Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 9/8 kur. 21-23
  • Nishindeje Huzuni ya Kifo cha Baba?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nishindeje Huzuni ya Kifo cha Baba?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Wakati wa Kulia”
  • Kujitahidi Kushinda Huzuni Yako
  • Ongea na Mtu Fulani
  • Kutegemeza Mzazi Wako
  • Ninaweza Kukabilianaje na Kifo cha Mzazi?
    Amkeni!—2009
  • Ni Kawaida Kuhuzunika Ninavyohuzunika?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kwa Nini Baba Alikufa?
    Amkeni!—1994
  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 9/8 kur. 21-23

Vijana Huuliza. . .

Nishindeje Huzuni ya Kifo cha Baba?

“Baba alifia kitini. Nilimkuta hapo. Alipatwa na ugonjwa wa moyo ghafula. Ilinishtua sana kwa sababu tulikuwa na ukaribu mwingi. . . . Bado mama yangu hulia usiku. Hali ni tofauti kufanya mambo bila baba yangu.”—Emily.[1]

“KIFO cha mzazi au mshiriki wa familia wa karibu ni jeraha kubwa kwa mbalehe,” asema mwandikaji Kathleen McCoy. “Aweza kuwa hoi kwa muda kutokana na kihoro, hatia, babaiko na hasira.”[2] Ikiwa umefiwa na mzazi, basi wayajua sana maumivu yenyewe.

Ingawa hivyo, ni kawaida kuhisi tumeshikwa na kiwewe cha hisia mpendwa wetu afapo. Biblia husema kwamba Yakobo mzee wa ukoo alipoambiwa kwamba Yusufu mwana wake amekufa, ‘alirarua mavazi yake’ kwa bubujiko la kihoro. Na hata ingawa ‘wanawe wote, na binti zake wote, waliondoka wamtulize, alikataa kutulizwa.’ (Mwanzo 37:34, 35) Huenda wewe ukahisi hivyohivyo kwamba yale maumivu ni makali sana yasipate kamwe kwisha.

Hatimaye, yaweza kwisha. Lakini jawabu ni kukabili maumivu yako, badala ya kujaribu kuyapuuza. Kwa kielelezo, kijana John hakuonyesha dalili zozote za nje kwamba alikuwa na kihoro kwa kufiwa na mshiriki wa familia. Hata hivyo, alianza kupigana-pigana shuleni. John alieleza hivi: “Ninaishi nikiwa na fundo kubwa linaloniumiza kwa ndani. Nilijaribu kuling’oa kwa kupigana lakini wapi.”[3]

Vijana wengine hujaribu kukandamiza umizo hilo kwa kufanya kukurukakara ya utendaji. Wengine wawaulizapo wanaendeleaje, baadhi yao huenda wakaepuka maulizo hayo kwa kusingizia ni wachangamfu. Kufanya hivyo huenda kukafunika hisi za maumivu kwa kitambo, lakini si kitambo kirefu. Yasema Mithali 14:13: “Hata wakati wa kucheka moyo huwa [“huenda ukawa una,” NW] na huzuni.”

Kwa kupendeza, makala katika gazeti moja kwa vijana yasema: “Katika uchunguzi mmoja, matineja waliokuwa wamekandamiza hisia zao za kiasili za kiroho, hasira au hatia baada ya kifo cha mtu wa ukoo . . . walionyeshwa kuwa wenye kuhusika zaidi na mwenendo wa uharibifu, kama vile utumizi mbaya wa dawa za kulevya na alkoholi, kuwa na ujasiri usiofaa (kama vile kuendesha magari kwa miendo ya kasi) na tabia ya kutotii.” Uzuri ni kwamba, kuna njia nzuri zaidi za kukabiliana na kihoro.

“Wakati wa Kulia”

Mhubiri 7:2 husema: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake.” Kifo chaweza kuogopesha sana. Na wakati rafiki au mpendwa afapo, huenda wengine wakajaribu kuepuka uhalisi huo wenye maumivu wa kifo kwa kuendea “nyumba ya karamu” na kujitia katika shamrashamra. Hata hivyo, Sulemani atia moyo kukabiliana na kifo uso-kwa-uso na kuiendea “nyumba ya matanga.” Sulemani aongezea: “Huzuni ni afadhali kuliko kicheko, maana simanzi ya uso ni faida ya moyo.”—Mhubiri 7:3.

Ingawa ushauri huu ulielekezwa hasa kwa marafiki na familia ya waliofiwa, una manufaa kwa mfiwa pia kukabili maumivu ya kufiwa kwake. Kuna “wakati wa kulia.” (Mhubiri 3:4) Hivyo wanaume na wanawake wahofu-Mungu nyakati za Biblia walijiruhusu kuonyesha, badala ya kukandamiza, hisia zao za kihoro.—Linganisha Mwanzo 23:2; 2 Samweli 1:11, 12.

Kujiruhusu uwe na kihoro kuna manufaa nyingi. Chasema kitabu The Art of Condolence: “Wafiwa wahitaji kuruhusu maumivu na uchungu wa mateso yao uwapate. Kupona huzuiliwa na kukinza utaratibu huo.”[5] Hata hivyo, kwa kuongozwa na ile ngano ya kwamba wanaume halisi huwa hawalii, huenda wavulana fulani wakaona ni vigumu hasa kuonyesha hisia zao. Lakini yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi ‘alilia machozi’ peupe wakati Lazaro rafiki yake alipokufa. (Yohana 11:35) Na hakika machozi yafaa wakati mtu amefiwa na mzazi. Basi jihisi huru kuomboleza na kulia. (Linganisha Yakobo 4:9.) Chasema kitabu Death and Grief in the Family: “Kulia ni mojapo njia kuu zaidi za kuiondoa huzuni.”[6]

Kujitahidi Kushinda Huzuni Yako

Nyakati za Biblia, Mfalme Daudi alionyesha kihoro chake kuhusu rafiki yake mkubwa zaidi, Yonathani, si kwa kulia machozi tu bali kwa kuandika pia hisia zake. “Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, ulikua ukinipendeza sana,” akaandika Daudi katika ombolezo maridadi aliloliita “Upinde.”—2 Samweli 1:18, 26.

Huenda wewe vilevile ukaona yasaidia kuandika hisia zako. Kitabu Giving Sorrow Words chasema: “Kuandika hisia zako kwaweza kusaidia kufungulia hisiamoyo zilizofungiwa ndani. . . . Upatwapo na hasira, uhisipo huzuni, uhuzunikapo, andika hayo.”[7] Msichana tineja mmoja jina lake Shannon asema: “Niliweka kitabu cha kumbukumbu. Niliandika hisia zangu zote. Niliziandika wazi kabisa hisia zangu zote katika karatasi. Hisia zangu zote zilibwagwa karatasini na hiyo ikanisaidia sana . . . kuandika kila kitu.”[8]

Msaada mwingine ni mazoezi ya kimwili. “Kujizoeza kupata nguvu za mwili kwafaa kidogo,” yasema Biblia. (1 Timotheo 4:8) Na chasema kitabu kimoja juu ya kuwa na kihoro: “Mazoezi ni njia nzuri ya kufungulia nishati.”[9] Mbio ya kukutia nguvu, matembezi ya haraka, au uendeshi baiskeli wa kuburudisha waweza kukusaidia sana kufungulia mikazo iwezayo kujazana uhuzunikapo na kuwa na kihoro.

Ongea na Mtu Fulani

Ingawa hivyo, jihadhari usijitenge kabisa na wengine. (Mithali 18:1) Husema Mithali 12:25: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” Mtu mwenye kusononeka angepataje “neno jema” hilo la kitia-moyo? Kama tu akiongea na mtu fulani na kuonyesha “uzito” wake. Mbona usifanye hivyo wewe mwenyewe? Fungulia maoni yako na uongee na mtu fulani uwezaye kumtumaini.

