Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 8/8 kur. 18-21
  • Kuzeeka Ukiwa na Ufahamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzeeka Ukiwa na Ufahamu
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matatizo ya Kisasa ya Uzee
  • Mitazamo Kuelekea Kuzeeka
  • Umri wa Uzee ni Wakati wa Pekee
  • Fungu la Kuthamini
  • Kukabili Wakati Ujao Ukiwa na Ufahamu
  • Wakristo wa Kweli Wanaheshimu Watu Wenye Umri Mkubwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Yehova Anawatunza kwa Upendo Watumishi Wake Waliozeeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Kuzeeka Mkiwa Pamoja
    Siri ya Furaha ya Familia
  • Utukufu wa Kichwa Chenye Mvi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 8/8 kur. 18-21

Kuzeeka Ukiwa na Ufahamu

MASIMULIZI ya kweli ya maisha ya mtu mmoja aliyezeeka kutoka Mashariki ya Kati aliyekuwa amepata matatizo mengi na mikasa mingi yamalizia kwa ukakikishio kwamba alikufa “akiwa mzee na kuridhika na siku.” Aliishi akawa na umri wa miaka zaidi ya 140.—Ayubu 42:16, 17, NW.

Mtu mwingine kutoka Mashariki ya Kati pia, aliishi kufikia umri wa uzee wa miaka 175. Masimulizi yasema kwamba “akafariki, naye akafa katika uzee mwema, mzee sana ameshiba siku [na kuridhika, NW].” Naam, inawezekana kwa watu waishi maisha yanayoridhisha hata kufikia maisha yao ya uzee.—Mwanzo 25:7, 8.

Katika umri ambao tungeona kuwa wa uzee sana, mmoja wa watu hao alijitolea kuacha makao yake yenye starehe ya mjini, na akiwa na familia yake yote, akahamia nchi nyingine. Mkondo wa kwanza wa safari hiyo ulikuwa wa umbali wa kilometa 970, na bila msaada wa usafiri wa kisasa. Yule mwingine alikuwa na matatizo mabaya sana ya afya. Wote hao wawili walilea familia katika miaka yao ya baadaye.

Mmoja wa watu hao aliona sehemu ya bara alilokalia likishambuliwa na majeshi ya muungano ya wafalme wanne. Ilimbidi akusanye kikosi cha wanaume wapatao 300 ili wafuate majeshi yale na kuokoa mtu mpendwa wa ukoo. Baadaye aliona majiji mawili yenye utajiri yakiharibiwa na tendo la Mungu. Mara mbili, mtu uyo huyo alinyang’anywa kwa muda mke wake mrembo na wafalme wenye nguvu.

Hawa wote wazee-wazee—Ayubu na Abrahamu—walipitia matukio yenye matatizo kwa mafanikio na bado wakaishi wakawa ‘wazee na kuridhika.’ Ni nini iliyokuwa siri yao?

Matatizo ya Kisasa ya Uzee

Je! matatizo yanayokabili wazee-wazee leo yako tofauti sana na yale yaliyokabili wazee-wazee wa kale? Je! si kweli kwamba watu wengine wenye umri wa uzee hupoteza mali au hata kupoteza njia ya kujipatia riziki?

Watu fulani hupoteza makao yao na kulazimika kuhamia sehemu wasizojua. Watu wa ukoo wa karibu, marafiki, na wenzi wa ndoa hufa. Matatizo ya afya ni jambo kubwa la kukabili. Kwa kusikitisha, watoto wengine huwaacha wazazi wao, wakiacha kuwategemeza na kuwaacha wajitegemeze.

Hatuhitaji kutaja matatizo hayo kwa sababu tunayajua sana. Lakini kwa hekima tunaweza kutafuta masuluhisho.

