Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 11/8 kur. 18-20
  • Je, Nimetenda Ile Dhambi Isiyosameheka?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Nimetenda Ile Dhambi Isiyosameheka?
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Ifanyayo Dhamiri Yetu Ituumize
  • Huzuni ya Kimungu
  • Hatia Juu ya Dhambi Zilizo Ndogo
  • Vyanzo vya Msaada na Faraja
  • Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Dhambi Isiyoweza Kusamehewa Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Yehova, Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Je, Kuna Dhambi Isiyosameheka?
    Amkeni!—2003
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 11/8 kur. 18-20

Vijana Huuliza. . .

Je, Nimetenda Ile Dhambi Isiyosameheka?

“SIKUWA nimehisi kuvunjika moyo kadiri hiyo. Sikujistahi tena, na nilifikiri kwamba Mungu hangenisamehe kamwe.”—Marco.a

“Nilivunjika moyo sana. Hatia ilifunika moyo wangu. Nilifikiri kwamba nilikuwa nimetenda makosa fulani yasiyosameheka.”—Alberto.

“Hakuna mtu asiyetenda dhambi,” husema Biblia. (1 Wafalme 8:46) Lakini nyakati fulani huenda kijana akahisi kwamba amefanya zaidi ya kosa la kawaida tu. Kama vile Marco na Alberto, huenda akakandamizwa na hisia ya hatia isiyoisha. Huenda akahisi kwamba lile ambalo ametenda ni baya sana, ovu sana, hivi kwamba Mungu hawezi kamwe kumsamehe.

Namna gani ikiwa hisia zilizo kama hii hukutaabisha sana? Jipe moyo. Hali yako si hoi.

Sababu Ifanyayo Dhamiri Yetu Ituumize

Ni kawaida kuhisi vibaya wakati umefanya kosa la upumbavu. Sote huzaliwa tukiwa na uwezo ambao Biblia huuita “dhamiri.” Hiyo ni hisi ya haki na ubaya, king’ora cha ndani kiliacho kwa kawaida tufanyapo ubaya fulani. (Warumi 2:14, 15) Fikiria Mfalme Daudi, kwa kielelezo. Yeye alifanya uzinzi na mke wa mwanamume mwingine. Baadaye, alifanya Uria, mume wa mwanamke huyo, apelekwe akafe hakika. (2 Samweli 11:2-17) Matokeo yakawa nini juu ya Daudi?

“Mchana na usiku mkono [wa Mungu] ulinilemea,” akakiri Daudi. Naam, alihisi uzito wa kuondolewa kibali cha kimungu. Daudi alisema hivi pia: “Hamna amani mifupani mwangu kwa sababu ya hatia zangu. Maana dhambi zangu zimenifunikiza kichwa, kama mzigo mzito zimenilemea mno. . . . Mchana kutwa nimekwenda nikihuzunika.” (Zaburi 32:4; 38:3-6) Dhamiri ya Daudi iliendelea kumtaabisha sana mpaka akasukumwa kuchukua hatua ifaayo na kutubu kosa lake.

Vivyohivyo, ikiwa wewe umeelimishwa na wazazi Wakristo na wapotoka kuacha viwango vya Biblia, utahisi vibaya. Hali hii ya majuto ni ya kawaida, yenye afya. Yaweza kuchochea mtu ajisahihishe au atafute msaada kabla kosa halijawa tabia iliyoimarika. Kwa upande mwingine, mtu adumuye katika dhambi huharibu dhamiri yake. Baada ya muda huja ikawa isiyohisi, kama ngozi iliyotiwa sugu. (1 Timotheo 4:2) Kisha ni hakika kutakuwa na ufisadi wa kukosa adili.—Wagalatia 6:7, 8.

Huzuni ya Kimungu

Basi, haishangazi kwamba Biblia hutaja “dhambi isiyo ya mauti.” (1 Yohana 5:16; linganisha Mathayo 12:31.) Dhambi hiyo ni udhaifu tu wa mwili. Hufanywa kimakusudi, kwa shingo ngumu, kwa moyo mgumu. Kile kifanyacho kwa kadiri kubwa dhambi hiyo iwe isiyosameheka si dhambi yenyewe hasa bali ni hali ya moyoni hasa ya mtenda-dhambi.

Hata hivyo, uhakika wa kwamba wewe wahisi umeumia na wasononeka juu ya mwenendo wako mbaya laonyesha kwamba hujafanya dhambi isiyosameheka. Biblia husema kwamba “huzuni iliyo kwa jinsi ya Mungu hufanya toba liletalo wokovu.” (2 Wakorintho 7:10) Kwa kweli, angalia himizo litolewalo kwenye Yakobo 4:8-10: “Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.”

Ni kweli, huenda kosa hilo likawa zito sana. Kwa kielelezo, Julie kijana alihusika katika kupapasana na kukumbatiana na rafiki-mvulana. “Nilijihisi mwenye hatia sana hapo kwanza,” aungama msichana huyo, “lakini kadiri wakati ulivyopita, nilizoea hilo. Halikusumbua sana dhamiri yangu.” Baada ya muda, vitendo visivyo safi vilipanda kidato vikafikia ngono. “Nilijihisi kuwa mashakani,” asema Julie. “Dhamiri yangu ilidhoofika kufikia kufanya hilo mara kadhaa.”

Je, hali hiyo haina tumaini? Si lazima. Namna gani Manase, mmojapo wafalme wa Yuda? Alifanya dhambi zilizo nzito mno, kutia na uwasiliani-roho na kudhabihu watoto. Hata hivyo, Mungu alimwia radhi kwa sababu ya toba yake ya moyo mweupe. (2 Mambo ya Nyakati 33:10-13) Namna gani Mfalme Daudi? Alipokwisha kutubu vitendo vyake viovu, alipata kwamba Yehova ni Mungu aliye ‘mwema, tayari kusamehe.’—Zaburi 86:5.

Wakristo leo wana uhakikishio huu: “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” (1 Yohana 1:9, italiki ni zetu.) Ni nani ambaye mtu apaswa kumfanyia ungamo hili? Kwa msingi, ni Yehova Mungu. “Ifunueni [“imwageni,” NW] mioyo yenu mbele zake.” (Zaburi 32:5; 62:8) Huenda ukapata yasaidia kusoma ungamo la Daudi la kuhisi kihoro katika Zaburi 51.

Kwa kuongezea, Biblia huhimiza Wakristo ambao wametumbukia katika dhambi nzito waseme na wazee wa kutaniko. (Yakobo 5:14, 15) Shauri na sala zao zenye bidii zaweza kukusaidia usimamishe upya uhusiano wako na Mungu na upate upya dhamiri safi. Wao waweza kutambua tofauti kati ya udhaifu na uovu. Yawapasa pia wahakikishe kwamba wewe wapata msaada uhitajiwao ili kuepuka kurudia kosa lako. Julie, akiwa yeye mwenyewe amekwisha kuchukua hatua hii yenye ujasiri, apendekeza hivi: “Nilijaribu ‘kujikaripia mwenyewe’ na hata nikafikiri kulikuwa na matokeo ya kadiri fulani. Lakini baada ya mwaka mmoja nilijua nilikosea sana. Huwezi kusuluhisha matatizo mazito bila msaada kutoka kwa wazee.”

Hatia Juu ya Dhambi Zilizo Ndogo

Ingawa hivyo, nyakati fulani kijana ‘hughafilika katika kosa.’ (Wagalatia 6:1) Au yeye huruhusu kichochezi fulani cha mwili kimlemee. Kijana aliye katika hali hii huenda akapatwa na hisia za hatia nyingi—labda hatia nyingi kuliko ile ambayo kosa hilo lastahili. Huzuni kali isiyohitajiwa hutokea. Hisia hizo za hatia ya kina kirefu zaweza kutokana na dhamiri yenye afya lakini yenye kugusika kwa urahisi mno. (Warumi 14:1, 2) Kumbuka, tutendapo dhambi “tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki.”—1 Yohana 2:1, 2.

Fikiria, tena, kisa cha Marco kijana, kilichonukuliwa katika utangulizi wetu. Mkristo kijana huyu alisadiki kwamba alikuwa ametenda dhambi isiyosameheka. Alikuwa akijiambia hivi: ‘Mimi najua kanuni za Biblia vizuri sana, hata hivyo siwezi kuacha kutenda dhambi!’ Dhambi yake ilikuwa nini? Tatizo la kupiga punyeto. ‘Mungu aweza kunisameheje ikiwa siwezi kuvunja tabia hiyo?’ Marco akawa akisababu hivyo. Alberto, ambaye vivyohivyo alikuwa na vipindi vya kujitumia vibaya, alisema: “Niliihisi hatia ndani sana kwa sababu singeweza kujiweka huru na dhambi hiyo.”

Kupiga punyeto ni tabia isiyo safi. (2 Wakorintho 7:1) Hata hivyo, Biblia haiweki tabia hiyo pamoja na dhambi zilizo nzito kama uasherati. Kwa kweli, haiitaji kamwe. Kwa hiyo, kutumbukia tena katika kupiga punyeto hakungeelekea kuwa kusikosameheka. Kuwa na maoni ya kwamba hakusameheki kwa kweli kungeweza kuwa hatari; kijana huenda akasababu kwamba hakuna faida ya kujaribu kushinda tatizo hilo. Lakini kanuni za Biblia zaonyesha kwamba Mkristo apaswa kujikaza kisabuni apigane na tabia hii.b (Wakolosai 3:5) Yehova ajua kwamba ‘twajikwaa sisi sote katika mambo mengi.’ (Yakobo 3:2) Mrudio ukitukia, kijana hahitaji kuhisi ameshutumiwa.

Ndivyo ilivyo kuhusu mighafiliko na makosa mengine. Yehova hataki tujiadhibu kwa hatia nyingi mno. Bali, yeye hufurahi tuchukuapo hatua za kulisahihisha tatizo.—2 Wakorintho 7:11; 1 Yohana 3:19, 20.

Vyanzo vya Msaada na Faraja

Ingawa hivyo, yaelekea utahitaji usaidizi wa kibinafsi katika kufanya hivyo. Wazazi wahofu-Mungu waweza mara nyingi kufanya mengi ili kusaidia na kutegemeza watoto wao. Na kutaniko la Kikristo hutoa njia nyingine za tegemezo. Marco akumbuka hivi: “Jambo lililonisaidia kwelikweli lilikuwa maongezi pamoja na mzee. Nililazimika kuwa na moyo mkuu ili kufungulia hisia zangu na kumwambia fikira zangu za ndani kabisa. Lakini alinitia uhakika, kwa hiyo nikaomba ushauri wake.” Alberto, pia, alitafuta ushauri kutoka kwa mzee. “Siwezi kusahau ushauri wake wenye kutia moyo,” asema Alberto. “Aliniambia kwamba alipokuwa kijana, yeye pia alikuwa na tatizo hilohilo. Singeamini hilo kamwe. Nilimsikiliza kwa uthamini mkubwa kwa sababu ya kufuata kwake haki.” Wakiwa na msaada na tegemezo hilo, Marco na Alberto walishinda matatizo yao. Wote wawili kwa sasa watumikia katika vyeo vya daraka katika makutaniko yao mbalimbali.

Sala ya bidii ni msaada mwingine. Kama Daudi, waweza kusali upate “moyo uliotakata” na “roho mpya, iliyo thabiti.” (Zaburi 51:10, NW) Kusoma Neno la Mungu ni chanzo kingine cha faraja. Kwa kielelezo, huenda ukaona ni jambo lenye kutia moyo kujifunza kwamba mtume Paulo pia alikuwa na taabu kubwa za ndani. Alikiri hivi: “Kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya.” (Warumi 7:21) Paulo alifaulu kudhibiti mielekeo yake mibaya. Hata wewe waweza. Huenda ukaona inafariji sana kuzisoma zaburi, hasa zile zinazoshughulika na msamaha wa Mungu, kama vile Zaburi 25, 86, na 103.

Katika tukio lolote, epuka kujiachilia ufikirie matatizo yako mwenyewe tu na kujiacha utawalwe na matazamio mabaya tu. (Mithali 18:1) Jifaidi kikamili na rehema ya Yehova. Kumbuka, yeye ‘husamehe kabisa’ kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi wa Yesu. (Isaya 55:7; Mathayo 20:28) Usipunguze ukubwa wa makosa yako, wala usikate shauri kwamba Mungu hawezi kukusamehe. Tia nguvu imani na azimio lako la kumtumikia. (Wafilipi 4:13) Baada ya muda utakuja kuwa na amani ya akili na shangwe ya ndani yenye kina kirefu ya kujua kwamba umesamehewa.—Linganisha Zaburi 32:1.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Madokezo yenye msaada yametolewa katika sura 25 na 26 za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kuongea na Mkristo astahiliye kwaweza kukupa mwono mpya juu ya mambo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki