Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • fy sura 14 kur. 163-172
  • Kuzeeka Mkiwa Pamoja

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzeeka Mkiwa Pamoja
  • Siri ya Furaha ya Familia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • BADILIKANA NA HALI YA KUJITEGEMEA YA WATOTO WAKO
  • KUIMARISHA TENA KIFUNGO CHENU CHA NDOA
  • FURAHIENI WAJUKUU WENU
  • FANYENI MAREKEBISHO KADIRI MZEEKAVYO
  • KUKABILIANA NA HALI YA KUMPOTEZA MWENZI
  • KUTHAMINIWA NA MUNGU KATIKA UMRI WA UZEE
  • Kuishi Pamoja kwa Upendo
    Amkeni!—1995
  • Ni Yapi Baadhi ya Hayo Matatizo?
    Amkeni!—1995
  • Babu na Nyanya—Shangwe na Magumu Yao
    Amkeni!—1999
  • Babu na Nyanya Wanapokuwa Wazazi
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Siri ya Furaha ya Familia
fy sura 14 kur. 163-172

SURA YA KUMI NA NNE

Kuzeeka Mkiwa Pamoja

1, 2. (a) Ni mabadiliko gani hutukia kadiri umri wa uzee ukaribiavyo? (b) Watu wamwogopao Mungu wa nyakati za Biblia walipataje uradhi katika umri wa uzee?

MABADILIKO mengi hutokea tunapozeeka. Udhaifu wa kimwili hupunguza sulubu yetu. Mtazamo kiooni hufunua makunyanzi mapya na kupungua kwa rangi za nywele hatua kwa hatua—hata kupungua kwa nywele. Huenda tukapatwa na hali ya kusahau-sahau. Mahusiano mapya husitawi wakati watoto wanapooa au wanapoolewa, na tena wakati wajukuu wanapowasili. Kwa watu fulani, kustaafu kazi ya kimwili hutokeza kawaida tofauti ya maisha.

2 Kwa kweli, kuzeeka kwaweza kuwa na magumu. (Mhubiri 12:1-8) Hata hivyo, fikiria watumishi wa Mungu katika nyakati za Biblia. Ingawa hatimaye walishindwa na kifo, walipata hekima na pia uelewevu, uliowaletea uradhi mwingi katika umri wa uzee. (Mwanzo 25:8; 35:29; Ayubu 12:12; 42:17) Wao walifanikiwaje katika kuzeeka wakiwa na furaha? Kwa hakika ilikuwa kwa kuishi kupatana na kanuni ambazo leo tunapata zimerekodiwa katika Biblia.—Zaburi 119:105; 2 Timotheo 3:16, 17.

3. Paulo alitoa shauri gani kwa wanaume na wanawake wenye umri mkubwa?

3 Katika barua yake kwa Tito, mtume Paulo alitoa mwongozo timamu kwa wale wanaozeeka. Yeye aliandika hivi: “Acha wanaume wenye umri mkubwa wawe wenye kiasi katika mazoea, wachukua-mambo kwa uzito, timamu katika akili, wenye afya katika imani, katika upendo, katika uvumilivu. Hivyohivyo acha wanawake wenye umri mkubwa wawe wenye kuhofu Mungu katika tabia, si wachongezi, wala waliofanywa watumwa wa divai nyingi sana, walimu wa lililo jema.” (Tito 2:2, 3) Kutii maneno haya kwaweza kukusaidia ukabili magumu ya kuzeeka.

BADILIKANA NA HALI YA KUJITEGEMEA YA WATOTO WAKO

4, 5. Wazazi wengi huitikiaje watoto wao waondokapo nyumbani, watu fulani hujipatanishaje na hiyo hali mpya?

4 Kubadili madaraka kwataka sifa ya kubadilikana. Hilo huthibitika kuwa kweli kama nini wakati watoto walio watu wazima wanapoondoka nyumbani na kufunga ndoa! Kwa wazazi wengi hicho ni kikumbusha cha kwanza kwamba wanazeeka. Ingawa wanafurahi kwamba wazao wao wamefikia utu mzima, mara nyingi wazazi huwa na wasiwasi kama walifanya yote waliyoweza kuwatayarisha watoto kwa ajili ya hali ya kujitegemea. Na huenda wakawakosa nyumbani.

5 Kwa kueleweka, wazazi huendelea kujihangaisha na hali njema ya watoto wao, hata baada ya watoto kuondoka nyumbani. “Kama tu ningeweza kupata habari kutoka kwao mara nyingi, ili kujihakikishia kwamba wako salama—hilo lingenifurahisha,” akasema mama mmoja. Baba mmoja husimulia hivi: “Binti yetu alipoondoka nyumbani, huo ulikuwa wakati mgumu sana. Hilo liliacha pengo kubwa katika familia yetu kwa sababu sikuzote tulikuwa tumefanya mambo yote pamoja.” Wazazi hawa wamekabilianaje na kutokuwapo kwa watoto wao? Katika hali zilizo nyingi, ni kwa kuonyesha wengine ufikirio na kuwasaidia.

6. Ni jambo gani husaidia kuweka mahusiano ya familia katika mahali payo pafaapo?

6 Watoto wanapofunga ndoa, daraka la wazazi hubadilika. Mwanzo 2:24 hutaarifu hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Italiki ni zetu.) Kutambua kanuni za kimungu za ukichwa na utaratibu mzuri kutasaidia wazazi waweke mambo katika mahali payo pafaapo.—1 Wakorintho 11:3; 14:33, 40.

7. Baba mmoja alisitawisha mtazamo gani bora mabinti wake walipoondoka nyumbani ili waolewe?

7 Baada ya mabinti wawili wa mume na mke fulani kuolewa na kuhama, hao wawili walihisi utupu maishani mwao. Mwanzoni, mume alikuwa na uchungu kuelekea wana-wakwe zake. Lakini alipofikiria kanuni ya ukichwa, aling’amua kwamba waume wa mabinti wake sasa walikuwa na daraka la nyumba zao kila mmoja. Kwa hiyo, mabinti wake walipomwomba awape shauri, aliwauliza maoni ya waume wao, kisha akahakikisha kuwa mwenye kuunga mkono kadiri iwezekanavyo. Sasa wana-wakwe zake humwona kuwa rafiki nao hukubali shauri lake.

8, 9. Wazazi fulani wamebadilikanaje na hali ya kujitegemea ya watoto wao ambao wamekua?

8 Namna gani ikiwa wale ambao wameoana karibuni, ingawa hawafanyi lolote lisilo la Kimaandiko, wanashindwa kufanya lile ambalo wazazi wanaona kuwa jambo lifaalo kabisa? “Sikuzote sisi huwasaidia waone maoni ya Yehova,” waeleza mume na mke fulani walio na watoto ambao wamefunga ndoa, “lakini tusipokubaliana na uamuzi wao, tunaukubali tukiwaunga mkono na kuwapa kitia-moyo chetu.”

9 Katika nchi fulani za Asia, akina mama fulani huliona kuwa jambo gumu sana kukubali hali ya kujitegemea ya wana wao. Hata hivyo, wakistahi utaratibu na ukichwa wa Kikristo, wao huona kwamba kupingana na mabinti-wakwe zao kunapunguzwa. Mwanamke Mkristo mmoja huona kwamba kuondoka kwa wana wake katika nyumba ya familia kumekuwa “chanzo cha shukrani yenye kuongezeka daima.” Anasisimuka kuona uwezo wao wa kusimamia nyumba zao mpya. Kisha, hilo limemaanisha kupunguzwa kwa uzito wa mzigo wa kimwili na wa kiakili ambao yeye na mume wake wanalazimika kuchukua kadiri wanavyozeeka.

KUIMARISHA TENA KIFUNGO CHENU CHA NDOA

Picha katika ukurasa wa 166

Kadiri mzeekavyo, hakikishianeni kupendana kwenu

10, 11. Ni shauri gani la Kimaandiko litakalosaidia watu waepuke baadhi ya mitego ya umri wa makamo?

10 Watu huitikia katika njia mbalimbali wanapofikia miaka ya makamo. Wanaume fulani huvaa tofauti wakijaribu kuonekana wachanga zaidi. Wanawake wengi huwa na wasiwasi kuhusu mabadiliko yaletwayo na koma-hedhi. Kwa kuhuzunisha, watu fulani wa makamo huchochea wenzi wao wawe wenye uchungu na wivu kwa kucheza-cheza na watu wenye umri mchanga wa jinsia tofauti. Lakini wanaume wamwogopao Mungu, walio na umri mkubwa zaidi, wako “timamu katika akili,” wakikinza tamaa zisizofaa. (1 Petro 4:7) Vilevile wanawake wakomavu hujitahidi kudumisha uthabiti wa ndoa zao, kwa sababu ya kupenda waume zao na tamaa ya kumpendeza Yehova.