Mitazamo Kuelekea Kuzeeka

Huenda mtazamo wa mtu ukahitaji kurekebishwa; huenda ukawa ndio chanzo cha ukosefu wake wa furaha. Kwa mfano, wazee-wazee wengine husisitiza kuishi peke yao hata wasipokuwa na uwezo wa kujitunza wenyewe. Mwanamke mmoja aliyekuwa hajiwezi na ambaye alikuwa akiishi peke yake katika kao kubwa aliangika ishara mlangoni pake iliyosema hivi: “Usiingie!” Alihisi kwamba kila mtu alitaka tu fedha zake au mali yake; hakutumaini mtu yeyote.

Mtu kama huyo anakuwa mzee bila kuwa na ufahamu. Ni hali yenye kusikitisha kama nini! Ni kweli kwamba si kila mtu anaweza kutumainiwa. Lakini ni jambo la hekima kama nini kufahamu kwamba watu fulani wanaweza kutumainiwa kisha upokee urafiki na msaada wa wale wanaojaribu kwa kweli kusaidia!

Huenda baadhi ya wazee-wazee wakahisi kwamba wametimiza maisha yao. Lakini bado wanaishi, nao wataona likiwa jambo lenye kunufaisha kutendesha akili zao na kutumia uwezo wao wa kufikiri kikamili. Wanaweza kujifunza mambo mapya na kunaweza kuwatajirisha ingawa kujifunza kunaweza kuchukua muda mrefu zaidi kuliko walipokuwa vijana.

Umri wa Uzee ni Wakati wa Pekee

Maagizo ya shule ya ustadi wa tiba ya matatizo ya uzee yasema kwamba wazee-wazee wanahitaji kuhisi kwamba wana uhuru wa akili na mwili. Ni lazima pia wahisi kwamba wanapendwa na kuhitajiwa, kwamba wanaweza kutumiwa na kujifanyia mambo yao wenyewe. Na zaidi, maagizo hayo yanasema kwamba wazee-wazee wanahitaji kujiona kuwa sehemu ya jamii inayoweza kupatikana katika familia na marafiki na kwamba wanaweza kunufaika na ushirika wa kidini.

Basi, ni mtazamo gani bora zaidi unaofaa kuonyeshwa na watu wanaozeeka? Maoni yanayofaa yanaweza kusaidia sana. Mwanamke mmoja aliyeona umri wa uzee kuwa sehemu mpya ya maisha alikuwa ni mama mwenye umri wa miaka 90 wa aliyekuwa rais wa U.S. Katika kumbukumbu lake aliandika hivi: “Umri wa uzee haupaswi kuogopwa . . . Unaweza kutajirisha na kuthawabisha . . . Hali ya maisha yetu ya baadaye itaamuliwa na maisha ambayo tayari tumeishi.” Mwelekeo kama huo huongezea thamani zaidi maisha ya miaka ya baadaye.

Kwa hiyo, yale maagizo yaliyotajwa hapo awali juu ya tiba ya matatizo ya uzee yalionelea kwamba wazee-wazee wenye furaha ni wale ambao wameweza kujifundisha kwa kuanza kufuatia mapendezi mapya yanayoridhisha, wakijifunza na kusitawisha mapendezi magumu, wakifurahia maono yanayofaa na urafiki unaofaa, wakijifunza kuthamini uhai na kuishi kulingana na uwezo wao wa kimwili.

Vipi juu ya kuvumilia matatizo yasiyoepukika ya maisha? Kitabu On Growing Old chasema hivi: “Inaweza kusemwa kwa hakika kwamba mtu akiweza kuwa na kanuni bora na hasa nguvu inayotegemea imani ataweza kuvumilia . . . Zaidi ya wengine wote wazee-wazee wanapaswa kujaribu kuimarisha uhusiano wao wa kidini.”

Watu wengine hutanguliza kutumia maisha kikamili mbele ya kitu kinginecho chote. Mwanamke mmoja mwenye mvi ambaye ana umri wa miaka 61 aliridhisha tamaa yake ya kuendesha pikipiki zenye nguvu kwa kuwa mwanachama wa kilabu cha pikipiki chenye washirika wenye umri zaidi ya 40 pekee. Si kwamba Amkeni! linapendekezea wazee-wazee waendeshe pikipiki!

Mume mmoja na mke wake ambao ni wazee-wazee wana shime hii: “Usisikitikie umri wako—na usiache utendaji unapostaafu.” Kwa kutimiza shime hiyo, waliendesha baiskeli kutoka Los Angeles hadi New York katika 1980. Wakati wa miaka minne baada ya kustaafu kwao katika 1976, mwanamume huyo akiwa na umri wa miaka 69, na mke wake, 64, waliendesha baiskeli kwa zaidi ya kilometa 25,000 kupitia Kanada, United States, Norway, Ubelgiji, Uholanzi, Ujerumani, Ufaransa, na Uingereza. Hapa vilevile hatupendekezi kwamba mtu ajaze maisha yake mambo kama hayo, kwa sababu wakati unaweza kuwa mchache zaidi au hata usiwepo wa kujifunza na kujihusisha na ibada ya kweli ya Mungu. Lakini mfano huo unaonyesha kwamba wazee-wazee wengine wana uwezo mkubwa wa kuishi maisha yenye utendaji.

Utendaji wenye matokeo na kufanya mambo kwa ajili ya wengine unaweza kusaidia mtu azeeke kwa uzuri. Kikundi cha mafundi waliostaafu, wengine wao wakiwa na umri zaidi ya 70, waliendeleza stadi zao kwa kufanya marekebisho ya nyumba kwa bei nafuu kwa wastaafu wengine katika sehemu ya Greater Vancouver, Kanada. Kuhusu matokeo ya kazi hiyo kwa mafundi hao wenyewe, mtu mmoja alisema hivi: “Ni tiba nzuri. Huwafanya wawe watendaji.” Ripoti moja ya gazeti yasema kwamba wao “hawajachoka, wamestaafu tu.” Watu hao wanafikiria pia kwamba ni yule mtu ambaye amechoka sana ndiye hutazama televisheni kwa maisha yake yote yanayobaki.

Fungu la Kuthamini

Kuthamini uhai kunahitajiwa pia. Mtu mmoja aliye chonjo mwenye umri wa miaka 87 kutoka British Columbia, Kanada, alionyesha uthamini mkubwa kwa kuwa hai tu. Shime yake ya kuzeeka akiwa na ufahamu ilikuwa: “Dumisha akili ikiwa yenye utendaji, na ubaki kijana moyoni. Ishi kwa ajili ya kila siku.” Kwa kweli yeye hakujitayarishia uzee mapema lakini alijishughulisha tu nje akitunza miti yake ya matunda. Ili apatane na hali yake iliyobadilika, alidumisha kupendezwa kwake na watu wengine na sikuzote alijitahidi kujua habari zilizo mpya.

Hata ingawa hali ya wazee-wazee katika familia na jamii hubadilika, hakuna haja ya wao kuacha kupendezwa kabisa na maisha au kutumbukia mshuko mkubwa wa kiakili. Ikiwa marafiki na watu wa ukoo wanamtegemeza wakati huo, hilo laweza kusaidia sana, kwa sababu kwa njia hiyo wazee-wazee wanaweza kushiriki maono na furaha yao. Mwanamume mmoja aliye mzee-mzee anayeishi peke yake katika makao yake katika British Columbia alisema hivi: “Wazee-wazee wakipuuzwa na familia zao, kuna mwelekeo wa kufikiria sana nyakati za zamani, na hilo si jambo zuri.” Anathamini sana familia yake kubwa na uaminifu wao katika kuwasiliana naye. “Simu,” anasema, “ni chombo kizuri ajabu kwa wazee-wazee.”

Mwanamume mmoja aliyelazimika kustaafu mapema kwa sababu ya matatizo makubwa ya moyo alitaja juu ya hatari ya kufikiria nyakati zilizopita. Maisha yake yalikuwa yamekuwa yenye utendaji sana, akisimamia biashara yenye mafanikio na vilevile kutumikia akiwa mzee aliyewekwa katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Je! aliishi akisikitikia utendaji aliopoteza? “La,” yeye asema, “Sivyo. Nimeridhika kwamba nilifanya yote niliyoweza. Niliwekea wengine msingi wa kufanyia kazi.”

Uhusiano wa mwanamume huyo na mabinti zake walioolewa na familia zao umekuwa, katika maneno yake, “karibu zaidi” kadiri ambavyo miaka imekuwa ikipita. Yeye na mke wake wanathamini wapendwa wao na wamejifunza kutoingilia maamuzi ya familia ya watoto wao ambao ni watu wazima—hao wayaamue wenyewe. Kukosa kufanya hivyo husababisha tu mzozano na ukosefu wa furaha, pamoja na lile tatizo linalojulikana sana la wakwe.

Kuna shangwe nyingi kama nini zinazokoswa wakati babu na nyanya hawathaminiwi! Lakini kuna furaha kama nini wakati unaposikia mjukuu akisema, kama vile babu huyu alivyosikia baada ya muda mrefu katika hospitali: “Bompa! [Babu!] umekuwa wapi? Tumekukosa sana!”

Kwa sababu ubinafsi na ukosefu wa shauku ya asili zimeenea sana katika ulimwengu wa sasa, si watu wote walio wagonjwa na wanaozeeka wanaopata utegemezo wa kiadili na wa kimwili unaohitajiwa sana ili kukabili matatizo kwa utulivu. Hivi ndivyo msimamizi mmoja wa kituo cha utunzaji wa dharura katika Kanada alivyokadiria hali hiyo: “Wengi wa wazee-wazee hao wanaacha makao mazuri ili waje hapa, ambapo wana kitanda na kabati tu. Wanapotoka, wakiwa wamekufa, kitu kinachobaki ni kisanduku kidogo tu chenye vitu vyao vyote. Ni ono lenye kutamausha sana.” Lakini, katika visa fulani makao haya yanaweza kuwa ndiyo suluhisho la pekee kwa familia zinazotafuta utunzaji kwa wapendwa wao wazee-wazee.

Kukabili Wakati Ujao Ukiwa na Ufahamu

Kulingana na wabashiri wengine, wakati utafika ambapo kutakuwa na dawa ya uzee, kama vile matatizo mengine ya afya yanavyodhibitiwa leo. Lakini, je, mabashiri hayo ya kindoto ya wanadamu wasiokamilika yataandaa tumaini la kweli lenye kudumu kwa mtu ambaye muda wake wa maisha unakaribia “miaka sabini” au “miaka themanini”?—Zaburi 90:10.

Maelfu ya wazee-wazee wamepata tumaini lenye kuendeleza uhai katika Neno la Mungu, Biblia. Sasa wanatumaini zile ahadi ambazo hazitakosa kutimizwa za yule “Mzee wa Siku,” Yehova Mungu. (Danieli 7:9, 13) Moja ya ahadi hizo ni kwamba ngozi ya mtu mzee-mzee “itakuwa laini kuliko ya mtoto,” naye ‘atarudia siku za ujana wake.’ (Ayubu 33:25) Hata wale wanaolala katika usingizi wa kifo wataamka wapate maisha kama hayo katika ulimwengu mpya wenye uadilifu wa Mungu, ambao utachukua mahali pa mfumo wa sasa wa mambo usioridhisha. (Matendo 24:15; 2 Petro 3:13) Ni tumaini hilo zuri lililowezesha Abrahamu na Ayubu waishi siku zao zote mpaka wakawa ‘wazee na kuridhika.’

Kwa kweli, kuishi leo kulingana na kanuni hizo zenye kuridhisha moyo ni kama kufungua akiba ya benki kwa ajili ya wakati ujao. Vilevile, mzee-mzee akiwa na familia inayomtegemeza na marafiki wanaomtegemeza pamoja na utendaji unaofaa, anaweza kufanikiwa. Zaidi ya yote, uhusiano wa karibu pamoja na Yule ambaye ameahidi kuleta kitulizo cha kuzeeka na kifo unakuwezesha uzeeke ukiwa na ufahamu. Kwa kweli, wale ambao wanapendelewa na Mungu “watazaa matunda hadi wakati wa uzee.”—Zaburi 92:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki