SURA YA KUMI
Wakati Mshiriki wa Familia Ni Mgonjwa
1, 2. Shetani alitumiaje msiba na ugonjwa ili kujaribu kuvunja uaminifu-maadili wa Ayubu?
NI LAZIMA kwa hakika mwanamume Ayubu ahesabiwe miongoni mwa wale waliokuwa na maisha ya familia yenye furaha. Biblia humwita “mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki.” Alikuwa na wana saba na mabinti watatu, watoto kumi kwa ujumla. Alikuwa pia na uwezo wa kuandalia vizuri familia yake riziki. La maana zaidi, yeye aliongoza katika utendaji mbalimbali wa kiroho naye alihangaikia msimamo wa watoto wake mbele ya Yehova. Hayo yote yalitokeza mahusiano ya familia yaliyo ya karibu na yenye furaha.—Ayubu 1:1-5.
2 Hali ya Ayubu haikukosa kuonwa na Shetani, adui mkuu wa Yehova Mungu. Shetani, anayetafuta daima njia za kuvunja uaminifu-maadili wa watumishi wa Mungu, alimshambulia Ayubu kwa kuiharibu familia yake yenye furaha. Kisha “akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.” Hivyo Shetani alitazamia kutumia msiba na ugonjwa ili kuvunja uaminifu-maadili wa Ayubu.—Ayubu 2:6, 7.
3. Dalili za ugonjwa wa Ayubu zilikuwa nini?
3 Biblia haitaji jina la kitiba la maradhi ya Ayubu. Lakini, hutuambia dalili zayo. Mwili wake ulikuwa umefunikwa kwa mabuu, na ngozi yake ilifanyiza maganda na kuoza. Pumzi kutoka kinywani mwa Ayubu ilikuwa yenye kuchukiza mno, na mwili wake ulinuka vibaya. Aliumizwa mno. (Ayubu 7:5; 19:17; 30:17, 30) Akiwa na maumivu makali Ayubu aliketi kati ya majivu naye akajikuna kwa kigae. (Ayubu 2:8) Mwono wa kusikitisha kwelikweli!
4. Kila familia hupatwa na nini mara kwa mara?
4 Wewe ungeitikiaje ikiwa ungekumbwa na ugonjwa mbaya sana hivyo? Leo, Shetani hawapigi watumishi wa Mungu na ugonjwa kama alivyompiga Ayubu. Hata hivyo, kwa sababu ya kutokamilika kwa binadamu, mikazo ya maisha ya kila siku, na mazingira yenye kuzorota tunamoishi, ni jambo la kutazamiwa tu kwamba mara kwa mara, washiriki wa familia watakuwa wagonjwa. Zijapokuwa hatua za kuzuia ambazo huenda tukachukua, sisi sote huweza kupatwa na magonjwa, ingawa wachache watateseka kadiri Ayubu alivyoteseka. Magonjwa yanapovamia nyumba yetu, hilo kwa kweli laweza kuwa jambo gumu. Kwa hiyo acheni tuone jinsi Biblia hutusaidia tukabiliane na adui huyu wa wanadamu aliyepo daima.—Mhubiri 9:11; 2 Timotheo 3:16.
WEWE WAHISIJE JUU YALO?
5. Washiriki wa familia huitikiaje kwa kawaida katika visa vya ugonjwa wa muda tu?
5 Mvurugo wa utaratibu wa kawaida wa maisha, hata usababishwe na nini, huwa jambo gumu sikuzote, na hilo ni kweli hasa ikiwa huo mvurugo unasababishwa na ugonjwa wa kudumu muda mrefu. Hata ugonjwa wa muda mfupi huhitaji marekebisho, radhi, na kujidhabihu. Washiriki wa familia wenye afya huenda wakalazimika kunyamaza ili kumruhusu mgonjwa apumzike. Huenda wakalazimika waache utendaji fulani-fulani. Hata hivyo, katika familia zilizo nyingi hata watoto wachanga huhurumia ndugu au dada yao au mzazi wao aliye mgonjwa, ingawa huenda mara kwa mara wakalazimika kukumbushwa kuwa wenye ufikirio. (Wakolosai 3:12) Kwa habari ya ugonjwa wa muda tu, kwa kawaida familia iko tayari kufanya yanayohitajiwa. Isitoshe, kila mshiriki wa familia angetumaini kuonyeshwa ufikirio uo huo ikiwa yeye angekuwa mgonjwa.—Mathayo 7:12.
6. Ni maitikio gani huonwa nyakati nyingine mshiriki wa familia akipigwa na ugonjwa mbaya sana, wenye kudumu?
6 Lakini, namna gani ikiwa huo ugonjwa ni mbaya sana na mivurugo ni mikubwa na yenye kudumu muda mrefu? Kwa kielelezo, namna gani ikiwa mtu fulani katika familia analemazwa na mshtuko wa akili, anafanywa asijiweze na ugonjwa wa kupungua akili, au anadhoofishwa na ugonjwa mwingine? Au namna gani ikiwa mshiriki wa familia anasumbuliwa na ugonjwa wa akilini, kama vile schizophrenia? Itikio la kwanza lililo la kawaida ni kuwa na sikitiko—huzuni kwamba mpendwa anateseka sana. Hata hivyo, huenda sikitiko likafuatwa na maitikio mengine. Washiriki wa familia wanapojipata wenyewe wameathiriwa sana na uhuru wao kuzuiwa na ugonjwa wa mtu mmoja, huenda wakahisi uchungu. Huenda wakajiuliza: “Kwa nini mimi nipatwe na hili?”
7. Mke wa Ayubu aliitikiaje ugonjwa wa mume wake, na yaonekana alisahau nini?
7 Laonekana wazo kama hilo liliingia akilini mwa mke wa Ayubu. Kumbuka, yeye alikuwa tayari amepotewa na watoto wake. Misiba hiyo ilipotendeka, bila shaka alizidi kuhisi kufadhaika. Hatimaye, alipoona mume wake aliyekuwa mwenye kutenda na mwenye sulubu wakati mmoja akiteseka na maradhi yenye maumivu, ya kuchukiza mno, yaonekana alisahau jambo la muhimu zaidi kuliko misiba yote hiyo—uhusiano ambao yeye na mume wake walikuwa nao pamoja na Mungu. Biblia husema: “Ndipo mkewe [Ayubu] akamwambia, Je! wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? umkufuru Mungu, ukafe.”—Ayubu 2:9.
Wakristo huonyesha kina cha upendo wao wenzi wao wanapokuwa wagonjwa
8. Mshiriki wa familia akiwa mgonjwa sana, ni andiko gani litakalosaidia washiriki wengine wa familia wawe na maoni yafaayo?
8 Wengi huhisi kufadhaika, hata hasira, maisha yao yanapobadilishwa sana na ugonjwa wa mtu mwingine. Hata hivyo, Mkristo anayesababu juu ya hiyo hali apaswa ang’amue hatimaye kwamba hilo linampa fursa ya kuonyesha ukweli wa upendo wake. Upendo wa kweli ni “wenye ustahimilivu na wenye fadhili . . . [nao] hautafuti masilahi yao wenyewe . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (1 Wakorintho 13:4-7) Kwa hiyo, badala ya kuruhusu hisia hasi ziongoze, ni muhimu kwamba tufanye kadiri tuwezavyo kabisa kuzidhibiti.—Mithali 3:21.
