopungua theluthi moja huja kuwa watenda watoto vibaya.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Mwokokaji mmoja wa miaka mingi ya kutendwa ngono kiukoo alisema: “Kutenda watoto vibaya huwaua, huua tumaini lao, haki yao ya kuhisi kutokuwa na hatia. Ndiyo sababu wanahitaji kulindwa. Kwa sababu sasa ninalazimika kujenga upya maisha yangu yote. Kwa nini kuwalazimu watoto wengi zaidi wafanye hivyo?”Kwa kweli, kwa nini?

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Wasikilize Watoto!

KATIKA British Kolumbia, Kanada, uchunguzi wa hivi karibuni ulifanywa juu ya kazi-maisha za watu 30 wazoevu wa kutenda watoto vibaya. Matokeo yalihofisha. Watu hao 30 walikuwa wamewatenda vibaya watoto 2,099 kati yao. Nusu yao kamili walikuwa na vyeo vyenye kutumainiwa—walimu, wahubiri, wasimamizi, na wafanyakazi wa utunzi wa watoto. Mtenda vibaya mmoja, daktari wa meno wa miaka 50, alikuwa amewatenda vibaya watoto karibu 500 katika kipindi cha miaka 26.

Hata hivyo, The Globe and Mail la Toronto lasema hivi: “Katika asilimia 80 ya visa, sehemu moja au zaidi ya jumuiya (kutia na marafiki, au washirika wa mkosaji, familia za waliotendwa vibaya, watoto wengine, baadhi ya waliotendwa vibaya) walikana au kupunguza uzito wa kitendo hicho.” Haishangazi kwamba “ripoti hiyo inadokeza kwamba kukanusha na kutoamini hufanya matendo mabaya yaendelee.”

Watendwa vibaya fulani walikuwa wamewashtaki watenda vibaya. Hata hivyo, The Globe and Mail lanukuu ripoti hiyo kuwa ikisema kwamba “wazazi wa watoto waliotendwa vibaya hawakutaka kukubali yale waliyokuwa wakiambiwa na watoto wao.” Vivyo hivyo, hivi karibuni ofisa mmoja wa serikali katika Ujerumani alitaja juu ya ripoti moja kwamba inawabidi watoto wanaotendwa vibaya kingono wawafikie watu wazima karibu mara saba wakiwa na malalamiko yao kabla ya wao kuaminiwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

“Tafuta Msaada Sasa”

“IKIWA wewe ni mwanamume na unahusika kingono na watoto, huenda ikawa unajiambia hivi, ‘Kisichana hicho chapenda,’ au “Kivulana hicho kilitaka,’ au ‘Ninafunza kisichana hicho juu ya ngono.’ Unajidanganya mwenyewe. Wanaume halisi hawajihusishi kingono na watoto. Ikiwa una hisia inayojali mtoto huyo, acha kumtenda vibaya. Tafuta msaada sasa.”—Tangazo lililopendekezwa la utumishi wa umma, lililonukuliwa katika kitabu By Silence Betrayed.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Watoto wahitaji uangalifu mwingi mchangamfu na wenye upendo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki