Kuishi Pamoja kwa Upendo
Kwa Nyanya na Babu wapendwa,
Je, mu wazima? Nafikiri nina homa.
Asanteni kwa kucheza nami ile siku. Mlikwenda nami kwenye bustani za umma na vyumba vya kuogea vya bafu ya umma. Nilifurahia sana.
Mwaka ujao Februari 11, tutakuwa na wonyesho wa muziki wa shule yetu. Ikiwa mwaweza kuja tena, tafadhali njooni.
Sisi hufurahia sana mnapokuja, Nyanya na Babu.
Tafadhali iweni waangalifu, na sikuzote mkae wazima. Halihewa itakuwa baridi, kwa hiyo iweni waangalifu msipate homa.
Natazamia wakati ujao mtakaokuja na kucheza nami. Tafadhali wasalimuni Yumi na Masaki kwa niaba yangu.
Mika (Mjapani)
JE, MJUKUU wako alipata wakati wowote kukuandikia barua kama hii? Ikiwa ndivyo, ulipoipokea, bila shaka ilikupa shangwe nyingi mno. Barua kama hizo ni uthibitisho wa ujamaa wenye kuvutia na wenye shauku baina ya wazazi-wakuu na wajukuu. Lakini ni nini kinachohitajika ili kuanzisha, kudumisha, na kutia nguvu aina hii ya uhusiano? Na uhusiano huu waweza kuthibitikaje kuwa wenye manufaa kwa vizazi vyote vitatu?
Upendo—“Kifungo Kikamilifu cha Muungano”
Roy na Jean, wazazi-wakuu wawili walio Waingereza, wasema: “Twahisi, kanuni kuu ni kutambua ukichwa na kuwa na uhusiano mwema baina ya mtu na mwenzake katika upendo.” Mashahidi hawa wa Yehova wawili kihususa walinukuu lile andiko kwenye Wakolosai 3:14, New World Translation, ambalo hufafanua upendo wa Kikristo kuwa “kifungo kikamilifu cha muungano.” Upendo hutokeza staha, uangalifu wenye ufikirio, shauku, na umoja wa familia. Baba ajapo nyumbani kutoka kazini, familia yote hukimbia kumlaki ili kumpa ukaribishaji wenye uchangamfu. Ikiwa kuna upendo katika familia, jambo lilo hilo hutukia wazazi-wakuu wafikapo. “Nyanya na Babu ndio hawa!” mtoto aliyesisimka anapaaza sauti. Jioni hiyo, familia inayotia ndani watu wa ukoo wa karibu inaketi chakulani, na babu, akifuata desturi ya kwao, anaketi mahali alipowekewa kwenye mahali panapoketi kichwa cha familia au mgeni anayestahiwa. Je, unaweza kujiona akilini wewe na familia yako katika mandhari hii yenye upendo? Je, nyinyi hufurahia baraka hii?
“Kichwa Chenye Mvi Ni Taji ya Utukufu”
Ni wazi kwamba, upendo na staha kwa wazazi-wakuu lazima vidhihirishwe sikuzote, si tu kwenye pindi za kipekee. Kwa sababu hii ni jambo muhimu kuelimisha watoto kila wakati. Ndani ya familia watoto hujifunza kupenda watu wa ukoo na wengine, wakifuata kigezo kilichowekwa na wazazi wao. Kielelezo chao ni cha msingi, kama ilivyotajwa na wengi wa wale waliohojiwa juu ya jambo hili. Macaiah, baba fulani kutoka Benin City, Nigeria, asema hivi: “Nafikiri kielelezo changu cha kustahi wazazi-wakwe wangu pia kimesaidia watoto wangu wawe wanyenyekevu na wenye staha. Mimi huwaita wazazi-wakwe wangu ‘Daddy’ na ‘Mummy.’ Watoto wangu wanasikia na kuona kwamba ninawaheshimu wazazi-wakwe kama wazazi wangu wenyewe.”
Ikiwa wajukuu wanakosa kustahi wazazi-wakuu wao, wazazi-wakuu huenda wakakasirika, sanasana si kwa sababu ya kosa lenyewe bali kwa sababu ya uhakika wa kwamba wazazi hawawarekebishi hao wajukuu. Demetrio, babu fulani kutoka Rome, Italia, asema hivi: “Naweza kuona upendo ambao binti na mwana-mkwe wangu wanatuonyesha kwa njia wanayoelimisha wajukuu wetu kutuheshimu na kutustahi.” Mara kwa mara, wajukuu huenda wakawatendea wazazi-wakuu katika njia ya kuzoeana kupita kiasi, kama kwamba wazazi-wakuu ni wenzi wa kucheza wa rika moja nao, au kwa mtazamo wa kujiona kuwa bora. Ni daraka la wazazi kusahihisha mwelekeo wowote kama huo. Paul, Shahidi fulani Mnigeria, asema hivi: “Mwaka mmoja hivi uliopita, watoto walianza kumdharau mama yangu. Nilipogundua hili, niliwasomea Mithali 16:31: ‘Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu,’ na niliwakumbusha pia kwamba Nyanya ni mama yangu. Jinsi wanavyoniheshimu, wanapaswa kumheshimu yeye pia. Pia nilijifunza nao sura ya 10 ya kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako,a iliyokuwa na kichwa ‘Wewe Unawaonaje Wazazi Wako?’ Sasa, hawana tatizo lolote katika kustahi nyanya yao.”
Manufaa za Kusitawisha Mahusiano ya Familia
Shauku ya kirafiki yaweza kusitawishwa hata wakati washiriki wa familia huishi mbali kutoka kwa mmoja na mwingine. Stephen, babu fulani Mnigeria, asema hivi: “Sisi huandika barua kwa kila mmoja wa wajukuu wetu mmoja-mmoja. Kazi hii ni yenye kudai, lakini thawabu katika kujenga na kudumisha ujamaa wa karibu pamoja na wajukuu imekuwa kubwa mno.” Jitihada za wazazi ni za maana kuhusu jambo hili. Wengine, kulingana na hali zao, hudumisha mawasiliano kupitia simu.
Giuseppe, babu fulani kutoka Bari, Italia, aliye na wajukuu 11, aeleza jinsi yeye husitawisha urafiki mchangamfu pamoja na washiriki wake wa karibu wa familia: “Kwa wakati huu, watatu kati ya sita wanaofanyiza ‘kabila’ langu huishi mbali sana. Lakini hicho si kizuizi kwa mahusiano yenye kupendeza na vikusanyiko miongoni mwetu. Tuna kawaida ya kukutana pamoja angalau mara moja kwa mwaka, sote 24.”
Wazazi-wakuu wanapoishi peke yao, ikiwa kutembeleana, kupigiana simu, au kuandikiana barua pamoja na washiriki wa familia si kwa kawaida, mahusiano yaweza kuwa ya mbali. Shauku lazima ionyeshwe sikuzote. Wazazi-wakuu fulani ambao wana umri wa makamo au wana afya nzuri wanataka kuishi peke yao wakiwa bado na nguvu na wawezao kujitegemeza. Hata hivyo, ikiwa wanajitenga kabisa kutoka washiriki wa familia, huenda wakapata kwamba wakati uhitaji wao wa shauku ni mkubwa zaidi, huenda wasiipate mara hiyo.
Dokezo jingine lenye msaada latoka kwa Michael, babu fulani Mnigeria: “Mimi hutumia Kanuni ya Kidhahabu ya Yesu—kuwatendea wengine kile utakacho wakutendee. Kwa sababu hiyo watoto wangu wananipenda sana. Twafurahia uwasiliano mwema.” Yeye aongeza hivi: “Ikiwa wowote wa wajukuu wangu wanafanya jambo linikasirishalo, mimi huzungumza nao ikiwa ni lazima. Lakini ikiwa ni jambo ambalo naweza kupuuza, mimi kwa kawaida hulisahau tu.”
Zawadi ndogo-ndogo na ishara ndogo-ndogo kwa upande wa wazazi-wakuu hutokeza tendo-itikio lifaalo. Maneno yenye fadhili na yenye kutia moyo, badala ya malalamiko ya daima, hufanya maisha ya familia yafurahishe. Kuweka kando wakati kwa ajili ya wajukuu, kuwafundisha michezo yenye kufurahisha na kazi ndogo-ndogo zenye manufaa, kuwahadithia hadithi za Biblia au hekaya fupi za kifamilia, hufanyiza kumbukumbu changamfu na zenye kudumu. Mambo hayo madogo lakini ya maana hufanya maisha yafurahishe zaidi.
Manufaa za Kustahiana
“Wazazi-wakuu,” asema daktari Gaspare Vella, “wanahitaji kuwa waangalifu wasije wakapinga au kushindana na mamlaka ya wazazi ya kulea watoto.” “Au sivyo,” yeye aongeza, “wanavuka eneo lao la utendaji wakiwa wazazi-wakuu na kuchukua mahali pa wazazi.” Dokezo hili lapatana na yasemayo Maandiko, kwamba wazazi wana daraka la msingi la kuzoeza watoto wao.—Mithali 6:20; Wakolosai 3:20.
Kwa sababu ya uzoefu wao katika maisha, ni rahisi kwa wazazi-wakuu kutoa shauri. Hata hivyo, ni lazima watahadhari katika kutotoa shauri lisilotakikana na nyakati fulani lisilopokelewa vyema. Roy na Jean wasema hivi: “Ni muhimu kuelewa kwamba wazazi wana daraka la kwanza la kuzoeza na kutia nidhamu watoto wao. Nyakati fulani mtu aweza kuhisi kwamba wameweka viwango vigumu sana na katika visa vingine hawaweki viwango vigumu vya kutosha. Hivyo kuna uhitaji wa kushindana na kishawishi halisi cha kujiingiliza.” Michael na Sheena, wazazi-wakuu wengine wawili wa Uingereza, wanathibitisha hoja hiyohiyo: “Ikiwa watoto wanaomba shauri letu, tutalitoa, lakini hatutazamii kwa uhakika kwamba watalikubali, wala hatukasiriki wasipolikubali.” Ni vema kwa wazazi wazee-wazee kuwa na matumaini katika wana na mabinti wao waliooana. Matumaini hayo huboresha mahusiano miongoni mwa hivyo vizazi vitatu.
Vivian na Jane, ambao huishi kusini mwa Uingereza, hujitahidi kutegemeza nyakati zote nidhamu itolewayo na mwana wao na binti-mkwe kwa wajukuu wao, ambao huishi nao: “Hatujaribu kuweka mawazo yetu wenyewe mahali ambapo twahisi tofauti. Wakitambua kwamba twaunga mkono mama na baba yao, watoto hawajaribu kamwe ‘kushindanisha kwa ujanja wazazi-wakuu dhidi ya wazazi.’” Hata wakati ambapo wazazi hawako, wazazi-wakuu lazima watahadhari kuhusu kutia nidhamu wajukuu. Harold kutoka Uingereza, asema hivi: “Nidhamu yoyote ionekanayo na wazazi-wakuu kuwa inahitajika wakati wazazi hawapo yapaswa kuwa ilizungumziwa kimbele pamoja na wazazi.” Harold aongeza kwamba neno la fadhili, lakini imara, kwa wajukuu au kikumbusha tu cha “kile ambacho mzazi angehitaji” mara nyingi hutosha.
Wakati Christopher, babu Mnigeria, aonapo makosa kwa upande wa watoto wake mwenyewe, yeye huepuka kusema kuyahusu wakati wajukuu wake wapo: “Mimi hutoa shauri lolote la lazima wakati tuko peke yetu na hao wazazi.” Wazazi nao vilevile, wanahitaji kufanya sehemu yao katika kuhakikisha kwamba fungu la wazazi-wakuu lastahiwa. “Ni jambo la msingi,” asema Carlo, kwa baba anayeishi Rome, Italia, “kutolalamika kamwe kuhusu mapungukio ya wazazi-wakuu au washiriki wengine wa familia mbele ya watoto.” Hiroko, mama Mjapani, asema hivi: “Tatizo lizukapo na wakwe zangu, mimi hulizungumza kwanza pamoja na mume wangu.”
Fungu la Kielimu la Wazazi-Wakuu
Kila familia ina historia yayo yenyewe, desturi na maono ambayo huitofautisha kutoka nyingine zote. Kwa ujumla, wazazi-wakuu ndio kiunganishi cha kumbukumbu la kihistoria la familia. Kulingana na msemo mmoja wa Kiafrika, “kila mwanamume mzee afaye ni maktaba inayoteketea.” Wazazi-wakuu hupitisha kumbukumbu za watu wa ukoo na matukio ya muhimu ya familia, na vilevile kanuni za familia ambazo mara nyingi huunganisha familia penye mizizi yayo. Bila kutia ndani mwongozo wa adili ambao Biblia hutoa, mtaalamu mmoja alisema kwamba ikiwa “vijana hawana ujuzi wowote wa historia ya familia, wanakua bila msingi wa maono ambayo yaliwatangulia, wakiwa na utovu wa kanuni, bila kujitumaini na walio na mashaka katika mahusiano na wengine.”—Gaetano Barletta, Nonni e nipoti (Wazazi-wakuu na Wajukuu).
Wajukuu hupenda kusikia hadithi ya wakati mama na baba na watu wengine wa ukoo walipokuwa wachanga. Kutazama kiwekeo cha picha kwaweza kuelimisha na kufurahisha sana. Ni wororo na uchangamfu ulioje utakaokuwa ukitokezwa wazazi-wakuu wanapohadithia hadithi za matukio yaliyopita kama yanavyoonyeshwa katika picha.
Reg na Molly, wazazi-wakuu wawili Waingereza ambao ni Mashahidi wa Yehova, wasema hivi: “Furaha imetujia kupitia kuweza kuwa katika ushirikiano na wajukuu na kufanya mambo pamoja nao, bila kujiingiliza kwenye muungano wao wa karibu pamoja na mama na baba, tukijibu maswali yao mengi, kucheza pamoja, kusoma pamoja, kuwaonyesha jinsi ya kuandika, kuwasikia wakisoma, kufuatia kwa ukaribu mambo yao ya shule kwa upendezi wenye upendo.”
Kosa zito sana ambalo wazazi-wakuu wengi hufanya ni lile la kuhangaikia tu hali-njema ya kimwili ya watoto na wajukuu wao. Reg na Molly waliotajwa hapo juu, wasema hivi: “Urithi mkubwa kupita wote tuwezao kuwapa watoto na wajukuu ni kuhakikisha wanalelewa katika ujuzi wa kweli wa Neno la Mungu.”—Kumbukumbu la Torati 4:9; 32:7; Zaburi 48:13; 78:3, 4, 6.
Kutenda Kupatana na Ufundishaji wa Kimungu
Biblia Takatifu, Neno la Mungu, “lina nguvu” juu ya watu. Lina uwezo wa kuwasaidia kudhibiti au kuondoa vitabia vya kugawanya, kama vile ubinafsi na kiburi. (Waebrania 4:12) Kwa hivyo, wale wanaotumia mafundisho yalo, hufurahia amani na umoja katika familia. Moja ya maandiko kadhaa ambayo husaidia hivyo vizazi vitatu kuondoa tofauti kubwa katika mtazamo ambayo huenda ikawa kati yao ni Wafilipi 2:2-4, ambalo hutia moyo wote kudhihirisha upendo na unyenyekevu, kudumisha umoja, ‘kuangalia si mambo yao wenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’
Wakitenda kupatana na ufundishaji wa kimungu, wazazi na wajukuu wote wanachukua kwa uzito himizo la “kufuliza kulipa wazazi na wazazi-wakuu wao malipo yapasayo,” kimwili, kihisia-moyo, na kiroho. (1 Timotheo 5:4, NW) Wakiwa na hofu ya Yehova ifaayo, wao wanadhihirisha staha ya kina kwa wazazi-wakuu, wakikumbuka maneno yake: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee; nawe mche Mungu wako.” (Mambo ya Walawi 19:32) Wazazi-wakuu wanadhihirisha wema kwa kuelekeza jitihada zao kwa hali-njema ya wazao wao: “Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi.”—Mithali 13:22.
Wazazi-wakuu, wazazi, na wajukuu, iwe wanaishi pamoja au sivyo, wanaweza kupata manufaa pamoja katika mahusiano yenye shauku yanayotegemea upendo na staha, kama tu Mithali 17:6 isemavyo: “Wana wa wana ndio taji ya wazee, na utukufu wa watoto ni baba zao.”
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Kukutana pamoja tena kwa familia kwaweza kuchangia umoja wa familia
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wazazi-wakuu wako wanatiwa moyo unapowaandikia barua
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kutazama kwa kupitia kiwekeo cha picha cha familia pamoja na wajukuu wako kwaweza kuwa ono lenye kutajirisha