Vijana Huuliza...
Naweza Kuachaje Kufikiria Watu wa Jinsia Tofauti?
‘SIKU baada ya siku, vyombo vya habari humomonyoa uthabiti wa kiadili wa matineja kwa kuwadhihaki na kuwachokoza kwa utani juu ya ngono; nyimbo za roki hukwaruza masikio yao kwa habari za ngono; miminiko la riwaya za mahaba ziuzwazo kwa wingi zaidi hupamba ngono ikawa kama tamutamu yenye usukari.’[1] Ndivyo alivyosema mwandikaji Lesley Jane Nonkin. Ndiyo, ukiwa tineja, waparamiwa na vitia-moyo kutoka vyombo vya habari uifikirie jinsia tofauti.
Bila shaka, ni kawaida kuwa na upendezi fulani katika jinsia tofauti.a Lakini mawazo ya kimahaba, ndoto za mchana, na fantasia zitawalapo mawazo yako kiasi cha kuvuruga usingizi, sala, masomo ya nyumbani, kusoma Biblia, au kazi zako za nyumbani, hiyo yaonyesha hali imekuwa hatari kwa muda. Kwa kweli, mshughuliko huo usiofaa ungeweza kuongoza kwenye mwenendo mbaya.—Yakobo 1:14, 15.
Si kwamba uache kufahamu kuna wasichana au wavulana. Lakini kama Mithali 23:12, NW, isemavyo, wahitaji ‘kuleta moyo wako kwenye nidhamu.’ La, hakuna suluhisho rahisi, hakuna dawa-mwujiza ya kukusaidia ufanye hivyo. Ingawa hivyo, waweza kufanya kufikiri kwako kusawazike zaidi. Acha tutazame njia chache zenye kutumika uwezazo kufanya hivyo.
Chunga Ushirika Wako
Chunguza sana ushirika wako. Kijana mmoja wa kiume akiri hivi: “Kila mtu aliye karibu na wewe hutaja ngono isiyo ya adili kama kwamba ni jambo la kawaida kama kwenda nje kula chakula.”[2] Je, kusikiasikia maongezi hayo kwaweza kukuathiri? Bila shaka. Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanyiwa vijana, robo tatu walikiri kwamba “kujipatanisha (au kutojipatanisha) na umati ndiko huamua mitazamo yao kuelekea ngono.”[3]
Namna gani rafiki zako? Je, kila maongezi huingilia mazungumzo marefu juu ya mtu fulani wa jinsia tofauti? Je, maongezi hayo huelekea kuruka mipaka na kuwa ya upujufu au ya kudokeza ngono? Ikiwa ndivyo, kujiunga—au kusikiliza tu—kutakutatiza kukaza akili yako juu ya mambo safi. Biblia yahimiza: “Yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu.”—Wakolosai 3:8.
Hata hivyo, itakuwa vigumu kutumia shauri hili, ikiwa waandamani wako hawathamini sana kanuni za Biblia; hakika mitazamo yao itakuathiri hatimaye. (Mithali 13:20) Fikiria ono la msichana mmoja Mkristo, aliyesema: “Sikutaka kuwaambia watoto shuleni kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hivyo wakati wote walisemasema nami juu ya ngono.”[4] Muda si muda alihusika katika ngono isiyo ya adili akachukua mimba. Mithali 9:6 huhimiza kwa hekima: “Acha uandamani wa watu wakosa-ujuzi, na uishi. Fuata njia ya ujuzi.” (Today’s English Version)[4a] Ndiyo, kaa karibu-karibu na marafiki washirikio maadili na viwango vyako vya Kikristo, marafiki watakaokujenga kiroho—si kukubomoa.
Bila shaka, hata Wakristo vijana ambao kwa ujumla huonyesha mtazamo wa kimungu huenda ‘wakajikwaa katika kunena’ mara kwa mara. (Yakobo 3:2) Hilo litokeapo na maongezi yaanze kwenda kombo, waweza kufanya nini? Biblia hutuambia kwamba Mfalme Sulemani alishikwa na mahaba kuhusu kisichana mchungaji. Hata hivyo, kisichana huyo hakurudisha upendezi huo wa mahaba. Waandamani fulani wachanga walipojaribu kumwamsha hisia apendezwe na Sulemani, hakujiruhusu aambiwe-ambiwe mahaba. Alisema kwa uthabiti: “Nawaapisha nyinywi . . . ya kwamba msizindue, wala msiamshe mapenzi, hata yapende yenyewe.” (Wimbo Ulio Bora 2:7, The Old Testament in Swahili [Mombasa]) Vivyo hivyo, huenda wewe ukahitaji kusema kwa uthabiti maongezi yarukapo mipaka. Si lazima uwasomee rafiki zako, hapana. Lakini ungeweza kujaribu kuibadili habari tu, kuelekeza maongezi upande ufaao zaidi.
Vitumbuizo—Uhitaji wa Kuwa Mteuzi
Eneo jingine la kuhangaisha ni vitumbuizo. Huenda sinema, vidio, au santuri ya karibuni zaidi ikaonekana inavutia. Hata hivyo, Biblia hutukumbusha: “Vitu vyote vya ulimwengu—tamaa mbaya za mwili, vitu wanavyoviona watu na kuvitamani, majivuno yasababishwayo na mali—vyote hivyo havitoki kwa Baba, bali vyatoka kwa ulimwengu.” (1 Yohana 2:16, Habari Njema kwa Watu Wote) Kama ilivyotajwa mwanzoni, vingi vya vitumbuizo vya leo hukusudiwa kuamsha hisia za ngono. Kwa kielelezo, nyimbo na sinema zipendwazo sana zimezidi kufunua mambo wazi—mara nyingi zikiwa za pornografia.
Ungeweza kuathiriwaje kwa kujifunulia vitumbuizo hivyo? Asema mwandikaji John Langone: “Machunguzo kadhaa yameonyesha . . . kwamba tufunuliwapo habari za mapenzi, sisi huelekea kuongea zaidi juu ya ngono. Nyakati nyingine, ufunulio huo hutuongoza kujaribu mambo ambayo tusingeyajaribu kikawaida.”[5] Ndiyo, ‘kuyafikiria mambo ya mwili’ kutakudhuru tu. (Warumi 8:5) Kutapotosha maoni yako juu ya upendo na ngono na kujaza akili yako fantasia zisizo safi. Shauri la Biblia ni nini? “Na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Hivyo epuka sinema, vidio, na sahani zichocheazo tamaa ya mahaba.
Mwanamume mseja Mkristo alitoa ushauri huu wakati mmoja: “Usijilishe yasiyofaa kabla tu ya kulala. Maonyesho mengi ya usiku sana katika TV hudokeza ngono.”[6] Kadhalika na vitabu vingi. Aungama Mkristo kijana aitwaye Sherry: “Nilikuwa nikisoma riwaya za mahaba. Nikawa na fantasia za ngono, nikiwazia hayo maisha ya kusisimua na kulala-lala na wenzi tofauti.”[7] Akili yake ikiwa imejaa fantasia za mahaba, alitumbukia rahisi katika kukumbatiana na kupapasana na kijana wa kiume. Matatizo kama hayo yaweza kuepukwa ukisoma yafaayo tu—kama jarida hili na andamani lalo, Mnara wa Mlinzi. Usomaji huo umesaidia vijana wengi ‘wayafikiri mambo ya roho,’ badala ya kufikiria ya mwili wenye dhambi.—Warumi 8:5.
Ondoa Fantasia Hizo!
Nyakati nyingine huenda mawazo juu ya jinsia tofauti yakaibuka akilini mwako bila onyo. Aungama Scott mwenye miaka 17: “Kuna nyakati ambazo huwa vigumu sana kuondoa akili yangu juu ya ngono.”[8] Au labda waona tu mvulana au msichana kisura. Ghafula bin vuu, wajikuta ukimfikiria. Lakini kuona kwamba mtu avutia ni tofauti kabisa na kufanya aliloonya Yesu, yaani, ‘kufuliza kutazama mwanamke ili kuwa na harara kwake.’ (Mathayo 5:28, NW; linganisha Mithali 6:25.) Ulipo mchanga mno kufunga ndoa, kugaa-gaa katika fantasia za mahaba yasiyofikika kwaweza kushusha na kuvunja moyo wako tu.—Linganisha Mithali 13:12.
Hivyo Scott asema: “Kinisaidiacho ni kuigeuza habari—kuondoa akili yangu kwenye mawazo yanisisimuayo. Mimi hujikumbusha kwamba hisia au vichocheo hivyo vitaisha hatimaye.”[9] (Linganisha Wafilipi 4:8.) Mtume Paulo alisema: “Nautesa mwili wangu na kuutumikisha.” (1 Wakorintho 9:27) Vivyo hivyo, huenda ukalazimika kujizuilia wakati mawazo juu ya jinsia tofauti yatiapo mzizi. Mawazo hayo yakiendelea, jaribu mazoezi fulani ya kimwili. “Kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo,” na matembezi ya kasi au dakika chache za kunyosha maungo huenda zikatosha kukusaidia urudishe akili pafaapo.—1 Timotheo 4:8.
Vijana wengi wamepata pia kwamba ‘kuzidi sana kutenda kazi ya Bwana’ husaidia sana. (1 Wakorintho 15:58) Debra kijana alieleza hivi: “Mimi huona kwamba dawa ni kujishughulisha mpaka uishiwe nguvu.”[10] Kujihusisha sana na kutaniko la Kikristo na utendaji walo wote kwaweza kukusaidia sana kusawazisha kufikiri kwako.
Ingawa hivyo, ujapojaribu sana, nyakati nyingine huenda bado ukatatizika kuondoa akili yako juu ya jinsia tofauti. Ikiwa ndivyo, tafuta msaada wa mtu mzima. Labda ungeweza kuongea na mmojapo wazazi wako. Fikiria alilosema Carl mchanga: “Nimesaidika kuongea na mtu fulani wa umri mkubwa zaidi na mwenye maarifa. Kusema wazi zaidi ndiko kupata matokeo mazuri zaidi.”[11] Juu ya yote, usisahau msaada uwezao kupata kwa Baba yako wa kimbingu. “Nihisipo vichocheo vya ngono vikiamka,” asema mwanamume mmoja mseja Mkristo, “Mimi husali wee.”[12] Yataarifu Biblia: “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.” (Waebrania 4:16) Mungu hataondoa upendezi wako wa jinsia tofauti, hapana. Lakini kwa msaada wake, waweza kugundua kwamba kuna mengine mengi ya kufikiria.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kwangu Kuacha Kufikiria Watu wa Jinsia Tofauti?” katika toleo letu la Julai 22, 1994.
[Picha katika ukurasa wa 17]
Maongezi juu ya jinsia tofauti yakiruka mipaka, uwe na moyo mkuu kuibadili habari