Ni Nini Kinachomaanishwa na Kuzeeka?
“KUZEEKA SI KUBAYA SANA UKIFIKIRIA KIFO.”—Maurice Chevalier.
UTARATIBU wa kuzeeka hatimaye huathiri kila mtu. Hauwezi kuepukika. Huanza polepole sana—kuumwa kidogo hapa, kunyanzi dogo hapa na pale, na nywele chache zilizo na mvi—lakini hatimaye humeza mtu katika mshiko wao usioachilia. Hakuna wakati wowote katika historia ambapo watu wengi mno walihisi athari za umri wa uzee kama wakati huu.
Sababu kuu ya ongezeko la idadi ya waliozeeka ni mafanikio ya sayansi ya kitiba katika kudhibiti maradhi yenye kuleta kifo. Kwa kielelezo, katika Marekani, wale walio na zaidi ya miaka 65 huwakilisha asilimia 12 hivi ya idadi ya watu, na katika Japani yapata asilimia 11 hivi. Wamarekani walio na umri wa zaidi ya miaka 85 waliongezeka kutoka 700,000 katika 1953 hadi milioni 2.1 katika 1978. Kwa kweli, Wamarekani 50,000 hivi na Wakanada wapatao 3,700 wana umri wa miaka 100 au wazee zaidi!
Ingawa waliozeeka wanaishi maisha yenye kutokeza zaidi kuliko walivyofanya wakati uliopita, miaka ya mtu ya baadaye inafifishwa na kupungua kwa uwezo fulani-fulani. Kusikia, kuona, hali ya misuli, na wepesi wa kwenda, vyote huathiriwa mtu azidipo kuzeeka. Baadhi ya waliozeeka hupatwa na upweke na hata ukongwe. Wengine huhisi wanapoteza uvutio wao na wanashuka moyo.
Mara nyingi ni namna ambayo mtu anajipatanisha na utaratibu wa kuzeeka inayoamua furaha ya mtu au ukosefu wayo. Mtu asemapo: “Nimezeeka sana kuweza kufanya hilo,” nyakati fulani huwa ni mtazamo, zaidi ya chochote cha kimwili, ambao huzuia utendaji uwezekanao.
Kijana mmoja alionyesha ufahamu wenye kina wa kadiri fulani aliposema hivi: “Kwa maoni yangu, yaonekana mzee ni yeyote ambaye ameacha kuishi maisha kwa utimilifu zaidi, yeyote ambaye hapendi maisha na hapati furaha katika maisha tena. Kwa kweli haiwezekani kuamua kihususa umri ambao mtu huchukuliwa kuwa ‘mzee’ kwa kuwa kuna matineja wanaoonekana kuwa wazee, na bado kuna waliostaafu wanaoonekana kuwa wachanga.”
Waliozeeka Lakini Wenye Furaha na Uradhi
Kwa wengine miaka ya baadaye huthibitika katika njia fulani-fulani, kuwa miaka ifaayo na yenye kuthawabisha. Waliozeeka hawa wenye furaha hufurahia uhuru kutokana na misongo na masharti ya kuajiriwa kwa kawaida. Kwao umri wa uzeeni humaanisha wakati zaidi wa kufurahia wajukuu wao. Wanatambua kwamba furaha yao haitegemei kile wengine hufikiria kuwahusu. Wanaweza kujihisi huru zaidi kueleza wanachofikiria, na wanaweza kustarehe zaidi na kuridhika.
Zaidi ya hilo, wao wanaweza kushughulikia mambo kando ya mahitaji yao na kupata shangwe katika kujitolea kusaidia wale wanaohitaji msaada. Wanasaidia vipofu kwa kuwasomea vichapo, hukaribisha mayatima kuandamana nao kwenye viziara, au kusaidia wale wasiojiweza wahisi vyema kujihusu. Wengine hujifunza stadi mpya na kufanya mambo ambayo hawakuweza walipokuwa wakilea familia au walipokuwa wakifanya kazi ili kujiruzuku. Mchoraji mashuhuri Mmarekani Grandma Moses alianza kazi-maisha yake ya uchoraji katika miaka yake ya mwisho-mwisho ya 70 na kumaliza picha 25 baada ya umri wa miaka 100!
