Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 6/1 kur. 8-13
  • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuwaheshimu Wajane
  • Wazee ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’
  • ‘Watu Mmoja Mmoja ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’
  • Familia ya Kikristo Huwasaidia Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Mungu Anawajali Waliozeeka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kutimiza Mahitaji ya Walio na Umri Mkubwa Kati Yetu—Takwa Gumu la Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 6/1 kur. 8-13

‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee

“Mkiendelea kuangalia, si masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yenu wenyewe tu, bali pia masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yale ya wengine.”​—WAFILIPI 2:4, NW.

1, 2. (a) Baraza linaloongoza ya karne ya kwanza lilionyeshaje kuhangaishwa na mahitaji ya wazee-wazee? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba kazi ya kuhubiri haikuachwa?

MUDA mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K. katika kundi la Kikristo “nung’uniko lilitokea kwa upande wa Wayahudi wasema-Kigiriki dhidi ya Wayahudi wasema-Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wakipitwa bila kuangaliwa katika ugawaji wa kila siku [wa chakula kwa wahitaji].” Bila shaka hesabu fulani ya wajane hao walikuwa wazee-wazee na hawangeweza kujitunza wenyewe. Kwa kadiri yo yote, mitume wenyewe waliingilia jambo hili, wakiagiza: “Jitafutieni wanaume saba waliothibitishwa kuwa wanafaa kutoka miongoni mwenu, wenye kujaa roho na hekima, ili tupate kuwaweka rasmi juu ya hii shughuli inayohitajiwa kabisa.”​—Matendo 6:1-3, NW.

2 Hivyo Wakristo wa kwanza waliliona jambo la kutunza wahitaji kama “shughuli inayohitajiwa kabisa.” Miaka mingi baadaye mwanafunzi Yakobo aliandika: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (Yakobo 1:27) Basi je! jambo hili lilimaanisha kwamba kazi ya kuhubiri iliyo ya maana kupita zote ilikuwa imeachiliwa? La, kwa sababu usimulizi katika Matendo unasema kwamba kazi ya kuwapa wajane msaada ilipokwisha kupangwa ifaavyo, “neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu.”​—Matendo 6:7.

3. Ni kitia-moyo kipi kinachotolewa katika Wafilipi 2:4, na kwa sababu gani kinafaa sana leo?

3 Leo tunakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, 2 NW) Kuyatunza mahitaji ya maisha ya jamaa na kazi ya kimwili huenda kukatuachia nishati kidogo—au tamaa—ya kujishughulisha na mahitaji ya watu wazee-wazee. Kwa kufaa, basi, Wafilipi 2:4 inatuhimiza sisi ‘tusiangalie mambo yetu wenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’ Jambo hilo linaweza kufanywaje katika njia iliyosawazika, yenye mafaa?

Kuwaheshimu Wajane

4. Kundi la karne ya kwanza ‘liliwaheshimuje’ wajane? (b) Je! maandalizi kama hayo yalihitajiwa kabisa sikuzote?

4 Katika 1 Timotheo sura ya 5, Paulo anaonyesha jinsi Wakristo wa kwanza walivyowatunza wajane wazee-wazee katika kundi. Yeye alimhimiza Timotheo hivi: “Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli.” 1 Timotheo 5(mstari 3) Wajane wazee-wazee walichaguliwa kama wenye uhitaji hasa wa kupokea heshima ikiwa kwa namna ya kupewa tegemezo la fedha kwa ukawaida. Wao walikuwa wamekatiliwa mbali kutoka njia zote zenye kuonekana za kujitegemeza na wangeweza tu ‘kumwekea Mungu tumaini lao, na kudumu katika maombi na sala mchana na usiku.’ (mstari 5) Sala zao za kutaka riziki zilijibiwaje? Kupitia kundi! Katika njia iliyopangwa kitengenezo, wajane waliostahili waliandaliwa riziki ya kiasi. Bila shaka, ikiwa mjane alikuwa na fedha au watu wa ukoo wenye kuweza kumpa tegemezo, maandalizi hayo hayakuhitajiwa kabisa.​—1 Timotheo 5mistari 4, 16.

5. (a) Huenda ikawa wajane wengine ‘wameingilia kutafuta utoshelezaji wa hisia’ kwa njia gani? (b) Je! kundi lilikuwa na wajibu wa kuwategemeza hao?

5 “Lakini yule [mjane] anayeingilia kutafuta utoshelezaji wa hisia,” akatahadharisha Paulo, “amekufa [kiroho] ingawa anaishi.” 1 Timotheo 5(mstari 6, NW) Paulo haelezi vile wengine walivyokuwa ‘wakijiendesha kwa kuamsha hisia,’ kama vile Biblia ya Kingdom Interlinear inavyofasiri maneno hayo kwa uhalisi. Huenda ikawa wengine walikuwa na pigano la kupambana na ‘nyege zao.’ 1 Timotheo 5(mstari 11, NW) Hata hivyo, kulingana na Liddell & Scott’s Greek-English Lexicon, ‘kujiendesha kwa kuamsha hisia’ kungaliweza kuwa kulitia ndani ‘kuishi kwa kujilegeza au katika starehe au anasa ya kupita kiasi.’ Labda, basi, wengine walitaka kundi liwatajirishe; ligharimie maisha ya kutapanya vitu, ya kujitia katika anasa nyingi na yasiyo na kiasi. Vyo vyote ilivyokuwa, Paulo anaonyesha kwamba wajane wa namna hiyo waliondolewa ustahili wa kupokea tegemezo la kundi.

6, 7, na maelezo yaliyo chini. (a) ‘Kuandikwa katika orodha’ kulikuwa nini? (b) Kwa sababu gani wale ambao walikuwa chini ya umri wa miaka 60 walikosa kupokea tegemezo hilo? (b) Paulo alizuiaje wajane vijana wasipokee “hukumu” kali?

6 Ndipo Paulo akasema: “Mjane asiandikwe [kati ya wale wenye kupokea tegemezo la kifedha] isipokuwa umri wake amepata miaka sitini.” Katika siku za Paulo mwanamke aliyekuwa na umri zaidi ya 60 kwa wazi alionwa kuwa hawezi kujitegemeza mwenyewea na haikuelekea kwamba wangeolewa tena. “Kwa upande ule mwingine,” Paulo akaagiza, “uwakatalie wajane wenye umri mdogo [wasiandikwe katika orodha] kwa maana wakati nyege zao zimekuja kati yao na Kristo, wao wanataka kuolewa, wakiwa na hukumu kwa sababu wamepuuza wonyesho wao wa kwanza wa imani.”​—1 Timotheo 5Mistari 9, 11, 12, NW.

7 Kama wajane wenye umri mdogo wangalikuwa wameruhusiwa kuandikwa katika “orodha,” labda wengine wangalitangaza haraka haraka nia ya kubaki wakiwa waseja. Wakati ulipopita, ingawa hivyo, labda wengine wangalipata tatizo la kuzuia “nyege” zao watake kuolewa tena, ‘wakiwa na hukumu kwa kupuuza wonyesho wao wa kwanza wa imani’ wa kubaki wakiwa waseja. (Linganisha Mhubiri 5:2-6.) Paulo alizuia matatizo kama hayo, kwa kutangaza zaidi kwamba, “napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto.”​—1 Timotheo 5Mstari 14.

8. (a) Miongozo ya Paulo ilililindaje kundi? (b) Je! wajane vijana na wanaume wazee-wazee wenye uhitaji walitunzwa pia?

8 Mtume Paulo pia aliweka mpaka ili wenye kuandikwa orodhani wawe ni wale tu waliokuwa wametenda kwa muda mrefu kazi bora za Kikristo. 1 Timotheo 5(mstari 10) Hivyo kundi halikuwa ‘makao ya kutunza masilahi’ ya watu wavivu na wenye pupa. (2 Wathesalonike 3:10, 11) Lakini namna gani wanaume wazee-wazee au wajane wenye umri mdogo? Ikiwa wao wangetumbukia katika uhitaji, bila shaka kundi lingaliwatunza kama mtu mmoja mmoja.—Linganisha 1 Yohana 3:17, 18.

9. (a) Kwa sababu gani mipango ya kutunza wazee-wazee leo inatofautiana na ile iliyofanywa katika karne ya kwanza? (b) Mazungumzo ya Paulo juu ya wajane katika 1 Timotheo sura ya 5 yanatusaidia tuthamini nini leo?

9 Inaelekea mipango hiyo iliyatoshelea mahitaji ya makundi ya karne ya kwanza. Lakini kama vile The Expositor’s Bible Commentary kinavyoonelea: “Kwa vile leo kuna mapato ya bima, mpango wa kiserikali wa kusaidia wenye shida, na nafasi za kazi, hali hiyo ni tofauti sana.” Kwa sababu ya badiliko la hali za kijamii na kiuchumi, ni mara chache sana leo makundi yatakapohitajika kabisa kudumisha orodha zenye majina ya wafadhiliwa wazee-wazee. Hata hivyo, maneno ya Paulo kwa Timotheo yanatusaidia tuthamini kwamba: (1) Matatizo ya walio wazee-wazee yanahangaisha kundi lote—hasa wazee. (2) Utunzaji wa walio wazee-wazee unapasa upangwe vizuri kitengenezo. (3) Utunzaji wa namna hiyo unawekewa mpaka uwe wa wale tu ambao kweli wana uhitaji.

Wazee ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’

10. Wazee leo wanaweza kuongozaje katika kuonyesha wanapendezwa kujua hali ya wenye umri mkubwa?

10 Waangalizi leo wanaongozaje katika kuonyesha wanapendezwa kujua hali ya watu wenye umri mkubwa? Mara kwa mara wanaweza kupanga mahitaji ya wazee-wazee katika orodha ya mambo yanayokusudiwa kuzungumzwa kwenye mikutano yao. Msaada halisi unapohitajiwa, wao wanaweza kupanga ili utolewe. Huenda wao binafsi wasitoe utunzaji huo, kwa kuwa mara nyingi kuna wengi wenye nia—kutia na vijana—katika kundi ambao wanaweza kusaidia. Hata hivyo, wao wanaweza kusimamia utunzaji huo kwa ukaribu, labda kwa kumpa ndugu mmoja mgawo wa kusawazisha utunzaji ambao mtu fulani anapewa na watu mbalimbali.

11. Wazee wanaweza kujifahamishaje na mahitaji ya wazee-wazee?

11 Sulemani alishauri hivi: “Fanya bidii kuijua hali ya makundi yako.” (Mithali 27:23) Hivyo waangalizi wanaweza kuwatembelea wazee-wazee kibinafsi ili waamue njia iliyo bora zaidi ya ‘kugawana . . . kulingana na mahitaji yao.’ (Warumi 12:13, NW) Mwangalizi anayesafiri alieleza jambo hilo hivi: “Wazee-wazee fulani wanajitegemea sana, na si vizuri kuwauliza tu ni jambo gani linahitaji kufanywa. Jambo bora zaidi ni kutambua jambo linalohitaji kufanywa na kuanza moja kwa moja kuwafanyia kazi hiyo!” Katika Japani waangalizi fulani walipata kwamba dada mmoja mwenye umri wa miaka 80 alihitaji kuangaliwa sana. Wao wanaripoti: “Sasa tunahakikisha kwamba mtu fulani anakuwa naye mara mbili kwa siku, asubuhi na usiku, kwa kumtembelea au kumpigia simu.”—Linganisha Mathayo 25:36.

12. (a) Wazee wanaweza kuhakikishaje kwamba wazee-wazee wananufaika kutokana na mikutano ya kundi? (b) Ni matumizi gani mazuri yanayoweza kufanywa kutokana na kanda za kunasa sauti ambazo zimetolewa na Sosaiti?

12 Waangalizi pia wanaweza kushughulika kuona kwamba wazee-wazee wananufaika kutokana na mikutano ya kundi. (Waebrania 10:24, 25) Je! wengine wanahitaji njia ya kusafiri? Je! wengine wanakosa ‘kusikiliza na kufahamu’ mikutano kwa sababu ya kupungukiwa nguvu za kusikia? (Mathayo 15:11) Labda ingefaa kuwawekea chombo cha kusaidia kusikia. Vivyo hivyo, hesabu fulani ya makundi zina njia ya kupitisha mikutano katika simu ili wenye vizuizi vya kimwili waweze kusikiliza wakiwa nyumbani. Wengine wanairekodi mikutano yao katika kanda za kunasia sauti kwa ajili ya wale ambao ni wagonjwa sana hivi kwamba hawawezi kuhudhuria—katika visa vingine wakiwanunulia vyombo vyenyewe vya unasaji sauti. Na kuhusu kanda za kunasia sauti, mzee mmoja katika Ujeremani alionelea hivi: “Nimetembelea watu kadha wazee-wazee ambao waliketi tu mbele ya televisheni na kutazama vipindi ambavyo hata haviwezwi kuelezwa kuwa vyenye kujenga kiroho.” Badala yake mbona msiwatie moyo wasikilize kanda za kaseti zinazotolewa na Sosaiti, zilizo na midundo mitamu ya Ufalme na usomaji wa Biblia?

13. Wenye umri mkubwa wanaweza kusaidiwaje kuwa watendaji wakiwa watangazaji wa Ufalme?

13 Washiriki fulani wa kundi wenye umri mkubwa wamekuwa wahubiri wasio wa kawaida au wasiotenda. Ingawa hivyo, kwa lazima uzee hauzuii mtu asiwe mtangazaji wa “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Huenda wengine wakaitikia mwaliko kidogo tu wa kufanya kazi pamoja nawe shambani. Labda wewe unaweza kuamsha upendo wao wa kuhubiri kwa kushiriki nao mambo yaliyoonwa katika utumishi wa shambani. Ikiwa kupanda ngazi ni tatizo, fanya mpango ili wafanye kazi katika nyumba zisizo na ngazi. Wahubiri wengine wanaweza kuwakaribisha wazee-wazee wajiunge nao katika mafunzo ya Biblia​—au wafanye funzo hilo katika nyumba ya mzee-mzee huyo.

14 na sanduku. (a) Wazee wanaweza kufanyaje ikiwa ndugu mzee-mzee anatumbukia katika shida kubwa ya kifedha? (b) Makundi mengine yamejitoaje kutimiza mahitaji ya wahubiri wazee-wazee?

14‘Fedha ni ulinzi.’ (Mhubiri 7:12) Hata hivyo, ndugu au dada wengi wazee wana shida kubwa sana ya kifedha na hawana watu wa ukoo ambao wana nia ya kusaidia. Ingawa hivyo, watu mmoja mmoja katika kundi mara nyingi wana furaha ya kusaidia wanapojulishwa uhitaji huo. (Yakobo 2:15-17) Wazee wanaweza pia kuchunguza waone kunapatikana utumishi gani wa serikali kusaidia wenye shida, mipango ya bima, malipo ya waliostaafu, na kadhalika. Hata hivyo, katika nchi nyingine, utumishi kama huo ni mgumu kupatikana, na huenda ikawa hakuna jambo jingine la kufanya isipokuwa kufuata kiolezo kilicho katika 1 Timotheo sura ya 5 na kupanga ili kundi zima litoe msaada. (Ona Tumefanywa Tengenezo Kutimiza Huduma Yetu, kurasa 122, 123.)

Wahubiri katika Naijeria walimsaidia kwa ukawaida painia wa kawaida mwenye umri wa miaka 82 pamoja na mke wake kwa kuwapa zawadi za kimwili. Baada ya serikali, kuratibu kwamba jengo waliloishi ndani yalo lingebomolwea, kundi liliwaalika wahamie katika chumba kimoja kilichofungamana na Jumba la Ufalme mpaka mahali pengine pa kuishi paweze kupangwa.

Katika Brazili kundi moja lilikodi mwuguzi wa kike ili awatunze mume na mke wazee-wazee. Wakati ule ule, dada mmoja alipewa mgawo wa kutunza nyumba iwe safi, kutayarisha chakula chao, na kutunza mahitaji yao mengine ya kimwili. Kila mwezi kundi linaweka akiba ya fedha kwa matumizi yao.

15. (a) Je! kuna mipaka kuhusu msaada ambao kundi linaweza kutoa? (b) Shauri lililo katika Luka 11:34 linaweza kuwafaaje watu fulani wanaokuwa wenye kudai mno?

15 Kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza, maandalizi kama hayo ni kwa wale wanaostahili na wanaoyahitaji kweli kweli. Waangalizi hawana wajibu wa kushughulikia maombi yanayopita kiasi au kushughulikia madai yasiyo ya kiakili. Ni lazima pia wazee-wazee waendelee kuwa na ‘jicho rahisi.’​—Luka 11:34, NW.

‘Watu Mmoja Mmoja ‘Kuendelea Kuangalia Masilahi Zao’

16, 17. (a) Kwa sababu gani ni jambo la maana kwa wengine kundini zaidi ya wazee kupendezwa na watu wazee-wazee? (b) Wahubiri wenye shughuli wanawezaje ‘kuukomboa wakati’ kwa ajili ya wazee-wazee?

16 Wakati fulani uliopita dada mmoja mzee-mzee alilazwa hospitalini. Uchunguzi ulionyesha kwamba alikosa chakula kinachoufaa mwili. “Kama wengi kundini wangependezwa naye kibinafsi,” akaandika mzee mmoja, “labda jambo hilo halingetukia.” Ndiyo, si wazee peke yao wanaopaswa kuwatunza watu wazee-wazee. Paulo aliandika: “Kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake.”​—Waefeso 4:25.

17 Bila shaka wengine wenu tayari mna mizigo ya madaraka ya kibinafsi. Lakini ‘endelea kuangalia, si masilahi ya kibinafsi juu ya mambo yako mwenyewe tu.’ (Wafilipi 2:4, NW) Kwa mpango mzuri, mara nyingi unaweza ‘kununua wakati.’ (Waefeso 5:16, NW) Kwa mfano, je! wewe unaweza kutembelea mmoja aliye mzee-mzee baada ya utumishi wa shambani? Mara nyingi siku za kati ya juma zinakuwa zenye upweke kwa wengine. Matineja, pia, wanaweza kuhusika katika kutembelea na kuwafanyia kazi wazee-wazee. Akasali dada mmoja aliyesaidiwa na kijana: “Asante Yehova kwa Ndugu kijana John. Yeye ni mtu mzuri sana.”

18. (a) Kwa sababu gani nyakati nyingine maongezi pamoja na mzee-mzee yanaweza kuwa magumu? (b) Mtu anaweza kufanyaje ziara au maongezi pamoja na ndugu mwenye umri mkubwa yawe yenye kuwajenga wote wawili?

18 Katika mikutano, wewe unawapa walio na umri mkubwa salamu ya juu-juu tu? Ni kweli kwamba huenda ikawa si jambo rahisi kuzungumza pamoja na mtu ambaye hasikii kwa wepesi au ana tatizo la kujieleza mwenyewe. Na kwa kuwa afya yenye kudhoofika polepole inatatiza sana pia, si wazee-wazee wote walio na maelekeo ya kuwa wachangamfu. Ijapokuwa hivyo, “afadhali mtu mwenye subira.” (Mhubiri 7:8, AW) Kwa kujitahidi kidogo, “mbadilishano wa kitia-moyo” halisi unaweza kutokea. (Warumi 1:12, NW) Jaribu kueleza jambo lililoonwa katika utumishi wa shambani. Shiriki nao jambo ulilosoma katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Hata hivyo jambo bora zaidi ni kusikiliza. (Linganisha Ayubu 32:7.) Watu wenye umri mkubwa wana mambo mengi ya kushiriki ukiwaruhusu wafanye hivyo. Akakiri hivi mzee mmoja: “Kumtembelea ndugu yule mzee mwenye umri kulinifaidi sana.”

19. (a) Hangaiko letu kwa wazee-wazee linanyooshwa kwa akina nani? (b) Ni nini baadhi ya njia tunazoweza kuthibitisha kwamba sisi tunasaidia jamaa ambazo zinawatunza wazazi wenye umri mkubwa?

19 Je! hangaiko lako kwa wazee-wazee halipasi linyooshwe lihusu pia jamaa zinazowatunza? Mume na mke wanaotunza wazazi wanaoendelea kuzeeka waliripoti: “Badala ya kututia moyo sisi, wengine kundini wamekuwa wenye kulaumu-laumu. Dada mmoja alisema: ‘Mkiendelea kukosa mikutano, mtakuwa wagonjwa kiroho!’ Lakini yeye hakuwa na nia ya kufanya jambo lo lote kutusaidia sisi tufike kwenye mikutano.” Zenye kuvunja moyo pia ni ahadi zinazotolewa bila uhakika kamili (‘Ukihitaji msaada wakati wo wote, nijulishe.’), ambazo mara nyingi zinakuwa kama kusema, ‘Ukaote moto na kushiba.’ (Yakobo 2:16) Ingekuwa vizuri zaidi kuacha hangaiko lako lionekane kwa kitendo! Wanaripoti hivi wenzi wawili waliooana: “Akina rafiki wamekuwa wazuri sana na wenye kutegemeza! Wengine wanaweza kumtunza Mama kwa siku kadha mfululizo ili kwamba nasi tupate pumziko pindi kwa pindi. Wengine wanampeleka kwenye mafunzo ya Biblia. Na inatutia moyo sana wakati wengine wanapouliza juu ya hali yake.”

20, 21. Wenye umri mkubwa wanaweza kufanya nini ili wasaidie wale ambao wanawapa utunzaji?

20 Kwa kadiri kubwa watu wenye umri mkubwa kati yetu wanatunzwa vizuri. Hata hivyo, Mashahidi wazee-wazee wanaweza kufanya nini wao wenyewe ili kwamba kazi hii ifanywe “kwa furaha wala si kwa kuugua”? (Linganisha Waebrania 13:17.) Mshirikiane na mipango ambayo wazee wanafanya kwa utunzaji wenu. Onyesheni shukrani na uthamini kwa matendo yo yote ya wema yanayofanywa na mwepuke kuwa wenye kudai mno au wenye kulaumu-laumu mno. Na ijapokuwa maumivu na uchungu wa uzee ni halisi, jaribuni kuonyesha mwelekeo wa uchangamfu, wa kutazamia mazuri.​—Mithali 15:13.

21 Wengi wenye umri mkubwa wamesikiwa wakisema hivi, ‘Akina ndugu ni wazuri sana. Sijui ningefanya nini bila wao.’ Hata hivyo, daraka kubwa la kuwatunza wazee-wazee ni la watoto wao. Hili linatia ndani nini, na mwito huo wa ushindani unaweza kukabiliwaje katika njia nzuri?

[Maelezo ya Chini]

a Walawi 27:1-7 linataja umri wa miaka 60 linapozungumza juu ya watu mmoja mmoja ‘waliotolewa kama mchango’ hekaluni (kwa kufanya nadhiri) wawe wafanya kazi. Bei ya kukombolewa ilitofautiana kulingana na umri. Kwenye umri wa miaka 60 bei hiyo ilianguka sana, inaonekana kwa sababu mtu mzee hivyo alionwa kuwa asiyeweza kufanya kazi kwa nguvu kama mtu mwenye umri mdogo. The Encyclopedia Judaica inaongezea hivi: “Kulingana na Talmudi, uzee . . . unaanzia miaka 60.”

