Vijana Huuliza. . .
Kwa Nini Baba Alikufa?
KILA mtu alishangaa wakati baba ya Al, mtu aliyejulikana kuwa na nguvu na mwenye afya nzuri alipolazwa hospitalini. Hata hivyo, Al alikuwa na uhakika kwamba baba yake angerudi nyumbani upesi. Lakini kwa ghafula hali yake ikawa mbaya zaidi, naye akafa. “Sikuamini kwamba mtu mwenye nguvu kadiri hiyo angeweza kufa,” akaomboleza Al.
Baba ya Kim alikuwa Mkristo mwenye upendo sana. Alikuwa amepata kulazwa hospitalini hapo awali kwa sababu ya ugonjwa wa kusedeka, lakini alionekana kuwa anapata nafuu. Kisha siku moja akaanguka katika bafu. “Nilijua amekufa nilipomwona tu,” akumbuka Kim. “Mama yangu na ndugu yangu walijaribu sana kumwokoa kwa kumpa pumzi. Nilikimbia chumbani mwangu na kusali: ‘Yehova, usiruhusu jambo hili litendeke. Tafadhali mwache aishi!’ Lakini alikufa.”
Kifo ni tukio baya sana katika ulimwengu huu. Biblia yasema hivi: “Kwa kila jambo kuna majira yake . . . wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa.” (Mhubiri 3:1, 2) Ikiwa umelelewa ukiwa Mkristo, unajua mafundisho ya Biblia juu ya sababu inayofanya watu wafe, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo.a
Hata hivyo, waweza kupata pigo kubwa sana kwa kupoteza mzazi. Ni mojapo maono magumu zaidi maishani. Laweza kukufanya uhisi kwamba umeachwa bila usalama. Bado unaendelea kukua, kimwili na kihisia-moyo pia, na ingawa huenda umesitawisha kiwango fulani cha kujitegemea, bado unahitaji wazazi wako kwa mambo mengi.b
Basi, si ajabu kwamba uchunguzi mmoja ulifunua kwamba hofu kuu zaidi ya tineja ni ile ya kupoteza wazazi. Kijana mmoja alikiri hivi: “Wazazi wangu huniudhi sana mara nyingi, lakini nisingefurahi kama jambo fulani lingewapata. Mimi hutiwa wasiwasi na jambo hilo.”—The Private Life of the American Teenager.
Basi, si ajabu kwamba mmoja wa wazazi wako akifa, unaweza kupata pigo kubwa la kihisia-moyo. Kwani, angalau hapo mwanzoni unaweza kushtuka hivi kwamba ushindwe kulia. Hilo ni jambo la kawaida. Alipokuwa na mkazo mkubwa, mtunga-zaburi alisema hivi: “Nimedhoofika na kuchubuka sana.” (Zaburi 38:8) Kitabu Death and Grief in the Family chasema: “Mtu apataye jeraha kubwa la kukatwa mwilini au avunjikaye mfupa hupata mshtuko mkubwa. Mshtuko huo ni kama ulinzi unaomzuia asipatwe na maumivu makali sana [mara hiyo]. Huzuni huwa vivyo hivyo pia.” Lakini ni nini kiwezacho kutukia baada ya mshtuko wa kwanza kwisha?
‘Nimeghadhabika Sana’
Kwenye Luka 8:52, twasoma kwamba baada ya kifo cha msichana mdogo, “watu wote walikuwa wakilia na kumwombolezea.” Naam, kifo kipatapo mpendwa wako, ni jambo la kawaida kuwa na hisiamoyo nyingi zenye nguvu, kutia ndani huzuni, kuwa na hatia, hofu—na hata hasira.
Kwa nini hasira? Kwa sababu wazazi wetu hutufanya tuhisi salama salimini. Mmoja wao anapokufa, ni kawaida kuhisi woga na kuwa umeachwa. Si kwamba mzazi wako alikuacha kimakusudi. Lakini kifo ni adui yetu. (1 Wakorintho 15:26) Mpendwa anapokufa, potezo hilo huwa halisi sana na bila shaka lenye uchungu sana. Ona jinsi Wendy mwenye miaka 18 asemavyo: “Nilihisi upweke katika ulimwengu na nikawa na woga baada ya kifo cha baba yangu. Nyakati nyingi sana nilitamani kwamba baba yangu awe pamoja nami ili anisaidie.” Ufikiriapo yale ambayo umepoteza—ule upendo, utegemezo, na mafunzo—unaweza kwa kufaa kukasirika.
Kwa kielelezo, Debbie mchanga alikuwa na uhusiano wa karibu na mjomba wake. Baada ya kifo chake yeye aliandika: “Haikuonekana kuwa haki kwa mtu yeyote mzuri hivyo, apendwaye sana, na ampendaye Yehova sana kuteseka na kufa kifo chenye maumivu makali kama chake. Ingawa nililelewa nikiwa Mkristo na najua sababu inayofanya watu wazeeke na kufa na sababu inayofanya watu wazuri wateseke, sikutarajia hisia za hasira zilizonipata.”
Watu fulani hata huhisi kadiri fulani ya hasira kuelekea mzazi aliyekufa. Victoria mchanga akiri hivi: “Babu yangu alikufa mwaka uliopita. Nilimkasirikia sana kwa sababu ya kufa, na hasira yangu ilipokwisha, nikawa na huzuni tele.” Kwa kweli watu wengine wamejaribu kuelekeza hasira zao mbinguni. “Nimemkasirikia Mungu,” akiri Terri mwenye miaka 14, aliyepoteza baba yake kwa sababu ya maradhi ya moyo yaliyotokea ghafula. “Kwa nini baba yangu alikufa, hali nilimpenda na kumhitaji sana?”
‘Nahisi Nina Hatia Sana’
Hisia ya kuwa na hatia ni itikio jingine la kawaida kwa kifo cha mzazi. “Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,” yasema Biblia. (Warumi 3:23) Kama tokeo, matineja wengi hukosana na wazazi wao mara kwa mara. Lakini mzazi anapokufa, kumbukumbu za makabiliano na mabishano hayo ya zamani zaweza kutokeza msononeko mkubwa.
Yaweza kusaidia kukumbuka kwamba hata watu wanaopendana hukosa kusikilizana sana nyakati nyingine. “Nilimpenda mama yangu,” akiri Elisa mchanga, “na najua alinipenda, lakini kwa miezi michache kabla awe mgonjwa, hatukuwa tukisikilizana. Nilikuwa nikimkasirikia—kwa mambo yaonekanayo kuwa si ya maana sasa—lakini yaliyokuwa ya maana kwangu wakati huo. Pindi moja, nilipomkasirikia sana, nakumbuka nikiingia chumbani mwangu kwa fujo na kutamani kisiri kwamba afe. Mama aliposhikwa na ugonjwa na kufa ghafula, kulikuwa na hisia hizi zote zisizotatuliwa ambazo kila mmoja wetu alikuwa nazo. Nahisi nina hatia sana.” Yajapokuwa yale mambo ambayo huenda uliyasema au kuhisi, wewe hukusababisha kifo cha mzazi wako. Halikuwa kosa lako.
Uchungu wa Huzuni
Hata hivyo, huenda ukawa una huzuni na kihoro kingi. Pata faraja kwa kujua kwamba wanaume na wanawake wenye imani katika nyakati za Biblia pia walipata kuwa na hisia kama hizo. Yusufu alipopoteza baba yake mpendwa kwa kifo, ‘alimwangukia babaye usoni, akamlilia, akambusu.’ (Mwanzo 50:1) Yesu Kristo pia ‘alilia machozi’ kwa sababu ya kifo cha rafikiye Lazaro.—Yohana 11:35.
Naam, mtu aombolezapo kifo cha mzazi, ni jambo la kawaida kushindwa na huzuni nyakati nyingine. Akijaribu kueleza msononeko wake, mtunga-zaburi alijilinganisha mwenyewe na mtu ‘ainamaye akilia kama aliyefiwa na mamaye.’ (Zaburi 35:14) Kwa kushindwa na huzuni, hata unaweza “kukosa usingizi kwa sababu ya huzuni.” (Zaburi 119:28, NW) Unaweza kukosa hamu ya chakula au kwa ghafula ushindwe kukaza fikira shuleni. Hata waweza kushuka moyo sana.
Na kwa ubaya zaidi, mzazi wako aliye hai na ndugu zako wachanga huenda pia wakalemewa sana na huzuni zao wasiweze kukusaidia sana na kukutegemeza. Kim akumbuka hivi: “Baada ya kumzika baba yetu, tulijaribu kurudia maisha zetu za kawaida. Mama sasa akawa kichwa cha familia yetu. Lakini kulikuwa na nyakati ambazo angeshindwa kujidhibiti katikati ya funzo letu la familia la Biblia na kulia. Ningeweza kumsikia akilia usiku, akiita jina la baba yangu.”
Kupata Faraja
Wakati mmoja nabii Yeremia alisema: “Kihoro kisichoweza kuponywa kimeingia moyoni mwangu. Moyo wangu u mgonjwa.” (Yeremia 8:18, NW) Unaweza pia kuhisi kana kwamba uchungu wako hautakwisha. Lakini ona maneno ya mtume Paulo: “Na ahimidiwe . . . Mungu wa faraja zote, atufarijiye katika dhiki zetu zote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Mungu hutoa faraja hizo hasa kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia. Isitoshe, roho yake yaweza kusukuma marafiki na washiriki wa familia kutoa msaada na utegemezo unaohitajiwa.
Usiruhusu hasira iliyoelekezwa kusikofaa ikuzuie kutafuta faraja ya kimungu. Ayubu mwadilifu alifanya kosa la kumlaumu Mungu kwa ajili ya mapotezo yake yaliyomtia uchungu sana. Yeye alisema hivi kwa uchungu: “Nilikuwa katika raha, naye [Mungu] akanivunja-vunja; naam amenishika shingo na kuniponda.” (Ayubu 16:12, 13) Lakini Ayubu alikosea. Ni Shetani, wala si Mungu, aliyesababisha matatizo ya Ayubu. Ilimbidi Elihu mchanga amkumbushe Ayubu kwamba “Mungu hatatenda mabaya, na wala Mwenyezi hatapotosha hukumu.” Baadaye Ayubu alitubu kabisa kwa sababu ya maneno aliyoyasema bila kufikiri.—Ayubu 34:12; 42:6.
Kwa njia kama hiyo, unaweza kuhitaji mtu fulani akusaidie kuona mambo kwa njia yenye usawaziko. Kim akumbuka: “Mzee mmoja wa Kikristo aliye na umri mkubwa alitukumbusha juu ya tumaini la ufufuo, akisoma nasi maandiko kama vile Yohana 5:28, 29 na 1 Wakorintho 15:20. Yeye alisema hivi: ‘Baba yenu atarudi, lakini ni lazima mbaki mkiwa waaminifu ikiwa mwataka kumwona katika Paradiso.’ Sitasahau kamwe maneno hayo! Yeye alisema pia kwamba kifo halikuwa kusudi la Mungu kwa binadamu. Nikang’amua kwamba Mungu hakusababisha kifo cha baba yangu.”
Kuona sababu ya Kimaandiko hakukuondoa mara hiyo uchungu aliohisi Kim, lakini kulikuwa ndiko mwanzo. Wewe pia waweza kuanza kushinda uchungu wako na kihoro chako. Jinsi unavyoweza kufanya hivyo hasa itazungumziwa katika makala yetu ifuatayo katika mfululizo huu.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Mazungumzo haya yatia ndani vijana ambao wamepoteza watu wao wengine wa ukoo, kama vile babu na nyanya, shangazi, na wajomba, ambao hasa walikuwa na uhusiano wa karibu nao.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kifo cha mzazi chaweza kuwa mojapo maono magumu zaidi maishani