Babu na Nyanya Wanapokuwa Wazazi
“Nilikuwa nimefika tu nyumbani kutoka mkutanoni kwenye Jumba la Ufalme. Mlango ulibishwa kwa nguvu, na huko nje walisimama polisi wawili pamoja na watoto wawili wachafu ambao nywele zao zilikuwa zimesokotwa na ambao walionekana kana kwamba hawakuwa wameoshwa kwa miezi kadhaa. Hungeweza kutambua kamwe kwamba walikuwa watoto! Walikuwa wajukuu wangu, na mama yao—mraibu wa dawa za kulevya—alikuwa amewatupa. Nilikuwa mjane, na tayari nilikuwa na watoto sita. Lakini singeweza kukataa kuwachukua.”—Sally.a
“Binti yangu aliniuliza ikiwa ningewachukua watoto wake hadi arekebishe maisha yake. Sikujua kwamba alikuwa mraibu wa dawa za kulevya. Niliishia kuwalea watoto wake wawili. Miaka kadhaa baadaye, binti yangu alipata mtoto mwingine. Sikutaka kumchukua, lakini mjukuu wangu wa kiume alinisihi, akisema, ‘Nyanya, je, hatuwezi kukubali mmoja zaidi?’”—Willie Mae.
HALI ya kuwa babu na nyanya ilikuwa ikifafanuliwa kuwa “raha bila madaraka.” Lakini haifafanuliwi hivyo tena kamwe. Wengine wanakadiria kwamba katika Marekani peke yake, watoto zaidi ya milioni tatu huishi na babu na nyanya yao. Na idadi hiyo inazidi kuongezeka.
Ni nini kinachochangia mwelekeo huu wenye kuhuzunisha? Watoto ambao wazazi wao wanatalikiana waweza kuishia kuishi pamoja na babu na nyanya yao. Vivyo hivyo, jambo hili laweza kuwapata watoto ambao wametupwa au waliotendwa vibaya na wazazi wao. Jarida Child Welfare lasema kwamba kwa sababu uraibu huwafanya wazazi washindwe kutekeleza wajibu wao, ‘kokeini yenye nguvu inatokeza kizazi kilichopotoka.’ Pia kuna mamilioni ya watoto “wasio na wazazi” kwa sababu ya kutupwa, kifo cha wazazi, na maradhi ya akili. Watoto ambao mama zao wanauawa na UKIMWI waweza pia kuishia kutunzwa na babu na nyanya yao.
Kutwaa madaraka ya kulea watoto wakati wa “siku zilizo mbaya” za uzeeni kwaweza kulemea. (Mhubiri 12:1-7) Kwa wazi watu wengi hawana nguvu za kukazia uangalifu wa kutosha watoto wadogo. Babu na nyanya wengine pia wanawatunza wazazi wao wanaozeeka. Na bado wengine ni wajane au wametalikiana na wanalazimika kuishi bila utegemezo wa mwenzi. Na wengine wanapata kwamba hawako tayari kifedha kutwaa mzigo huo. Katika uchunguzi mmoja, babu na nyanya watunzaji 4 kati ya 10 walikuwa na mapato yanayokaribia kufikia kiwango cha ufukara. “Watoto walikuwa wagonjwa,” akumbuka Sally. “Nililazimika kulipa pesa nyingi sana kwa dawa. Sikupata msaada wowote kutoka kwa serikali.” Mwanamke mmoja mzee-mzee akumbuka hivi: “Nililazimika kutumia malipo yangu ya uzeeni kuwatunza wajukuu wangu.”
Mikazo na Shida
Haishangazi kwamba, uchunguzi mmoja ulifunua kwamba “kutunza wajukuu kulisababisha mkazo mkubwa kwa babu na nyanya, huku asilimia 86 ya babu na nyanya 60 waliofanyiwa uchunguzi wakiripoti kuwa ‘wameshuka moyo au kuhangaika wakati mwingi.’” Kwa kweli, wengi huripoti kuwa na matatizo ya afya. “Kuliniathiri kimwili, kiakili, na kiroho,” asema Elizabeth, mwanamke aliyemtunza mjukuu wake wa kike. Willie Mae, anayesumbuliwa na matatizo ya moyo na msukumo mkubwa wa damu, asema: “Daktari wangu anaamini kwamba unahusiana na mkazo wa kulea watoto.”
Wengi hawako tayari kubadilika ili kufaana na mtindo-maisha wa kulea watoto. “Kunakuwa na pindi ambapo siwezi kwenda mahali,” asema babu mmoja. “Ningehisi kuwa na hatia . . . kuwaacha na mtu mwingine, hivyo badala ya kwenda mahali fulani au kufanya jambo fulani, siendi au silifanyi.” Mwingine alifafanua wakati wa kufanya mambo yake ya kibinafsi kuwa “haupo.” Kujitenga na wengine na upweke ni mambo ya kawaida. Nyanya mmoja alisema: “Katika rika letu wengi wa marafiki zetu hawana watoto [wachanga] na kama tokeo mara nyingi hatukubali mialiko ya kwenda kwa sababu watoto wetu [wajukuu] hawajaalikwa.”
Mikazo ya kihisia-moyo husababisha maumivu pia. Yasema makala moja katika U.S.News & World Report: “Wengi wao [babu na nyanya] wanasumbuliwa na aibu na hatia ya kwamba watoto wao wameshindwa kufanikiwa wakiwa wazazi—na wengi hujilaumu, wakishangaa ni wapi walipokosea wakiwa wazazi. Ili waweze kuandaa makao salama na yenye upendo kwa wajukuu wao, babu na nyanya fulani wanalazimika kuwaondoa akilini watoto wao wenye kutenda vibaya au waraibu wa dawa za kulevya.”
Uchunguzi mmoja waripoti kwamba: “Zaidi ya sehemu moja kwa nne . . . walisema kwamba uradhi wao katika uhusiano wa ndoa ulipungua likiwa tokeo la kuandaa utunzaji.” Mara nyingi waume hasa, huhisi kuwa wametupwa huku wake zao wakibeba fungu kubwa katika kuwatunza watoto. Waume fulani huhisi kwamba hawawezi kung’ang’ana na mkazo huo. Mwanamke mmoja asema hivi kuhusu mume wake: “Alitutupa. . . . Nafikiri alihisi tu akiwa katika hali ambayo hangeweza kujiepusha nayo.”
Watoto Wenye Hasira
Lasema U.S.News & World Report: “Mikazo hiyo inaongezwa na uhakika wa kwamba baadhi ya watoto ambao [babu na nyanya] hurithi ni miongoni mwa watoto wanaohitaji sana utegemezo wenye upendo, waliovurugika zaidi kihisia-moyo na wenye hasira zaidi katika nchi.”
Mfikirie mjukuu wa kike wa Elizabeth. Baba ya mtoto huyo alimtupa kihalisi kwenye pembe moja ya barabarani ambapo Elizabeth alikuwa akifanya kazi ya kusaidia kuvusha watoto. “Yeye ni mtoto mwenye hasira,” asema Elizabeth. “Ameumizwa.” Wajukuu wa Sally wamepatwa na madhara kama hayo. “Mjukuu wangu wa kiume amefungia kinyongo. Anahisi kwamba hakuna mtu yeyote anayemtaka.” Kuwa na baba na mama mwenye upendo ni haki ya kuzaliwa ya mtoto. Ebu wazia jinsi mtoto anavyohisi anapotupwa, anapoachiliwa, au anapokataliwa nao! Kuelewa hisia hizi kwaweza kuwa ufunguo wa kushughulika kwa njia ya saburi na watoto wanaositawisha matatizo ya kitabia. Mithali 19:11 yasema: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.”
Kwa kielelezo, mtoto aliyetupwa aweza kukinza jitihada zako za kumtunza. Kuelewa hofu za mtoto na mahangaiko yake kwaweza kukusaidia umtendee kwa huruma. Labda kukiri hofu zake na kumhakikishia kwamba utafanya yote uwezayo kumtunza kutasaidia sana kupunguza hofu yake.
Kukabiliana na Mikazo
‘Nimekuwa nikihisi nimeumizwa sana na kujisikitikia. Hatustahili kupatwa na mambo haya.’ Ndivyo alivyosema nyanya mmoja mlezi. Ikiwa uko katika hali hiyo, waweza kuwa na hisia za namna hiyo. Lakini jambo hilo si lenye kukatisha tumaini. Sababu moja ni kwamba, huenda umri ukapunguza nguvu zako za kimwili, lakini umri ni kitu chenye manufaa, hekima, saburi, na ujuzi vinapohusika. Haishangazi kwamba, uchunguzi ulifunua kwamba “watoto waliolelewa na babu na nyanya peke yao walifanikiwa zaidi walipolinganishwa na watoto katika familia zenye mzazi mmoja wa asili.”
Biblia hutuhimiza ‘tutupe hangaiko letu lote juu ya Yehova, kwa sababu yeye hutujali sisi.’ (1 Petro 5:7) Hivyo, sali daima akupe nguvu na mwongozo, kama alivyofanya mtunga-zaburi. (Linganisha Zaburi 71:18.) Kazia uangalifu mahitaji yako ya kiroho. (Mathayo 5:3) “Mikutano ya Kikristo pamoja na kuhubiria wengine ni mambo yaliyonisaidia niendelee,” asema mwanamke mmoja Mkristo. Inapowezekana, jaribu kufundisha wajukuu wako njia za Mungu. (Kumbukumbu la Torati 4:9) Kwa hakika Mungu atategemeza jitihada zako za kulea wajukuu “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4.b
Usiogope kutafuta msaada. Mara nyingi marafiki wanaweza kusaidia, hasa ndani ya kutaniko la Kikristo. Sally akumbuka hivi: “Ndugu na dada kutanikoni waliandaa utegemezo kwelikweli. Niliposhuka moyo walikuwapo ili kunitegemeza. Wengine hata walinipa msaada wa kifedha.”
Usiachilie msaada unaoweza kupatikana kutoka kwa serikali. (Waroma 13:6) Kwa kupendeza, kulingana na uchunguzi mmoja uliofanyiwa babu na nyanya, “wengi hawajui ni msaada gani unaopatikana au mahali pa kutafuta msaada.” (Child Welfare) Wafanyakazi wa huduma za jamii na mashirika ya mahali penu yanayosaidia wazee-wazee yaweza kukuelekeza upate huduma zinazosaidia.
Katika visa vingi, babu na nyanya walezi ni miongoni mwa watu wanaopatikana katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Kwa uzuri, nyakati hizi ngumu ni ishara kwamba karibuni Mungu ataingilia kati na kuumba “dunia mpya” ambayo hali zenye msiba zinazopata familia nyingi leo zitapitilia mbali. (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kwa wakati uliopo, babu na nyanya walezi watalazimika kufanya yote wawezayo ili kufanikiwa katika hali yao. Wengi wanafanikiwa sana katika jitihada zao! Sikuzote kumbuka kwamba kujapokuwa kukatishwa tamaa, shangwe yaweza kupatikana. Kwani, huenda ukapata shangwe ya kuwaona wajukuu wako wakiwa wapenda-Mungu walio wanyofu! Je, hustahili kufanya kazi ngumu ili kufanikiwa?
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia (kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.) kina kanuni nyingi za Biblia zenye kusaidia ambazo babu na nyanya walezi wanaweza kutumia kuwalea wajukuu wao.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Masuala ya Kisheria
Kama utachukua hatua za kisheria kuwa mlezi wa mjukuu wako ama la, ni swali linalohitaji kushughulikiwa kwa uangalifu sana na lililo tata. Mtaalamu wa habari hii, Mary Fron aeleza hivi: “Kwa upande mmoja, una haki chache za kisheria bila kuwa mlezi wa mtoto. Katika visa vingi, wazazi wa asili wanaweza kurudi na kumchukua mtoto au watoto wakati wowote. Kwa upande mwingine, babu na nyanya wengi wanasitasita kutafuta kuwa walezi wa mtoto, kwa sababu hiyo inamaanisha kutoa ushahidi mahakamani ya kwamba mtoto wako ni mzazi asiyefaa.”—Good Housekeeping.
Bila haki ya kisheria ya kuwa mlezi mara nyingi babu na nyanya wanapata ugumu wa kuandikisha watoto wao shuleni au hata kuwapatia matibabu. Hata hivyo, kupata malezi, kwaweza kuwa masaibu yenye gharama kubwa, yanayochukua wakati, na yenye kuchosha kihisia-moyo. Na hata yanapopatikana, huenda babu na nyanya wakanyimwa msaada wa kifedha kutoka kwa serikali. Hivyo jarida Child Welfare lawashauri babu na nyanya “watafute mashauri kuhusu mambo ya kisheria kutoka kwa wakili aliye na uzoefu katika sheria ya familia ya nchi, kesi za malezi, na hali njema ya mtoto.”
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Kuhesabu Gharama
Kumwona mtoto akiwa katika uhitaji—hasa aliye wa jamaa yako—ni jambo la kuhuzunisha sana. Na Biblia huwaamuru Wakristo wawatunze ‘walio wao wenyewe.’ (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, katika hali nyingi nyanya au babu atakuwa mwenye hekima kufikiria jambo hili kwa uzito kabla hajachukua daraka hili. (Mithali 14:15; 21:5) Lazima mtu ahesabu gharama.—Linganisha Luka 14:28.
Fikiria mambo haya kwa sala: Je, uko tayari kimwili, kihisia-moyo, kiroho, na kifedha kutimiza mahitaji ya mtoto huyu? Mwenzi wako anahisije kuhusu hali hiyo? Je, kuna njia yoyote ya kutia moyo au kusaidia wazazi wa mtoto ili waweze kumtunza mtoto wao wenyewe? Kwa kusikitisha, wazazi fulani wasiowajibika wanafuatia tu mtindo-maisha usio na adili. Nyanya mmoja akumbuka hivi kwa uchungu: “Nilichukua baadhi ya watoto wake. Lakini aliendelea kutumia dawa za kulevya na kuzaa watoto zaidi. Nilifikia mahali ambapo nililazimika kukataa!”
Kwa upande mwingine, usipowajali wajukuu wako, ni nini kitakachowapata? Je, unaweza kukabiliana na mkazo wa kujua kwamba wanatunzwa na wengine, labda na watu usiowajua? Vipi juu ya mahitaji ya kiroho ya watoto? Je, wengine wataweza kuwalea kulingana na viwango vya Mungu? Huenda wengine wakafikia mkataa kwamba kujapokuwa magumu yanayohusika, hawana jingine ila kutwaa daraka hilo.
Haya ni mahangaiko yanayohuzunisha sana, na lazima kila mtu ajiamulie mwenyewe.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Babu na nyanya wengi hupata ugumu wa kutimiza madai ya kulea watoto wadogo
[Picha katika ukurasa wa 10]
Babu na nyanya wenye kumhofu Mungu wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawategemeza katika jitihada zao