Kutimiza Mahitaji ya Walio na Umri Mkubwa Kati Yetu—Takwa Gumu la Kikristo
MIEZI mitatu imepita. Lakini hakuna hata mmoja wa watoto wa yule mama mzee-mzee ambaye amejishughulisha kumtembelea. Yeye ni mkazi mwenye upweke wa makao ya wazee katika Cape Town, Afrika Kusini. Watoto wake wanaishi karibu na mahali hapo.
Katika makao ya wazee huko Johannesburg, mwanamke mmoja mzee anatumia mwingi wa wakati wake akiwa kwenye roshani ya chumba chake. Mara nyingi yeye huonekana akiwa analia.
Mandhari zenye kutia uchungu kama hizi zinaanza kuwa za kawaida zaidi na zaidi, hata katika nchi ambako wazee-wazee walitunzwa vizuri kulingana na desturi. Katika Soweto, sehemu kubwa sana inayoishi weusi wengi karibu na Johannesburg, watu wazee wamepoteza heshima ya kidesturi, mamlaka na utunzaji kutoka kwa jamaa zao, kulingana na ripoti moja ya magazeti. Hali inayolingana na hiyo imesitawi miongoni mwa idadi kubwa ya Wahindi katika Afrika Kusini. Ijapokuwa kulingana na desturi Wahindi wamewaangalia wazazi wao wazee, ofisa mmoja alieleza hivi majuzi kwamba wenzi vijana Wahindi waliooana ‘hawataki kuwekewa mzigo na wazazi wao.’
Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanatii amri ya Biblia: “Waheshimu baba yako na mama yako.” (Kutoka 20:12; Waefeso 6:2) Takwa hili halikomi wakati wazazi wao wanapozeeka. Yasema 1Timotheo 5:8; “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” Wazazi wazee wamo miongoni mwa wale ambao Mkristo angelazimika kutunza, hata kama jambo hilo lingetia ndani dhabihu za kadiri fulani—kimoyoni na kifedha.
Sana sana, washiriki wa kundi la Kikristo leo wamefanya kazi yenye kufurahisha katika kutunza mahitaji ya kimoyoni na kimwili ya wazazi wao. Ingawaje, ni nini kinachotokea wakati Wakristo wazee-wazee hawana watoto au wajukuu wanaomwogopa Mungu ili wawatunze? Mahitaji yao yanatimizwaje?
Daraka la Kundi
Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao.” Pia Yakobo alitaarifu hivi: “Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini? Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake.”—Yakobo 1:27; 2:15-17.
Kwa hiyo ikiwa Mkristo mzee-mzee anahitaji msaada, hili ni jambo la kushughulikiwa na kundi nzima. Wazee wanaweza kuongoza katika jambo hili. Kama alivyoelekeza Paulo kwenye 1 Timotheo 5:4, kwanza wanapaswa kuamua ikiwa mzee-mzee ana watoto au wajukuu ambao wana nia ya “kuwalipa wazazi wao [na nyanya]. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu.” Ikiwa hawana, wazee wanaweza kuchunguza-chunguza waone ni bima gani au maandalizi yanayodhaminiwa na serikali yanayopatikana. Huenda hata ikawa kwamba wengine kundini wanaweza kusaidia kifedha kwa kiwango cha kibinafsi.
Hata hivyo, ikiwa mipango kama hiyo haiwezi kufanywa, wazee wanaweza kufikiria ikiwa mtu mmoja mmoja anastahili kupokea msaada kutoka kwa kundi lenyewe. Akasema Paulo: “Mjane asiandikwe isipokuwa umri wake amepata miaka sitini; naye amekuwamke wa mume mmoja; naye ameshuhudiwa kwa matendo mema.”—1 Timotheo 5:9, 10.
Ingawaje, mara nyingi, si pesa zinazohitajiwa. Wazee wanaweza kuamua ni nini kinachohitajiwa. Je! mzee-mzee anahitaji msaada wa kununuliwa vitu? Je! anahisi upweke au anahitaji kitia-moyo? Je! anahitaji njia ya kusafiri ili afike mikutanoni? Je! anahitaji mtu wa kumsomea Biblia na vichapo vya Kikristo? Ikiwa mzee-mzee hawezi kufika mikutanoni kwa sababu ya hali ya mwili, je! anaweza kurekodiwa mikutano katika kanda za kunasia sauti ili aweze kuzisikiliza nyumbani? Inaweza kuchukua ziara nyingi na mazungumzo kabla jambo lenyewe halijajulikana. Lakini wakiwa wachungaji, wazee ‘wanahitaji kujua hali ya makundi.’—Mithali 27:23.
Jinsi Makundi Yamesaidia
Mara mahitaji ya mzee-mzee yanapojulikana, mipango mahususi inaweza kufanywa. Mahali ambapo pana roho changamfu, yenye kutaka kutoa utunzaji, na isiyo ya ubinafsi katika kundi, si jambo gumu kupata hesabu kubwa ya akina ndugu na dada ambao wana nia ya kutoa msaada. Hilo linasaidia kutowawekea watu wachache mmoja mmoja mzigo usio wa haki. Mathalani, kundi moja limetengeneza ratiba ya wahubiri kuwatembelea wazee-wazee. Akina ndugu na dada wanafurahia kuwa na shirika katika kufanya hivyo, na hakuna ye yote wa wenye umri mkubwa asiyetunzwa.
Katika kundi lingine, Shahidi mzee-mzee aliacha kuangaliwa na watoto wake wasioitikadi. Hata hivyo, vijana Mashahidi wenyeji walifua nguo zake zote, wakapiga pasi, na wakasafisha, na pia wakatunza ua wake. Akina ndugu walisaidia kulipia kodi yake ya nyumba na chakula. Walimpeleka kwenye makusanyiko na mikutano. Na alipokufa, wao wakafanya mipango yote ya mazishi na kulipia gharama zote.
Katika kundi moja dogo la Afrika Kusini, ndugu mmoja mchotara aliyekuwa mzee mzee alilemazwa kabisa na pigo. Kwa kuwa hakukuwa na mtu ye yote wa jamaa yake wa kumtunza, dada mmoja katika lile kundi—yeye mwenyewe akiwa mjane—na mwana wake walimchukua ili kumtunza. Wanaume kundini walichukua zamu za kumwogesha. Kwa kuongezea, ndugu mzungu painia angemtembeza nje ndugu huyo mzee katika kiti chake chenye magurudumu. Ono hilo, ambalo si la kawaida katika Afrika Kusini, lilisisimua kweli kweli. Kundi lilimtunza kwa upendo ndugu huyo mzee-mzee mpaka alipokufa.
Ingawaje, hilo halimaanishi kwamba kutimiza mahitaji ya ndugu na dada wazee-wazee ni jambo rahisi. Inaweza kuhitaji kuchukua hatua ya kwanza na kupiga moyo konde kushinda matatizo yanayoweza kutokea.
Kuwasaidia Wazee-Wazee Wafike Mikutanoni
Dada mmoja mzee-mzee, mjane na mwenye ugonjwa wa moyo, alitembelewa na mzee siku moja. Mzee huyo alipokuwa huko, jirani mmoja alitembelea na kulalamika, akisema: “Ninakuja hapa mara nyingi nami nampata akilia kwa sababu hakuna mtu aliyekuja kumchukua ili ampeleke kwenye Jumba la Ufalme.” Tatizo halikuwa mbaya sana kama vile jirani huyo alivyolifanya lionekane, kwa kuwa jamaa moja katika kundi lile ilikuwa ikitoa njia ya kusafiri kwa ukawaida. Hata hivyo, pindi chache baba alikuwa amefanya ovataimu na akakosa kuja kumchukua dada yule. Kwa kweli, mipango mingine ya kusafiria ingefanywa.
Basi, ni jambo zuri kukumbuka kwamba kuhudhuria mikutano ni jambo la muhimu kwa walio na umri mkubwa. (Waebrania 10:24, 25) Mzee mmoja huangalia sikuzote aone kama Shahidi mmoja mzee-mzee yupo. Ikiwa hayupo kwa sababu hakuna njia ya kusafiri, mzee huyo huingia kwenye gari lake na kwenda kumchukua mwanamke huyo. Tabasamu yenye kupendeza inayoonyeshwa huthawabisha sana mzee huyo kwa jitihada yake ya ziada.
Wenye Busara Lakini Wenye Kuendelea Kuuliza-uliza Bila Kubadilika
Hata hivyo, nyakati fulani fulani, watu walio na umri mkubwa wanaweza kuwa wenye kujitegemea kidogo. Huenda wakawa na uhitaji wa msaada lakini wakakataa kuukubali. Na wazee, au wale ambao wamegawiwa kusaidia wasipokuwa macho, wenye umri mkubwa hao huenda wakawa na mwelekeo wa kujaribu ‘kufanya mambo katika njia yao wenyewe.’
Mjane mmoja mzee-mzee alikuwa na ugonjwa wa kansa lakini hakuwa amemwambia ye yote. Alihitaji msaada wa kuhamisha vitu vyake vya kibinafsi mahali palipokuwa umbali wa maili moja. Badala ya kuwaambia wengine uhitaji wake, mwanamke huyo alitafuta msaada wa rafiki mwenye umri wa miaka 84. Wakiwa pamoja walipanga vitu kwenye mkokoteni na kujaribu kuusukuma wao wenyewe. Hata hivyo, upesi, waling’amua kwamba hawangeweza kufanya kazi hiyo, na rafiki ya mjane huyo alimwendea mzee aliyekuwa karibu ili apate msaada.
Basi, huenda ikahitaji busara fulani lakini kuendelea kuuliza-uliza bila kubadilika kwa upande wetu ili kuamua ni jambo gani linaloweza kufanywa kuwasaidia watu hao. Ikiwa tunajitoa kwa njia isiyo ya waziwazi, kama vile: ‘Ikiwa unahitaji kitu fulani, unijulishe,’ huenda kukawa na itikio fupi na la haraka: ‘Asante, lakini sihitaji cho chote.’ Ingawaje, kumbuka kwamba Lidia alipoonyesha mtume Paulo na wengine ukarimu, yeye hakuzuiwa na katao lao mara ya kwanza lililoonekana wazi. Bali, ‘aliwashurutisha.’ (Matendo 16:15) Kwa hiyo uwe mwenye kuendelea kuuliza-uliza bila kubadilika. Tafuta mambo ambayo walio na umri mkubwa wanahitaji na kupenda kabla hawajalazimika kuomba msaada.
Bila shaka, walio na umri mkubwa wanahitaji kuwa wenye kuthamini jitihada za wengine na wasiwe wepesi kukasirika, wenye kudai mno, au wenye kulaumu-laumu. Mathalani, ikiwa njia ya kusafiri inaandaliwa, kujitoa kulipia gharama za kusafiri kungefaa sana. Dada mmoja mzee-mzee hupika keki na kuwashonea wanaompeleka kwenye mikutano zawadi ndogo-ndogo. Ingawaje, katika visa vingi, kupiga asante tu ndilo jambo linalohitajiwa.
Leo, Wakristo wanajitahidi kutii amri inayopatikana kwenye Mambo ya Walawi 19:32: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee.” Watumishi wa Yehova hawafuati mtindo wa ulimwengu wa kuwakatalia mbali watu wazee na kuepuka daraka la kuwapenda wazazi. Badala yake, wakati unavyopita, kwa kuwa na subira, na msaada wa Yehova, Wakristo wanajitahidi kukabili takwa gumu la kuwatunza walio na umri mkubwa kati yetu kwa mafanikio.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mara nyingi vijana walio kundini wanaweza kufanya mengi kuwasaidia watu walio na umri mkubwa