11 Chini ya upulizio, Mfalme Lemueli alirekodi pongezi kwa ajili ya “mke mwema” anayemthawabisha mume wake na “mema wala si mabaya, siku zote za maisha yake.” (Italiki ni zetu.) Mume Mkristo hatashindwa kuthamini jinsi mke wake hujitahidi kukabiliana na kuudhika kokote kwa hisia-moyo anakopata katika miaka yake ya makamo. Upendo wake utamchochea mume ‘amsifu.’—Mithali 31:10, 12, 28.

12. Waume na wake waweza kukaribianaje zaidi kadiri miaka ipitavyo?

12 Katika ile miaka yenye shughuli ya kulea mtoto, huenda ikawa nyote wawili mliweka kando kwa nderemo tamaa zenu za kibinafsi ili kushughulikia mahitaji ya watoto wenu. Baada ya wao kuondoka ni wakati wa kukazia fikira tena maisha yenu ya ndoa. “Mabinti wangu walipoondoka nyumbani,” asema mume mmoja, “Nilianza mara nyingine tena kutafuta uchumba na mke wangu.” Mume mwingine asema hivi: “Tunahangaikiana afya na kukumbushana uhitaji wa kufanya mazoezi.” Ili wasihisi upweke, yeye na mke wake huonyesha ukaribishaji-wageni kwa washiriki wengine wa kutaniko. Ndiyo, kuonyesha kupendezwa na wengine huleta baraka. Zaidi ya hayo, kwampendeza Yehova.—Wafilipi 2:4; Waebrania 13:2, 16.

13. Kusema waziwazi na kufuatia haki kuna sehemu gani kadiri mume na mke wazeekavyo pamoja?

13 Usiruhusu pengo katika uwasiliano lisitawi kati yako na mwenzi wako. Ongeeni pamoja kwa wazi. (Mithali 17:27) “Tunaongeza kina cha kuelewana kwetu kwa kujali na kuwa wenye ufikirio,” aeleza mume mmoja. Mke wake akubali, akisema: “Kadiri ambavyo umezeeka, tumekuja kufurahia kunywa chai pamoja, kuzungumza, na kushirikiana.” Kusema kwenu waziwazi na kufuatia haki kwaweza kusaidia kutia nguvu kifungo chenu cha ndoa, mkikipa uwezo tena wa kupinga mashambulio ya Shetani, aliye mvunjaji wa ndoa.

FURAHIENI WAJUKUU WENU

14. Kwa wazi nyanya wa Timotheo alikuwa na sehemu gani katika kukua kwake akawa Mkristo?

14 Wajukuu ni “taji” ya wazee-wazee. (Mithali 17:6) Ushirika wa wajukuu waweza kuwa wenye kupendeza kikweli—mchangamfu na wenye kuburudisha. Biblia husema vema juu ya Loisi, nyanya ambaye, pamoja na binti yake Eunike, alishiriki itikadi zake na mwana-mjukuu wake Timotheo kitoto kichanga. Kijana huyo alikua akijua kwamba mama yake na pia nyanya yake walithamini kweli ya Biblia.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.

15. Kwa habari ya wajukuu, ni mchango gani wenye thamani uwezao kufanywa na wazakuu, lakini wao waepuke nini?

15 Hapa, basi, ni sehemu ya pekee ambamo wazakuu (babu na nyanya) waweza kufanya mchango wenye thamani zaidi. Wazakuu, tayari mmeshiriki ujuzi wenu juu ya makusudi ya Yehova pamoja na watoto wenu. Sasa mwaweza kufanya vivyo hivyo na kizazi kinginecho bado! Watoto wachanga wengi husisimuka kusikia wazakuu wao wakisimulia hadithi za Biblia. Bila shaka, hamchukui daraka la baba ili mkazie kikiki kweli za Biblia katika watoto wake. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Bali, mnakamilisha daraka hilo. Sala yenu na iwe ile ya mtunga-zaburi: “Na hata nikiwa ni mzee mwenye mvi, Ee Mungu, usiniache. Hata niwaeleze watu wa kizazi hiki nguvu zako, na kila atakayekuja uweza wako.”—Zaburi 71:18; 78:5, 6.

16. Wazakuu waweza kuepukaje kuwa chanzo cha mkazo unaositawika katika familia yao?

16 Kwa kuhuzunisha, wazakuu fulani huwaendekeza sana watoto wadogo hivi kwamba mikazo husitawika kati ya wazakuu na watoto wao ambao wamekua. Hata hivyo, fadhili yenu ya moyo mweupe huenda labda ikafanya iwe rahisi zaidi kwa wajukuu wenu kuongea nanyi kwa siri wasipohisi mbetuko wa kuwafunulia mambo wazazi wao. Nyakati nyingine vijana hutumaini kwamba wazakuu wao waendekevu watawaunga mkono dhidi ya wazazi wao. Halafu nini? Tumieni hekima na watieni moyo wajukuu wenu waseme waziwazi na wazazi wao. Mwaweza kueleza kwamba kufanya hivyo kwampendeza Yehova. (Waefeso 6:1-3) Ikiwa lazima, huenda mkajitolea kuwafungulia njia vijana hao kwa kusema na wazazi wao. Semeni kwa wazi na wajukuu wenu kuhusu yale ambayo mmejifunza muda wa miaka iliyopita. Kufuatia haki kwenu na kusema kweli kwaweza kuwanufaisha.

FANYENI MAREKEBISHO KADIRI MZEEKAVYO

17. Ni azimio gani la mtunga-zaburi liigwe na Wakristo wanaozeeka?

17 Kadiri miaka ipitavyo, mtaona kwamba hamwezi kufanya yote ambayo mlikuwa mkifanya au yote ambayo mnataka kufanya. Mtu anakabilianaje na mwendo wa kuzeeka? Akilini mwako huenda ukahisi wewe u mwenye umri wa miaka 30, lakini mtupo wa macho kiooni wafunua uhalisi tofauti. Usivunjike moyo. Mtunga-zaburi alimsihi Yehova hivi: “Usinitupe wakati wa uzee, nguvu zangu zipungukapo usiniache.” Nuia kuiga azimio la mtunga-zaburi. Yeye alisema: “Nitatumaini daima, nitazidi kuongeza sifa zake zote.”—Zaburi 71:9, 14.

18. Mkristo mkomavu aweza kufanya utumizi gani wa thamani wa hali ya kustaafu?

18 Wengi wametayarisha kimbele ili kuongeza sifa yao kwa Yehova baada ya kustaafu kazi ya kimwili. “Nilipanga kimbele lile ambalo ningefanya wakati binti yetu alipomaliza shule,” aeleza baba mmoja ambaye amestaafu sasa. “Niliazimia kwamba ningeanza katika huduma ya kuhubiri wakati wote, nami nikauza biashara yangu ili niwe huru kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Nilisali ili nipate kuomba mwelekezo wa Mungu.” Ikiwa unafikia umri wa kustaafu, pata faraja kutokana na tangazo hili la Muumba wetu Mtukufu: “Hata uzee wenu mimi ndiye, na hata wakati wenu wa mvi nitawachukueni.”—Isaya 46:4.

19. Ni shauri gani wanalopewa wale wanaozeeka?

19 Kubadilikana na hali ya kustaafu kazi ya kimwili huenda kusiwe rahisi. Mtume Paulo aliwashauri wanaume wenye umri mkubwa wawe na “kiasi katika mazoea.” Hilo lataka kujizuia kwa ujumla, kutoshindwa na mbetuko wa kutafuta maisha ya starehe. Huenda kukawa na uhitaji hata mkubwa zaidi wa kuwa na kawaida na kujitia nidhamu baada ya kustaafu kuliko wakati wa kabla ya hapo. Basi, mwe na shughuli, “sikuzote [mkiwa] na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.” (1 Wakorintho 15:58) Panueni utendaji wenu mbalimbali ili kusaidia wengine. (2 Wakorintho 6:13) Wakristo wengi hufanya hivyo kwa kuhubiri habari njema kwa bidii wakiwa na mwendo uliorekebishwa. Kadiri mnavyozeeka, mwe “wenye afya katika imani, katika upendo, katika uvumilivu.”—Tito 2:2.

KUKABILIANA NA HALI YA KUMPOTEZA MWENZI

20, 21. (a) Katika mfumo wa mambo uliopo, ni jambo gani ambalo ni lazima hatimaye litenganishe mume na mke? (b) Ana huandaaje kielelezo chema kwa wenzi waliofiwa?

