Vijana Huuliza. . .
Naweza Kuzifanyaje Hisia Hizi Ziondoke?
“Hata ingawa sasa naona ugoni-jinsia-moja kuwa wenye kuchukiza, nyakati nyingine ninajikuta nikivutiwa nao. Hisia hizi hunisumbua, nyakati nyingine usiku na mchana. Nimesali kwa Yehova bila kuacha, ‘Ondolea mbali hisia hizi mbaya!’ Je, zitapata kuondoka wakati wowote?”—Dennis.a
BAADHI YA vijana Wakristo—wa kiume na wa kike—wametoa maombi kama hayo ili wapate msaada. Wanahisi wakivutwa kuelekea ugoni-jinsia-moja lakini hawataki kushiriki uholela, ugonjwa, na ufilisi wa kiadili ambao ndio kawaida ya mtindo-maisha huo. La maana zaidi, wao hutaka kumpendeza Mungu, na katika Neno lake yeye hushutumu waziwazi ugoni-jinsia-moja.—Warumi 1:26, 27; Wakolosai 1:10.
Hudaiwa mara nyingi kwamba wagoni-jinsia-moja hawawezi kubadilika. Hata hivyo, hilo si kweli. Baadhi ya Wakristo wa mapema mbeleni walizoea ugoni-jinsia-moja, lakini walibadilika. (1 Wakorintho 6:9-11) Ndiyo, kinyume cha ngano zipendwazo na wengi, watu wanaweza kubadilika na hubadilika. Hata hivyo, ingawa huenda kijana akaepuka vitendo vya ugoni-jinsia-moja, yeye huenda akapata kuwa vigumu kuondosha kabisa tamaa ya ugoni-jinsia-moja. Mwanamume mmoja kijana aliungama hivi: “Nimejaribu kubadili hisia zangu. Nimesali kwa Yehova ili nipate msaada. Mimi husoma Biblia. Nimesikiliza hotuba juu ya jambo hilo. Lakini sijui nigeukie wapi.”
Hakuna tiba ya kimzungu au ya dakika moja. Dennis akumbuka: “Nilijiingiza katika utendaji wa uholela wa ugoni-jinsia-tofauti katika jitihada ya kuwa ‘mwanamume.’ Kote huku kulikuwa kujitaabisha na kulitokeza maumivu zaidi tu.” Hata hivyo, kwa kutumia kanuni za Biblia, mtu aweza kukabiliana na hisia kama hizo.
Kutambua Njia Mbaya za Kufikiri
Kwanza kabisa, tambua kwamba vitendo hutanguliwa na mawazo. (Isaya 55:6, 7; Yakobo 1:14, 15) Kwa kweli, aonelea Dakt. Wayne W. Dyer: “Huwezi kuwa na hisia (hisia-moyo) kabla ya kwanza kuwa umepata wazo fulani.” Hivyo kwenye mzizi wa tamaa za ugoni-jinsia-moja huenda kukawa na njia za kufikiri kulikopotoka kuhusu mtu mwenyewe, mtu wa jinsia-tofauti, upendo, na kadhalika. Kabla ya mtu ‘kufanya upya nia yake’ na kubadili mawazo hayo, mtu lazima ayatambue. (Warumi 12:2) Kufanya hilo kwaweza kumpa mtu uelewevu mwingi wa ndani wenye thamani katika kujua kwa nini yeye avutwa kuelekea watu wa jinsia ileile.
Mtu aweza kufanyaje hilo? Njia moja ni kusali, kama alivyofanya mtunga-zaburi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu.” (Zaburi 139:23, 24) Huenda ikasaidia pia kuzungumza hisia zako na Mkristo mwenye hekima na aliye mkomavu. Kama Mithali 27:17 inavyoeleza, ‘chuma hunoa chuma.’ Mwanamume mmoja kijana alimtolea moyo wake mzee mmoja Mkristo aliyejulikana kwa kuwa mwenye kuelewa na mwenye huruma. Haikuwa rahisi kwake kutumaini mtu yeyote kuficha siri yake, lakini uhusiano wenye thamani ulikuzwa. “Naweza kuongea naye kuhusu chochote,” yeye asema. Mzee huyo hasikilizi tu bali kwa kuuliza maswali kwa ustadi, husaidia kuvuta hisia na mawazo ya mwanamume huyo kijana.—Linganisha Mithali 20:5.
Ikiwa kijana wa kiume amekuwa na baba mwenye kutojali au mwenye kudhulumu, huenda akapata kuwa uvutio wake kwa watu wa jinsia ileile kwa kweli ni jaribio lisilo na matokeo la kupata upendo wa kibaba. Kwa kutopata kuwa na mtu wa kiume wa kuiga, huenda akahisi kile Dakt. Joseph Nicolosi aita “hisi ya udhaifu na kutofaa kuhusu zile sifa zinazoshirikishwa na kuwa wa kiume, yaani, uwezo, uthabiti, na nguvu.” Ikiwa mtu afikiria kila moja ya vitabia hususa ambavyo katika hivyo ahisi amepungukiwa, huenda akagundua kwa kushangazwa kwamba hivi ni vitabia hasa ambavyo avipata kuwa vyenye kuvutia katika wanaume wengine.
“Masomo” Machungu Kutoka Wakati Uliopita
Vijana wengine huja kung’amua kwamba tatizo lao linahusiana na kumbukumbu mbaya za wakati uliopita. Akumbuka msichana mmoja: “Nilikuwa nikisoma vichapo vya kipornografia vyenye vichwa vinavyohusu ugoni-jinsia-moja. Nikaanza kukuza tamaa zisizo za asili.” Mwanamume mmoja kijana ataarifu hivi: “Nililawitiwa na baba yangu. Kama tokeo, kufanya ngono na mwanamume kulionekana kuwa jambo la kawaida kwangu.” Maono hayo yenye kufadhaisha huenda yakafunza wapatwao na tatizo hili kuchukia au hata kuhofu mtu wa jinsia-tofauti au kulinganisha upendo na ukaribiano wa kimwili. Msichana mmoja aliyepatwa na tatizo hili aelezea tamaa zake za kingono kuwa “uhitaji wa kihisia-moyo, si wa kimwili—uhitaji wa wororo na hali ya kuelewa.”
Ingawa kwa kukubalika, visababishi vya ugoni-jinsia-moja ni vyenye utata, na visa vingi hutaka maelezo mengi.b Hata hivyo, licha ya kile ambacho kimesababisha kufiri kwenye kosa, kuna mengi ambayo mtu aweza kufanya ili kukirekebisha.
Kufanya Upya Nia Yako
Njia bora zaidi ni kutumia Neno la Mungu. Chukua kwa mfano, mwanamume kijana anayejikuta akivutiwa na wanaume ambao huonyesha sifa za kiume ambazo yeye ahisi hana. Au mwanamke kijana ambaye ni mwenye kuhofu watu wa jinsia-tofauti. Njia moja ambayo wote waweza kukuza maoni yafaayo ya sifa ya kiume ni kujifunza kielelezo cha Yesu. (1 Petro 2:21) Yeye alikuwa kiolezo kikamilifu cha uwezo wa kiume uliosawazishwa na upole. (Mathayo 19:14; Yohana 19:5) Kwa hiyo mwanamume mmoja kijana hupata kukiwa kwenye msaada kujifunza kile kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.c “Kupata kumjua Yesu hurekebisha upya mawazo yangu juu ya jinsi mwanamume apaswavyo kuwa,” yeye asema.
Kutafakari juu ya maandiko ya Biblia ambayo hushughulika na habari kama vile maoni ya Mungu kuhusu ngono, upendo, na urafiki wa jinsia-moja ni kwenye msaada vilevile katika kurekebisha kufikiri kwa mtu.—Mwanzo 1:27, 28; Ruthu 1:16, 17; 1 Samweli 18:1; Mithali 5:18, 19; 1 Wakorintho 13:4-8.
Ni jambo la maana vilevile kutodumu katika mawazo mabaya. Mara nyingi tamaa hizo huwa hasa na nguvu wakati mtu ni mwenye upweke, ameshuka moyo, au kukasirishwa. (Mithali 24:10) “Njia pekee ya kubadili vile tulivyo ni kubadili mawazo mabaya kuwa mema,” asema mwanamke mmoja Mkristo. Tamaa zisizo safi kiadili zinapomjia, yeye hujikumbusha juu ya maoni ya Mungu kuhusu ugoni-jinsia-moja. Mvulana mmoja tineja asema hivi: “Wakati wowote ninapokuwa na tamaa za ugoni-jinsia-moja, ninatafakari juu ya andiko la Biblia nilipendalo zaidi.” (Linganisha 2 Wakorintho 10:4; Wafilipi 4:8.) Wengine wamepata kulala usingizi wakisikiliza kaseti tofauti-tofauti za Kibiblia za Watch Tower Society kukiwa kwenye kusaidia.
Kama tu vile jinsi tufikirivyo huathiri jinsi tutendavyo, ndivyo jinsi tutendavyo kuwezavyo kuathiri jinsi tufikirivyo na kuhisi. Kwa hiyo, mtu apaswa kuacha mwenendo na ushirika ambao waweza kuanzisha au kuongezea nguvu tamaa mbaya. (1 Wakorintho 15:33) Huenda mtu akahitaji pia ‘kulinda’ inapokuja kwenye vyoo vya umma, kwenye bichi, vyumba vya kubadilishia mavazi, na mahali penginepo ambapo pangeweza kumweka mtu katika hali ya kishawishi.—Zaburi 119:9.
Kupiga punyeto ni zoea jingine lisilofaa la kuepuka. Kwa wanaume na wanawake wengi walio wagoni-jinsia-moja, ni shurutisho lisiloweza kudhibitiwa. “Nimekuwa na shida ya kupiga punyeto tangu nilipokuwa mwenye umri wa miaka sita,” aungama mwanamume mmoja kijana. “Kuwazia-wazia raha za kingono kulitia nguvu hisia zangu za ugoni-jinsia-moja.” Pinga zoea hili chafu!d—Wakolosai 3:5.
Kwa upande ule mwingine, ni jambo la maana kwamba mtu aimarishe njia za mwenendo ufaao. Wengine wamedokeza kwamba mwanamume kijana akikuza vitabia vya kiume, huenda asivutiwe sana na wanaume wengine. Bila shaka, huenda mwanamume kijana asijue jinsi ya kufanya hivyo ikiwa hakuwa kamwe na mtu wa kuiga alipokuwa mtoto. Huenda hata akaudhika na mwili wake mwenyewe na kuhisi vibaya au kutokuwa mwanamume. Kujihusisha katika kazi inayotaka nguvu, mazoezi ya mwili ya kiasi, au utendaji wa michezo wenye kutuliza mara nyingi husaidia katika hali hii. (Linganisha 1 Timotheo 4:8.) Lakini kama vile tu mwanamume kijana Timotheo alivyokuwa kama mwana kwa mtume Paulo, ndivyo mtu awezavyo kuona kukuza uelewevu ufaao na mwanamume Mkristo aliye mkubwa kwa umri kukiwa kwenye msaada. (Wafilipi 2:19-22; 2 Timotheo 3:10) Kwa kuimarisha mipaka ya kimwenendo iliyo wazi na kukuza uwasiliano wa wazi, uhusiano huo waweza kuwa mchangamfu na wenye kutumaini, na bado uwe bila uhusiano wowote wa kimahaba.
Zaidi ya yote, lazima mtu awe na nguvu nyingi za kiroho. Funzo la Biblia la kawaida, sala, na kushiriki imani yako pamoja na wengine husaidia kuweka akili kwenye kijia cha kiroho. (Zaburi 55:22; 119:11; Warumi 10:10) Nyakati fulani hisia za kutofaa kitu huenda zikafanya iwe vigumu kuwa miongoni mwa Wakristo-wenzi, lakini Biblia inaonya dhidi ya kujitenga mwenyewe. (Mithali 18:1) Ushirika wenye kujenga pamoja na Wakristo wa jinsia zote waweza kusaidia mtu abaki na usawaziko.—Waebrania 10:24, 25.
Ikiwa unakumbwa na tamaa ya ugoni-jinsia-moja, huenda madokezo haya yakathibitika kuwa yenye kusaidia. Ingawa hivyo, usivunjike moyo kupita kiasi ikiwa hisia mbaya zaendelea. Mungu aelewa hisia zako naye ana huruma kwa wale ambao hujikakamua kumtumikia. (1 Yohana 3:19, 20) Katika ulimwengu mpya, wanadamu watapata kutibiwa maradhi yote yanayotupata. (Ufunuo 21:3, 4) Kwa wakati uliopo, mtegemee Mungu na upigane dhidi ya tamaa mbaya. (Wagalatia 6:9) Baada ya wakati na bidii yenye kuazimia, labda hata tamaa hizo mbaya zaweza kupotelea mbali.
(Kuanzia toleo letu lijalo, “Vijana Huuliza . . .” itatokea mara moja kwa mwezi.)
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Ona “Vijana Huuliza . . .” katika toleo letu la Februari 8, 1995.
c Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
d Sura 25 na 26 za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi (kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.) kina madokezo yanayotumika ili kusaidia kijana ashinde uraibu huu.
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Kuza maoni yafaayo ya sifa za kiume kwa kujifunza kielelezo cha Yesu