Kwa kawaida, mzazi wako mhofu-Mungu ndiye angefaa kufikiwa. Lakini namna gani ikiwa amelemewa na maumivu yake mwenyewe asisaidie sana? Basi, kuna washiriki wakomavu wa kutaniko la Kikristo wawezao kusaidia. Mithali 17:17 husema: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Kijana Morfydd aliegemea sana kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova baada ya mama yake kufa. “Wazee wote walikuwa wenye kutegemeza sana,” akumbuka, “lakini mmoja hususa alikuwa tayari sikuzote kunisikiliza.”[10]

Kwa nini usijitahidi kupata msaada na utegemezo huo? Julisha mtu fulani kwamba wahitaji kuongea. Labda wahisi ukiwa na hasira, woga, au hatia. Au labda wahisi ukiwa mpweke na wasikitika kutokuwa na mzazi wako. Kuongea na msikilizaji mwenye huruma juu ya hisia zako kwaweza kusaidia kikweli.

Kutegemeza Mzazi Wako

Hata hivyo, vijana fulani huongezea msononeko wao kwa kujitwika madaraka wasiyo tayari kuyabeba. Huenda sasa hali nyumbani ikaonekana ya vurugu na isiyo na mpango. Yaeleweka kwamba mzazi wako aliyebaki hai aweza kuwa na mkazo, mwenye kuudhika—tena mwenye huzuni.[11] Kwa kuona maumivu yake, ni kawaida kwamba wataka kusaidia. Mjuzi mmoja wa kihoro asema kwamba “wabalehe . . . huenda wakakandamiza ombolezo lao wakidhania isivyofaa kwamba wanajaribu kusaidia wazazi wao.” Huenda “wakajifanya ‘watu wazima’ mapema mno, labda hata kutwaa madaraka ya ziada.”[12]

Bila shaka, huenda usiwe na la kufanya ila kutwaa madaraka fulani ya ziada kwa sababu ya kifo cha mzazi wako. Lakini hii haikufanyi uwe mwanamume au mwanamke wa nyumba. Mzazi wako aliyebaki hai angali ndiye msimamizi, nawe waweza kumtegemeza vizuri zaidi, si kwa kunyakua madaraka yake, bali kwa kuwa mshirikiani na mtii. (Waefeso 6:1) Kumbuka kwamba ‘hekima i pamoja na wenye kiasi.’ (Mithali 11:2, NW) Kiasi chahusisha kujua mapungukiwa yako.

Hili ni jambo la maana kukumbuka hasa ikiwa mzazi wako aliyebaki hai aanza kukuegemea kwa ushauri au akianza kukutwika mizigo mizito ya mahangaiko ya mtu mzima. Wataka kuwa mwenye fadhili na mtegemezaji, lakini kiasi kitakusaidia kutambua kwamba maarifa yako maishani ni haba sana. (Linganisha Waebrania 5:14.) Kwa hiyo ukianza kuhisi walemewa kidogo, ongea na mzazi wako waziwazi lakini kwa staha. (Mithali 15:22) Labda ungeweza kudokeza kwamba atafute tegemezo fulani la mtu mzima kutanikoni.

Si rahisi kamwe kukabiliana na kifo cha mzazi. Lakini uwe na hakika kwamba, hatimaye, hisia za huzuni hazitazidi kutawala. (Linganisha Mwanzo 24:67.) Kumbukumbu za kuhuzunisha juu ya mzazi wako aliyeondoka bado zitaingia akilini mwako mara kwa mara. Hata hivyo una kumbukumbu nyingi changamfu na zenye kufariji za kufikiria. Usisahau kamwe kwamba Yehova hukujali na kuelewa huzuni yako. Uhisipo u mpweke na umeachiliwa, fikiria maneno ya mtunga-zaburi: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.”—Zaburi 27:10.

Fuliza kufikiria, pia, tumaini la ufufuo lenye msingi wa Biblia na taraja la kuona mzazi wako tena—katika dunia-paradiso. (Luka 23:43, ZSB; Matendo 24:15) Asema kijana Kim aliyefiwa na baba yake: “Mimi hufikiria baba yangu kila siku. Lakini najua hangependa tuache au turuhusu chochote kikomeshe utumishi wetu kwa Yehova. Nataka kuwako nimsalimu arudipo katika ufufuo.”[13]—Yohana 5:28, 29.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kujiruhusu ulie machozi kwaweza kusaidia ule utaratibu wa kupona

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki