Utukufu wa Kichwa Chenye Mvi
LINGEKUWA jambo lenye kusisimua kama nini kusema na wanaume na wanawake waaminifu wa zamani! Ebu wazia kuongea na wanaume kama vile Noa, Abrahamu, Musa, na Yohana Mbatizaji, pamoja na wanawake kama vile Sara, Rahabu, Ruthu, na Debora! Je! usingesisimuka kuwasikia wakisimulia masimulizi waliojionea wenyewe ya matukio yenye kutokeza ya nyakati zilizopita zamani?
Hata leo, je, usingefurahia kusikia wazee-wazee waaminifu wakishiriki maono juu ya jinsi wao na wengine walivyoshika uaminifu-maadili wao kwa Mungu chini ya majaribu, kutia na marufuku, mapigo, na kufungwa gerezani kwa ajili ya uadilifu? Bila shaka ndiyo! Upendo wetu kwa Mungu na staha yetu kwao ingekua wakati ambapo wangetuambia juu ya hisia zao na hasa uthamini wao wa kuhisiwa moyoni kwa ajili ya utunzaji wa Yehova wenye upendo.
Miongoni mwa watu wa Mungu, wazee-wazee waaminifu wanaume na wanawake wamestahiwa sikuzote kwa ajili ya maarifa, ujuzi, na hekima yao. Kwa kweli, amri ifuatayo ilitiwa ndani katika Sheria iliyopewa na Mungu kwa Waisraeli: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako, Mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].” (Mambo ya Walawi 19:32) Neno la Kiebrania kwa umri au umri wa uzee latokana na maana ya msingi “kuza mvi” na linafasiriwa pia “kichwa chenye mvi.” Kwa hiyo Waisraeli walitazamiwa wamwondokee mtu mzee-mzee ikiwa ishara ya staha, wakifanya hivyo katika hofu ya Mungu yenye kicho.
Je! mtazamo huo wenye staha uko leo? Kwa mfano, je, vijana huwafungulia wazee-wazee milango kwa madaha? Je! vijana au watu wazima wachanga kwa kawaida humpa mtu mzee-mzee mahali pao katika lifti iliyojaa watu? Au je, watu wachanga kwa ujumla huwapa wazee-wazee kiti chao kwenye basi au gari-moshi lililosongamana? Ukosefu wa kufanya mambo hayo umeonwa hata miongoni mwa Wakristo.
Hata hivyo, ili kumpendeza Yehova Mungu, ni lazima Wakristo watende kulingana na maoni yake na waepuke njia ya kufikiri, ya kusema na ya kutenda ya wale walio ‘wenye kujipenda wenyewe, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, na wasiopenda mema.’ (2 Timotheo 3:1-5) Kwa hiyo, Neno la Mungu husema nini juu ya ujana kuhusiana na kichwa chenye mvi?
Nguvu za Ujana
Biblia hutambua nguvu za ujana na faida zazo, ikitaarifu hivi: “Fahari ya vijana ni nguvu zao.” (Mithali 20:29) Katika Israeli ya kale nguvu za Walawi wachanga zilitumiwa hekaluni, mara nyingi katika kazi nzito zaidi zilizokuwa nyingi. Leo, kazi nyingi katika viwanda, makao ya Betheli, na miradi ya ujenzi ya Watch Tower Society hufanywa na wanaume na wanawake wachanga ambao wametoa nguvu na uwezo wao mbalimbali ili kuendeleza masilahi ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Hivyo wanafurahia mapendeleo mazuri katika utumishi wa Mungu.
Mithali iliyotoka kunukuliwa yamalizia kwa maneno haya, “na uzuri wa wazee ni kichwa chenye mvi.” Nguvu za ujana zinapounganishwa na ujuzi na hekima ya miaka, muunganisho wenye nguvu sana unafanyizwa.
Kwa kutoa kielezi: Mwanafunzi mchanga wa useremala ambaye ameombwa aweke paneli ajaribu kutimiza mgawo huo kwa nguvu ya ujana. Seremala mwenye umri mkubwa zaidi, mwenye ujuzi zaidi aona kwamba zijapokuwa nguvu zake, msaidizi huyo mchanga hugonga msumari mara kadhaa kabla ya kuuingiza. Mfanyakazi mwenye umri mkubwa zaidi adokeza kwamba kijana huyo ashikilie mwisho wa nyundo, badala ya kuishikilia karibu na kichwa chayo. Hilo lamwezesha kijana huyo aigonge misumari kwa nguvu nyingi zaidi, akiokoa wakati na nishati.