20 Ni jambo la kuhuzunisha lakini ni la hakika kwamba katika mfumo wa mambo uliopo, waume na wake hutenganishwa hatimaye na kifo. Wenzi Wakristo waliofiwa hujua kwamba wapendwa wao wanalala usingizini sasa, nao wana uhakika kwamba watawaona tena. (Yohana 11:11, 25) Lakini hasara hiyo bado hutia kihoro. Yule anayebaki aweza kukabilianaje na hali hiyo?a

21 Kukumbuka lile ambalo mtu fulani katika Biblia alilofanya kutasaidia. Ana alikuwa mjane baada ya miaka saba ya ndoa, na tunaposoma juu yake, alikuwa mwenye umri wa miaka 84. Twaweza kuwa na hakika kwamba alitiwa kihoro alipompoteza mume wake. Yeye alikabilianaje na hali hiyo? Alitoa utumishi mtakatifu kwa Yehova Mungu hekaluni usiku na mchana. (Luka 2:36-38) Maisha ya Ana yenye utumishi wa sala bila shaka yalipunguza sana huzuni na upweke aliohisi akiwa mjane.

22. Wajane fulani wa kike na wa kiume wamekabilianaje na upweke?

22 “Ugumu mkubwa zaidi kwangu umekuwa kutokuwa na mwenzi wa kuongea naye,” aeleza mwanamke mwenye umri wa miaka 72, aliyekuwa mjane miaka kumi iliyopita. “Mume wangu alikuwa msikilizaji mzuri. Tulikuwa tukiongea kuhusu kutaniko na ushiriki wetu katika huduma ya Kikristo.” Mjane mwingine asema: “Ingawa wakati huponya, nimeona kwamba ni sahihi zaidi kusema kwamba lile ambalo mtu hufanya na wakati wake ndilo humsaidia apone. Umo katika hali bora zaidi kusaidia wengine.” Mjane mwanamume mwenye umri wa miaka 67 hukubali, akisema: “Njia nzuri ajabu ya kukabiliana na hali ya kufiwa ni kujitoa mwenyewe katika kufariji wengine.”

KUTHAMINIWA NA MUNGU KATIKA UMRI WA UZEE

23, 24. Biblia hutolea faraja gani kubwa wale wenye umri mkubwa, hasa wale ambao wamekuwa wajane?

23 Ingawa kifo kinamwondoa mwenzi mpendwa, Yehova huendelea kuwa mwaminifu, hakika sikuzote. “Neno Moja nimelitaka kwa BWANA,” akaimba Mfalme Daudi wa zamani, “nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu, niutazame uzuri wa BWANA, na kutafakari hekaluni mwake.”—Zaburi 27:4.

24 “Heshimu wajane ambao ni wajane kwelikweli,” ahimiza mtume Paulo. (1 Timotheo 5:3) Shauri linalofuata agizo hili laonyesha kwamba wajane wanaostahili wasio na watu wa ukoo wa karibu huenda wakawa walihitaji utegemezo wa kimwili kutoka kwa kutaniko. Hata hivyo, maana ya agizo la ‘kuheshimu’ latia ndani wazo la kuwathamini. Wajane wa kike na wa kiume wamwogopao Mungu waweza kupata faraja iliyoje kutokana na kujua kwamba Yehova huwathamini na atawategemeza!—Yakobo 1:27.

25. Ni mradi gani ambao bado huendelea kwa wazee-wazee?

25 “Uzuri wa wazee ni kichwa chenye mvi,” Neno la Mungu lililopuliziwa hutangaza. Ni “taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki.” (Mithali 16:31; 20:29) Basi, uwe umefunga ndoa au ni mseja mara nyingine tena, endelea kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwako. Kwa njia hiyo utakuwa na jina zuri na Mungu sasa na taraja la uhai wa milele katika ulimwengu ambamo maumivu ya umri wa uzee hayatakuwako tena.—Zaburi 37:3-5; Isaya 65:20.

a Ili kupata mazungumzo zaidi juu ya habari hii, ona broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

KANUNI HIZI ZA BIBLIA ZAWEZA KUSAIDIAJE . . . WAUME NA WAKE KADIRI WAZEEKAVYO?

Wajukuu ni “taji” ya wazee-wazee.—Mithali 17:6.

Umri wa uzee huenda ukaleta fursa zilizoongezeka za kumtumikia Yehova.—Zaburi 71:9, 14.

Wale wenye umri mkubwa watiwa moyo wawe “wenye kiasi katika mazoea.”—Tito 2:2.

Wenzi waliofiwa, ingawa wametiwa kihoro sana, waweza kupata faraja katika Biblia.—Yohana 11:11, 25.

Yehova huthamini wale wenye umri mkubwa walio waaminifu.—Mithali 16:31.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki