Ugonjwa—Kuna Tumaini Gani la Kupata Faraja?
HAIWEZI kukanwa kwamba, wakiwa na ufahamu mwingi zaidi wa visababishaji vya ugonjwa wa kibinadamu, madaktari wamefanya maendeleo yenye kutokeza sana katika kupunguza maradhi fulani. Hata hivyo matatizo ya kijamii yamezuia wengi wasifurahie faida hizo za maendeleo ya tiba. Kwa hiyo, kuna nafasi kubwa ya kufanya maendeleo.
Hata hivyo, kuna kisababishaji cha msingi cha ugonjwa na kifo ambacho madaktari hawana uwezo wa kukiondoa. Kwa sababu hiyo, wanadamu kwa kujitegemea hawatafaulu kabisa kamwe katika pigano lao na maradhi. Walakini kama tunaweza kujua kisababishaji hicho cha msingi, tutasaidiwa kuona kama tunaweza kutumainia faraja kutokana na adui huyo.
KWA SABABU GANI TUNAPATWA NA MAGONJWA?
Sababu ya msingi ya watu kuwa wagonjwa na kufa inafunuliwa katika ahadi ya kutokeza sana ya Mungu aliyowapa Waisraeli wa kale: “Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.” (Isa. 33:24) Ni hapa ambapo ugonjwa unahusianishwa na “uovu,” au dhambi. Na kuwa huru na ugonjwa kunahusianishwa na msamaha wa dhambi.
BASI, JE! UGONJWA NI ADHABU YA DHAMBI?
Ugonjwa unaweza kuwa matokeo ya moja kwa moja ya dhambi. Biblia inatuonya hivi: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Kama tulivyotangulia kuona, wale ‘wanaopanda’ uasherati, wale wanaovuta sigara, wale wenye hatia ya ulevi na ulafi ‘wanavuna’ maradhi mengi. Ni kweli kwamba si magonjwa yote yanayosababishwa na mambo hayo. Hata hivyo, kisababisho cha magonjwa yote kikifuatwa kinatufikisha kwa “uovu,” au dhambi.
KWA SABABU GANI WATU WANAKUWA WAGONJWA?
Ni kwa sababu dhambi ambayo ndiyo chanzo chenye kutokeza maradhi si yetu wenyewe. Ilitokea zamani za kale, pale-e-e mwanzoni mwa historia ya kibinadamu. Biblia inatuambia kwamba Mungu alimwumba mwanamume wa kwanza, Adamu, akiwa mkamilifu, mwenye afya, na akiwa na taraja la kuishi milele. Ili aendelee kujifurahisha hayo yote ilitegemea kumtii Muumba. Adamu alichagua kuasi na hivyo akajitenga na Mungu, ambaye ndiye “chemchemi ya uzima.” Kwa hiyo, mwanamume huyo wa kwanza akawa asiyekamilika, mwenye kupatwa na ugonjwa, na hatimaye kufa.—Mwa. 2:17; 3:1-19; Zab. 36:9.
Inajulikana vizuri kwamba maradhi mengine ni ya kurithi. Vivyo hivyo, dhambi, kutokukamilika na kifo ni mambo ya kurithi. “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Rum. 5:12) Urithi ambao Adamu aliwapa watoto wake ulikuwa uzima usiokamilika pamoja na hali ya kuweza kupatwa na ugonjwa na kifo. Hiyo ndiyo sababu ya msingi ya kuwapo kwa maradhi leo.
JE! MUNGU ANAPENDEZWA NA KUTUNZA AFYA YA WATU?
Hakika anapendezwa! Kwa mfano, yeye aliwaambia Waisraeli hivi: ‘‘[Yehova] atakuondolea ugonjwa wote.”—Kum. 7:15.
MUNGU ALIIHIFADHIJE AFYA YA WAISRAELI?
Yeye aliwapa orodha ya sheria ambayo ilitia mipango ya kulinda afya yao. Kuhusu sheria hizo, daktari mmoja alisema: “Wachunguzi wenye maarifa sana wa tiba ambao sasa wanafanya kazi bora zaidi wanafikia umalizio kwamba Biblia ni kitabu cha kisayansi kilicho sahihi sana . . . Mambo ya hakika ya maisha, utambuzi wa vyanzo vya maradhi, utibabu, na tiba ya kuzuia maradhi iliyoandikwa katika Biblia ni bora sana na yenye kutegemeka zaidi ya mawazo ya Hippocrates.” Hippocrates, ambaye nyakati nyingine anaitwa “baba wa tiba ya kisasa,” aliishi karibu miaka 1,000 baada ya Mungu kuwapa Waisraeli Torati.
JE! MUNGU ANATUSAIDIA TUENDELEE KUWA NA AFYA LEO?
Ndiyo, Biblia ina amri tulizowekewa leo ambazo zinatumika kulinda afya yetu iwapo tunazifuata. Ulevi, ulafi, kulalana kwa watu wa namna moja, uzinzi na uasherati, ambayo ni mambo yanayotokeza matatizo mengi ya moyoni pamoja na magonjwa ya kimwili, yanakatazwa moja kwa moja katika Biblia. (Mit. 23:20, 21, 29-35; 1 Kor. 6:9-11) Vivyo hivyo, ‘tukijitakasa na uchafu wote wa mwili na roho,’ tutaepuka maradhi yanayoletwa na uvutaji wa sigara, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kutafuna tambuu. (2 Kor. 7:1) Hata kujisafisha kwa ukawaida kunalinda afya yetu.
Pamoja na hayo, tunaambiwa hivi: “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.” (Mit. 17:22) Leo, matokeo ya wasiwasi, kushuka moyo, upweke na maono mengine yanaonekana wazi. Daktari mmoja alisema kwamba karibu asilimia 90 ya wagonjwa wote waliokuwa wakija kwenye kiliniki (hospitali) yake walikuwa na mkazo wa maono ya ndani. Biblia inaonyesha jinsi ‘moyo mchangamfu’ ulivyo wa maana na inatupa msaada unaofaa juu ya namna tunavyoweza kuendelea kuwa na mioyo michangamfu.
Tukifuata hayo pamoja na kanuni kama hizo za Biblia, tutalindwa na magonjwa mengi yanayowapata watu leo.
JE KUNA WAKATI WO WOTE TUTAKUWA NA AFYA NJEMA YA KUDUMU?
Ndiyo, kunao, iwapo tutafanya jambo lile ambalo Adamu alishindwa kufanya—kumtumaini Mungu kabisa na kumtii Yeye. Kukombolewa kwetu kabisa na ugonjwa kutatimizwa kupitia Yesu Kristo. Yesu alizaliwa katika njia isiyo ya kawaida, kwa uhai wake kuhamishwa kwa uwezo wa Mungu Mweza Yote kutoka cheo chake chenye utukufu mbinguni mpaka kwa chembe ya yai katika tumbo la uzazi la bikira mmoja. Kwa hiyo, akiwa hana baba ya kibinadamu, yeye hakurithi uhai usio mkamilifu ambao Adamu alitupa sisi wengine wote kama urithi.
Yesu alikuwa mkamilifu. Likiwa ni tendo la upendo mwingi, yeye alitoa dhabihu uhai wake mkamilifu kwa ajili yetu, ili kwamba turudi kwenye ukamilifu ule uliopotezwa na Adamu. Wakati kufaa kwa dhabihu hiyo kutakapotumiwa kikamilifu kwa wanadamu, ugonjwa, kifo na matatizo yote yanayoletwa na kutokukamilika yataondolewa.—Mt. 1:18-23; 20:28; Ebr. 7:26.
Katika njia hiyo, unabii juu ya Yesu utatimizwa: “Alijeruhiwa kwa makosa yetu, . . na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”—Isa. 53:5; 1 Pet. 2:24.
JE! KWELI KWELI YESU ALIKUWA NA UWEZO WA KUWAPONYA WATU?
Ndiyo, mbele ya mashahidi wasiohesabika Yesu aliponya “udhaifu wa kila aina.”(Mt. 9:35) Hata yeye aliwafufua wafu. (Yohana 11:43, 44) Yesu alitimiza hayo si kwa uchunguzi wa sayansi ya tiba bali kwa uwezo wa roho ya Mungu. Kwa njia hiyo ilionyeshwa kwamba siku moja ugonjwa wote, na hata kifo, kinaweza kuondolewa na kitaondolewa. Bila shaka, maponyo yaliyofanywa na Yesu yalikuwa ya muda tu. Wale walioponywa wangeweza kuwa wagonjwa tena, na wale waliofufuliwa walikufa tena.
KWA SABABU GANI TUNGALI TUNAPATWA NA MARADHI, NA AMBAPO YESU ALIKUFA KWA AJILI YETU KARIBU MIAKA 2,000 ILIYOPITA?
Jibu ni kwamba kuondolewa kwa ugonjwa kunahusiana na makusudi mengine ya Mungu—kama kutatuliwa kwa suala la enzi kuu ya ulimwengu, kuondolewa kwa Shetani Ibilisi, kuhukumiwa kwa wanadamu, kuokolewa kwa wale watakaoonekana kuwa waaminifu na kuwekwa kwa serikali yenye kutosheleza kwa ulimwengu huu. Makusudi hayo yote yatatimizwa kupitia ufalme wa Mungu chini ya Kristo. (Mt. 6:9; 10) Makusudi hayo bora sana yanahitaji wakati ili yatimizwe.—2 Pet. 3:5-13.
NI WAKATI GANI HATIMAYE UGONJWA UTAONDOLEWA?
Tunajua kwamba hautapita muda mrefu! Yesu aliwapa wafuasi wake “ishara” yenye habari kwa urefu ili kwamba waweze kutambua wakati huo alipokuwa amekwisha kuanza kutawala akiwa mfalme katika mbingu—ambalo ndilo tukio linaloongoza kwenye utimizo wa makusudi mengine ya Mungu. “Ishara” hiyo ilitia vita vya ulimwengu, woga mwingi sana wa wakati ujao, njaa yenye kuenea sana, maradhi ya kuambukia na matukio kama hayo tunayoyaona yakitokea leo. Mbona usiyasome maneno ya Yesu, na habari zaidi inayoongezwa na mtume Paulo? Na uone kama hukubali tunaishi katika wakati ambao Yesu alitaja.—Ona Mathayo, sura ya 24, Marko, sura ya 13, Luka, sura ya 21, na 2 Timotheo 3:1-5.
Sasa ndio wakati kwa ufalme wa Mungu kujiingiza katika mambo ya kibinadamu. (Mt. 24:14; 25:31-46; Dan. 2:44) Tukijifunza ni nini mapenzi ya Mungu kwetu na kuyatimiza, tunaweza kuishi tushuhudie utimizo wa baadhi ya ahadi hizo bora sana katika Biblia. Hali kama zile Mungu alizowaahidi Waisraeli wa kale zitaonekana: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isa. 35:5, 6.
Wazazi hawatahuzunishwa tena na magonjwa ya watoto wao. Wala ahadi ya kuwa vijana haitashindwa; wala umri mkubwa hautafanywa uwe wenye magumu kwa udhaifu wa kimwili. Mahali pake, itakuwa kama mtume Yohana alivyoona katika njozi: “Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena: wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufu. 21:4.
Je! mambo hayo yatatokea kweli kweli? Hakika ndiyo. Yohana alisikia Yehova mwenyewe akitoa uhakikisho wa jambo hilo, kwa maana twasoma hivi: “Yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.” (Ufu. 21:5) Katika wakati huo unaokaribia haraka sana, wanadamu watafurahia faraja kamili kutokana na ugonjwa. Katika njia nzuri sana itakuwa kweli kwamba “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa; watu wakaao humo watasamehewa uovu wao.”—Isa. 33:24.