Vivyo hivyo, mwanamke mchanga, mwenye nishati, huenda akajifunza kwa kujaribu-jaribu kwamba nguo nyingine zitaharibika ikiwa hazifuliwi kulingana na maagizo. Lakini, mwanamke mwenye ujuzi ajua thamani ya kuchukua wakati wa kupanga nguo kwa aina-aina na kufua mavazi mengine peke yayo. Amejifunza pia kwamba aweza kuepuka kupiga pasi baadhi ya mavazi kwa kuyakunja anapoyaondoa kutoka kwa kamba ya kuanikia nguo au kutoka kwa mashine ya kukaushia nguo.
Kujifunza kutoka kwa watu wenye ujuzi kwaweza kufanya maisha yawe rahisi zaidi. Hata hivyo, wakati hufika ambapo hata mtu mwenye ujuzi zaidi hawezi kushughulikia kazi fulani ambazo yeye alikuwa akitimiza kwa urahisi miaka michache mapema zaidi. Mwandikaji mmoja alionelea hivi kwa kufaa: “Ingekuwa vema kama nini ikiwa vijana wangekuwa na ujuzi na wazee-wazee kuwa na nguvu.” Lakini ni vema kama nini wakati wazee-wazee wathaminipo nguvu za vijana na kushiriki nao kwa saburi ujuzi uliopatikana kwa muda wa miaka mingi iliyopita—na vijana kukubali madokezo kwa unyenyekevu! Kwa njia hiyo, vikundi vyote viwili vya umri vyanufaishwa.
Kupata Utukufu
Umri tu hautoshi. “Sio wakuu [wale wenye miaka mingi, NW] walio wenye akili, wala sio wazee watambuao hukumu,” akasema kijana Elihu. (Ayubu 32:9; Mhubiri 4:13) Ili mzee-mzee athaminiwe kikweli kwa ajili ya kichwa chenye mvi, angehitaji kuwa amefanya zaidi na maisha yake kuliko kutumia siku zake akitazama televisheni, kuhudhuria michezo, au vinginevyo akijifurahisha. Hata katika siku za baadaye, wazee-wazee wanahitaji kuendelea kujifunza.
Watu wengine hujigamba juu ya kufanya mambo kwa njia yao wenyewe, au wanasema: “Kujionea mwenyewe ndio mwalimu bora zaidi.” Hata hivyo Neno la Mungu hushauri hivi: “Mwenye hekima [atasikia] na kuongezewa elimu, na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia.” (Mithali 1:5; linganisha 1 Wakorintho 10:11.) Kujionea mwenyewe sio mwalimu bora zaidi sikuzote, kwani twaweza kujifunza kutoka kwa makosa ya wengine bila kulazimika kufanya makosa ayo hayo wenyewe. Isitoshe, Mkristo angetaka kukumbuka kwamba “kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” (Mithali 16:31) Maisha yenye kutumiwa katika utumishi mwaminifu kwa Yehova ni yenye kupendeza kutoka kwa maoni yake na yastahili staha ya wengine yakiwa kielelezo kizuri. Bila shaka, kujifunza kutoka kwa Mungu na kupata ujuzi “katika njia ya haki” kwaweza kuanza mapema maishani na kwapasa kuwa utaratibu usiokoma kamwe.—Warumi 11:33, 34.
Hilo laweza kutolewa kielezi kwa ono lililohusu mvulana mmoja katika Sweden mwenye umri wa miaka saba. Alimwomba mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kundi kama angeweza kujiandikisha katika shule. Mwangalizi huyo aliuliza, “Kwa nini?” Ndipo kijana huyo akajibu: “Mtu hawezi kuketi kitako maisha yake yote!” (Mhubiri 12:1) Hicho ni kielelezo kinachofaa kama nini kwa vijana na wazee vilevile!
Kuheshimu Kichwa Chenye Mvi
Mwelekeo usiofaa katika jamii ya ki-siku-hizi ni kukazia thamani juu ya ustahili wa kimwili na uwezo wa kiriadha na kuwadharau wazee-wazee. Mtazamo wa Mkristo wapasa kuwa nini kuelekea wale wenye vichwa vyenye mvi kundini?
Badala ya kuwapuuza Wakristo wazee-wazee, tunapaswa kuwafikiria na kutumia wakati pamoja nao. Kwa mfano, kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova ya kila juma katika Jumba la Ufalme, je, wewe hujitahidi kuwasalimia walio wazee-wazee? Wao huthamini kikweli salamu za walio wachanga na za wengine. Na jinsi wazee-wazee wanavyofurahia kuwapo kwenye vikusanyiko vya kijamii vya waamini wenzao wa umri tofauti-tofauti! Ingawa wenzi wa ndoa wachanga zaidi huenda wakawa na mambo mengi zaidi ya kushirikiana na wenzi wa ndoa wengine wa rika lao, ingethawabisha kuwatia ndani walio wazee-wazee katika vikusanyiko hivyo vya furaha.—1 Wathesalonike 3:12; 5:15.
Ni jambo la maana kama nini kuwa na ufikirio tunapoongea na wazee-wazee! Ndugu mmoja mzee-mzee aliyekuwa na miaka 40 ya utumishi kwa Yehova wakati mmoja alisema na mzee mmoja juu ya jinsi yeye mwenyewe angeweza kutumiwa kundini, yule mwenye umri mdogo akasema: “Wewe huna uwezo wa kutumikia sana.” Hayo yalikuwa maneno yaliyokosa fadhili kama nini! Ndugu huyo mzee-mzee hakuwa na nishati nyingi kadiri alivyokuwa nayo wakati mmoja, ushirika wake katika huduma ya shambani ilikuwa imepungua kwa kadiri fulani, na baadhi ya mapendeleo ya uangalizi yalikuwa magumu mno kwa uwezo wake wa sasa; hata hivyo, alikuwa na mengi ya kutoa. Alikuwa na miaka mingi ya hekima na ujuzi uliolimbika katika njia ya uadilifu. Kwa sababu wazee-wazee hao walijitahidi wakiwa wahubiri wa Ufalme, wakavumilia mnyanyaso, wakachukua mizigo mizito ya daraka la Kikristo, na kuwazoeza wengine, watu wa Mungu sasa hufurahia tengenezo lenye nguvu lililotegemezwa na roho yake. Kwa hiyo, na tuwaonyeshe wazee-wazee hao staha wakiwa washauri wenye hekima, wachungaji wenye upendo, na walimu wenye matokeo.
Pia kuna sababu nzuri ya kufikiria kwa uzito madokezo yanayotolewa na wazee-wazee. Kwa kielelezo, ndugu mwenye ujuzi alidokeza kwamba mlango wa Jumba la Ufalme fulani usiwekwe kwenye upande wa magharibi wa jengo. Ndugu wachanga zaidi wakihangaikia zaidi eti uzuri wa jengo hilo hawakufuata dokezo lake. Hata hivyo, baada ya miaka kadhaa, mlango ulilazimika uwekwe mahali pengine kwa sababu upepo na mvua ya daima kutoka magharibi ilikuwa imeuchakaza. Hekima yenye mafaa sana ya ujuzi ilishinda nadharia za uzuri. Watu wachanga wakiwaheshimu walio wazee-wazee kwa kuyasikiliza maoni na hekima yao ya kutumika, hilo laweza kuokoa sana wakati na fedha. Hata kama dokezo la mtu mzee-mzee halifuatwi, yeye aweza kuheshimiwa kwa kumjulisha kwamba lilifikiriwa, lakini mambo mengine yaliongoza kwenye uamuzi mwingine.—Linganisha Mithali 1:8.
Tazama Mbele, Si Nyuma
Wazee-wazee wengine huwa na maoni haya: “Hakuna wakati mwingine ulio kama nyakati za zamani tulipokuwa vijana mimi na wewe.” Hata hivyo badala ya kukazia fikira nyakati zilizopita, wazee-wazee hao waweza kutiwa moyo kutazama mbele hadi siku watakapopata ama thawabu yao ya kimbingu ama kupata tena nguvu za ujana chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Kwa sasa, wanahitaji kufahamu mipaka yao kwa sababu ya umri. Ufahamu huo na ufurahifu ni wenye thamani kubwa wakati inapoonekana kana kwamba mtu mzee-mzee amepuuzwa kwa ajili ya mapendeleo ya utumishi.
Kwa kielelezo, huenda ikawa ndugu mzee-mzee alikuwa ametumiwa kwa kawaida kwenye programu za mkusanyiko wa wilaya miaka iliyopita. Sasa kuna wazee wengine wenye uwezo na wanaume wengi zaidi wa kuchaguliwa wenye uwezo wa kufundisha. Ingawa ni wachanga kwa kulinganishwa, baadhi ya wazee hao wameonyesha bidii na uwezo, wanaweza kufundisha vizuri na kutoa himizo lenye fadhili, na wanaweza pia kuwatia moyo wengine. (1 Wathesalonike 5:12, 13; 1 Timotheo 5:17) Likiwa tokeo, ndugu mzee-mzee ambaye hayumo katika programu ya kusanyiko huenda akahisi amepuuzwa na huenda asiwe na furaha kwamba mapendeleo yamepewa wazee wachanga zaidi. Hata hivyo, hisia hiyo isiyofaa ambayo hutokana na kutokamilika kwa kibinadamu yaweza kushindwa. Kwa kweli, wote kundini waweza kusaidia kwa kuwajulisha walio wazee-wazee kwamba wanahitajiwa, kwamba wanapendwa kwa ajili ya uaminifu wao, na kwamba maoni yao yanathaminiwa.
Bila shaka, mtu mzee-mzee anahitaji kukumbuka kwamba waabudu wenzake wanapaswa kuheshimiwa pia jinsi ambavyo yeye angependa kuheshimiwa. (Mathayo 7:12; Warumi 12:10) Badala ya kuhisi kwamba wamelazimishwa kustaafu kwa sababu ya umri na kuteseka kwa ajili ya maoni yasiyofaa, walio wazee-wazee wanapaswa washangilie juu ya miaka yao ya utumishi mwaminifu. Na kwa hakika, sisi sote twapaswa kuwa na shukrani kwamba kwa sababu ya baraka ya Yehova, kuna idadi yenye kuongezeka ya waangalizi wenye sifa za kustahili wa kushiriki ile kazi nyingi na kuchukua madaraka ya kundi wakati makutano ya “kondoo wengine” yanapomiminika kwenye tengenezo la Kikristo.—Yohana 10:16; Isaya 60:8, 22; 2 Timotheo 2:2.
Kwa sababu ya maumivu, afya yenye kudhoofika, au mambo mengine, wale wenye vichwa vyenye mvi huwa wenye kuudhika-udhika nyakati nyingine. Hilo lataka ufahamu na hisia-mwenzi kwa upande wa washiriki wengine wa familia au kundi. Hilo lataka pia kwamba walio wazee-wazee wajitahidi kudumisha mtazamo ufaao, kubaki vijana moyoni na akilini. Mshiriki wa chumba mchanga zaidi wa mshiriki mmoja wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alipokuwa akiondoka Betheli miaka kadhaa iliyopita, mwanamume huyo mzee-mzee alimwuliza mshiriki huyo wa chumba adokeze mtu ambaye angeweza kuchukua mahali pake akisema kwamba angependelea ndugu mchanga zaidi, aliye mkomavu ili amsaidie abaki mchanga na mwenye kutenda. Ndugu huyo mzee-mzee mpakwa-mafuta hakutaka kustaafu au kupunguza mwendo, kwani kuna kazi nyingi ya kufanywa. Hicho ni kielelezo kizuri kama nini cha kutazama mbele na kudumisha maoni yafaao!
Bila shaka, “fahari ya vijana ni nguvu zao, na uzuri wa wazee ni kichwa chenye mvi.” Ni jambo zuri ajabu kama nini wakati vijana wanapotumia nishati zao na walio wazee-wazee wanapotumia hekima yao katika kufuatia njia ya uadilifu! Wakristo wazee na vijana vilevile huona shangwe nyingi wanapoendeleza kwa umoja ibada ya kweli ya Yehova Mungu, “huyo mzee wa siku.”—Danieli 7:13.
[Picha katika ukurasa wa 28]
Wakristo wenye vichwa vyenye mvi wana mengi ya kutoa kwa ajili ya manufaa ya wengine