‘Asante kwa Kunileta Nyumbani, Mama’
SIKUZOTE nilikuwa mwenye wasiwasi wakati Glen, mume wangu, aliporuka kwa ndege, na nilitamani aje nyumbani. Kwa kawaida yeye aliruka kwa ndege ili kufurahia tu. Wakati huu alikuwa amekodiwa ili kupiga picha za kutoka angani. Mwana wetu mchanga zaidi, Todd, aliandamana naye. Glen sikuzote alikuwa rubani mwangalifu na hakujihatarisha kamwe isivyofaa.
Simu ilipolia Jumapili hiyo alasiri, Aprili 25, 1982, niliijibu kwa hisi ya kutazamia matokeo mabaya. Ilikuwa ndugu-mkwe wangu. “Glen na Todd wamekuwa katika aksidenti ya ndege,” yeye akasema. “Tutakutana nawe kwenye hospitali.”
Mwana wangu mwenye umri wa miaka 13, Scott, nami tulisali na kukimbia hospitali. Tulipofika, tulipata kujua kwamba ndege ya Glen ilianguka yapata kilometa 100 magharibi mwa New York City. (Kisababishi hasa cha kuanguka huko hakikutambuliwa kamwe.) Glen na Todd walikuwa hai lakini katika hali mahututi.
Nilitia sahihi fomu za kisheria nikipatia hospitali ruhusa ya kuandaa utibabu uliohitajika. Lakini nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, singekubali utumizi wa utiaji-damu mishipani. Kufanya hivyo kungevunja amri ya Biblia ya ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:28, 29) Glen alikuwa na hati ya kitiba ambayo ilitaarifu waziwazi usadikisho wake kuhusiana na hili. Hata hivyo, tulipatia madaktari ruhusa ya kutumia vitanua kiasi visivyo na damu.a
Glen alikuwa na majeraha makubwa na mabaya sana ya kichwa na kifua. Yeye alikufa mnamo saa chache. Jambo gumu kuliko yote ambalo nilikuwa nipate kulifanya wakati wowote katika maisha yangu lilikuwa kutembea kuingia ndani ya chumba cha kungojelea na kumweleza mwana wangu Scott kwamba baba yake alikuwa amekufa. Yeye alinizungushia mikono na kusema hivi: “Nitafanya nini sasa? Nimetoka tu kumpoteza rafiki yangu bora zaidi!” Ndiyo, Glen alikuwa amekuwa rafiki bora zaidi kwa wana wake wawili, akitumia wakati pamoja nao katika tafrija na katika ibada. Yeye pia alikuwa rafiki yangu bora zaidi na mume wangu. Kifo chake kilikuwa potezo baya zaidi.
Kudumisha Itikadi Zetu
Todd alikuwa amevunjika mguu na kidole, kupondeka mifupa ya mashavuni, na alikuwa na majeraha mabaya mno ya ubongo. Yeye alitokomea katika koma. Jinsi ilivyokuwa vigumu kumtazama mwana wangu mwenye umri wa miaka tisa, ambaye saa chache tu zilizopita alikuwa mwenye uchangamfu tele! Sikuzote Todd alikuwa kijana mdogo mwenye utendaji ipendezavyo. Alikuwa mwongeaji na alipenda kuimba na kucheza. Sasa alikuwa hata hatambui kuwapo kwetu.
Wakihofia kwamba huenda Todd akahitaji upasuaji, madaktari walidai kwamba nikubali utiaji-damu mishipani. Nilikataa. Waliitikia kwa kupata amri ya mahakama ya kuwaruhusu kutumia damu. Ingawa hivyo, ilitokea kwamba upasuaji haukuwa wa lazima, na Todd hakuwa amevuja damu kwa ndani. Hata hivyo, siku chache baadaye, niliambiwa na madaktari kwamba kwa vyovyote walikuwa watampa damu. Tulishangaa! “Tunahitaji kufanya hilo tu!” lilikuwa ndilo elezo pekee alilotupa daktari wake. Walipuuza itikadi zetu za kidini na kumpa Todd yuniti tatu za damu. Nilijihisi kutokuwa na uwezo kabisa.
Kwa siku kadhaa kufuatia hiyo aksidenti, habari yetu ilitokea kwenye ukurasa wa mbele wa magazeti. Gazeti la mahali petu lilifanya wasomaji waamini kwamba Glen alikufa kwa sababu alikuwa amekataa damu na hata likamnukuu daktari wa hapo ambaye alieleza maoni hayo! Jambo hili halikuwa kweli. Mchunguzi wa miili ili kupata kisababishi cha kifo alihakikisha baadaye kwamba Glen hangeliweza kuokoka majeraha yake makubwa na mabaya ya kichwa na kifua. Kwa uzuri, wahudumu kadhaa Mashahidi walikaribishwa na kituo cha redio cha kwetu ili kueleza msimamo wetu unaotegemea Biblia. Hili lilitokeza ushahidi mzuri, na msimamo wa Mashahidi wa Yehova juu ya damu ukawa kichwa cha mazungumzo cha kawaida katika huduma ya mlango kwa mlango.
Jitihada za Kumhuisha Todd
Todd alibaki katika koma. Halafu Mei 13 mwuguzi alimgeuza kitandani mwake, na hatimaye akafunua macho yake! Nilimkumbatia na kujaribu kuongea naye, lakini hakukuwa na itikio. Hakuweza hata kupesa macho au kufinya mkono wangu. Lakini kuanzia wakati huo na kuendelea alianza kufanya maendeleo thabiti. Tulipoingia hicho chumba, kichwa chake kingegeuka kuelekea mlango. Tulipomsemesha, alikuwa akituangalia. Je, kweli Todd alijua tulikuwa pale? Hatukujua. Kwa hiyo tulianza kufanya kazi ili kumweka akiwa ameamka kiakili na kimwili. Kuanzia na siku ya kwanza tulimsemesha, kumsomea vitabu, na kumchezea kanda za kimuziki na zinazohusiana na Biblia. Hata nilimpigia gita yangu; ilikuwa tiba kwetu sote.
Tulipata msaada mwingi kutoka kutaniko la Mashahidi wa Yehova la kwetu. Mwana wangu mkubwa zaidi, Scott, majuzi alikumbuka hivi: “Familia mbili zilinikubali nyumbani kwao kama kwamba nilikuwa mwana wao, zikienda nami kwenye likizo pamoja na washiriki wazo.” Isitoshe, wengine walifyeka bustani yetu, kufua nguo zetu, na kutupikia milo. Marafiki na washiriki wa familia pia walipokezana zamu ya kukaa usiku wote na Todd kwenye hospitali.
Ingawa hivyo, kwa majuma mengi Todd hakuwa akiitikia uangalifu huo—si hata kwa tabasamu. Halafu akapatwa na Pneumonia. Madaktari wakaniomba ruhusa ya kumrudisha Todd kwenye mashine ya kusaidia kupumua. Hatari ilikuwa kwa yeye kuitegemea kabisa. Ebu wazia: Uamuzi huu wa uhai-na-kifo uliwekwa mikononi mwangu! Walakini, kuhusiana na utiaji-damu mishipani, matamanio yangu yalikuwa yamepuuzwa kabisa! Kwa vyovyote, tulichagua mashine ya kusaidia kupumua na kutumaini matokeo mazuri.
Alasiri hiyo nilienda nyumbani ili kujitia nguvu. Kwenye bustani yangu ya mbele alisimama ofisa wa serikali. Alitupasha habari kwamba lazima tuuze nyumba yetu ili kuwe na nafasi kwa ajili ya upanuzi wa barabara. Sasa tukawa na tatizo jingine zaidi la kushindana nalo. Sikuzote nilikuwa nimewaambia wengine kwamba Yehova hangetuacha kamwe tupitie hali tusizoweza kushinda. Nilikuwa nikinukuu maneno ya 1 Petro 5:6, 7: “Nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake, huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana na mambo yenu.” Sasa imani na tumaini langu katika Mungu zilikuwa zikiwekwa kwenye mtihani zaidi ya wakati mwingineo wote uliopita.
Majuma yalikuja na kwenda, Todd akipata ambukizo moja baada ya jingine. Siku zilijawa na majaribio ya damu, taratibu za kutoa kimiminiko cha uti kutoka kwenye uti wa mgongo, machunguo ya mifupa, machunguo ya ubongo, taratibu za kutoa kimiminiko mapafuni, na eksi-rei zisizokoma. Kufikia Agosti halijoto ya Todd mwishowe ilirudia kawaida. Katika Agosti waliweza kutoa mirija ya kula na kupumulia ya Todd! Sasa tulikabili tatizo kubwa zaidi ya yote.
Kurudi Nyumbani
Madaktari walituambia kwamba hospitali maalum ingekuwa bora zaidi kwa Todd. Daktari mmoja alitukumbusha kwamba Scott nami tulihitaji kuwa na wakati na nishati kwa ajili yetu wenyewe. Hata rafiki wenye nia njema walisababu vivyo hivyo. Ingawa hivyo, kile walichokosa kutambua kilikuwa kwamba Todd alikuwa sehemu ya maisha yetu! Na ikiwa tungeweza kumtunza nyumbani, angezungukwa na wale waliompenda na walioshiriki imani yake.
Tulinunua gari-magurudumu na kitanda cha hospitali. Kwa msaada wa marafiki fulani, tulivunja ukuta katika chumba changu cha kulala, tukaweka milango ya kuteleza ya kioo, na kujenga eneo lisilo na paa lililo tambarare ambalo lingemwezesha Todd kupelekwa na gari-magurudumu lake hadi kwenye chumba chake cha kulala.
Asubuhi ya Agosti 19, ilikuwa wakati wa kumleta nyumbani mwana wangu aliyekuwa bado nusu katika koma. Todd angeweza kufunua macho yake na kusogeza kidogo mguu na mkono wake wa kushoto, lakini daktari wake alitabiri kwamba hangeboreka zaidi ya hapo. Majuma machache baadaye, tulimpeleka Todd kwa daktari wa tiba ya mfumo wa akili aliyependekezwa sana, na kwa kusikitisha alirudia maneno ya daktari wa Todd. Hata hivyo, ilikuwa hisi ya ajabu kama nini kumleta nyumbani! Mama yangu na rafiki wachache wa karibu walikuwa nyumbani kwetu wakitungoja. Jioni hiyo hata tulikwenda kwenye Jumba la Ufalme pamoja. Hili lilitupa mwonjo wa kwanza wa jitihada kubwa mno ya kile kingehusika katika kumtunza Todd.
Kumtunza Todd Nyumbani
Kutunza mtu asiyejiweza kulithibitika kuwa kwenye kutumia wakati mwingi mno isivyowazika. Ilimchukua Todd zaidi ya saa nzima kula mlo mmoja. Bado hunichukua karibu saa nzima kumwosha kwa kumpangusa, kumvisha, na kuosha nywele zake. Kuoga kwa kitiba kwa mikondo ya maji moto yazungukayo na yenye nguvu kwaweza kumchukua saa mbili nzima. Kusafiri ni kazi kubwa mno, kukihitaji jitihada nyingi za kimwili. Ingawa hivi majuzi amepata nafuu kwa kiwango kikubwa, Todd amekuwa na tatizo kubwa kuketi wima, hata kwa msaada wa kiti-magurudumu kiwezacho kurekebishwa; yeye kwa kawaida amekuwa akilazimika kujinyoosha kwenye sakafu. Kwa miaka mingi niliketi naye kwenye sakafu katika sehemu ya nyuma ya Jumba la Ufalme. Hata hivyo, hatukuacha hili litusimamishe kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kwa ujumla tulifika kwa wakati.
Jitihada zetu zenye subira zimetokeza matokeo. Kwa muda fulani madaktari walifikiri aksidenti ilimfanya Todd kuwa kiziwi na kipofu. Hata hivyo, kabla ya aksidenti nilikuwa nimeanza kufunza wavulana wangu lugha ya ishara. Wakati wa juma la kwanza nyumbani, Todd alianza kuashiria ndiyo au la kwa maswali ambayo tulikuwa tukiuliza. Baadaye alisitawisha uwezo wa kuelekezea kidole. Tulikuwa tukimwonyesha picha za marafiki na kumuuliza atambulishe wengine wao, na alifanya hivyo kwa usahihi. Pia alikuwa akiweza kutambulisha kwa usahihi nambari na herufi. Baadaye tulisonga mbele kwa maneno. Stadi zake za utambulishaji zilikuwa kamili. Katika Novemba, miezi saba tu baada ya aksidenti, tukio lililongojewa kwa muda mrefu lilitukia.
Todd alitabasamu. Kufikia Januari tabasamu yake iliandamana na kicheko.
Kama ukumbukavyo, tulilazimishwa kuuza nyumba yetu. Lakini jambo hilo ingawa lilionekana kuwa baya mara ya kwanza hatimaye liligeuka kuwa baraka, kwa kuwa nyumba yetu ya orofa mbili ilikuwa ndogo na ilizuia mwendo wa Todd. Kwa kuwa tulikuwa na fedha chache tu, ilikuwa iwe vigumu kupata nyumba ambayo ilitosheleza mahitaji yetu. Ingawa mwakilishi mwenye fadhili wa mali katika hali ya majengo na ardhi alipata moja. Nyumba hiyo ilikuwa ya mjane ambaye mke wake alikuwa amekuwa kwenye kiti-magurudumu; nyumba hiyo ilikuwa imebuniwa kwa mahitaji ya mke huyo. Ilimfaa Todd kabisa!
Bila shaka, hiyo nyumba ilihitaji kusafishwa na kupakwa rangi. Lakini tulipokuwa tayari kupaka rangi, zaidi ya marafiki 25 kutoka kutaniko letu walifika, na burashi za rangi mkononi.
Kupambana na Maisha ya Siku-kwa-Siku
Sikuzote Glen alikuwa akishughulikia shughuli za familia, bili, na kadhalika. Niliweza kuchukua sehemu hii ya maisha kwa shida kidogo. Hata hivyo, Glen hakuhisi ilikuwa muhimu kuwa na wosia au bima ifaayo. Tungeliepuka magumu mengi ya kifedha—matatizo yanayoendelea hadi siku hii—ikiwa angelichukua wakati kushughulikia mambo haya. Baada ya ono letu, wengi wa marafiki wetu walianza kupanga shughuli zao kama vile kufanyiza wosia au kupata bima.
Ugumu mwingine ulikuwa kutosheleza mahitaji yetu ya kihisia-moyo na kiroho. Baada ya Todd kuja nyumbani kutoka hospitali, wengine walitenda kama kwamba hilo tatizo lilikuwa limekwisha. Ingawa hivyo, Scott aliendelea kuhitaji msaada na kitia-moyo. Zile kadi, barua, na simu tulizopata zitakuwa kumbukumbu zenye kutamanisha sikuzote. Nakumbuka barua moja kutoka mtu mmoja ambaye alitupa msaada wa kifedha. Hiyo barua ilisema hivi: “Sitaweka jina barua hii, kwa kuwa sitaki mnishukuru lakini mshukuruni Yehova, kwa kuwa yeye ndiye ambaye hutusukuma kuonyeshana upendo.”
Hata hivyo, tumejifunza kutokuwa wenye kutegemea wengine kupita kiasi kwa ajili ya kitia-moyo bali kuchukua hatua chanya katika kujisaidia. Ninapojihisi nikiwa nimeshuka moyo, mara nyingi mimi hujaribu kufikiria wengine. Mimi hufurahia kuoka na kupika, na mara kwa mara, mimi huwatumbuiza marafiki au kuoka tu vitu vichache na kuwapa. Ninapoungua nishati kwelikweli au kuhitaji kipindi cha kitulizo, sikuzote yaonekana mimi hupata mwaliko kwa mlo mkuu, chakula cha mchana, au kwa mwisho-juma pamoja na marafiki. Nyakati fulani, hata mtu hujitolea kukaa pamoja na Todd kwa muda ili niweze kwenda kwenye shughuli kwa niaba ya wengine au dukani.
Mwana wangu mkubwa zaidi, Scott, amekuwa pia baraka ya ajabu. Wakati wowote ilipowezekana, Scott alienda na Todd kwa vikusanyiko vya kijamii. Sikuzote alikuwa tayari kusaidia katika njia moja au nyingine katika utunzaji wa Todd, naye hakulalamika kamwe kuhusu kuwa na daraka kubwa mno. Wakati mmoja Scott alisema hivi: “Ikiwa nyakati fulani najipata nikitamani ningekuwa na maisha ya ‘kawaida’ zaidi, nilikumbuka mara moja kwamba ono langu lilinivuta karibu zaidi na Mungu.” Namshukuru Yehova kila siku kwa kuniruhusu kuwa na mwana mwenye upendo, na mwenye kufikiri mambo ya kiroho. Yeye anatumika katika kutaniko lake akiwa mtumishi wa huduma na afurahia kuwa mweneza-evanjeli wa wakati wote pamoja na mkeye.
Na Todd? Ameendelea kufanya maendeleo mazuri. Mnamo miaka michache, alianza kusema tena. Mara ya kwanza ilikuwa maneno machache, halafu sentensi. Sasa, anaweza hata kutoa maelezo kwenye mikutano ya Kikristo. Anafanyia bidii kusema kwa ufasaha zaidi, na tiba ya usemi imesaidia. Yeye bado apenda kuimba—hasa kwenye Jumba la Ufalme. Yeye pia aendelea kuwa mwenye maoni yafaayo sikuzote. Sasa yeye aweza kusimama kwa msaada wa mfanyizo wa fremu ya vyuma. Wakati fulani uliopita, tulikuwa na fursa ya kueleza ono letu kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova. Alipoulizwa kile angependa kusema kwa marafiki wake wote waliohudhuria, Todd alisema hivi: “Msijali. Nitapata nafuu.”
Twatoa sifa zote kwa Yehova kwa kututegemeza kupitia yote haya. Kwa kweli, tumejifunza kumtegemea zaidi ya wakati wowote uliopita. Usiku wote huo mbalimbali tuliokosa usingizi, kazi yote ngumu iliyohusika katika kushughulikia mahitaji na hali nzuri ya kibinafsi ya Todd, kujidhabihu kote ambako tumefanya kumestahiki sifa kwa Yehova. Wakati fulani uliopita, tulipokuwa tukifurahia kiamsha-kinywa, niliinua kichwa kutazama na nikapata Todd akinitazama akiwa na tabasamu kubwa usoni pake. Yeye alisema hivi: “Nakupenda, mama. Asante kwa kunileta nyumbani kutoka hospitali.”—Kama ilivyosimuliwa na Rose Marie Boddy.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari juu ya maoni ya Biblia kuhusu utiaji-damu mishipani na utumizi wa vifanyizwa visivyo na damu, ona broshua “Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako?” kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 13]
Jambo gumu kuliko yote lilikuwa kumweleza mwana wangu Scott kwamba baba yake alikuwa amekufa
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nikiwa na wana wangu