Karibuni Hakutakuwa Tena Ugonjwa Wala Kifo!
HAKUNA mtu huonea shangwe kuwa mgonjwa, wala wanadamu hawataki kufa. Profesa mmoja wa somo la ujamii wa kitiba ashikilia hivi: “Utafutaji wa maisha marefu zaidi waonekana kuwa kama wa ulimwenguni pote katika historia yote na katika jamii zilizo nyingi. Wahusiana na kichocheo cha msingi cha kujihifadhi binafsi . . . Ponce de Leon ndiye pekee aliye maarufu zaidi kati ya mstari mrefu wa wanadamu waliotumia maisha yao wakitafuta maisha marefu zaidi. Kadiri kubwa ya sayansi ya kitiba imewekwa wakfu kwa kuhifadhi maisha marefu zaidi kupitia kupambana na maradhi na kifo.
Kifo huharibu na kusababisha maumivu kwa asili yetu ya kindani hivi kwamba wakati kiwashindapo marafiki na washiriki wa familia, kwa njia ambayo karibu ni ya kiasili sisi hujaribu kupunguza uzito wacho. Kitabu Funeral Customs the World Over chaonelea hivi: “Hakuna kikundi chochote, hata kiwe ni cha kishamba mno kwa upande mmoja au chenye uungwana mno kwa upande mwingine, ambacho kikiachwa huru peke yacho na ndani ya uwezo wacho wa kufanya mambo hakiondolei mbali maiti za washiriki wacho kwa sherehe. . . . Jambo hilo hutosheleza hisia za kina kirefu za ulimwenguni pote. Kutekeleza hilo huonekana kuwa ndilo jambo ‘la haki,’ na kutolitekeleza, hasa kwa ajili ya wale wenye kuunganishwa na vifungo vya kifamilia, vya hisia, maisha ya ushirika, maono mamoja au vifungo vinginevyo, huonekana kuwa jambo ‘la makosa,’ ukosefu usio wa kiasili, jambo la kuombewa radhi au la kuaibikia. . . . [Binadamu] ni mtu ambaye huzika wafu wake kwa sherehe.”
Chanzo cha Ugonjwa na Kifo
Hivyo wazo la kwamba siku moja ugonjwa na kifo zitakomeshwa lina uvutio wenye nguvu, lakini je! kuna msingi wa imani ya jinsi hiyo? Kwa kweli kunao, nao una sababu nzuri, ni wenye kutegemeka, na hauwezi kushindwa. Huo ni Neno la Muumba wetu lililovuviwa roho —Biblia Takatifu.
Kitabu hicho chaeleza wazi chanzo cha taabu ya kibinadamu. Chatuambia kwamba mwanadamu wa kwanza, Adamu, aliumbwa na Mungu na kuwekwa katika kao la bustani ya paradiso iliyokuwa mahali fulani katika Mashariki ya Kati. Adamu aliumbwa mkamilifu; ugonjwa na kifo zilikuwa hazijulikani kwake. Muda si muda aliungwa na mke aliye mkamilifu hali moja, na pamoja wakaonea shangwe tazamio la uhai wa milele duniani.—Mwanzo 2:15-17, 21-24.
Hali hii bora haikuendelea kwa muda mrefu. Kwa nini? Kwa sababu Adamu alichagua kwa ubinafsi njia ya maisha ya kutomtegemea Mungu. Kazi ngumu, maumivu, ugonjwa, na hatimaye kifo zilitokea. (Mwanzo 3:17-19) Wazao wake walirithi namna ya maisha yasiyo na furaha ambayo Adamu alikuwa amechagua. Warumi 5:12 yaeleza hivi: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” Warumi 8:22 yaongezea hivi: “Twajua ya kuwa viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.”
Duniani au Mbinguni?
Hata hivyo, Biblia yatuhakikishia kwamba karibuni Mungu atarudisha ainabinadamu tiifu kwenye ile hali ya furaha ambayo Adamu na Hawa walipoteza. Wasema hivi Ufunuo 21:3, 4: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Nabii mmoja wa kale alitangulia hivyo hivyo kuuona wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
Je! waweza kuwazia ulimwengu bila hospitali, majengo ya kuwekea maiti, na makaburi? Je! waweza kuwazia ukiishi na kuishi, ukiwa huru hata na tisho la kuteseka na kufa? Ndiyo, ahadi ya Mungu hugusa hisia-moyo kwa kina kirefu ndani yetu sote. Hata hivyo, twaweza kuwaje na uhakika kwamba tazamio hilo zuri sana ni kwa ajili ya Dunia-sayari yetu—si kwa ajili ya mbingu? Angalia habari inayozunguka Maandiko yaliyotangulia kutajwa. Mistari ya kwanza ya Ufunuo sura ya 21, ZSB, yanena juu ya “mbingu mpya na dunia mpya.” Taarifa ya wazi yafanywa kwamba Mungu atakuwa pamoja na ainabinadamu na kwamba wao watakuwa watu wake. Ahadi iliyo katika kitabu cha Isaya kwamba hakuna mtu atakayekuwa mgonjwa yafuatwa na rejezo kwa “watu wakaao humo,” ambao ‘wamesamehewa uovu wao.’
Hivyo basi ahadi hizo zinazotia moyo zarejezea uhai duniani! Nazo zapatana na sala ya Yesu kwa Baba yake: “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:10.
Kwa Nini Karibuni?
Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni kuja kwenye utambuzi wa kwamba ahadi hizo zitatimizwa wakati ujao ulio karibu. Ingawa hivyo, ni kwa msingi gani wao huhisi wakiwa na uhakika sana wa jambo hilo? Ni kwa msingi wa uthibitisho mwingi mno kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo, au mpango, uliopo wa mambo duniani. (2 Timotheo 3:1-5) Wanafunzi wa Yesu waliomba ishara juu ya wakati ambapo umalizio wa mfumo wa mambo ungekuwa. Kwa kujibu Yesu alitabiri kirefu matukio ya ulimwengu yenye kupanda juu ambayo yametukia tangu mtokeo wa Vita ya Ulimwengu 1 katika 1914.a Halafu akaongezea hivi: “Myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” Hivyo basi kadiri fulani ya kizazi kilichokuwa hai katika 1914 kitaishi kuuona mwisho wa mfumo wa ulimwengu uliopo.—Mathayo 24:33, 34.
Wakati huo Yehova Mungu atampa utume Mwana wake, Kristo Yesu, aende akaharibu visababishi vyote vya mteseko na huzuni vitoke katika uso wa Dunia-sayari hii yenye upendezi. Biblia husema juu ya kuondolewa kwa uovu kuwa ndiyo “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.
Idadi kubwa sana ya wanadamu wanaomhofu Mungu itaokoka tukio hilo la kutisha waishi wakaone ule utawala wenye amani wa Kristo Yesu ukianza. (Ufunuo 7:9, 14; 20:4) Ingawa utawala wake utakuwa wa kutoka mbinguni, matokeo yenye manufaa ya utawala huo yataonewa shangwe na wote wenye kuishi duniani—waokokaji wa ile vita ya Har–Magedoni na pia wale mamilioni kwa mamilioni ambao kisha watainuliwa kutoka kwa wafu. Ndipo ile ahadi itakapotimia: “Kristo sharti atawale mpaka Mungu atakapowashinda adui zake na kuwaweka chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:25, 26, HNWW.
Hivyo sisi twaweza kupaaza mshangao kwa uhakika hivi: “Karibuni hakutakuwa tena na ugonjwa wala kifo!” Hiyo si ndoto ya kuwazia-wazia tu, wala si kudhania-dhania. Hiyo ndiyo ahadi hakika ya Yehova Mungu, “asiyeweza kusema uongo.” Je! wewe utaweka itibari yako katika tumaini hilo? Laweza kukunufaisha milele!—Tito 1:2.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa uthibitisho zaidi kwamba ainabinadamu inaishi katika siku za mwisho, ona sura ya 18 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, chenye kuchapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ugonjwa na kifo karibuni vitaondolewa na mahali pavyo pachukuliwe na afya yenye kusitawi sana na uhai wa milele