Kuwafariji Watu Wazima Waliookoka Ono Lenye Kutaabisha Walipokuwa Watoto
MUME na mke hao wachanga walikuwa wenye urafiki na wenye kustahiwa sana kutanikoni. Lakini sauti ya mume huyo ilisikika kuwa yenye kutaka msaada wa haraka alipoomba waweze kutembelewa na mzee huyo wa kutaniko, naye mke wake alilengwa-lengwa na machozi machoni pake. Mke wake alikuwa akipatwa na vipindi vya mshuko mkubwa wa moyo na kujichukia, hata mawazo ya kujiua. Yeye alikuwa ametendwa vibaya kingono akiwa mtoto. Mzee huyo wa kutaniko alisoma barua za Sosaiti kwa wazee kutia na makala za Amkeni! la Oktoba 8, 1991, na makala ya Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1983 (za Kiingereza), zilizozungumzia kichwa hicho, huku akiwa mwenye shukrani kwamba tengenezo la Yehova limeandaa mwelekezo juu ya jinsi ya kusaidia wale waliopatwa na uhalifu huo. Hapa pana mambo machache yenye mafaa yanayotokana na vyanzo hivyo.
1. Sikiliza, sikiliza, sikiliza. Mtoto anapojichubua goti, hatua yake ya kwanza ni kumkimbilia mama au baba ili afarijiwe. Lakini labda mtoto aliyetendwa vibaya hata hakuwa na chaguo hilo kamwe. Kwa hiyo akiwa mtu mzima, bado yeye ana uhitaji uo huo—kusema, kuzungumzia, kufarijiwa na msikilizaji mwenye kuhurumia. (Linganisha Ayubu 10:1; 32:20.) Mzee huyo alipotembelea mume na mke hao waliotajwa hapo juu, mume alishangaa jinsi yule mzee alivyosikiliza sana, na wala hakusema mengi. Huyo mume akiwa mtu mwenye kutenda mambo kihalisi, na mwenye kusaidia, alipata kwamba alikuwa amekuwa akijaribu kutatua tatizo hilo kwa kusababu alipoambiwa mambo ya kihisiamoyo, huku akijaribu kukosoa hisia mbalimbali zilizoonekana kuwa zisizofaa kwake. Alijifunza kwamba mke wake alihitaji hisia-mwenzi zaidi ya majibu. (Linganisha Warumi 12:15.) Yeye alihitaji kusikia kwamba alikuwa na sababu zifaazo kwa kuhisi vile alivyokuwa akihisi.
2. Funua mambo ya uwongo. Kutendwa vibaya hufunza watoto kwamba wao ni wachafu sana, wasiopendeka, wasiostahili. Kama vile mafundisho bandia ya kidini, mawazo hayo yaweza kufanya uhusiano ufaao pamoja na Yehova uwe mgumu sana. Kwa hiyo funua mambo ya uwongo, na uyabadili na kweli—kwa upole, kwa kurudia-rudia, kwa subira. Sababu kwa kutumia Maandiko. (2 Wakorintho 10:4, 5) Kwa kielelezo: “Ninaelewa kwamba unahisi kuwa mchafu. Lakini Yehova anahisije juu yako? Ikiwa alimruhusu Mwanae afe na kuandaa fidia kwa ajili yako, je, hiyo haimaanishi kwamba yeye akupenda? [Yohana 3:16] Je! machoni Pake kutendwa vibaya huko kulikufanya wewe uwe mchafu, au kulifanya huyo mtenda vibaya awe mchafu? Kumbuka, Yesu alisema hivi: ‘Hakuna kitu kilicho nje ya mtu ambacho kikimwingia chaweza kumtia unajisi, bali vile vimtokavyo, ndivyo vimtiavyo unajisi yule mtu.’ [Marko 7:15] Kwa kweli, je, kutendwa vibaya huko kulitokana na wewe, mtoto mdogo? Au mtenda vibaya huyo alinuia kufanya hivyo katika akili yake mwenyewe?”
3. Sema kwa kufariji. Kila mtu mmoja-mmoja halingani na mwingine, kwa hiyo shauri la Paulo ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ hutumika kwa njia zinazotofautiana katika hali zote. (1 Wathesalonike 5:14, NW) Hata hivyo, mazungumzo ya kisahili, mara nyingi huwa hayafariji. Mathalani, kumwambia yule aliyeokoka baada ya kutendwa vibaya kwamba asome tu Biblia zaidi, ahubiri zaidi, au ‘amtwike tu Yehova mzigo wake’—ingawa madokezo hayo ni yenye kusaidia nyakati nyingine—huenda kusilete matokeo. (Zaburi 55:22; linganisha Wagalatia 6:2.) Tayari wengi wanafanya mambo hayo vizuri kadiri wawezavyo na hujilaumu wenyewe bila huruma kwa kutofanya vema zaidi.—Linganisha 1 Yohana 3:19, 20.
Vivyo hivyo, kuwaambia wale waliookoka baada ya kutendwa vibaya kwamba wasahau tu yaliyopita kwaweza kuleta madhara zaidi kuliko mafaa. Kama wangaliweza kufanya hivyo, inaelekea wangalifanya hivyo—na wasingalihitaji msaada ili kufikia utatuzi sahili kama huo.a Kumbuka, ono walilopata ni lenye kutaabisha sana kihisiamoyo. Ili kutoa tu ulinganisho, ebu wazia ukimpata mjeruhiwa katika aksidenti ya gari anayelala huku akilia kwa uchungu kati ya mabaki ya gari hilo. Je! wewe ungemwambia asahau tu uchungu huo? Kwa wazi, mengi zaidi yanatakwa.
Ikiwa huna uhakika kwamba yale unayosema ni yenye kufariji na kusaidia, mbona usimuulize huyo aliyeshuka moyo? Kwa vyovyote, hata shauri la kweli na la Kimaandiko hutakwa liwe la wakati ufaao na lenye kufaa pia.—Linganisha Mithali 25:11.
Baada ya ziara chache, dada huyo alianza kuona maendeleo fulani katika mtazamo wake, naye mume wake aliweza kumsaidia vizuri zaidi katika nyakati ngumu. Tangu wakati huo wote wawili wameweza kusema kwa kuwafariji wengine ambao wamepatwa na maono ayo hayo yenye kutaabisha. Jinsi inavyotia nguvu imani kuona Yehova, “Mungu wa faraja yote,” akifanya kazi kupitia Neno lake na watu wake ili “kuwaganga waliovunjika moyo” katika nyakati hizi zenye taabu.—2 Wakorintho 1:3; Isaya 61:1.
[Maelezo ya Chini]
a Ni kweli, mtume Paulo aliwashauri Wakristo ‘wayasahau mambo waliyoacha.’ Lakini Paulo hapa alikuwa akirejezea umashuhuri wake wa mbeleni na ufanisi wa kilimwengu, ambao sasa ulikuwa “kama mavi” kwake. Yeye hakuwa akirejezea dhiki yake ya wakati uliopita, ambayo alisema juu yayo kwa uhuru.—Wafilipi 3:4-6, 8, 13; linganisha 2 Wakorintho 11:23-27.