Je! Wewe Unakumbuka?

◻ Ni maandalizi gani yaliyofanywa katika karne ya kwanza kwa wajane wazee-wazee?

◻ Waangalizi wanaweza kupangaje utunzaji wa watu wenye umri mkubwa katika kundi?

◻ Watu mmoja mmoja katika kundi wanaweza kuonyeshaje upendezi katika ndugu na dada wazee-wazee?

◻ Watu wenye umri mkubwa wanaweza kufanya jambo gani ili wawasaidie wale wanaowatunza?

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Kuwasaidia Wazee-Wazee​—Yale Ambayo Wengine Wanafanya

Kundi moja katika Brazili lilipata njia inayofaa ya kuyatunza mahitaji ya kimwili ya ndugu mmoja anayeishi karibu na Jumba la Ufalme lao: Kikundi cha funzo cha kitabu ambacho kimepewa mgawo wa kusafisha Jumba ndicho kinachosafisha nyumba yake pia.

Kundi jingine huko lilipata njia rahisi ya kumfanya ndugu mmoja mwenye kizuizi cha kimwili aendelee kuwa mtendaji katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Zamu yake inapofika kutoa hotuba, ndugu anapewa mgawo wa kuchukua wahubiri wawili au watatu pamoja naye ili wamtembelee ndugu huyo. Mkutano mfupi unafunguliwa kwa sala, na ndugu huyo anatoa mgawo wake. Shauri linalofaa linatolewa. Ni kitia-moyo kilichoje ambacho ziara hii inatoa!

Waangalizi wasafirio wameweka mfano mzuri wa kuongoza. Katika kundi moja, ndugu mmoja mzee-mzee aliyekuwa akikaa daima kwenye kiti-magurudumu cha wagonjwa alikuja kuwa mwenye kuudhika sana na kama matokeo hakutembelewa sana. Hata hivyo, mwangalizi asafiriye alipanga kumwonyesha ndugu huyo hotuba yake yenye slaidi faraghani. Ndugu huyo mwenye umri mkubwa alivutiwa sana na yale aliyoyaona mpaka akalia machozi. Anasema hivi mwangalizi huyo: “Nilihisi kuwa nimethawabishwa sana kwa kuona jinsi kumwelekezea fikira na upendo kidogo tu kulivyoweza kuleta matokeo mazuri kama hayo.”

Wazee fulani katika Naijeria walifanya ziara ya uchungaji kwa ndugu mmoja mzee wakagundua kwamba alikuwa mgonjwa mahututi. Walimpeleka mara moja hospitalini. Ndugu huyo mwenye umri mkubwa alipatikana kuwa anahitaji utibabu wa muda mrefu lakini hangeweza kuulipia. Kundi lilipojulishwa uhitaji wake, wahubiri walichanga fedha za kutosha kulipia gharama zake. Wazee wawili walipokezana zamu za kumpeleka kwa gari hadi hospitalini na kumrudisha ijapokuwa jambo hilo lilihitaji waombe ruhusa kutoka kazini mwao. Ingawa hivyo, walipata furaha kuona ndugu huyo akipona ugonjwa wake na kufanya upainia msaidizi mpaka kifo chake miaka minne baadaye.

Katika Ufilipino, dada mmoja mzee-mzee hakuwa na jamaa. Kundi lilimfanyia mpango ili atunzwe wakati wa miaka mitatu ya ugonjwa. Walimpa mahali padogo pa kuishi, wakamletea chakula kila siku nyakati za kula, na kutunza hali yake ya usafi.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wote wanaweza kushiriki katika kuheshimu watu wenye umri mkubwa walio kati yetu kundini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki