Je, Watahubiri Mlango kwa Mlango?
“PAPA Awatuma Wahubiri Kwenye Barabara za Rome.” Hicho kilikuwa kichwa cha ripoti za habari na Greg Burke. Aliandika hivi: “Papa John Paul amewasihi Wakatoliki katika Italia kufuata kielelezo cha madhehebu kama vile Mashahidi wa Yehova wanaojishindia wageuzwa nchini, na waanze kuhubiri mlango kwa mlango.
“‘Si wakati wa kuonea haya Gospeli, ni wakati wa kuihubiri hadharani,’ Jumatatu Papa aliwaambia wahubiri wasafirio 350 na wafundishaji wa dini. . . .
“‘Natumai mradi wenu wa kupigia mbiu Gospeli kwenye barabara . . . utaleta matunda mengi,’ aliwaambia. ‘Mmevumbua upya mbinu ya kuhubiri ambayo huwafikia hata wale ambao walipeperuka kutoka kwa imani.’”
Ripota Burke aliandika hivi: “Hudhurio la Kanisa Katoliki limepungua haraka sana katika Italia kwa muda wa miongo miwili iliyopita, na idili ya Papa ya wahubiri wa mlango kwa mlango yaonyesha aghalabu dalili ya ufifiaji wa uvutano walo.”
Himizo kama hilo la “kuanza kuhubiri mlango kwa mlango” si jipya kabisa. Papa wa awali, Paul 6, alisema kwamba Kanisa Katoliki “liko ili lieneze evanjeli.” Na Papa wa sasa, John Paul 2, aliandika barua Redemptoris Missio kwa maaskofu wote katika 1991 ili kuliweka chonjo kanisa lake kuhusu uhitaji wa kuendeleza amri ya Yesu ya kuhubiri hadharani.
Mwandikaji wa Katoliki ya Roma Peter Hernon alitokeza swali katika Catholic Herald la London: “Ni nini kiliupata ueneza-evanjeli?” Alikuwa akihangaikia ule “mwongo wa ueneza-evanjeli” wenye kutangazwa sana ambao sasa una umri wa miaka kadhaa. Alipouliza askofu kuhusu ule ukosefu wa maendeleo, askofu alijibu hivi: “Ni lazima usiwe na haraka. Kanisa limekuwako kwa miaka 2000 tu.”
Si ajabu Hernon aliuliza hivi: “Ule udharura uko wapi uliowasilishwa na Yesu Alipowatuma wanafunzi Wake ili waeneze evanjeli katika vijiji vilivyowazunguka? Ama na Mt Paulo: ‘Ole wangu nisipoihubiri Injili [“Gospeli,” NW]! (1 Kor. 9:16).’” Je, Wakatoliki kwa kweli wataiga Wakristo wa mapema waliohubiri hadharani “na kutoka nyumba hadi nyumba”?—Matendo 5:42; 20:20, Douay Version.
Hernon alikubali kuhusu ueneza-evanjeli wa mlango kwa mlango, kwamba yeye “aweza kusikia washuku-shuku wakinung’unika ‘nadharia, katu haitumiki.’ La sivyo,” Hernon ajibu. “Ili kuthibitisha dai hilo nahitaji kutumia neno lisilofaa. Najua halifai kwa sababu wakati wa mwisho nilipolitumia katika makala ya Katoliki sehemu yote iling’olewa (ingawa hakuna chochote kingine kilichobadilishwa). Neno hilo ni Shahidi wa Yehova. . . . Kila Shahidi pia hufunzwa kwamba, kwa wito wake mwenyewe, yeye kwa lazima ni mishonari.”
Ingawa Hernon hakubaliani na itikadi za Mashahidi wa Yehova, yeye akubali kwamba mtu afikiriapo mbinu zao za kuhubiri, “ni rahisi mmoja kukumbushwa Kanisa la mapema kama lilivyoonyeshwa katika matendo ya Mitume.”
Mashahidi wa Yehova waendeleza huduma yao ya bidii ya mlango kwa mlango, hivyo wakitimiza katika nyakati hizi za kisasa amri ya Yesu Kristo: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hata mwisho wa nchi.”—Matendo 1:8.