Afya Kamilifu kwa Wote
KAMA vile tabia, mazingira, na utunzaji wa afya, umbo letu la kibiolojia pia huathiri afya yetu. Umbo hilo huathiriwa na urithi na magonjwa ambayo huenda yakatokea baadaye kwa sababu ya kuwa na silika ya kijeni ya kuweza kupatwa nayo.
“Umbo la kibiolojia ulilozaliwa nalo,” asema mtaalamu mmoja wa afya, “huamua kwa kiwango kikubwa kama utaishi vizuri, utaishi muda mrefu, au hutaishi kamwe.”
Hata iwe ni katika njia ipi tunayopata, kuumwa na kichwa, misuli iliyonata, neva zilizofinyika, mifupa iliyonyauka, moyo unaofanya kazi kwa kushindwa, na magonjwa mengine hutukumbusha kila siku kwamba afya yetu inafanyizwa na mwili na akili iliyo na kasoro. Ni nini sababu ya matatizo haya ya afya yaeneayo kote?
Sababu ya Msingi
Daktari fulani wa kitiba aitwaye Luka aliyeishi katika karne ya kwanza W.K. ajibu swali hili katika hadithi iliyopuliziwa aliyoandika kuhusu maisha ya Yesu Kristo. Siku moja, aandika Luka, mtu fulani aliyepooza aliletwa kwa Yesu kwa matumaini kwamba angeponywa. Yesu alimwambia mpooza hivi: “Umesamehewa dhambi zako.” Kisha, ili kuonyesha kwamba kwa kweli alikuwa na uwezo wa kusamehe dhambi, Yesu alimwamuru mtu huyo hivi: “Ondoka, ujitwike kitanda chako, ukaende zako nyumbani kwako.” Mwanamume huyo akafanya hivyo! Kama tokeo, “ushangao ukawashika wote” walioshuhudia maponyo hayo, na “wakamtukuza Mungu.”—Luka 5:17-26.
Yesu alirejezea dhambi gani? Jibu latusaidia kuelewa kwa nini sisi huwa wagonjwa, huzeeka, na kufa. Tukiwa tumehakikishiwa kwamba “kila andiko, [ni] lenye pumzi ya Mungu,” twaweza kutumaini Biblia kwa jibu hilo. (2 Timotheo 3:16; 2 Petro 1:21) Hiyo hutuambia kwamba mwanadamu wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mkamilifu kiafya. Alifurahia afya nzuri mradi alimtii Muumba wake.
Hata hivyo, Adamu, alichagua kuvunja sheria ya Mungu. Kwa kuwa asiyetii na kuasi kimakusudi dhidi ya Muumba wake, alikuwa akitenda dhambi. Kama tokeo, akawa asiyekamilika, awezaye kupatwa na magonjwa, na baada ya muda alikufa. Hivyo basi, dhambi, ilikuwa chanzo cha magonjwa na kifo cha Adamu.
Sawa na vile maradhi fulani hupitishwa kutoka kwa wazazi hadi kwa watoto ukiwa utendaji wa kanuni urithi-tabia, ndivyo kutokamilika na magonjwa yalipitishwa kutoka kwa Adamu hadi kwa wazao wake, jamii ya kibinadamu. Hivyo, maradhi yote ni tokeo la dhambi ya kwanza ya Adamu. (Mwanzo 2:17; 3:1-19; Warumi 5:12) Je, kuna njia ya kutokea?
Njia ya Kutokea
Lile badiliko la kutoka kwa afya kamili hadi kwa afya mbaya lilisababishwa na dhambi—uasi wa Adamu dhidi ya sheria ya Mungu. Badiliko la kutoka kwa afya mbaya hadi kwa afya kamilifu lawezekana tu kwa kuondolewa kwa dhambi. (Warumi 5:18, 19) Jinsi gani? Binadamu mwingine mkamilifu, mfano halisi wa Adamu alipokuwa mkamilifu, angelazimika kudhabihu uhai wake kuwa fidia. Sheria ya Mungu ni kwamba “nafsi itakuwa kwa ajili ya nafsi,” yaani, uhai kwa ajili ya uhai.—Kumbukumbu la Torati 19:21, New World Translation.
Hata hivyo, hakuna mzawa wa Adamu mwenye dhambi angeweza kuandaa fidia kama hiyo. Hivyo, Yehova mwenyewe kwa upendo aliandaa Mwanaye, Yesu, akiwa binadamu mkamilifu ili kutoa uhai wake kuwa “fidia ya wengi” ili kwamba “tupate uzima kwa yeye.”—Mathayo 20:28; 1 Yohana 4:9; Zaburi 49:7.
Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba Baba yake, Yehova, alikuwa amempa uwezo kuondoa dhambi alipomwambia yule mpooza, “umesamehewa dhambi zako,” na mwanamume aliyeponywa akaenda nyumbani. Mara kwa mara Yesu alitumia uwezo wake kutoka kwa Mungu kwa kuponya mara hiyo vipofu, viziwi, na wengine waliokuwa na magonjwa ya kila aina.
Kuhusu maponyo haya ya kimuujiza ya Yesu, Biblia husimulia hivi: “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; hata ule mkutano wakastaajabu, walipowaona mabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanakwenda, na vipofu wanaona.” (Mathayo 15:30, 31) Hata lenye kutokeza zaidi, Yesu aliweza kuwarudisha watu waliokufa kwenye uhai. Biblia husimulia baadhi ya ufufuo huo mbalimbali.—Luka 7:11-16; 8:49-56; Yohana 11:14, 38-44.
Uponyaji huo mbalimbali wa kimuujiza hutuhakikishia kwamba hakuna maradhi yawezayo kushinda uwezo wa kuponya wa Yesu. Je, atatumia tena uwezo huo aliopewa na Mungu? Twaweza kunufaika?
Kupata Afya Kamilifu Ni Uhakika
Unabii mbalimbali wa Biblia waonyesha kwamba Yesu tayari anatawala katika mbingu akiwa Mfalme wa serikali ya kimbingu ya Mungu. Mungu amempa mamlaka ili aondoe serikali zote za binadamu zilizopo sasa na kutawala dunia nzima. (Zaburi 110:1, 2; Danieli 2:44) Itakayotimizwa ni ile sala ambayo Yesu alifunza wafuasi wake: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Chini ya utawala wa Ufalme huo wa kimbingu, sehemu ya mapenzi ya Mungu kwa ajili ya dunia hii itakuwa kuboresha hali ya afya kwa kiasi kikubwa kwa familia ya binadamu.
Kisha, katika njia halisi na pia katika maana ya kiroho, “macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” “Hapana mwenyeji atakayesema: Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; 35:5, 6.
Chini ya Ufalme wa Mungu wa kimbingu, afya kamilifu itamaanisha kwamba watu hawatalazimika kufa kama wafanyavyo sasa. Neno la Mungu laahidi hivi: “Kila mmoja azoeaye imani katika yeye [ata]pata uhai udumuo milele.” “Zawadi apayo Mungu ni uhai udumuo milele kupitia kwa Kristo Yesu Bwana wetu.” (Yohana 3:16, NW; Warumi 6:23, NW) Ndiyo, kale sana zaburi iliyopuliziwa roho iliahidi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29) Kama alivyofanya alipokuwa duniani, wakati huo Yesu atafufua wafu na kuwapa nafasi ya kunufaika na afya kamilifu. Biblia yaahidi hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 24:15.
Dunia yenyewe itanawiri chini ya utawala wa Ufalme hivi kwamba njaa, ichangiayo afya mbaya, kamwe haitakuwapo tena. Unabii wa Biblia hutuambia hivi: “Mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao.” (Ezekieli 34:27) “Nchi imetoa mazao yake, MUNGU, Mungu wetu, ametubariki.” (Zaburi 67:6) “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi.” (Zaburi 72:16) “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.”—Isaya 35:1.
Kikisema kwa ufupi juu ya hali itakayokuwako katika ulimwengu mpya wa Mungu, kitabu cha unabii cha mwisho cha Biblia hutangaza hivi: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.
Je, wasema, ‘Ni vigumu kuamini hilo’? Basi, fikiria hili. Kabla ya Adamu kuwa mtenda dhambi, alikuwa na afya kamilifu. Ebu wazia kwamba mtu fulani angeweza kuongea naye wakati huo na kumwambia kwamba siku moja dunia ingejazwa watu wenye kuumwa, wagonjwa, na wenye kuzeeka. Je, unafikiri kwamba Adamu angeona hilo kuwa vigumu kuamini? Ilhali, hilo ni jambo la hakika sasa.
Kinyume cha hayo, afya kamilifu itakuwa jambo la hakika chini ya Ufalme wa Mungu. Neno la Yehova latuhakikishia hivi: “Maneno hayo ni amini na kweli.” (Ufunuo 21:5) Lile analosema Mungu kwamba litatukia, litatukia kwani “Mungu hawezi kusema uongo.”—Waebrania 6:18.
Unaweza kufanya nini sasa ili uwe na uhakika wa kufurahia baraka hizo zijazo? Njia ya kuelekea kwenye afya kamilifu na uhai udumuo milele iliwekwa wazi na yale Yesu aliyosema katika sala kwa Baba yake: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
Waombe Mashahidi wa Yehova mtaala wa Biblia bila malipo nyumbani mwako. Watafurahi kukusaidia kujifunza zaidi kuhusu ahadi za ajabu za Mungu. Hiyo itakuwa hatua yako ya kwanza kwenye njia ielekeayo kwenye afya kamilifu!
[Picha katika ukurasa wa 14]
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, wanadamu wote watafurahia afya kamilifu