Je, Afya Kamili Ni Ndoto Tu?
JE, UMEWAHI kuwa mgonjwa sana au kufanyiwa upasuaji mkubwa? Ikiwa umewahi, yaelekea sasa wathamini uhai hata zaidi. Bila kujali hali yako ya kimwili, je, waamini kwamba yawezekana kufurahia afya kamili? Huenda jambo hili lisionekane kuwa halisi kwa sababu ya kuenea kwa magonjwa yenye kudhoofisha kama kansa au maradhi ya moyo. Kwa kweli, sote huwa wagonjwa mara kwa mara. Na bado, kuwa na afya kamili si ndoto tu.
Mwanadamu aliumbwa afurahie afya bora, si ang’ang’ane na magonjwa na kifo. Hivyo, ili kukinza magonjwa na kifo, Yehova aliandaa msingi kwa ajili ya afya kamili na uhai wa milele kupitia kwa dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Watakaoishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa hawatang’ang’ana na afya mbaya au uzee. Kwa kuwa ndivyo hali itakavyokuwa, itakuwaje kwa magonjwa?
Kitulizo Kutokana na Ugonjwa
Njia ambayo Yesu Kristo aliwaponya wagonjwa huandaa kiolezo. Kuhusu maponyo hayo ilisemekana hivi: “Vipofu wanaona tena, na vilema wanatembea huku na huku, wenye ukoma wanasafishwa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa, na maskini wanatangaziwa habari njema.” (Mathayo 11:3-5) Ndiyo, wasiojiweza wote waliomkaribia Yesu ‘waliponywa kabisa.’ (Mathayo 14:36) Likiwa tokeo, “umati ukahisi mshangao ulipoona mabubu wakisema na vilema wakitembea na vipofu wakiona, nao ukatukuza Mungu wa Israeli.”—Mathayo 15:31.
Kwa kweli, ingawa hakuna mtu yeyote leo awezaye kufanya maponyo ya namna hiyo, twaweza kuwa na uhakika kwamba chini ya utawala wa Mungu wanadamu watafikia ukamilifu, wakiponywa maradhi yote ya kiakili na kimwili. Ahadi ya Mungu imerekodiwa katika Ufunuo 21:3, 4: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”
Wazia ulimwengu usiohitaji kiwanda cha dawa au hospitali, upasuaji, au tiba! Zaidi ya hayo, katika Paradiso itakayorudishwa, mshuko-moyo na maradhi ya kiakili yatakuwa mambo ya zamani. Maisha yatapendeza kihalisi; na furaha itadumu. Kwa kweli, nguvu za Mungu zisizo na mipaka zitatendesha utaratibu wa mwili wa kujifanya upya, na manufaa za fidia zitaondoa matokeo yenye kudhoofisha ya dhambi. “Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
Ni tumaini ajabu kama nini—kufurahia afya kamili ya kimwili na ya kiroho chini ya Ufalme wa Mungu! Udumishapo mtindo-maisha uliosawazika na wenye afya sasa, tazamia kwa hamu baraka za ulimwengu mpya wa Mungu. Yehova na ‘aushibishe mema uzee wako, ujana wako ukarejezwe kama tai’!—Zaburi 103:5.