Bila shaka, mtu hapaswi kufanya mambo yasiyo ya kawaida ili apate shangwe. Katika umri wa miaka 86, mcheza-sinema wa jukwaani wa kike ajulikanaye sana ulimwenguni alitoa maelezo hivi: “Nafurahia maisha yangu sasa zaidi ya wakati mwingineo wote! Kuchelewa mno? Wajiuliza. Faida ya kuwa katika hatua hii maishani mwangu ni kwamba siangalii nyuma wala mbele—zaidi ya siku kadhaa kwa wakati mmoja. Nafurahia tu wakati wa sasa.” Yeye aliongeza hivi: “Ili kuridhika kujihusu, kuhusu maisha yako, si lazima uwe mashuhuri au uwe milionea.”
Faida nyingine ya kuzeeka ni hekima na uzoefu ambazo kwa kawaida hupatikana njiani mwa uzee. Je, wewe wathamini rasilimali hizi? Mwanamke mmoja anayezithamini alisema hivi: “Nathamini hekima ambayo nimepata kwa miaka mingi. Kujifunza kilicho cha maana kwelikweli kumenisaidia kukabili kwa mafanikio matatizo ya maisha. Kwa hakika, wanawake wengi wachanga zaidi huja kuniuliza mashauri. Wao kwa kawaida husema hivi baadaye: ‘Ninafurahi sana kwamba niliongea nawe. Sikuwa nimelifikiria kwa njia hiyo mbeleni.’ Singetaka kubadilishana uzoefu huo na chochote. Ninashukuru sana naweza kuwa mwenye kusaidia, hasa kwa walio wachanga.”
Maoni Kuhusu Waliozeeka
Wakati mmoja waliozeeka walistahiwa sana, na shauri lao lilifuatwa. Katika mabara mengi hili limebadilika. Sasa waliozeeka mara nyingi hupuuzwa na kutendewa vibaya. Hili lasikitisha, kwa kuwa waliozeeka wanawakilisha rasilimali ya hekima na uzoefu ambazo watu wachanga wanaweza kutwaa kwa faida yao. Bila shaka, hili haliwapi wazee haki ya kujiingiliza katika maisha ya wengine.
Kwa kufurahisha, katika tamaduni fulani waliozeeka hupewa staha wanayostahili. Kwa kielelezo, katika Japani na nchi nyingi za Afrika, wao mara nyingi hubaki wakiwa kiini cha familia na jamii ya kikabila. Katika Jamhuri ya Abkhaz, Georgia, katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, ambako watu kwa kawaida huishi zaidi ya miaka 100, watu wenye umri wa miaka 100 hustahiwa na vizazi vichanga. Maoni yaliyotolewa na waliozeeka mara nyingi huonwa kuwa sheria miongoni mwa familia.
Vijana watwaapo rasilimali hii ya hekima, muungo wa familia hunufaika. Kwaweza kuwa na uhusiano wa kipekee kati ya wazazi-wakuu na wajukuu. Ni kupitia ujamaa huu wa hayo marika mawili kwamba watoto mara nyingi hujifunza subira, huruma, hisia-mwenzi, na staha kwa wazee wao. Wanapopoteza ukaribiano huu, wachanga wanaweza kuathiriwa vibaya.
Wao Hutaka Kutendewaje?
Waliozeeka hutaka kustahiwa. Wao huhitaji kufanya maamuzi na kujihisi kwamba wana udhibiti juu ya maisha yao. Ingawa uwezo wao wa kimwili hupungua kadiri miaka isongavyo, wale wawekao akili zao zikiwa zenye kutenda mara nyingi hubaki waelekevu kiakili. Ni kweli, huenda wasifikiri kwa wepesi kama walivyofanya walipokuwa wachanga au kujifunza mambo mapya kwa uharaka. Lakini hawapaswi kuchukuliwa kama wasiofaa kitu na kunyang’anywa fungu lao katika familia, wala wengine hawapaswi kuchukua kazi ndogo-ndogo ambazo waliozeeka wangependelea kuzifanya wenyewe. Kufanya hivi kungewafadhaisha na kuwavunja moyo na kuwafanya wajihisi kuwa wamepungukiwa na hata wajihisi kuwa bure.
Utendaji wenye kutokeza kwa waliozeeka ni muhimu sana; husaidia kuwapa hisi ya ustahiki. Kwa kufaa, wenye umri wa miaka 100 katika Jamhuri ya Abkhaz, Georgia, mara nyingi huwa na kazi ndogo-ndogo nyingi za kila siku za kushughulikia, kama vile kufanya kazi mashambani, kulisha kuku, kufua nguo, kusafisha nyumba, na kutunza watoto wadogo—yote ambayo bila shaka huchangia kuwa kwao na maisha marefu. Kwa kweli, waliozeeka wanapokuwa na kazi yenye umaana ya kufanya, wao huendelea kuishi. Kwa nini? Kwa sababu wana kusudi katika maisha.
