Vijana Huuliza. . .
Kwa Nini Ni Vigumu Sana Kwangu Kuacha Kufikiria Watu wa Jinsia Tofauti?
“Udadisi wako juu ya ngono ni jambo la maana unapokuwa mchanga,” akaeleza kijana Lorraine. “Unajishughulisha zaidi na zaidi na mambo ya ngono.”[1]
JE! WEWE hutumia wakati wako mwingi wa mchana ukifikiria, kusema, au kuwatazama watu wa jinsia tofauti? Je! wewe huketi chini ili umalize kazi ya shule ya kufanyia nyumbani, na kujipata ukiota mchana juu ya mvulana mwenye sura nzuri au msichana mrembo uliyeona alasiri hiyo? Je! mazungumzo yako hukatizwa-katizwa ukiwatazama kisiri wapita-njia wenye kuvutia? Je! wewe huona vigumu kusoma, kujifunza, au hata kukazia mambo fikira kwenye mikutano na mikusanyiko ya Kikristo—kwa sababu tu huwezi kuacha kufikiria watu wa jinsia tofauti?
Ikiwa ndivyo, huenda ukahofu kwamba unapata kichaa! Kijana mmoja alikiri hivi: “Nafikiri nimelewa kwa ngono. Yaani, mara nyingi nawafikiria wasichana, nikiwaza mambo yasiyo kweli . . . Je! wafikiri niko timamu?”[2] Kama vile mwandikaji Lynda Madaras asemavyo, unapokuwa mchanga, “hisia za mahaba au za ngono zaweza kuwa zenye nguvu sana. Nyakati nyingine, huenda hata ikaonekana kana kwamba mahaba na ngono ndio mambo tu unayoweza kufikiria!”a[3]
Hisia za ngono si za uovu. Mungu aliumba mwanamume na mwanamke wakiwa na uvutio mkubwa kati yao. Hilo lilipatana na kusudi lake kwamba waoane na ‘kujaza dunia’ kwa wazao waadilifu. (Mwanzo 1:28) Biblia pia iko wazi ikionyesha kwamba uhusiano wa kingono waweza kuwa chanzo cha furaha kuu kwa mume na mke.—Mithali 5:19.
Tatizo ni kwamba, tukiwa binadamu wasio wakamilifu, mara nyingi sisi huona vigumu kudhibiti hisia zetu. (Linganisha Mwanzo 6:5.) “Tamaa ya mwili” yaweza kuonekana kuwa yenye nguvu na kulemea! (1 Yohana 2:16) Na kwa kuwa wewe ni kijana, huenda hasa ikawa vigumu kwako kuacha kufikiria watu wa jinsia tofauti. Kwa nini hivyo?
Mikazo ya Ubalehe
Sababu moja ni kwamba wewe wakaribia “uzuri wa ujana”—wakati ambao tamaa za kingono ziko kileleni. (1 Wakorintho 7:36) Dakt. Bettie B. Youngs aeleza hivi: “Wakati wa kubalehe, kiasi cha hormoni huzidi sana. Hormoni hizo huanzisha mabadiliko yote ya kimwili yanayoubadili mwili wa mtoto kuwa wa mtu mzima. Kiasi chenye kuongezeka cha hormoni kinachotokea wakati wa ubalehe huleta mabadiliko mengi ya kihisiamoyo na kitabia.”[5]
Mabadiliko ya aina gani? Mara nyingi mabadiliko makubwa zaidi ni yale ya hisia za mtu kuelekea watu wa jinsia tofauti. Mwandikaji Ruth Bell asema: “Mara nyingi mabadiliko ya mwili wakati wa ubalehe husababisha hisia za ngono zenye nguvu zaidi. Huenda ukajipata ukifikiria zaidi ngono, ukiamshwa kingono vyepesi zaidi, hata nyakati nyingine ukijishughulisha na mambo ya ngono tu. Matineja kadhaa [tuliohoji] walieleza juu ya kutembea barabarani au kuketi ndani ya basi wakihisi kana kwamba mwili wao wote uliwaka kwa nishati na msisimuko wa kingono.”[6] Kujishughulisha huko na watu wa jinsia tofauti ni mojawapo “tamaa za ujanani” ambazo lazima vijana wakabili.—2 Timotheo 2:22.
Uvutano wa Vyombo vya Habari na Marafiki
Hata hivyo, mara nyingi moto wa tamaa hiyo huchochewa na uvutano wa nje. Twaishi katika jamii ambayo imeazimia kuchochea utendaji wa ngono kupitia programu za televisheni, utangazaji, vitabu, magazeti, muziki, na sinema. Kijana mmoja Mkristo aliyeangukia upotovu wa ngono aliripoti hivi “Pornografia [vitabu vya uchi] ni ya kawaida shuleni, na hiyo hutokeza tamaa kubwa ya ngono. Nilijua yaliyofaa, lakini hisia zangu za ngono zilikuwa zenye nguvu.”[7]
Hivyo kitabu kilichoandikiwa wazazi chasema hivi: “Vyombo vya habari [vina] uvutano mkubwa. Matineja wetu huona vijana waonyesha-mitindo ya nguo wa umri wao wenyewe wakitenda kwa njia ya kuamsha nyege na kuuza nguo zenye kuamsha nyege; wao huona ngono ya vijana ikichochewa kwenye sinema na televisheni.”[8] Kwa kweli, televisheni ya kebo na mashine za video zimefanya vijana wengi wakapata pornografia ya waziwazi kwa njia rahisi. “Vyombo vya habari huamsha udadisi na tamaa ya kijana,” akiri kijana mmoja.[9]
Hata hivyo, si lazima kitabu kiwe na pornografia kwenye kila ukurasa ili kiwe kisichofaa. Fikiria ono la msichana mmoja Mkristo. Yeye akumbuka hivi: “Nilisoma kitabu kizuri kwa kadiri fulani kilichokuwa na fungu moja au mawili tu ya ngono. Nilianza kuruka mafungu hayo, lakini jambo fulani lilinifanya nirudi nyuma na kuyasoma. Hilo lilikuwa kosa lililoje! Kama tokeo nilipata ndoto mbaya sana.”[10]
Marafiki na washiriki wako waweza pia kuwa na uvutano mkubwa juu ya kufikiri kwako. Kitabu kimoja juu ya ukuzi wa ubalehe chasema: “Kutazama wasichana na wavulana ni kipisha-wakati maarufu kwenye kona za barabara, katika vijia vya shuleni, kwenye kafeteria, na maduka makubwa.”[11] Na wakati vijana hawatazami wale wa jinsia tofauti, mara nyingi wao hupiga domo juu yao. “Nilipokuwa mchanga zaidi,” akiri Robert mwenye miaka 18, “mkazo wa kufanya ngono ulikuwa mkubwa sana . . . Katika vyumba vya kubadilishia nguo, gumzo lilikuwa juu ya hayo tu.”[12] Kijana mwingine akiri hivi: “Ngono ndiyo ilikuwa jambo la kuzungumziwa la namba moja miongoni mwa wanashule, kwa hiyo ilikazwa kikiki akilini mwako.”[13]
Ni vigumu kuwa tofauti na wengine. Marika wako wanapozungumza kila wakati juu ya watu wa jinsia tofauti—labda kwa njia ya kushusha heshima, kukebehi—hilo laweza kuwa kishawishi cha kujiunga nao. Lakini Biblia huonya: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”—Mithali 13:20.
Uhitaji wa Kuwa na Usawaziko
Je! yote hayo yamaanisha kwamba haifai kutazama au kutaka kuzungumza juu ya watu wa jinsia tofauti? La, hata waandikaji wa Biblia waliandika juu ya uhakika wa kwamba wanaume na wanawake fulani walivutia kimwili. (Linganisha 1 Samweli 9:2; Esta 2:7.) Kwa hiyo, Yesu hakumshutumu mtu kwa kuona tu kwamba mwanamke avutia. Lakini yeye alihimiza Wakristo ‘wasiendelee kumtazama mwanamke kwa kumtamani.’ (Mathayo 5:28) Kwa njia iyo hiyo, huwezi kujiruhusu uongozwe na tamaa tupu. Kwenye 1 Wathesalonike 4:4, 5 twaambiwa hivi: “Kila mmoja wenu apaswa kujifunza kuudhibiti mwili wake mwenyewe kwa njia iliyo takatifu na yenye kuheshimika, si katika tamaa ya mahaba kama vile wapagani, wasiomjua Mungu.”—New International Version.[14]
Ingawa fikira za mahaba zaweza kuingia akilini wakati mmoja au mwingine, kuendelea kuwaza-waza juu yazo kwaweza kugeuka kuwa karibu kama kulewa nazo, halafu matatizo mazito huzuka. Mhubiri 5:3 husema: “Kwa maana ndoto huja kwa sababu ya shughuli nyingi.” Naam, mtu anayejishughulisha na tamaa za kibinafsi mara nyingi huanza kusitawisha mawazo yasiyo ya kweli na ndoto za mchana.b
Ingawa ni kawaida kuwa na mawazo ya kimahaba wakati mmoja au mwingine, kuendelea kuwaza-waza juu yayo ni jambo jingine. Mwandikaji Ruth Bell aandika kwamba “mara kwa mara mtu atajipata mwenyewe akitumia karibu mchana na usiku wote akiwaza mambo yasiyo ya kweli. Mambo hayo yaweza kuonekana kuwa halisi kuliko uhalisi.”[15] Fikiria msichana mmoja mchanga ambaye amenaswa na upendo wa kipumbavu. Yeye asema hivi: “Nina miaka 12 1/2, na nampenda sana mvulana anayehudhuria kwenye Jumba la Ufalme letu. Najua mimi si mkubwa vya kutosha kutembea naye kirafiki, lakini ni vigumu sana kudhibiti hisiamoyo zangu kumwelekea.”[16] Vivyo hivyo, vijana fulani huona vigumu kusoma, kujifunza, kusikiliza kwa uangalifu darasani, au kutayarisha mikutano ya Kikristo, akili zao zinapojaa mawazo ya kimahaba au yenye kuamsha nyege.
Matatizo mazito yaweza kutokea pia kijana akijaribu kuondosha nyege kwa kupiga punyeto. Biblia huhimiza Wakristo: “Vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani.” (Wakolosai 3:5) Kupiga punyeto ni tendo chafu la kuepukwa na Wakristo na ni kinyume kabisa cha ‘kufisha tamaa ya ngono.’ Kinyume cha hayo, kupiga punyeto huchochea na kusitawisha tamaa. Mara nyingi, tamaa ya aina hiyo huja kuwa uhalisi. Mwandikaji wa Biblia Yakobo aeleza hivi: “Kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi.”—Yakobo 1:14, 15.
Basi, wewe waweza kufanya nini ili uache kufikiria watu wa jinsia tofauti? Tafadhali soma makala ifuatayo ya mfululizo huu.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa upande mwingine, mwandikaji Alvin Rosenbaum akumbusha vijana hivi: “Hisia na mitazamo ya ngono hutofautiana sana. Watu fulani hawawezi kuacha kufikiria ngono hali wengine hawatamani ngono kabisa. . . . Miitikio hiyo miwili ni kawaida.” Yeye aongeza hivi: “Kila mtu hukua kwa kadiri tofauti.”[4]
b Ona makala juu ya ndoto za mchana zilizotokea katika matoleo ya Julai 8 na Julai 22, 1993 za jarida hili.
[Blabu katika ukurasa wa 25]
“Hisia za mahaba au za ngono zaweza kuwa zenye nguvu sana”
[Picha katika ukurasa wa 26]
Maonyesho ya televisheni na matangazo ya magazeti mara nyingi huchochea upendezi usiofaa katika watu wa jinsia tofauti