Ziara ya Kurudi Urusi
MOJAPO MABADILIKO YALIYO MAKUBWA KUPITA YOTE KATIKA ULE ULIOKUWA MUUNGANO WA SOVIETI LIMEKUWA UHURU WA KUIZUNGUMZA DINI. WARUSI WENGI WAMETUMIA UHURU HUO ILI KUCHUNGUZA MAFUNDISHO YA BIBLIA. MATOKEO YAMEKUWA, MUUJIZA WA SIKU ZA KISASA.
JINSI nilivyoshangaa Julai 28, 1993, nilipochukua gazeti la asubuhi la New York Times na kuona kwenye ukurasa wa kwanza picha kubwa ya ubatizo katika Moscow! Ilikuwa na maelezo haya mafupi: “Kuwekwa huru kwa dini katika Urusi kulileta wageuzwa kwenye Stediamu ya Locomotive ya Moscow kwa ajili ya ubatizo mwingi wakiwa Mashahidi wa Yehova.”
Mke wangu nami tulikuwa tumerudi kutoka Urusi siku moja tu iliyotangulia. Tulihudhuria ubatizo huo wa watu 1,489. Upendo wa Kikristo ulioonyeshwa na Warusi na upendezi wao katika mambo ya kiroho kweli ulituvutia. Ono moja tulilokuwa nalo baada ya kipindi cha kumalizia cha mkusanyiko jioni ya Jumapili laonyesha hili.
Nilipokuwa nikirudi kwa Metro hotelini mwetu, nilikaa karibu na mwanamume kijana labda mwenye umri wa miaka 18 au 19. Nilimpa ile trakti ya Biblia, katika Kirusi, Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?a Baada ya kuiangalia kifupi, alimpitishia mama yake. Hivyo nilimpa kijana huyo nyingine. Kwenye hiyo alielekeza kidole kwenye swali la ufunguzi, “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” na, kwa sauti iliyoonyesha mashaka, akauliza kwa Kiingereza, “Je, unaamini hili?”—Ayubu 14:14, King James Version.
Niligeuka ili kumtazama machoni, na nikiwa na usadikisho thabiti, nikamjibu: “Hakika ninaliamini!” Mara nikaongezea hivi: “Ebu fikiria hivi. Maisha yetu tukiwa watu wenye akili, wanaofikiri ni muujiza. Mtu fulani Aliye Juu Zaidi lazima awe aliweka sheria zinazoongoza ukuzi wetu wa kuwa wanadamu. Kwa hivyo ninaamini kwamba Mmoja huyu Aliye Mkuu aweza pia kumuumba upya mtu aliyekufa ili aishi tena.”
Mara hiyo kijana huyo alianza kuisoma trakti hiyo. Alipomaliza, nilimpa broshua, katika Kirusi, Je! Kweli Mungu Anatujali?* Alitaka kujifunza zaidi, lakini tulihitaji kushuka kwenye kituo kilichofuata. Ingawaje kijana huyo na mamaye walikuwa wawahi gari-moshi jioni hiyo, walishuka pamoja nasi kituoni ili kuongea kwa dakika chache zaidi. Baada ya kutoa maelezo mafupi kuhusu programu yetu ya kujifunza Biblia, nilimwonyesha anwani fulani nyuma ya broshua ambayo angeliweza kuandikia ili kupata habari zaidi.
Tuliondoka Urusi siku iliyofuata, lakini mikabiliano kama hiyo ilitokeza alama zisizobandulika.
Urusi Akilini Mwetu
Niliendelea kufikiri kuhusu idadi ya kustaajabisha ya wapya waliobatizwa baada ya marufuku juu ya Mashahidi wa Yehova katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti yaliyoondolewa hatimaye katika Machi 1991. Mikusanyiko saba ilipangwa upesi sana kwa ajili ya kiangazi cha 1991, na 7,820 walizamishwa katika maji. Kisha, kwenye mikusanyiko ya kiangazi ya 1993—kutia ndani ule tuliohudhuria katika Moscow—11,238 walizamishwa.
Bidii ya kueneza evanjeli ya Mashahidi katika Urusi haikosi kutambuliwa na wengi wa watu wa Urusi. Unapofikiri juu ya itikio la Warusi kwa mafundisho ya Biblia, yaonekana kuwa muujiza.
‘Ukuzi wa haraka hivyo wawezekanaje?’ tulishangaa. ‘Kwa kweli Warusi hawa wana msingi kiasi gani katika mafundisho ya Kikristo?’
Wenzi wa ndoa wanaoishi katika Moscow waliposema wangetupangia mahali pa kulala ikiwa tungezuru Urusi tena, tulianza kufanya mipango ya usafiri. Tazamio letu la hamu ya safari hiyo lilikua tulipopata ripoti za ziada kuhusu kupendezwa kusiko kwa kawaida kwa Warusi katika kweli za Biblia.
Familia Changamfu ya Kirusi
Tuliwasili Julai 24 tukiwa na masanduku yetu mkononi mahali tungekuwa tukiishi katika Moscow—kao lenye orofa mbili lililokuwa karibu mwendo wa miguu wa dakika kumi kutoka kwenye makao ya jengo la marafiki zetu. Kuhusu familia ambayo tungeishi nayo, ni Katia tu mwenye umri wa miaka 15 alikuwa nyumbani kutulaki. Ilikuwa jioni ya Jumapili, na wale wengine wote wa familia walikuwa wangali kwenye huduma ya Kikristo.
Muda mfupi, washiriki wale wengine wa familia walianza kurudi nyumbani—Galina, mama; Zhenia, mwenye umri wa miaka 13; na binti mdogo zaidi; na hatimaye, Viktor, baba. Hakuna yeyote wao aliyejua Kiingereza sana, nasi hata tulijua Kirusi kidogo mno. Mawasiliano yalikuwa angalau nafuu marafiki zetu waongeao Kiingereza walipokuwepo wakiwa wakalimani lakini ilikuwa vigumu walipoondoka. Tungetumia kamusi ya Kirusi-Kiingereza na ishara za kueleza. Katia na Zhenia walijua kuwasiliana, wakiwa wamejifunza lugha ya ishara.
Familia yote ilikuwa imebatizwa kwa wakati mmoja, miaka miwili tu iliyopita. Viktor alikuwa mtumishi wa huduma kutanikoni, na wasichana walitumia likizo zao ili kutumia wakati mwingi kwenye huduma. Wakati wanahudhuria shule, hawasiti kuongea juu ya imani yao. Hakika, kuhubiri kwao hata kulivuta uangalifu wa mamlaka za nje ya wilaya ya shule yao. Tulivutiwa kujua kwamba familia hiyo ilikuwa ikiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 28 kila juma na watu wenye kupendezwa!
Kwa wazi, uangalifu wa kila mshiriki wa familia ulikuwa juu ya funzo la Biblia na huduma ya Kikristo, na tungeliweza kuona kwamba maisha yao yalikuwa yametajirishwa. Walinururisha furaha.—Matendo 20:35.
Wenye Msingi Thabiti Katika Biblia
Kabla ya kwenda kulala wakati wa jioni, niliwauliza familia hiyo maswali juu ya maandiko ya Biblia. Kwanza niliuliza Ufunuo 21:3, 4 lisemavyo. Mara moja, karibu kwa umoja, wasichana hao wangeliweza kulinukuu. Kisha nikauliza Isaya 2:4. Walilijua hilo pia, hata kwa kutumia ishara ili kuonyesha kufuliwa kwa mapanga kuwa majembe.
Niliendelea na maandiko katika Isaya yale yasemayo kuhusu utawala wa Ufalme na baraka za ulimwengu mpya, hayo ni, Isaya 9:6, 7; 11:6-9; 25:8; 33:24; 35:5, 6; na 65:21, 22. Bila kuangalia katika Biblia zao, familia iliweza kutambulisha maelezo ya kila andiko. Wasichana hao pindi kwa pindi wangeonyesha kwamba walijua maandiko hayo na ishara za maelezo, kama vile za mtoto akiongoza simba.
Katika jioni nyingine tulifikiria maandiko juu ya utambulisho wa Mungu, tukielekeza uangalifu kwa yale ambayo huonyesha Yesu ni mdogo kuliko Mungu na kwamba Mungu na Yesu si mtu mmoja bali umoja wa muungamano. Familia hiyo ingeliweza kutambulisha maelezo ya maandiko kama vile Yohana 10:30, Yohana 17:20, 21, na 1 Wakorintho 11:3. Mke wangu nami tulistaajabu jinsi walivyozifahamu Biblia zao.
Jumanne asubuhi tukiwa karibu 12 tulikutana na kusafiri pamoja kwa Metro kwenye bustani fulani maridadi ambapo tulitumia muda wa saa mbili na nusu tukizungumza na watu kuhusu Biblia. Tuligawanywa na kuhubiri tukiwa wawili-wawili. Mmoja wa wenzi wangu alikuwa Nadia, msichana Mrusi aliyeonyesha hali nzuri ya kuwafikia watu na kuwashirikisha katika mazungumzo. Alikuwa mstadi katika kuelekeza uangalifu kwa maoni ya Mungu katika Biblia. Nilijisemea mwenyewe, ‘Huyu ni mhubiri mwenye uzoefu.’ Baadaye nilishangaa kujua kwamba alikuwa na umri wa miaka 17 tu na alikuwa amebatizwa kwa miezi miwili tu!
Tulipata maono mengi kama hayo, yaliyotuonyesha kwamba hali katika Urusi ilikuwa isiyo na kifani. Tangu kuanguka kwa Ukomunisti, Warusi wamejionyesha kuwa na tamaa ya kuchunguza mafundisho ya Biblia. Walio wengi wao wameelimika, na wanapenda kusoma. Hata walio wachanga wanasoma na kuelewa vizuri, kama ilivyothibitika tulipozuru familia fulani ya Warusi ambayo ilijifunza kweli za Biblia wakati Mashahidi walikuwa wangali chini ya marufuku.
Mwana mdogo wa wenzi hao wa ndoa alisema kwamba alitaka kuuliza swali fulani. Kupitia kwa mkalimani, alitoa ombi fulani. Nilivutiwa nalo sana hivi kwamba nilisema ikiwa angetoa ombi lake kwa kuandika, ningelipeleka kwa wachapishaji wa Amkeni! Mara hiyo alikaa kitako na kuandika barua. Ifuatayo ni tafsiri ya aliyoandika. Barua hiyo imetokezwa upya kwenye ukurasa 25.
“Serosha anaandika kutoka Urusi kwa Watchtower Society. Nina umri wa miaka saba, na tayari nahubiri pamoja na baba na mama. Napenda kuongea na watu juu ya Ufalme wa Mungu. Pia napenda kusoma gazeti la Amkeni! Hilo huja Urusi katika Kirusi mara moja tu kwa mwezi lakini katika lugha ya Kiingereza mara mbili kwa mwezi. Ningependa sana kupata gazeti hili mara mbili kwa mwezi, kwa sababu nalipenda kupita kiasi. Tafadhali fanyeni hivyo.”
Kuwaacha marafiki tuliowapata Moscow haikuwa rahisi. Kwa muda huo mfupi, tulikuja kuwapenda mno.
Walinganishwa na Ukristo wa Mapema
Tuliondoka kuelekea Tallinn, Estonia, kwa gari-moshi la usiku. Huko tuliona majengo mapya maridadi ambayo katika hayo kazi ya kuhubiri sasa yaelekezwa katika ile iliyokuwa jamhuri ya Muungano wa Sovieti. Siku tatu baadaye tulipanda gari-moshi hadi St. Petersburg. Katika mahali kote kuwili Wakristo wenzetu waliuliza kuhusu kazi ya kuhubiri katika Moscow. “Kuwapo pale na kujionea ukuzi,” nilijibu, “kulinisaidia kufahamu vizuri yaliyoandikwa katika sehemu ya kwanza ya Matendo 17 na katika zile barua kwa Wathesalonike.”
Sikuzote nilikuwa nastaajabia jinsi kutaniko lilivyoweza kuanzishwa katika Thesalonike yaonekana kwa muda wa majuma machache ya huduma ya Paulo huko. Linistaajabishalo pia ni kwamba kwa muda upatao mwaka au zaidi, Paulo aliwaandikia Wakristo hawa wapya barua mbili kuhusu mambo ya kiroho mazito zaidi kama vile ufufuo na ‘kunyakuliwa . . . katika mawingu,’ “siku ya Yehova,” kilio cha “amani na usalama!,” na “kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo.” (1 Wathesalonike 4:13-17; 5:1-3; 2 Wathesalonike 2:1, 2, linganisha na NW.) Tokeo ni kwamba, utendaji wa bidii wa Wakristo hao wa mapema, ulitokeza muujiza wa karne ya kwanza—tengenezo la kimataifa la wahubiri wakomavu na wenye nguvu kiroho kwa muda mfupi sana. Karibu miaka kumi baadaye, Paulo aliandika kwamba “habari njema” ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu’!—Wakolosai 1:23, italiki ni zetu.
Kilichokuwa kikitukia katika Urusi nilikiona kuwa chenye kulinganika na kilichotukia katika karne ya kwanza.
Jitihada ili Kumudu Ukuzi
Urusi ndiyo nchi iliyo kubwa kupita zote duniani, kwa hiyo kuandaa mwelekezo kwa maelfu huko wanaohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa wazi ni kazi kubwa.—Mathayo 24:14.
Biblia husema kuhusu wale waliousikia Ukristo katika karne ya kwanza: “Mkono wa Yehova ulikuwa pamoja nao, na idadi kubwa waliopata kuwa waamini wakageuka kuelekea Bwana.” (Matendo 11:21, NW) Jinsi tulivyopata kwamba maneno hayo yanatumika sana kwa ndugu zetu Wakristo katika Urusi! Shamba la Kirusi na libaki likiwa limeiva kwa ajili ya uvunaji wa kiroho, na maelfu zaidi huko na wajiunge na lile pendeleo lenye thamani la kusaidia hata na wengine kwenye barabara ya uhai.—Imechangwa.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Juu: Familia tuliyokaa nayo. Juu na kulia: Kutoa ushahidi katika bustani. Chini-kulia: Serosha na barua yake
[Picha katika ukurasa wa 26]
Majengo mapya ya Watch Tower katika Tallinn, Estonia