Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Usingizi Asanteni kwa ile makala “Sababu ya Mwili Wako Kuhitaji Usingizi.” (Juni 8, 1995) Lazima niseme kwamba ilinifundisha. Nikiwa mwanafunzi wa kitiba, napoteza muda wa saa nyingi wenye thamani wa kulala ili nijifunze. Nimepatwa na baadhi ya athari zilizotajwa kwenye hiyo makala. Nitajaribu kusitawisha mazoea mazuri ya kulala usingizi.
L. H., Trinidad
Babu na Nyanya Nililia machozi ya furaha niliposoma ule mfululizo “Je, Wewe Huthamini Babu na Nyanya?” (Julai 8, 1995) Nilikuwa napitia wakati mgumu pamoja na wakwe zangu, kwa hivyo makala yenu ilikuja wakati barabara. Ilinifanya nitambue kwamba sikuwa nikiwatendea kwa staha ifaayo waliyostahili. Nikafanya mabadiliko ya lazima, nasi sasa tu wenye furaha zaidi.
A. T., Kanada
Tulipolazimika kumweka baba yangu kwenye makao ya kutunzia wazee-wazee, tuliazimia kumtembelea mara tatu kila juma. Tumetimiza ahadi hiyo kwa miaka miwili. Habari ndogo-ndogo za kila siku za nyumbani ni zenye maana sana kwake! Inahitaji azimio lenye nguvu kuendelea vivyo hivyo, lakini babu na nyanya pamoja na wajukuu hufaidika.
P. L., Marekani
Nikiwa Mkatoliki, nilipendezwa sana na uhakika wa kwamba makala hizo hazikutolea uangalifu imani au dini badala ya hivyo zilikuwa zisizopendelea. Ninyi mmeshughulikia kwa ujasiri uhitaji ambao kihalisi umepuuzwa.
A. B., Kosta Rika
Msiba wa Familia Nilisoma kwa machozi ile makala “Asante kwa Kunileta Nyumbani, Mama.” (Julai 8, 1995) Mimi pia nilimpoteza mume wangu katika aksidenti katika 1982. Nililemazwa—nikiwa na watoto sita na mama wa kutunza. Kusoma makala hiyo kulikuwa sawa na kusoma hadithi yangu mwenyewe. Yehova hutupa sisi moyo mkuu wa kusonga mbele.
C. R., Marekani
Simulizi hilo liligusa sana moyo wangu. Nina umri wa miaka 16, nami sikuzote nimekuwa nikifikiria jinsi ningeweza kukabiliana na matatizo kama hayo ikiwa yangepata kutokea. Maono ya Todd yamenisaidia kung’amua kwamba Yehova yuko nasi sikuzote maadamu tunamtegemea.
N. F., Dominika
Hilo simulizi lilitolewa vizuri sana hivi kwamba nilikuwa karibu kulia. Majaribu yaliyoipata familia ya Boddy yalifanya vivunja moyo vyangu vidogo kuonekana kuwa visivyo na umaana. Ingawa hali zetu zinatofautiana, kuona jinsi Yehova alivyowatunza kumenisaidia kusonga mbele.
V. S., Filipino
Mume wangu mwenye miaka 33, Shahidi mwaminifu ambaye ametumikia akiwa mzee kwa miaka mingi, ana maradhi ya Pick—ugonjwa wa muda mrefu, wenye kuvunja moyo unaotaabisha mgonjwa na familia yake. Nguvu alizokuwa nazo Bi. Boddy licha ya kumpoteza mumeye, pamoja na miaka mingi ya ujitoaji usio na ubinafsi wa kumtunza mwanae, zilinivutia sana. Yehova na ambariki yeye na wanaye.
E. N., Marekani
Pumzi Mbaya Lazima niwashukuru kwa ajili ya makala yenu yenye mafunzo “Waweza Kufanya Nini Kuhusu Pumzi Mbaya?” (Julai 8, 1995) Hilo lilikuwa tatizo langu! Ni kweli kwamba kuwa na pumzi mbaya hukufanya ushuke moyo. Nilikwenda kumwona daktari wa meno mara mbili, lakini hiyo harufu mbaya iliendelea. Nilitumia madokezo yaliyoko kwenye hiyo makala, nayo yanafanya kazi. Tafadhali endeleeni kuwasaidia watu tufeni pote.
R. O. I., Nigeria
Kosta Rika Ile makala “Kosta Rika—Nchi Ndogo, Unamna Mwingi” (Julai 8, 1995) ilifika siku chache tu kabla ya safari yangu ya kwenda huko; nikaitwaa ili kuirejezea. Kweli kweli hiyo ni nchi ya ajabu na yenye kusisimua! Kila mahali tulipokwenda, watu wangetabasamu na kutupungia mikono. Hebu wazia ulimwengu mpya wakati ambapo kila mtu kila mahali atakuwa mwenye urafiki kama huo!
T. N., Marekani