Familia ya Kikristo Huwasaidia Wazee-Wazee
“Usinitupe wakati wa uzee, nguvu zangu zipungukapo usiniache.”—ZABURI 71:9.
1. Wazee-wazee wanatendwaje katika tamaduni nyingi?
“UCHUNGUZI mbalimbali unaonyesha kwamba karibu sita kati ya saba (86%) ya watu waliozeeka wanaotendwa vibaya hutendwa vibaya na familia zao wenyewe,” likasema jarida The Wall Street Journal. Gazeti Modern Maturity lilisema hivi: “Kutendwa vibaya kwa wazee-wazee ni [jeuri ya familia] ya hivi karibuni tu ambayo imekuja kufunuliwa kwenye kurasa za magazeti ya habari ya taifa hili [yaani, U.S.A.].” Naam, wazee-wazee katika tamaduni nyingi wamekuja kutendwa vibaya sana na kupuuzwa. Kwa kweli wakati wetu ni ule ambapo wengi ni ‘wenye kujipenda wenyewe, hawana shukrani, si waaminifu-washikamanifu, hawana shauku ya asili.’—2 Timotheo 3:1-3, NW.
2. Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, Yehova huwaonaje wazee-wazee?
2 Lakini, hivyo sivyo jinsi wazee-wazee walivyopaswa kutendwa katika Israeli la kale. Sheria ilisema hivi: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako, Mimi ndimi BWANA [Yehova, NW].” Kile kitabu cha mithali zenye hekima zilizopuliziwa chatushauri hivi: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” Chaamuru hivi: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” Sheria ya Kimusa ilifundisha kuonyesha staha na heshima kwa watu wazee wa jinsia zote mbili. Kwa wazi, Yehova hutaka sana wazee-wazee waheshimiwe.—Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 1:8; 23:22.
Kuwatunza Wazee-Wazee Katika Nyakati za Biblia
3. Yusufu alionyeshaje huruma kwa baba yake aliyezeeka?
3 Staha ilipaswa kuonyeshwa katika maneno na pia katika matendo yenye ufikirio. Yusufu alimwonyesha baba yake mzee-mzee huruma nyingi. Alimtaka Yakobo afunge safari ya kutoka Kanaani hadi Misri, mwendo wa zaidi ya kilometa 300. Kwa hiyo Yusufu alimpelekea Yakobo “punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani.” Yakobo alipowasili Gosheni, Yusufu alienda kumlaki “akamwangukia shingoni, akalia shingoni mwake, kitambo kizima.” Yusufu alimwonyesha baba yake shauku nyingi. Hicho ni kielelezo chenye kuchochea kama nini cha kuwaonyesha wazee-wazee ufikirio!—Mwanzo 45:23; 46:5, 29.
4. Kwa nini Ruthu ni kielelezo chema cha kufuata?
4 Mfano mwingine mzuri wa kufuata katika kuwaonyesha wazee-wazee fadhili ni wa Ruthu. Ingawa hakuwa Mwisraeli, alishikamana na Naomi, mama-mkwe wake wa Kiyahudi, aliyekuwa mjane mzee-mzee. Aliwaacha watu wake mwenyewe akajiingiza katika hali yenye uwezekano wa kutopata mume mwingine. Naomi alipomsihi arudi kwa watu wake mwenyewe, Ruthu alijibu kwa maneno ambayo ni baadhi ya yaliyo ya kupendeza zaidi katika Biblia: “Usinisihi nikuache, nirejee nisifuatane nawe; maana wewe uendako nitakwenda, na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu; pale utakapokufa nitakufa nami, na papo hapo nitazikwa; BWANA [Yehova, NW] anitende vivyo na kuzidi, ila kufa tu kutatutenga wewe nami.” (Ruthu 1:16, 17) Ruthu alionyesha pia sifa zilizo nzuri alipokubali kuolewa na Boazi mzee-mzee chini ya mpango wa ndoa ya ndugu-mkwe.—Ruthu, sura 2 hadi 4.
5. Yesu alionyesha sifa zipi katika kuwashughulikia watu?
5 Yesu aliweka kielelezo icho hicho katika shughuli zake na watu. Alikuwa mwenye subira, mwenye huruma, mwenye fadhili, na mwenye kuburudisha. Alionyesha kupendezwa kibinafsi na mwanamume mmoja maskini aliyekuwa amekuwa mlemavu, asiweze kutembea kwa muda wa miaka 38, akamponya. Aliwaonyesha wajane ufikirio. (Luka 7:11-15; Yohana 5:1-9) Hata alipokuwa katika yale maumivu makali ya kifo chake chenye uchungu kwenye mti wa mateso, alihakikisha kwamba mama yake, ambaye labda alikuwa mwanzoni mwa miaka yake ya 50, angetunzwa. Yesu alikuwa mshiriki mwenye kuburudisha kila mtu, isipokuwa adui zake wa kinafiki. Hivyo, aliweza kusema hivi: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.”—Mathayo 9:36; 11:28, 29; Yohana 19:25-27.
Ni Nani Wanaostahili Ufikirio?
6. (a) Ni nani wanaostahili utunzaji wa pekee? (b) Tunaweza kujiuliza maswali gani?
6 Kwa kuwa Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, huweka vielelezo vyema kama hivyo kwa habari ya kujali, yafaa kabisa Wakristo waliojiweka wakfu waige kigezo chao. Kati yetu tuna watu fulani ambao wamesumbuka na kulemewa na mzigo kwa miaka mingi—ndugu na dada wazee-wazee ambao wamefikia miaka yao ya maisha yenye udhaifu. Baadhi yao waweza kuwa wazazi wetu au babu na nyanya zetu. Je! tunawachukua vivi hivi tu? Je! tunawasaidia kwa kujiona sisi tuna cheo cha maana kuliko wao? Au kwa kweli tunathamini maarifa na hekima yao nyingi? Ni kweli, baadhi yao wanaweza kutahini subira yetu kwa vitabia na vikasoro ambavyo ni vya kawaida katika uzee. Lakini jiulize hivi, ‘Ningekuwa tofauti nao kadiri gani chini ya hali hizo?’
7. Ni nini kinachotoa kielezi cha uhitaji wa kuwa na hisia-mwenzi kuwaelekea watu wazee?
7 Kuna hadithi moja yenye kugusa moyo kutoka Mashariki ya Kati juu ya huruma ya msichana mmoja mchanga kwa wazee-wazee. Nyanya mmoja alikuwa akisaidia jikoni, akaangusha na kuvunja sahani ya kauri bila kukusudia. Aliudhika kwa sababu ya upumbavu wake mwenyewe; binti yake alikuwa ameudhika hata zaidi. Kisha binti huyo akamwita msichana wake mwenyewe mdogo akamtuma kwenye duka la hapo amnunulie nyanya huyo sahani ya mbao isiyoweza kuvunjika. Msichana huyo alirudi akiwa na sahani mbili za mbao. Mama yake akataka kujua: “Kwa nini ulinunua sahani mbili?” Huyo binti aliye mjukuu wake akajibu hivi, akisita-sita: “Moja ni ya nyanya na ile nyingine ni yako utakapozeeka.” Naam, katika ulimwengu huu sisi sote tunakabili taraja la kuzeeka. Je! tusingethamini kutendewa kwa subira na fadhili?—Zaburi 71:9.
8, 9. (a) Tunapaswa kuwatendeaje watu wazee walio miongoni mwetu? (b) Baadhi ya wale waliokuja kuwa Wakristo hivi karibuni wanapaswa kukumbuka nini?
8 Usisahau kamwe kwamba ndugu na dada zetu wengi wazee-wazee wana rekodi ndefu nyuma yao ya utendaji mwaminifu wa Kikristo. Kwa hakika wanastahili heshima yetu na ufikirio wetu, msaada wetu na kitia-moyo chetu chenye fadhili. Yule mwanamume mwenye hekima alisema hivi kwa usahihi: “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” Na kichwa hicho chenye mvi, kiwe ni cha kiume au cha kike, kinapasa kuheshimiwa. Baadhi ya wanaume na wanawake hao walio wazee wangali wakitumikia wakiwa mapainia waaminifu, na wanaume wengi wanaendelea kutumikia kwa uaminifu wakiwa wazee katika makutaniko; wengine hufanya kazi ya kielelezo chema wakiwa waangalizi wasafirio.—Mithali 16:31.
9 Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Mzee usimkemee, bali umwonye kama baba; na vijana kama ndugu; wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote.” (1 Timotheo 5:1, 2) Wale ambao wameingia katika kutaniko la Kikristo hivi karibuni kutoka katika ulimwengu usio na staha wanapaswa hasa kutia maanani maneno ya Paulo, ambayo msingi wayo ni upendo. Vijana, msiige ile mitazamo mibaya ambayo huenda ikawa mliiona shuleni. Msichukie shauri lenye fadhili la Mashahidi wenye umri mkubwa zaidi. (1 Wakorintho 13:4-8; Waebrania 12:5, 6, 11) Hata hivyo, wazee-wazee wanapohitaji msaada kwa sababu ya afya mbaya au matatizo ya kifedha, ni nani walio na daraka kuu la kuwasaidia?
Daraka la Familia Katika Kuwatunza Wazee-Wazee
10, 11. (a) Kulingana na Biblia, ni nani wanaopaswa kuongoza katika kuwatunza wazee-wazee? (b) Kwa nini haiwi rahisi sikuzote kuwatunza wazee-wazee?
10 Katika kutaniko la Kikristo la mapema, matatizo yalitokea juu ya utunzaji wa wajane. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba mahitaji kama hayo yanapasa kutimizwa? “Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.”—1 Timotheo 5:3, 4, 8.
11 Katika nyakati za uhitaji, washiriki wa familia wa karibu wanapaswa kuwa wa kwanza kuwasaidia wazee-wazee.a Kwa njia hiyo, watoto ambao wamekuwa watu wazima wanaweza kuonyesha uthamini kwa ile miaka mingi ya upendo, kazi, na utunzaji ambayo wazazi wao waliandaa. Huenda hilo lisiwe rahisi. Watu wanapozeeka, wanakuwa wanyonge kiasili, na baadhi yao hata ni wasioweza lolote. Huenda wengine wakaanza kujifikiria wenyewe na wenye kudai, labda bila kutambua hivyo. Lakini tulipokuwa watoto wachanga, je, hatukuwa wenye kujifikiria wenyewe na wenye kudai? Na je, wazazi wetu hawakuharakisha kutusaidia? Sasa, hali imebadilika katika uzee wao. Kwa hiyo, ni nini kinachohitajiwa? Huruma na subira.—Linganisha 1 Wathesalonike 2:7, 8.
12. Ni sifa zipi zinazohitajiwa katika kuwatunza watu wazee—na wengine wote katika kutaniko la Kikristo?
12 Mtume Paulo alitoa shauri lenye mafaa alipoandika hivi: “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana [Yehova, NW] alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.” Ikiwa ni lazima tuonyeshe aina hiyo ya huruma na upendo katika kutaniko, je, tusiionyeshe hata zaidi katika familia?—Wakolosai 3:12-14.
13. Ni nani, zaidi ya wazazi wazee-wazee au babu na nyanya, ambao huenda wakahitaji msaada?
13 Nyakati fulani huenda isiwe ni wazazi au babu na nyanya tu wanaohitaji msaada wa aina hiyo bali pia watu wengine wa ukoo wazee-wazee. Watu wazee fulani ambao hawana watoto wametumikia kwa miaka mingi katika utumishi wa mishonari, huduma ya kusafiri, na utendaji mwingine wa wakati wote. Wameuweka Ufalme kwanza kikweli muda wote wa maisha zao. (Mathayo 6:33) Je! isingefaa, basi, kuwaonyesha roho ya kujali? Kwa hakika tuna kielelezo chema katika njia ambayo Watch Tower Society huwajali washiriki wayo wa Betheli walio wazee-wazee. Kwenye makao makuu ya Betheli katika Brooklyn na kwenye matawi kadhaa ya Sosaiti, ndugu na dada kadhaa waliozeeka hutunzwa kila siku na washiriki wa familia waliozoezwa ambao wamepewa mgawo wa kufanya kazi hiyo. Wanafurahi kuwatunza hawa watu wazee kana kwamba ni wazazi au babu na nyanya zao wenyewe. Wakati uleule, wanajifunza mengi kutokana na maarifa ya hao watu wazee.—Mithali 22:17.
Daraka la Kutaniko Katika Kujali
14. Ni uandalizi gani uliofanywa kwa ajili ya wazee-wazee katika kutaniko la Kikristo la mapema?
14 Nchi nyingi leo zina mifumo ya malipo ya uzeeni pamoja na utunzaji wa kitiba unaoandaliwa na Serikali kwa ajili ya wazee-wazee. Wakristo wanaweza kutumia maandalizi hayo kikamili mahali ambapo wana haki za kufanya hivyo. Hata hivyo, katika karne ya kwanza, maandalizi hayo hayakuwako. Kwa hiyo kutaniko la Kikristo lilichukua hatua chanya ili kuwasaidia wajane wenye uhitaji sana. Paulo alielekeza hivi: “Mjane asiandikwe isipokuwa umri wake amepata miaka sitini; naye amekuwa mke wa mume mmoja; naye ameshuhudiwa kwa matendo mema; ikiwa amelea watoto, ikiwa amekaribisha wageni, ikiwa amewaosha watakatifu miguu, ikiwa amewasaidia wateswao, ikiwa amefuata kwa bidii kila tendo jema.” Hivyo, Paulo alionyesha kwamba kutaniko pia lina daraka la kuwasaidia wazee-wazee. Wanawake wenye akili za kiroho ambao hawakuwa na watoto waamini walistahili msaada huo.—1 Timotheo 5:9, 10.
15. Kwa nini msaada huenda ukahitajiwa ili kupata msaada wa Serikali?
15 Mahali ambapo pana maandalizi ya Serikali kwa ajili ya wazee-wazee, hayo mara nyingi huhusisha kazi ya kujaza hati fulani-fulani ambayo yaweza kuonekana kuwa ya kutatiza. Katika hali kama hizo yafaa kwa waangalizi katika kutaniko kupanga msaada utolewe ili wazee-wazee waweze kuomba msaada huo, kuupata, au hata kuuongezea. Nyakati fulani mabadiliko ya hali yaweza kutokeza malipo zaidi ya uzeeni. Lakini kuna mambo mengine pia yenye mafaa ambayo waangalizi wanaweza kupanga ili wazee-wazee watunzwe. Ni nini baadhi yayo?
16, 17. Tunaweza kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa wazee-wazee katika kutaniko katika njia zipi tofauti?
16 Kuonyesha ukaribishaji-wageni ni desturi ya tangu nyakati za Biblia. Hadi leo katika nchi nyingi za Mashariki ya Kati, ukaribishaji-wageni huonyeshwa kwa watu wasiojulikana, angalau kufikia hatua ya kuwatolea kikombe cha chai au kahawa. Basi, haishangazi kwamba Paulo aliandika hivi: “Kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni, mkijitahidi.” (Warumi 12:13) Neno la Kigiriki kwa ukaribishaji-wageni, phi·lo·xe·niʹa, humaanisha kihalisi “kupenda (kuonea shauku, au kuwa wenye fadhili kuelekea) watu usiowajua.” Ikiwa Mkristo anapaswa kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa watu asiowajua, je, asingepaswa kuwa mkaribishaji-wageni hata zaidi kwa wanaohusiana naye katika imani? Mara nyingi kualikwa kwenye mlo huburudisha mtu mzee kwa kumpumzisha na shughuli zake za kawaida. Ikiwa wataka kusikia maneno ya hekima na ya maarifa kwenye vikusanyiko vyako, basi waalike wazee-wazee.—Linganisha Luka 14:12-14.
17 Kuna njia nyingi ambazo watu wazee wanaweza kutiwa moyo. Ikiwa tunakwenda kwenye Jumba la Ufalme au kwenye kusanyiko kwa gari tukiwa kikundi, je, kuna watu wazee fulani ambao wangependa kwenda nasi? Usiwangoje wakuombe. Jitolee kuwapeleka. Msaada mwingine wenye mafaa ni kuwanunulia vitu. Au ikiwa wanaweza, je, twaweza kwenda pamoja nao tunapoenda kujinunulia vitu? Lakini uhakikishe kwamba kuna mahali-mahali ambapo wanaweza kupumzika na kujiburudisha iwapo hilo linakuja kuhitajika. Bila shaka subira na fadhili zitahitajiwa, lakini shukrani ya moyo mweupe kutoka kwa mtu mzee-mzee yaweza kuwa yenye kuthawabisha sana.—2 Wakorintho 1:11.
Faida Yenye Kupendeza kwa Kutaniko
18. Kwa nini watu wazee ni baraka kwa kutaniko?
18 Ni baraka iliyoje kuona vichwa kadha vyenye mvi (na pia vyenye upara wa uzee) katika kutaniko! Yamaanisha kwamba miongoni mwa nguvu na uwezo wa vijana, tuna mnyunyizio wa hekima na maarifa—faida ya kweli katika kutaniko lolote. Ujuzi wao ni kama maji yenye kuburudisha ambayo ni lazima yachotwe kutoka katika kisima. Ni kama vile Mithali 18:4 inavyosema: “Maneno ya kinywa cha mtu ni kama maji ya vilindi; kijito kibubujikacho; chemchemi ya hekima.” Inatia moyo kama nini kwa watu wazee kuhisi kwamba wanatakwa na kuthaminiwa!—Linganisha Zaburi 92:14.
19. Watu fulani wamejidhabihuje kwa ajili ya wazazi wao wazee-wazee?
19 Watu fulani katika utumishi wa wakati wote wamehisi uhitaji wa kuacha mapendeleo yao ili kurudi nyumbani kuwatunza wazazi wagonjwa, walio wazee-wazee. Wamejidhabihu kwa ajili ya wale waliojidhabihu kwa ajili yao wakati uliopita. Mume na mke fulani, waliokuwa wamishonari wakati uliopita na ambao wangali katika utumishi wa wakati wote, walirudi nyumbani kuwatunza wazazi wao wazee-wazee. Wamefanya hivyo kwa miaka zaidi ya 20. Miaka minne iliyopita ilikuwa lazima mama wa mwanamume huyo apelekwe kwenye makao ya kuwauguza wazee-wazee. Mume huyo ambaye sasa yumo katika miaka yake ya 60, humtembelea mama yake wa miaka 93 kila siku. Aeleza hivi: “Ningewezaje kumwacha? Yeye ni mama yangu!” Katika hali nyingine makutaniko na watu mmoja mmoja wamejitolea kuwatunza watu wazee ili watoto wao waweze kuendelea katika migawo yao. Upendo huo usio wenye ubinafsi wastahili pia kupongezwa sana. Kila hali inapasa kushughulikiwa kwa kudhamiria kwa sababu wazee-wazee hawapaswi kupuuzwa. Onyesha kwamba unawapenda wazazi wako wazee-wazee.—Kutoka 20:12; Waefeso 6:2, 3.
20. Yehova ametupa sisi kielelezo kipi katika kuwatunza wazee-wazee?
20 Kwa kweli, ndugu na dada zetu walio wazee ni taji la uzuri kwa familia au kwa kutaniko. Yehova alisema hivi: “Na hata uzee wenu mimi ndiye, na hata wakati wenu wa mvi nitawachukueni [nitaendelea kustahimili, NW]; nimefanya, nami nitachukua; naam, nitachukua na kuokoa.” Na tuonyeshe subira na utunzaji uo huo kuelekea ndugu na dada zetu walio wazee katika familia ya Kikristo.—Isaya 46:4; Mithali 16:31.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata madokezo zaidi juu ya yale ambayo washiriki wa ona Mnara wa Mlinzi, Juni 1, 1987, kurasa 13-18.
Je! Wakumbuka?
◻ Tuna vielelezo vipi vya Biblia juu ya kuwatunza wazee-wazee?
◻ Tunapaswa kuwatendeaje wazee-wazee?
◻ Washiriki wa familia wanaweza kuwatunzaje wapendwa wao walio wazee-wazee?
◻ Kutaniko linaweza kufanya nini kuwasaidia wazee-wazee?
◻ Kwa nini wazee-wazee ni baraka kwetu sote?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Ruthu alionyesha fadhili na staha kwa Naomi mzee-mzee
[Picha katika ukurasa wa 24]
Wazee-wazee ni washiriki wa kutaniko wanaothaminiwa