Hata wakati waliozeeka wanapodhoofishwa nguvu na mshtuko wa ubongo au ugonjwa mwingineo, bado wao hutaka kutendewa kwa heshima. Hawathamini kupigiwa kelele au kugombezwa kama mtoto. Ikiwa hawawezi kuzungumza, kwa kawaida wanaweza kusikia, na hisia zao kwa kueleweka huwa nyepesi. Nyakati fulani, kwa sababu ya kutumia dawa zenye nguvu mno, huenda wakaonekana kuwa wakongwe hali kwa uhalisi sivyo walivyo. Kwa hiyo hisia-mwenzi zaidi ya hisia-moyo nyingineyo yote yaweza kuwa ufunguo kwa kuwatunza ifaavyo.
Kwa kuwa waliozeeka huenda wakawa hawawezi kutoka nyumbani mwao, wanahitaji kuhisi kwamba hawajasahauliwa. Wao huthamini wageni. Inasikitisha kama nini wakati mshiriki wa kutaniko la Kikristo akosapo kuwatembelea au kuwapigia simu washiriki wazee-wazee waliodhoofishwa na ugonjwa ambao katika wakati uliopita huenda walichangia kwa njia yenye kutokeza sana kupanuka kwa kazi ya Ufalme! Kwelikweli, ziara kama hizo au kupigiwa simu huchukua wakati mfupi na jitihada kidogo kwa kulinganishwa na manufaa nyingi mno watakazopata hao wazee-wazee!
Hata hivyo, haidhuru jinsi wengine wanavyowatendea, mengi hutegemea jinsi waliozeeka wanavyojiona. Kama mwanamke fulani mwenye umri wa miaka 75 alivyosema waziwazi: “Kwa kawaida kile kinifanyacho niendelee licha ya kizuizi ni kuwa na jambo la kufanya sikuzote. Singeweza kutimiza chochote ikiwa singekuwa na mipango na miradi. Bila shaka nina matatizo ya kimwili. Lakini ndivyo ilivyo na watu wengi wenye umri kama wangu.”
Waliozeeka wanapaswa kuepuka kuwa walalamikaji wa sikuzote na kutokuwa wenye kushirikiana. Hili huenda lisiwe rahisi wakati mtu anateseka. “Hata ingawa nina matatizo ya kimwili,” akasema mwanamume mmoja mzee-mzee “magonjwa yangu hayajapunguza shangwe yangu katika kuishi. Nafikiri mtazamo ndio jambo la maana kupita yote. Kupata kuishi miaka yote hii kumekuwa kwenye kutajirisha kwangu. Nami nahisi ufunguo wa kubaki mchanga ni kushirikiana na vijana. Wao hunufaika kutokana na hekima yangu, nami hutwaa nishati yao. Waona, kwelikweli mimi ni mchanga moyoni.”
Ni Nini Kiwezacho Kufanywa?
Ikiwa wewe ni mchanga, je, wahitaji kuboresha maoni yako kuhusu umri wa uzee na jinsi yako ya kutendea wazee-wazee? Ikiwa wewe ni aliyezeeka, kwa nini usijiulize maswali yaliyoorodheshwa katika kisanduku kinachoambatana na makala hii? Je, kuna mambo unayoweza kufanya ili kuboresha hali yako?
Ikiwa wajibu maswali yote kwa njia chanya, hutakosa marafiki wazee au wachanga. Wengine watataka kuwa karibu nawe kiasili. Jambo jema zaidi, utakuwa na furaha hata ukiwa peke yako na kupata kwamba maisha, katika umri wowote ule, yaweza kuwa yenye kupendeza na yaliyojaa maana.
[Sanduku katika ukurasa wa 16]
Kujichunguza kwa Waliozeeka
◻ Je, mimi hutazama wakati ujao nikiwa na matumaini?
◻ Je, bado mimi ni mdadisi na nina hamu ya kujifunza mambo mapya?
◻ Je, mimi hujaribu kubaki nikiwa mtendaji kadiri iwezekanavyo?
◻ Je, mimi huhangaikia siku kama ijavyo na kufanya marekebisho yafaayo?
◻ Je, mimi huwa mwenye shauku na mwenye kutia moyo ninapokuwa miongoni mwa wengine?
◻ Je, mimi hujaribu kudumisha ucheshi wangu?
◻ Kwa kusema kisahili—je, ninazeeka kwa madaha?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Je, wewe huwatembelea wazee-wazee?