9. Ni uhakikishio gani mbalimbali uwezao kusaidia familia kiroho na kihisia-moyo wakati mshiriki ni mgonjwa sana?
9 Ni jambo gani liwezalo kufanywa ili kulinda salama hali njema ya kiroho na ya kihisia-moyo ya familia wakati mmoja wa washiriki wayo ni mgonjwa sana? Bila shaka, kila ugonjwa hutaka utunzi na matibabu yao wenyewe hasa, na isingefaa katika kichapo hiki tupendekeze taratibu zozote za kitiba au za utunzaji wa nyumbani. Hata hivyo, kwa maana ya kiroho, Yehova “huwainua wote walioinama chini.” (Zaburi 145:14) Mfalme Daudi aliandika hivi: “Heri amkumbukaye mnyonge; BWANA atamwokoa siku ya taabu. BWANA atamlinda na kumhifadhi hai, . . . BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani.” (Zaburi 41:1-3) Yehova huwahifadhi hai kiroho watumishi wake, hata wanapojaribiwa kihisia-moyo kupita uwezo wao wenyewe. (2 Wakorintho 4:7) Washiriki wengi wa familia wanaokabili ugonjwa mbaya sana nyumbani mwao wamerudisha mwangwi wa maneno haya ya mtunga-zaburi: “Nimeteswa mno; Ee BWANA, unihuishe sawasawa na neno lako.”—Zaburi 119:107.
ROHO YENYE KUPONYA
10, 11. (a) Ni jambo gani lililo la muhimu ikiwa familia itakabiliana na ugonjwa kwa mafanikio? (b) Mwanamke mmoja alikabilianaje na ugonjwa wa mume wake?
10 “Roho ya mtu itastahimili udhaifu wake [“maradhi yake,” NW],” husema mithali ya Biblia, “bali roho iliyovunjika nani awezaye kuistahimili?” (Mithali 18:14) Mkazo wa akilini waweza kusumbua roho ya familia na pia “roho ya mtu.” Hata hivyo, “moyo ulio mzima [“mtulivu,” NW] ni uhai wa mwili.” (Mithali 14:30) Iwe familia yakabiliana kwa mafanikio na ugonjwa mbaya sana au sivyo yategemea kwa kadiri kubwa mtazamo, au roho, ya washiriki wayo.—Linganisha Mithali 17:22.
11 Mwanamke mmoja Mkristo alilazimika kuvumilia kumwona mume wake akidhoofishwa na mshtuko wa akili miaka sita tu baada ya wao kufunga ndoa. “Usemi wa mume wangu uliathiriwa vibaya, ikawa karibu haiwezekani kuzungumza naye,” yeye akumbuka. “Mkazo wa akilini wa kujaribu kuelewa lile alilokuwa aking’ang’ana kusema ulikuwa mkubwa sana.” Ebu wazia pia, maumivu makali na kufadhaika ambako huyo mume lazima awe aliona. Hao wawili walifanya nini? Hata ingawa waliishi mbali sana na kutaniko la Kikristo, huyo dada alifanya kadiri alivyoweza kabisa kuendelea kuwa imara kiroho kwa kwenda sambamba na habari ya karibuni zaidi ya kitengenezo na pia na ugavi wenye kuendelea wa chakula cha kiroho katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hayo yalimpa nguvu za kiroho za kumtunza mume wake mpendwa hadi kifo chake miaka minne baadaye.
12. Kama ionwavyo katika kisa cha Ayubu, mgonjwa hutoa nini nyakati nyingine?
12 Katika kisa cha Ayubu ni yeye, mwenye kuteseka, aliyeendelea kuwa imara. “Je! tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya?” akamuuliza mke wake. (Ayubu 2:10) Si ajabu kwamba mwanafunzi Yakobo alimtaja Ayubu baadaye kuwa kielelezo chenye kutokeza cha subira na uvumilivu! Kwenye Yakobo 5:11 twasoma hivi: “Nyinyi mmesikia juu ya uvumilivu wa [Ayubu] na mmeona tokeo alilotoa Yehova, kwamba Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema.” Vivyo hivyo leo, katika visa vingi mtazamo wenye moyo mkuu wa mshiriki wa familia aliye mgonjwa umesaidia wengine katika hiyo nyumba wadumishe mtazamo chanya.
13. Ni ulinganisho gani usiopasa kufanywa na familia ambayo imepatwa na ugonjwa mbaya sana?
13 Wengi wa wale ambao ni lazima washughulikie ugonjwa katika familia hukubali kwamba mwanzoni ni jambo la kawaida kwa washiriki wa familia kuwa na wakati mgumu wa kukabili uhalisi wa mambo. Wao huonyesha pia kwamba njia ambayo mtu anakuja kuona hiyo hali ni jambo la maana sana. Mabadiliko na marekebisho katika utaratibu wa nyumba huenda yakawa magumu mwanzoni. Lakini mtu akijitahidi kikweli, yeye aweza kujipatanisha na hali mpya. Katika kufanya hivyo, ni jambo la maana kwamba tusilinganishe hali zetu na zile za wengine wasio na ugonjwa katika familia, tukifikiri kwamba maisha zao ni rahisi zaidi na kwamba ‘hilo si jambo la haki hata kidogo!’ Kwa kweli, hakuna yeyote ajuaye kikweli ni mizigo gani ya kulemea ambayo wengine hulazimika kuhimili. Wakristo wote hupata faraja katika maneno haya ya Yesu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.
KUWEKA MAMBO YA KUTANGULIZWA
14. Mambo ya kutangulizwa yaweza kuwekwaje?
14 Katika kukabili ugonjwa mbaya sana, familia ingefanya vema kukumbuka maneno haya yaliyopuliziwa: “Kwa wingi wa washauri [makusudi] huthibitika [“kuna matimizo,” NW].” (Mithali 15:22) Je, washiriki wa familia wangeweza kukusanyika na kuzungumzia hali inayosababishwa na huo ugonjwa? Kwa hakika ingefaa kufanya hivyo kwa njia ya sala na kuendea Neno la Mungu ili kupata mwongozo. (Zaburi 25:4) Ni mambo gani yafikiriwe katika mazungumzo hayo? Kuna maamuzi ya kufanywa ya kitiba, kifedha, na kifamilia. Ni nani atakayetoa utunzaji wa msingi? Familia yaweza kushirikianaje ili kutegemeza utunzaji huo? Mipango inayofanywa itaathirije kila mshiriki wa familia? Mahitaji ya kiroho na mengine ya yule mtunzaji wa msingi yatatimizwaje?
15. Yehova huandaa utegemezo gani kwa familia ambazo zimepatwa na ugonjwa mbaya sana?
15 Kusali kwa bidii ili kuomba mwelekezo wa Yehova, kutafakari juu ya Neno lake, na kufuata kwa moyo mkuu njia inayoonyeshwa na Biblia mara nyingi hutokeza baraka zinazopita matazamio yetu. Maradhi ya mshiriki wa familia anayeugua huenda yasiingie hali ya kupungua sikuzote. Lakini kumtegemea Yehova huongoza sikuzote kwenye matokeo yaliyo bora zaidi katika hali yoyote ile. (Zaburi 55:22) Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Rehema yako, Ee BWANA ilinitegemeza. Katika wingi wa mawazo yangu ndani yangu faraja zako zinafurahisha nafsi yangu.”—Zaburi 94:18, 19, Zaire Swahili Bible; ona pia Zaburi 63:6-8.
KUWASAIDIA WATOTO
Familia inapofanya kazi pamoja, matatizo yaweza kushughulikiwa
16, 17. Ni mambo gani yawezayo kukaziwa wakati wa kuzungumza na watoto wachanga juu ya ugonjwa wa ndugu au dada yake?
16 Ugonjwa mbaya sana waweza kusababisha matatizo kwa watoto katika familia. Ni jambo la maana kwamba wazazi wawasaidie watoto waelewe mahitaji ambayo yametokea na lile ambalo huenda wakafanya ili kusaidia. Ikiwa yule ambaye amekuwa mgonjwa ni mtoto, ni lazima ndugu na dada zake wasaidiwe kuelewa kwamba uangalifu na utunzaji wa ziada ambao yule mgonjwa anapokea haumaanishi kwamba wale watoto wengine wanapendwa kidogo. Badala ya kuruhusu uchungu au ushindani usitawi, wazazi waweza kuwasaidia wale watoto wengine wafanyize uhusiano wa karibu zaidi na mmoja na mwenzake na wawe na shauku ya kweli wanaposhirikiana katika kushughulikia hali inayosababishwa na huo ugonjwa.
17 Kwa kawaida watoto wachanga wataitikia kwa utayari zaidi ikiwa wazazi wanavutia hisia zao badala ya kuwatolea maelezo marefu au yenye kutatanisha kuhusu hali za kitiba. Kwa hiyo wangeweza kutolewa wazo fulani kuhusu lile linalompata mshiriki wa familia aliye mgonjwa. Watoto walio na afya wakiona jinsi ugonjwa unavyomzuia yule aliye mgonjwa asiweze kufanya mambo mengi ambayo wao wenyewe huyachukua hivi hivi, wataelekea kuwa na “shauku [zaidi] ya kidugu” na kuwa na “huruma kwa njia ya wororo.”—1 Petro 3:8.
18. Watoto wenye umri mkubwa zaidi waweza kusaidiwaje waelewe matatizo yanayosababishwa na ugonjwa, na hilo huenda likawanufaishaje?
18 Watoto wenye umri mkubwa zaidi wapaswa wasaidiwe kung’amua kwamba kuna hali ngumu na hiyo yataka kujidhabihu kwa upande wa kila mtu katika familia. Kukiwa na malipo ya madaktari na ya kitiba, huenda isiwezekane kwa wazazi kuwaandalia wale watoto wengine kama vile wangependa kufanya. Je, watoto wataona uchungu na kuhisi kwamba wananyimwa kitu? Au wataelewa hali na kuwa tayari kujidhabihu inavyohitajiwa? Mengi hutegemea njia ambayo jambo hilo linazungumziwa na roho inayochochewa katika familia. Kwa kweli, katika familia nyingi ugonjwa wa mshiriki wa familia umesaidia katika kuwazoeza watoto wafuate shauri hili la Paulo: “[Msifanye] jambo lolote kwa ugomvi au kwa majisifu ya bure, bali kwa hali ya akili ya kujishusha chini mkifikiria kwamba wengine ni wakubwa kuliko nyinyi, mkifuliza kuangalia, si masilahi ya kibinafsi ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi yale ya wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.
JINSI YA KUONA MATIBABU
19, 20. (a) Vichwa vya familia huwa na madaraka gani wakati mshiriki wa familia ni mgonjwa? (b) Ingawa Biblia si kitabu cha mafundisho ya kitiba, inaandaa katika njia gani mwongozo katika kushughulikia ugonjwa?
19 Wakristo wenye usawaziko hawakatai utibabu wa kitiba maadamu hauwi kinyume cha sheria ya Mungu. Mshiriki wa familia yao anapokuwa mgonjwa, wana hamu ya kutafuta msaada ili kuondoa kuteseka kwa huyo mwenye kuugua. Hata hivyo, huenda kukawa na maoni ya kitiba yenye kupingana ambayo ni lazima yapimwe. Kwa kuongezea, katika miaka ya juzijuzi magonjwa na maradhi mapya yamekuwa yakitokea, na kwa mengi yayo, hakuna njia ya kutibu inayokubaliwa na wote kwa ujumla. Hata nyakati nyingine ni vigumu kupata uchunguzi sahihi wa ugonjwa. Kwa hiyo, Mkristo afanye nini?
20 Ingawa mwandishi mmoja wa Biblia alikuwa tabibu na mtume Paulo alimtolea rafiki yake Timotheo shauri la kitiba lenye kusaidia, Maandiko ni mwongozo wa kiadili na wa kiroho, si kitabu cha mafundisho ya kitiba. (Wakolosai 4:14; 1 Timotheo 5:23) Kwa sababu hiyo, katika mambo ya utibabu wa kitiba, vichwa vya familia Vikristo vyapaswa kufanya maamuzi yavyo vyenyewe yenye usawaziko. Huenda vikahisi kwamba vyahitaji kupata maoni ya kitiba zaidi ya moja. (Linganisha Mithali 18:17.) Kwa hakika vitataka msaada bora zaidi unaopatikana kwa ajili ya mshiriki wavyo wa familia aliye mgonjwa, na wengi hutafuta huo miongoni mwa madaktari wa kawaida wa kitiba. Watu fulani huhisi starehe zaidi wakitumia njia za kutibu za badala. Huo pia ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, wanaposhughulikia matatizo ya kiafya, Wakristo hawakomi kuruhusu ‘neno la Mungu liwe taa ya miguu yao, na mwanga wa njia yao.’ (Zaburi 119:105) Wao huendelea kufuata miongozo iliyowekwa katika Biblia. (Isaya 55:8, 9) Kwa njia hiyo huepuka njia za kuchunguzia ugonjwa zinazohusisha uwasiliani-roho, na wanaepuka matibabu yanayokiuka kanuni za Biblia.—Zaburi 36:9; Matendo 15:28, 29; Ufunuo 21:8.
21, 22. Mwanamke mmoja Mwasia alisababuje juu ya kanuni ya Biblia, na uamuzi aliofanya ulithibitikaje kuwa sawa katika hali yake?
21 Fikiria kisa cha mwanamke kijana Mwasia. Muda mfupi tu baada ya yeye kuanza kujifunza kuhusu Biblia likiwa tokeo la kujifunza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alijifungua kitoto kisichana kabla ya wakati, kilichokuwa na uzani wa gramu 1,470 pekee. Mwanamke huyo alivunjika moyo daktari alipomwambia kwamba ukuzi wa hicho kitoto ungekawizwa vibaya sana na kisingeweza kutembea kamwe. Daktari alimshauri mama huyo akipeleke kitoto kwenye mahali watunzwako watoto. Mume wake hakuwa na uhakika kuhusu jambo hilo. Yeye angemwendea nani?
22 Yeye asema: “Nakumbuka nikijifunza kutoka Biblia kwamba ‘wana ndio urithi kutoka kwa Yehova; tunda la tumbo ni thawabu.’” (Zaburi 127:3, NW) Akaamua kuupeleka “urithi” huu nyumbani na kumtunza. Mambo yalikuwa magumu mwanzoni, lakini kwa msaada wa marafiki Wakristo katika kutaniko la kwao la Mashahidi wa Yehova, mwanamke huyo aliweza kumtunza na kumwandalia mtoto huyo na utegemezo wa pekee uliohitajiwa. Miaka 12 baadaye, mtoto huyo alikuwa akienda mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme na kufurahia ushirika wa vijana huko. Mama huyo aeleza: “Nashukuru sana kwamba kanuni za Biblia zilinisukuma nifanye lililo sawa. Biblia ilinisaidia nidumishe dhamiri iliyo wazi mbele ya Yehova Mungu na kutokuwa na majuto ambayo ningekaa nayo kwa baki la maisha yangu.”
23. Biblia hutolea faraja gani walio wagonjwa na wale wanaowatunza?
23 Ugonjwa hautakuwa nasi milele. Nabii Isaya alielekeza mbele kwenye wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Ahadi hiyo itatimizwa katika ulimwengu mpya unaokaribia upesi. Hata hivyo, hadi wakati huo, ni lazima tushindane na ugonjwa na kifo. Kwa furaha, Neno la Mungu hutupa sisi mwongozo na msaada. Kanuni za msingi za mwenendo ambazo Biblia huandaa ni zenye kudumu, na ni bora zaidi kuliko maoni ya wanadamu wasiokamilika yanayobadilika daima. Kwa sababu hiyo, mtu mwenye hekima hukubaliana na mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima. . . . Hukumu za BWANA ni kweli, zina haki kabisa. . . . Katika kuzishika kuna thawabu nyingi.”—Zaburi 19:7, 9, 11.